Wewe Unaongozaje Maisha Yako?
“Wenye furaha ni wale ambao njia yao haina kosa, wale wanaotembea katika sheria ya Yehova.”—Zaburi 119:1, NW.
1. Historia inaonyesha ni jambo gani la maana ili kuwa na furaha?
‘INAHITAJIWA nini ili kuwa na maisha yenye furaha?’ Watu wengi wangejibu kwa kutaja vitu vya kimwili, kama chakula, mavazi na nyumba, au namna-namna za tafrija na anasa. Hata hivyo historia inathibitisha mambo ya maana zaidi ili uwe na furaha ni maoni yako juu ya maisha na njia yako ya maisha. Unaposhughulika na aliyekuajiri kazi, wenzako na jamaa—je, wewe utasema kweli? je, wewe utachukua kitu kisicho chako? je, wewe utashiriki katika kazi au tafrija fulani yenye kutiliwa mashaka?
2. Watu wengine huongozaje maisha zao, na hilo linatokeza maulizo gani?
2 Katika kuamua maulizo hayo, wengine wanapendelea amri zilizo wazi ambazo ama wanazijua ama wanazitafuta wanapozihitaji. Wengine hufanya ‘wanaloonelea’ ni haki kulingana na dhamiri yao. Hata hivyo, inaelekea huenda ukauliza, Kwa kuwa Biblia inasema mengi juu ya “dhamiri,” hiyo dhamiri ni nini? Inafanyaje kazi? Je! inatimiza sehemu ya lazima katika ufanyaji wetu wa maamuzi na kupata furaha? Na twawezaje kusema, kama mtume Paulo: “Mimi kwa dhamiri safi kabisa nimeishi mbele za Mungu hata leo hivi”?—Matendo 23:1.
Dhamiri Yako—Ni Nini?
3, 4. “Dhamiri” ni nini, na ni nani walio nayo?
3 Watu wengi hufikiri dhamiri ni ufahamu tu wa yaliyo haki na yaliyo kosa. Hata hivyo, tuna chanzo chenye kutoa habari sahihi zaidi juu yake—Neno la Mungu. Biblia inatusaidia kuthamini kwamba dhamiri ni mshuhudiaji wa kindani. Kwa hiyo Paulo alisema: ‘Dhamiri yangu inanishuhudia katika roho takatifu.’ (Warumi 9:1) Yeye alitumia neno la Kigiriki syneiʹdesis, ambalo kwa halisi linamaanisha, maarifa yaliyo mwenzi na mtu binafsi. Kwa hiyo dhamiri ni uwezo wa kujiangalia na kutoa uamuzi juu yako mwenyewe, kujishuhudia mwenyewe.
4 “Dhamiri si jambo tu lililositawishwa na ujamii, kwa maana Biblia inaonyesha kwamba Mungu aliitia katika wanadamu wawili wa kwanza. (Mwanzo 3: 7, 8) Akizungumza juu ya kutozwa hesabu kwa Wayahudi na watu wa Mataifa, Paulo aliandika hivi: “Kwa maana watu wa Mataifa wasio na sheria wafanyapo kwa tabia zao yaliyo ndani ya torati, hao wasio na sheria wamekuwa sheria kwa nafsi zao wenyewe. Hao waionyesha kazi ya torati iliyoandikwa mioyoni mwao, dhamiri yao ikiwashuhudia, na mawazo yao, yenyewe kwa yenyewe, yakiwashitaki au kuwatetea.” (Warumi 2:14, 15) Ndiyo, hata wasio na sheria iliyoandikwa kutoka kwa Mungu wamekuwa na maoni kwamba, mambo kama kuua, kuiba na ndoa za maharimu, ni kosa. Vilevile kutokana na mistari hiyo tunaona kwamba dhamiri ni ushirikiano wa moyo na akili (“mawazo”).
5. Ni nini moja ya njia ambazo dhamiri yako inafanya kazi?
5 Kazi ya dhamiri ambayo yaelekea twafahamiana nayo sana ni kuhukumu kwayo mwenendo wetu ‘baada ya jambo la hakika,’ baada ya tendo baya. Tunapokata kauli kwamba tumefanya kosa au tukatenda kwa njia ya kuvunjia heshima, dhamiri yetu inatushtaki na kutulaani. (Linganisha 2 Samweli 24:10; 1 Yohana 3:20.) Tukiiitikia, sehemu hiyo inayotimizwa na dhamiri yaweza kutusaidia kwa kutusukuma tuepuke kurudia kosa. Na huenda ikatusaidia tutubu, tuombe msamaha au hata kufutilia mbali umizo hilo ikiwa twaweza.—Zaburi 32:3, 5; Mathayo 5:23, 24; Luka 19:1-8.
6. Ni kwa njia gani nyingine dhamiri yako inaweza kutenda?
6 Dhamiri yetu inaweza kutumika katika njia nyingine. Ingawa wengine husema kwamba dhamiri nzuri inakaa kimya, tunapokabili uamuzi fulani au tatizo, dhamiri yetu inapasa kusema waziwazi na kutuchoma-choma tufanye yaliyo haki. Mfano mzuri ni kukataa kwa Yusufu vishawishi vya mke wa Potifa. Ingawa Mungu alikuwa bado hajatoa sheria iliyoandikwa ya kukataza uzinzi, dhamiri ya Yusufu ilimsukuma akatae uasherati. (Mwanzo 39:1-9) Ikiwa, kabla ya kutenda, tunaisikiliza dhamiri yetu, huenda tukaepuka huzuni kuu ya dhamiri iliyosumbuliwa.
7. Tunatamani kutambua nini waziwazi kutokana na funzo hili?
7 Ulizo hili bado limebaki: Dhamiri inapasa kuwa na uvutano wa kadiri gani? Je! wewe unakubali kwamba masuala mengi ya kiadili na ya kibinafsi yapasa kuamuliwa kwa msingi wa dhamiri? Au ni afadhali amri? Tunahitaji kujua. Vilevile, je, kuna hatari ambazo twapaswa kuzijua? Neno la Mungu, linalosema “lafaa kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki” linaonyesha nini?—2 Timotheo 3:16.
Maoni ya Kupita Kiasi
8. Adili zimeangaliwa kwa maoni gani mawili yenye kupita kiasi?
8 Pambano lililoko kati ya amri na dhamiri ni la kale sana. Katika makala “Uamuzi wa Yaliyo Haki na Yaliyo Kosa” kitabu Encyclopaedia Britannica (chapa ya 11) kinaeleza kwamba adili “nyakati nyingine imedhaniwa kuwa sheria ya nje-nje, nyakati nyingine kuwa maelekeo ya ndani-ndani. . . . Wanaoamini sheria wameweka tumaini lao katika mamlaka au mawazo; hali wanaoamini kufuata maelekeo wanatumaini hasa uwezo wetu wa kufanya mambo kwa kisilika—dhamiri, mawazo ya akili au maono ya ndani.” Maoni hayo mawili yenye kupita kiasi yalikuwapo wakati Yesu na mitume wake walikuwa duniani. Twaweza kuthamini vizuri zaidi msaada wa Biblia uliosawazika na hekima ya kimungu kwa kuchunguza hali iliyokuwapo wakati huo.
9, 10. (a) Mafarisayo walionyeshaje njia moja ya kupita kiasi? (b) Kinyume cha hilo, ni nini yaliyokuwa maoni ya kawaida kati ya Wagiriki na Warumi?
9 Mafarisayo wa Kiyahudi walikuwa wakitetea amri kwa juhudi. Kwa kutoridhika na sheria ya Musa, walitokeza amri nyingi au “maagizo ya wanadamu” ambayo yalitangua amri za Mungu. Licha ya kutokeza amri hizo ambazo zilipita cheo cha mambo ambayo Mungu alitaka, maoni yao ya sheria yalitia moyo maoni ya kwamba haki ingeweza kupatikana kwa kujua na kufuata maagizo hayo ya wanadamu. —Mathayo 15:1-20; 23:1-5; Luka 18:9-12.
10 “Upande mwingine ilikuwa Ugiriki ya kale,” ndivyo anavyoeleza mtaalamu mkubwa Samuel H. Butcher. “Kati ya Wagiriki . . . hakuna mfumo wa mafundisho ya kidini na sherehe, hakuna vitabu vyenye amri zenye kuonyesha adili, zilizopokezwa kwa watu kwa njia ya maandishi. .. . watu hawakuweza kuchukua hatua iliyowapasa kwa sababu amri zilikuwa za namna moja tu.” Kwa habari ya Warumi, kitabu Encyclopaedia Britannica kinasema: “Sisero na Seneka waliongozwa na hali ya kufikiria mambo kwa akili timamu. Waliamua kila tatizo kwa kulingana na lilivyostahili, wakiangalia kusudi la amri wala si maandishi tu yenye kuitaja amri yenyewe.” Falsafa hii ya Kigiriki/Kiroma ilipendwa na watu wengi katika karne ya kwanza. Je! ingevutia Wakristo? Paulo aliandika hivi: “Angalieni mtu asiwafanye mateka kwa elimu yake ya bure na madanganyo matupu, . . . kwa jinsi ya mafundisho ya awali ya ulimwengu, wala si kwa jinsi ya Kristo.”—Wakolosai 2:8; Matendo 17:18-21.
11. Maoni hayo mawili ya kupita kiasi yalionekanaje wazi baadaye katika historia?
11 Vilevile, katika karne za baadaye kulikuwa na watu wenye kutetea maoni hayo mawili yenye kupita kiasi kinachofaa, hata kati ya watu walioitwa Wakristo. Wayesuiti walijulikana kwa ajili ya kukazia adili zenye kutegemea sheria za Kanisa zisizohesabika. Baada ya Urekebishaji wa Kidini, Uprotestanti ulikazia mtu kutenda atakavyo na dhamiri, jambo ambalo limeongoza kwenye maoni ya wakati huu yanayojulikana kama “wema wa hali,” yaliyopendekezwa kwa watu na Askofu Dakt. Joseph Fletcher. Jarida The National Observer linaripoti hivi: “Dakt. Fletcher amesema waziwazi mwongozo wenye kutokeza mabishano wa mtu binafsi kutenda atakavyo na kuwa na daraka lake, ambao msingi wake ni wema wa upendo wa kidugu, ambao anasema wapasa kuwaweka huru watu wa kisasa kutokana na amri zisizobadilikana za kikale na orodha ya sheria kama zile ‘Amri Kumi.’ . . . Upendo ukiwa ndio uongozi pekee, basi, kutoa mimba, ngono kabla ya ndoa, talaka, . . . na mambo mengine yanayoonwa kuwa kosa mahali pote yanakubalika kiadili kwa Dakt. Fletcher katika hali fulani.”
12. Ni hatari gani iliyo mbele yetu tunayohitaji kuiepuka?
12 Kwa wazi, wanadamu wanaelekea kupita kiasi—ama wanaongozwa na amri ama na dhamiri. Wengine ambao wanaona kasoro za upande mmoja wanapita kiasi kwa kwenda kwenye upande ule mwingine. Kwa mfano, wakati wa Zamani za Karne ya Sita Mpaka ya Kumi na Sita maoni yaliruka kutoka yale ya kufikiria amri ya Wayesuiti mpaka kuwa yale ya Warekebishaji wa Kidini ya kukazia uhuru wa mtu kutenda atakavyo na dhamiri. Vilevile, huenda ukawa unajua wazazi waliokuwa wakitoa amri nyingi mno walipokuwa wakiwalea watoto wao. Lakini watoto hao walipokua, walipita kiasi kwa kwenda upande ule mwingine, na kuwaruhusu watoto wao wenyewe wafanye watakavyo kabisa, kukawa na matokeo yenye msiba. Twaweza kuona ukweli wa maelezo haya ya Biblia: “Ee [Yehova], najua ya kuwa njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.”—Yeremia 10:23.
Uongozi wa Mungu Wenye Kiasi na Msaada
13. Biblia inatupa msaada gani juu ya adili na dhamiri?
13 Yehova amekwisha kutoa msaada wenye kiasi kwa Wakristo katika Maandiko ili tuepuke: (1) kuwa na maoni ya kisheria ya kukazia amri kupita kiasi, ambalo ni jambo linaloweza kutokeza maoni ya fikira zenye upungufu, za kushikilia jambo mno kwa njia isiyofaa katika maisha ya ibada, au kukazia kupita kiasi juu ya dhamiri kutenda itakavyo, jambo ambalo limefanya wengine wawe na mawazo yanayotetea mabaya. Ili kuwa na kiasi cha Neno la Mungu na kufaidika na uongozi walo, tunahitaji nia ya Daudi: “Ee [Yehova], unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako, uniongoze katika kweli yako, na kunifundisha. Maana Wewe ndiwe Mungu wa wokovu.”—Zaburi 25:4, 5.
14, 15. Tunaweza kujifunza nini kutokana na Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo juu ya maoni ya Wayahudi kuhusu Sheria na yale ya Mungu?
14 Biblia inaonyesha wazi Yesu alikataa mawazo ya kushikilia mno amri ya waandishi na Mafarisayo. Wayahudi wachache ambao hawakutaka kutumia uwezo wao wa kufikiri waliopewa na Mungu huenda wakawa walipenda maagizo juu ya mkono usafishwe kufika wapi, “kazi” ilikuwa nini katika sabato, ni mazao gani yaliyopasa kutolewa zaka, na kadhalika. Mwongozo huo ulitokeza amri zenye kulemeza, ukawa na mafasiri yasiyo na mwisho na ukaondosha fikira kutoka kwa kusudi na sehemu za maana zaidi za Maandiko. Yesu aliwaambia hivi viongozi wa kidini: “Mnalipa zaka za mnanaa na bizari na jira, lakini mmeacha mambo makuu ya sheria, yaani, adili, na rehema, na imani.”—Mathayo 23:23; Marko 7:3, 4.
15 Sheria ya Musa ilitokeza hali njema ya kiroho, kiadili na ya afya ya Wayahudi, na pia kuwathibitishia kwamba wakiwa watenda dhambi walimhitaji Masihi. (Wagalatia 3:19, 23-25; Warumi 7:7-14) Kwa sababu ilikuwa kanuni kamilifu, hakuna Mwisraeli angeweza kuifuata bila kosa na hivyo kuwa na dhamiri kamilifu. (Waebrania 9:9, 10) Kwa hiyo, hata ingawa orodha hiyo ya sheria ilitokana na Mungu, mara tu kusudi la Mungu la orodha hiyo ya sheria lilipokwisha, yeye aliiondolea mbali. Halafu, badala ya kushughulika na watu wa Jina lake kwa msingi wa orodha ndefu iliyoandikwa, Mungu ‘angeweka sheria zake katika akili na mioyo yao.’—Yeremia 31:33, NW; Waebrania 10:16; 2 Wakorintho 3:5-11.
16. Ni somo gani linalotolewa hapo kwa (a) watu wanaojitolea amri kali-kali, na (b) kwa sisi na maoni yetu juu ya amri?
16 Wakiwa wanakumbuka jambo hilo, leo watu ambao wanaangalia au kusawazisha utendaji wa wengine wanapaswa kujihadhari wasiwalemeze kwa matakwa ya kibinadamu yasiyo ya lazima. Maelekeo ya kufanya hivyo huenda yakawa yenye nguvu sana ndani ya wale wenye kutoa amri kali-kali au wenye kujiwekea wenyewe madai mengi na hivyo kuonelea kwamba wengine wanapaswa kuyaona mambo kwa njia iyo hiyo. Hata hivyo, Paulo aliwaandikia hivi Wakristo: “Si kwamba sisi tu mabwana wanaosimamia imani yenu, bali sisi tu wafanyi kazi wenzi kwa ajili ya furaha yenu, kwa maana mnasimama kwa imani yenu.” (2 Wakorintho 1:24, NW) Kuhusiana na hilo, kwa ujumla Wakristo wanapaswa kujihadhari na kutaka mtu mwenye mamlaka afanye amri juu ya kila jambo. Badala yake, twapasa kuongeza maarifa juu ya yale ambayo Neno la Mungu linasema ili tuzoeze dhamiri na nguvu zetu za ufahamu.—Waebrania 5:14.
17. Tunahitaji kujihadhari na maoni gani mengine yasiyo sahihi?
17 Hatari nyingine, hata hivyo, ni kupita kiasi kwa kuruka upande ule mwingine, kuonelea kwamba kila Mkristo yuko huru kufanya karibu kila jambo ambalo dhamiri yake inamruhusu kufanya. Hivi karibuni wachache wametokeza ubishi juu ya jambo hilo, na kusema “Ukristo si dini ya amri-amri” na kutaja vifungu vya maneno kama haya: “Maana ninyi, ndugu, mliitwa mpate uhuru; lakini uhuru wenu usiwe sababu ya kuufuata mwili, bali tumikianeni kwa upendo. Maana torati yote imetimilika katika neno moja, nalo ni hili, Umpende jirani yako kama nafsi yako.” (Wagalatia 5:13, 14) Ni kweli kwamba Wakristo hawako chini ya sheria ya Musa wala orodha nyingine ya sheria nyingi za kimungu. Hata hivyo twapaswa kujihadhari ‘mtu ye yote asitudanganye kwa maneno ya kushawishi (“hoja zenye kushawishi na kuvutia na usemi wa hila,” Amplified Bible),’ kwa maana uchunguzi wa unyofu wa Biblia unaonyesha kwamba inatupa sheria au amri.—Wakolosai 2:4.
Wakristo Si Watu Wasio na Sheria
18, 19. Msimamo wa Wakristo ni nini kuhusu sheria na amri za Biblia?
18 Paulo aliwaandikia Wakorintho kwamba mtu mwenye hatia ya uasherati apaswa kufukuzwa. Aliongeza kwamba waabudu sanamu, wazinzi, wanaume wenye kulalana na wanaume wenzao, wevi, watu wenye pupa, walevi, watukanaji na wanyang’anyi “hawataurithi ufalme wa Mungu.” (1 Wakorintho 5:1, 6, 7, 11-13; 6:9-11) Vilevile twasoma kwamba lazima Wakristo ‘kujiepusha na vitu vilivyotolewa sadaka kwa sanamu, na damu, na nyama zilizosongolewa, na uasherati’ na kwamba wanaodai kuwa ndugu ambao wanaendeleza mafundisho ya uongo wapasa kukataliwa. (Matendo 15:28, 29; Tito 3:10; 2 Yohana 9-11) Kwa wazi, hapa sheria zinahusika. Mzoevu wa dhambi hizo hawezi kuwa Mkristo wa kweli. Na ikiwa mtumishi wa Mungu anaendelea kufanya dhambi hizo bila kutubu, lazima atengwe na ushirika.
19 Vilevile tuna amri za Biblia kuhusu mambo yasiyo makosa ya kutenga na ushirika. Kwa mfano, Paulo aliandika kwamba Wakristo waseja wanapaswa kuoa (au kuolewa) “katika Bwana tu,” naye aliamuru kwamba “ikiwa mtu hataki kufanya kazi, basi, asile chakula.” (1 Wakorintho 7:39; 2 Wathesalonike 3:10) Huenda mtu akawaza hivi, ‘Kwa kuwa singefukuzwa kwa kutokutii shauri hilo, hakika amri hizo hazina uzito.’ Huko ni kuwaza kwa kipumbavu kama nini! Mungu huziona amri hizo kwa uzito. Je! Paulo hakuwaambia Wathesalonike ‘wamtie alama’ na ‘kutoshirikiana’ na watu wavivu wanaokosa kutii kwa makusudi amri juu ya kufanya kazi?—2 Wathesalonike 3:14, 15, NW.a
20, 21. Twaweza kujifunza nini juu ya maagizo ya kuliongoza kundi, nasi twapaswa kuyaonaje?
20 Amri nyingine ziko kwa ajili ya faida ya kundi hasa. Kwa mfano, katika wakati uliopita kuna Wakristo ambao wangeweza kuzungumza katika lugha. Paulo aliagiza kwamba wawili au watatu tu kati yao wazungumze katika pindi moja, kwamba wapokezane zamu, na kwamba awepo mtafsiri—amri hizo zilitokeza amani na utaratibu. (1 Wakorintho 14:26-33) Vivyo hivyo wazee wa kundi la Kikristo leo wanaweza kutoa maagizo juu ya kutokusimama katika milango ya Jumba la Ufalme kwa njia inayozuia wengine kupita, kutoweka viti akiba isivyo lazima, au kuegesha motokaa kwa kuwafikiria jirani na kwa ajili ya usalama. Amri hizo za kundi si kinyume cha maandiko kwa maana zina kusudi lile lile (amani na utaratibu mzuri) sawa na shauri la Paulo juu ya kuzungumza katika lugha. Shauri la Biblia linahusiana na hayo: “Watiini wenye kuwaongoza.” (Waebrania 13:17) Kwa kuwa kuepuka kwetu dhambi kama kusema uongo au kuiba ni kumtii Mungu, lazima andiko hilo liwe linahusu kutii kwetu uongozi wa wazee katika mambo yanayohusu kundi. Wala si vigumu kuwatii ikiwa hawapigi “ubwana juu ya wale ambao ni urithi wa Mungu” kwa kuweka sheria.—1 Petro 5:3, NW.
21 “Amri” nyingine au njia za kufanya mambo zaweza kufaidi kundi la ulimwenguni pote. Kwa mfano, Mashahidi wa Yehova huombwa warudishe ripoti za ushuhuda wanaoutoa. (Linganisha Matendo 2:41, 42; 8:14.) Mtu anayepita kiasi kwa kuruka upande wa maoni ya mtu binafsi kufanya atakavyo huenda asikubaliane na mpango huo. Lakini ebu fikiria mema yaliyotimizwa kwa sababu wale wanaoliangalia kundi wameweza kujua kutokana na ripoti kadiri ambayo utoaji wa ushuhuda juu ya ufalme umetolewa, mahali ambako msaada unahitajiwa, na wakati ambapo wanafunzi wapya wanaweza kufanywa wawe kundi. Na je, sisi hatujafurahia kusoma ripoti za ulimwenguni pote? (Ezekieli 9:11; Marko 6: 30; Matendo 14:21-23; 15:3; 19:1-6) Tukiamini kwamba Mungu anawaongoza watu wake, tunaweza kuonyesha roho ya utegemezaji na ushirikiano.
22. Kwa sababu gani tunahitaji kujifunza zaidi habari hii ya dhamiri?
22 Zaidi ya sheria au amri fulani-fulani, Maandiko yana kanuni zinazosaidia ambazo Wakristo wenye hekima wanaweza kufuata ili wawe ‘kamili katika njia zao.’ (Zaburi 119:1) Kanuni zinasaidia sana-sana ili tupatanishe dhamiri zetu na mawazo ya Mungu. Lakini maana yake hiyo ni nini kwa habari ya ‘mambo yanayohusu dhamiri’? Wengine wamekuwa na maono, ‘Iwapo jambo fulani linategemea dhamiri yangu, basi nitakavyofanya ni jambo la kibinafsi kabisa.’ Ebu tuchunguze jambo hilo katika makala inayofuata na kujifunza zaidi jinsi tunavyoweza kuzoeza dhamiri yetu ili itupe faida kubwa zaidi iwezekanavyo.
[Maelezo ya Chini]
a Ona Mnara wa Mlinzi wa Desemba 15, 1981, kurasa 11, 12; Februari 1, 1983, ukurasa 22.
Je! Wewe Unaweza Kueleza?
◻ Dhamiri yako ni nini, nayo inaweza kukusaidia katika njia gani?
◻ Yamekuwapo maoni gani mawili ya kupita kiasi juu ya adili?
◻ Biblia inatusaidiaje tuwe na maoni yanayofaa juu ya uongozi wa adili?
◻ Tunahitaji maoni gani ya Kimaandiko juu ya sheria au amri?
[Blabu katika ukurasa wa 10]
Watu wenye kujiwekea madai mengi wanahitaji kujihadhari na maelekeo ya kufanyia na kutekelezea wengine amri nyingi
[Blabu katika ukurasa wa 11]
Kwa kukosea wengine wameonelea kwamba Mkristo yuko huru kufanya lo lote ambalo dhamiri yake inamruhusu kufanya