Jinsi Ndoa Inavyookoka Shambulio Hilo
MWANAMKE mmoja aliyefunga ndoa alisema hivi wakati mmoja: “Hakuna vitu vingi maishani ambavyo furaha yavyo yaweza kulingana na ile ya ndoa yenye kufanikiwa. Na hakuna vitu vingi vibaya zaidi ya ndoa isiyo na furaha.” Jambo hilo linafanya ndoa isikike kuwa kama kamari (karata) ya kucheza pesa nyingi unazoweza kushinda au kupoteza. Wenzi waliooana wanaweza ama kushinda kwa kupata furaha ya maisha au kupatwa na huzuni.
Hata hivyo, si lazima ndoa iwe kama kucheza kamari. Katika njia fulani inafanana na kusafiri kupitia eneo ambalo hujapata kupitia tena. Ukifunga safari ukiwa na wazo dogo tu jinsi ya kufika mahali unapokwenda, hakika unajihatirisha. Lakini unaweza kupunguza hatari hiyo sana ukipata mawaidha (mashauri) kutoka kwa mtu ambaye amekwisha kufunga safari hiyo akafanikiwa hapo mbele. Na kuna ndoa nyingi zenye kufanikiwa leo. Twaweza kujifunza nini kutokana nazo?
Viongozi Wenye Ujuzi
Uchunguzi mmoja ulifanywa katika Kanada juu ya hesabu fulani ya wenzi ambao walikuwa wameoana kwa miaka 15 au zaidi. Profesa Schlesinger wa Chuo Kikuu cha Toronto aliuliza ni nini baadhi ya mambo yaliyotokeza kufanikiwa kwa ndoa zao. Uchunguzi wake ulikazia umaana wa sifa nne: upendo, heshima, kutumainiana na kupashana habari.
Wenzi ambao walikuwa wameoana kwa furaha kwa miaka sabini (70) walihojiwa na gazeti moja. Siri ya kufanikiwa kwao ilikuwa nini? Wao walitaja kutumainiana, kujitahidi wasibishane, kuonyeshana shauku ya upendo, na kuwa na mradi mmoja wa kusaidia watu wengine.
Huenda mawazo hayo yakaonekana kuwa ya kizamani, lakini yalikuwa na matokeo mazuri. Iwapo unawajua watu ambao wamefunga ndoa zenye kufanikiwa kwa miaka kadha, kwa sababu gani usiwaulize siri ni nini? Inaelekea watasema mambo kama hayo.
Hata hivyo, huenda ukawa na maoni kwamba jambo lenye kuwa na matokeo mazuri kwa watu wengine lisingefaulu kwako. Hali yako ya kulelewa, utu au matatizo kwa njia fulani ni tofauti. Katika safari ya kupitia eneo lisilojulikana, jambo linalofaa lingekuwa kuwa na kitabu cha kuongoza kinachoonya juu ya hatari zote zinazoweza kuwapo ili upange safari yako katika njia ya kukuepusha na magumu yanayoweza kukutatiza hasa. Je! kuna kitabu cha kuongoza hivyo katika ndoa? Ndiyo, kipo. Na hakuna mtu anayepaswa kufunga safari ya kuendea ndoa bila kupata mashauri yacho.
Kitabu cha Kuongoza Kinachohitajiwa
Muda mfupi uliopita kijana mmoja mwanamume anayeitwa Alex alikigundua kitabu hicho cha kuongoza. Alex alikuwa amelelewa katika hali ya kuvunja sheria, kulewa pombe na matumizi mabaya ya dawa za kulevya. Pamoja na hayo yeye alikuwa amekwisha kupigana katika Vietnam na kukatishwa tamaa. Alikuwa na mke mchanga na mtoto aliyezaliwa karibuni, lakini ndoa yake ilikuwa inapatwa na magumu. Asubuhi moja, baada ya kutumbuiza rafikize waliokuwa wamekuwa wanajeshi hapo mbele kwa karamu ya kulewa usiku kucha katika nyumba yake, mkewe alisema: “Unanipuza. Hata unasahau kwamba nipo!”
Kwa furaha, Alex na mkewe walichunguza mashauri ya kitabu cha kuongoza. Upesi baadaye, yeye aliripoti hivi: “Tumepoteza wengi wa rafiki zetu wa kwanza, lakini sisi tu wenye furaha . . . sana sana tukiwa mume na mke. Siwezi kueleza uzuri huo kwa maneno—ni maono yasiyoelezeka kwa maneno. . . Nyutu zetu zimebadilika na jamaa yetu inavutiwa nasi sana.”
Ni kitabu gani cha kuongoza kilichowaonyesha Alex na mkewe njia ya kutoa ugomvi wa ndoa na kuwa na ndoa yenye furaha? Kitabu hicho kilikuwa ni Biblia. Kitabu hicho, ingawa ni cha kale, kinatoa mashauri ya hekima zaidi na matokeo mazuri juu ya ndoa zenye furaha zaidi ya chanzo kinginecho chote kilichopo leo. Ebu chunguza baadhi ya mambo inayosema.
Maneno ya Hekima
Hakuna mtu mkamilifu. Wenzi waliooana wanapaswa kujifunza kuishi pamoja na udhaifu wa mtu na mwenzake. Kwa hiyo, Biblia inasema: “Jivikeni moyo wa rehema, utu wema, unyenyekevu, upole, uvumilivu, mkichukuliana, na kusameheana, mtu akiwa na sababu ya kumlaumu mwenzake; kama [Yehova] alivyowasamehe ninyi, vivyo na ninyi. Zaidi ya hayo yote jivikeni upendo, ndio kifungo cha ukamilifu.”—Wakolosai 3:12-14.
Je! ndoa yo yote haingefaulu iwapo mume na mke wangefuata shauri hilo? Hakika wangeshinda matatizo mengi ya maisha ya kila siku. Hata watu waliooana karibuni ambao ni wageni kwa mmoja na mwenzake wangekuwa wanaelekea kwenye ndoa yenye furaha ikiwa wangesitawisha sifa hizo.
Habari zinaeleza juu ya waume ambao hawana huruma, wachoyo au hata wakatili. Hata hivyo Biblia inashauri hivi: “Enyi waume, wapendeni wake zenu, kama Kristo naye alivyolipenda [kundi] . . . Vivyo hivyo imewapasa waume nao kuwapenda wake zao kama miili yao wenyewe.” (Waefeso 5:25, 28) Mume anayehangaikia hali njema ya mkewe na kujinyima mambo fulani kwa ajili ya mapenzi ya mkewe inaelekea ataona ndoa yake ikifanikiwa.
Waume wengine hulalamika juu ya kuteta kwa wake wao na kusumbuliwa-sumbuliwa nao wakati wote. Hata hivyo Biblia inasema: “Mke anapaswa kumheshimu sana mume wake.” (Waefeso 5:33, NW) Mke anayefuata shauri hilo kwa sehemu kubwa anajiletea furaha yake mwenyewe.
Vile vivunja ndoa viwili, ulevi na uasherati, vinalaaniwa kabisa katika Biblia. “Waasherati hawataurithi ufalme wa Mungu, . . . wala wazinzi, . . . wala walevi.” (1 Wakorintho 6:9, 10) “Ndoa na iheshimiwe na watu wote, na malazi yawe safi; kwa maana waasherati na wazinzi Mungu atawahukumia adhabu.”—Waebrania 13:4.
Namna gani jamaa inapojiingiza? Biblia inaonyesha kwamba wenzi wachanga wanapaswa kuheshimu wazazi wao. Hata hivyo, jukumu la kwanza la mtu ni kwa mke wake. Yesu alisema hivi: “Mtu atamwacha babaye na mamaye, ataambatana na mkewe; na hao wawili watakuwa mwili mmoja. . . . Basi aliowaunganisha Mungu, mwanadamu asiwatenganishe.” (Mathayo 19:5, 6) Wenzi wachanga wanapaswa kukubali kwa furaha shauri kutoka kwa wazazi wao. Lakini hawapaswi kuwaruhusu wayaongoze maisha yao.
Uongozi Wenye Matokeo Mazuri
Huenda wengine wakaliona shauri hilo kuwa la kizamani katika ulimwengu wa leo. Lakini maandishi ya ulimwengu ya ndoa yakoje? Mabaya sana. Hata hivyo, je, ulisoma kwa uangalifu waliyosema wale waliokwisha kufanikisha ndoa zao? Wawe walijua au hawakujua, walisema sababu ya furaha yao ni sifa zinazopendekezwa katika Maandiko. Je! unaweza kubisha juu ya njia yenye kuleta fanaka?
Tukisitawisha nia ya kutoa inayopendekezwa na Biblia, je, tutapata hasara kwa njia fulani? Hapana. Kwa kweli kutoa ni sehemu ya msingi ya ndoa. Wote wanaofunga ndoa wanajinyima jambo fulani, lakini, ndoa yao inapofanikiwa, wanarudishiwa furaha mara mia moja. Kwa sababu gani? Kwa sababu, “Kuna furaha nyingi katika kutoa kuliko zilivyo katika kupokea.”—Matendo 20:35, NW.
Huenda ukasema ‘Jambo hilo linafaa kwa kusema. Lakini kwa njia halisi hakuna ndoa inayokuwa hivyo.’ Jibu ni kwamba kuna ndoa nyingi sana zenye furaha leo kwa sababu wenzi hao wanajitahidi kufuata shauri la Biblia. Hata mahali ambako kuna matatizo mazito—kama ilivyokuwa katika kisa cha Alex na mkewe—Maandiko yanaonyesha mradi unapasa kuwa nini. Wenzi wakijitahidi kufikia mradi huo, matokeo ya furaha yanafuata baada ya muda mfupi.
Hata hivyo, namna gani ikiwa ni mwenzi mmoja wa ndoa anayejaribu kutumia kanuni hizo? Tatizo hilo linakuwa gumu zaidi, lakini kuna tumaini. Ni afadhali zaidi mwenzi mmoja afanye mambo inavyofaa kuliko wote wawili wakifanya mambo isivyofaa. Na kwa kuvumilia, kungali kwaweza kuwa na matokeo mazuri.
Mume mmoja katika Korea alikuwa akimpiga-piga mkewe akiwa amelewa. Mkewe hakujaribu kumaliza uhusiano wao, hata ingawa maisha yalikuwa magumu. Mke huyo alikuwa anajitahidi kufikia mradi unaostahili wa ndoa yenye furaha. Kwa hiyo, akiwa peke yake, yeye alifuata shauri la Biblia, sana sana shauri layo kwa wake kwamba wasitawishe “roho tulivu na ya upole, ambayo ni ya thamani kuu machoni pa Mungu.”—1 Petro 3:4, NW.
Kwa muda wa miaka 11 mke huyo alivumilia. Je! jambo hilo lilistahili? Ndiyo, kwa sababu hatimaye mume wake alichochewa ajiangalilie kitabu hicho cha kuongoza. Kwa sababu gani? Ukimwuliza, yeye angekujibu kwamba “roho tulivu na ya upole” ya mkewe ilimchochea atafute ni nini siri ya mwenendo wake mwema. Yeye aliona hekima ya shauri la Biblia akabadili njia zake.
Ni kweli ndoa “yaweza kuwa njia mojayapo ya maisha yenye kuridhisha na kutosheleza zaidi.” Pengine hatupaswi kushangazwa na hilo, kwa sababu yeye aliyetupa uzima, Yehova Mungu, Ndiye huyo huyo aliyetupa ndoa. (Zaburi 36:9; Mwanzo 2:18-24) Na Ndiye aliyetoa kitabu kile cha kuongoza, Biblia, ili atusaidie tufanikishe ndoa zetu.
Leo mpango wa ndoa unashambuliwa kwa sababu ya mikazo ya ulimwengu tunamoishi. Lakini, kwa kuwa ndoa inatoka kwa Mungu, inaokoka shambulio hilo. Na ukifuata shauri la Mungu lililoandikwa katika Biblia, ndoa yako itaokoka, na wewe, pia, utaiona kuwa ni njia yenye kuridhisha zaidi ya maisha.