Ule Ufalme na “Mahali Patakatifu”
“Habari njema hizi za ufalme zitahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja. Kwa hiyo, mkionapo kile kitu chenye kuchukiza chenye kuharibu, kama kilivyosemwa kupitia kwa Danieli nabii, kikisimama katika mahali patakatifu, (msomaji na atumie ufahamu,) basi walio Yudea na waanze kukimbia kwenye milima.”—Mathayo 24:14-16, NW.
1. Leo watangazaji wenye juhudi wa ufalme uliosimamishwa wa Mungu wanapendezwa na nini?
JE! WEWE umekuwa ukishiriki katika kuzihubiri “habari njema hizi za ufalme”? Ikiwa ndivyo, unatazamia kwa hamu nyingi ‘kuja kwa ule mwisho.’ Katika habari hiyo, unapendezwa sana pia na kufahamu kinachomaanishwa leo na “kile kitu chenye kuchukiza chenye kuharibu” na ‘kusimama kwacho katika mahali patakatifu.’ Utataka kujua matumizi ya kisasa ya mambo ambayo nabii Danieli alisema juu ya vitu hivi na namna, leo, unavyoweza kuwa kati ya wale wanaopata wokovu kwa “kukimbia kwenye milima.”—Mathayo 24:3-16, NW.
2. (a) Mengine ni gani kati ya maandiko yanayotusaidia tuwajue “watakatifu” wa unabii wa Danieli? (b) Ni kikundi kingine gani ambacho kimetokea hivi majuzi, na vikundi vyote hivi viwili vinapendezwa na kufanya nini?
2 Unabii wa Danieli unasema mengi juu ya “wale walio watakatifu” wanaourithi ufalme. (Danieli 7:27, NW) Hao ndio kile kikundi kidogo cha Wakristo ‘waliozaliwa tena,’ Waisraeli wa kiroho, ambao wameshika ukamilifu chini ya mashambulio ya Shetani, na hivyo wakastahili kuwa na nafasi ya kukaa katika ufalme wa mbingu. (Yohana 3:3; Luka 12:32) Katika miaka ya majuzi, wale waliobaki wa hawa mashahidi watiwa mafuta wa Mungu wameungwa na “kundi kubwa . . . kutoka kwenye mataifa yote,” wanaotumainia kuishi milele katika dunia ya paradiso. Je! wewe ni wa kimoja cha vikundi hivyo viwili? Ikiwa ndivyo, una pendeleo sasa la kumtolea Mungu “utumishi mtakatifu” katika patakatifu pa kidunia pa hekalu la kiroho lake. Huu ni utumishi mtakatifu unaofanyiwa katika “mahali patakatifu” panapolingana na patakatifu pa hekalu la Yehova katika Yerusalemu wa kale.—Ufunuo 7:4, 9, 15, NW; Warumi 12:1, 2.
3, 4. (a) Sasa ni ‘Yerusalemu’ tatu gani tunazoangalia? (b) Neno la Mungu linaelezaje juu ya kila moja ya ‘Yerusalemu’ hizo?
3 Kwa sababu ya uasi-imani wa Wayahudi, ambao walimwua hata Mwana wa Mungu, Yerusalemu wa kidunia ulitupiliwa mbali, ukaachwa na Mungu. (Mathayo 23:37, 38) Walakini, Yerusalemu mkubwa zaidi uliendelea kupendelewa na Yehova. Wagalatia 4:26 unauita “Yerusalemu wa juu.” Ni “mwanamke” wa Yehova, tengenezo lake mwenyewe la kimbingu lililo mfano wa mke. Yerusalemu huo ndio uliomzaa Mwana wa kiroho wa Mungu, Yesu Kristo, ambaye, katika mwaka wa 33 WK, alitoa ‘nafsi yake ya kibinadamu iwe ukombozi’ kwa ajili ya wanadamu.—Mathayo 20:28, NW.
4 Baada ya Yesu kufufuliwa akiwa roho, yeye alitukuzwa kwenye mkono wa kuume wa Baba yake wa kimbingu. Katika wakati uliowekwa, mwaka wa 1914 WK, Yehova alimsimamisha katika ufalme wake, ambao Waebrania 12:22 pia inaushirikisha na jina Yerusalemu kwa kuuita “Yerusalemu wa mbinguni.” Baada ya muda fulani, ufalme huu ungeharibu mfumo mbovu wa Shetani na kurudisha paradiso kwenye dunia yetu.—Mathayo 6:9, 10.
Kuacha “Mahali Patakatifu” Ukiwa
5. (a) Yesu alisema nini juu ya Yerusalemu wa kidunia? (b) Basi ni ulizo gani na unabii gani uliotokea?
5 Ebu na tufungue Biblia zetu sasa kwenye Mathayo, sura ya 23. Hapo katika mstari wa 38 utayaona maneno ya Yesu kwamba ‘nyumba ya Yerusalemu imeachwa hali ya ukiwa.’ Halafu, ndipo Yesu anapowaambia wanafunzi wake walioshangaa maneno ya Mathayo 24, mstari wa 2, kuhusu hekalu la huo Yerusalemu wa kidunia: “Amin, nawaambieni, Halitasalia hapa jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomoshwa.” Jambo hilo likafanya wanne wa wanafunzi wamwulize Yesu ulizo la mstari wa 3, NW: “Tuambie, Mambo haya yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” Ndipo Yesu akautoa unabii wake unaojulikana vizuri sana ambao unaendelea mpaka mwisho wa Mathayo, sura ya 25.
6, 7. (a) Katika utimizo wa unabii huo, ni kitu gani sasa kilitishwa? (b) Kwa njia hiyo “kile kitu chenye kuchukiza” kilionekanaje kuwa ‘kimesimama katika mahali patakatifu’?
6 Kile walichotaka kujua wanafunzi wa Yesu huko nyuma mwaka wa 33 WK kilikuwa mwisho wa mfumo wa Kiyahudi, ambao makao makuu yake yalikuwa katika Yerusalemu wa kidunia na hekalu lake. Ulikuwa mfumo wa kidini uliokuwa umeasi imani. Lakini ujapoasi imani, Yerusalemu uliendelea kujulikana kuwa “mji mtakatifu,” hata baada ya Yesu kufa. (Mathayo 27:53) Katika utimizo wa unabii wa Yesu, dhiki ziliuzidia Yerusalemu na Yudea na mataifa mengine ya karibu. Halafu, mwaka wa 66 WK, malejioni (majeshi) ya Kirumi yakiwa chini ya Jemadari Galo yakaushambulia Yerusalemu. Kama Yesu alivyotabiri (kulingana na Luka 21:20), Yerusalemu ‘ulizungukwa na majeshi yaliyopiga kambi.’ (NW) Kama ilivyosemwa na mwanahistoria Yosefo, hata yaliuingia mji yakiwa na bendera zao za kisanamu na yakaanza kuufukua ukuta wa hekalu.
7 Hayo majeshi ya Kirumi kwa uhakika yalikuwa yamesimama katika “mahali patakatifu.” Yalikuwa yamejiandaa kuufanya ukiwa huo ‘mji wa Yehova,’ mji ambao ulikuwa umeshirikishwa kwa karne nyingi na ibada ya Yehova. (Zaburi 101:8) Kilikuwa “kitu chenye kuchukiza” kama nini kwa maoni ya waasi-imani wa Kiyahudi na pia kwa Wakristo wa Kiyahudi! Walakini, Wakristo peke yao ndio waliotambua kwamba hali hiyo ndiyo iliyokuwa imesemwa na Yesu katika unabii. Zaidi ya huo “mji mtakatifu” na hekalu lake la ibada kutishwa, hata Wakristo waliokuwa ndani wakiwa washikamanifu kwa Yehova na neno la kweli lake walitishwa. Wangeweza kuokokaje?
8. Basi Yehova aligeuzaje mambo kwa kutumia maarifa, na matokeo yakawa nini?
8 Kwa mwujiza Yehova aligeuza matukio. Kwa ghafula jeshi la Kirumi likajiondoa, likaacha wazi njia ya Wakristo kutii unabii wa Yesu. Ndio hao! Walitii na “kukimbia kwenye milima” ya Gileadi! Halafu, mwaka wa 70 WK, “kile kitu chenye kuchukiza chenye kuharibu” kikarudi. Kwa muda wa miezi minne tu, jeshi la Kirumi likiwa chini ya Jemadari Tito liliufanya Yerusalemu ukiwa, likapaacha palipodhaniwa kuwa “mahali patakatifu” pakiwa lundo la mawe yaliyobomoka. Wayahudi zaidi ya milioni moja walikufa katika maangamizi hayo makuu, na waokokaji wakawa wachache. (Danieli 9:26) Lakini Wayahudi waliokuwa wamefanywa Wakristo walikuwa salama! Kwa sababu gani? Kwa sababu walilitii neno la kweli la kiunabii lililonenwa na yule Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo.—Marko 13:1, 2, 14.
Ulinganifu wa Kisasa
9. Kwa sababu gani inatupasa tutake kujua matukio hayo ya karne ya kwanza leo?
9 Hayo matukio ya karne ya kwanza yana maana kubwa kwetu sisi leo. Kwa sababu gani? Kwa sababu yana ulinganifu wa kustaajabisha katika hii karne ya 20. Ni katika siku zetu unabii mkubwa wa Yesu utafikia utimizo wake wa mwisho, wenye kuudhoofisha ulimwengu! Walakini, safari hii si ule mji wa Yerusalemu na nchi ya Yudea tu unaohusika, bali ni dunia yote inayokaliwa na watu, ikiwa na miji yake iliyo makumi ya maelfu, mamia yake ya vikundi vya kitaifa na kikabila na watu wake walio milioni 4,400, ndiyo, mfumo mzima wa mambo ya ulimwengu.
10. (a) Ni kipindi gani kilichomalizika mwaka wa 1914, na namna gani? (b) Kwa sababu gani sasa kuna “ole” usiopata kuwa na kifani duniani?
10 Hata wanahistoria wa kilimwengu wamesema kwamba mwaka wa 1914 WK ulileta badiliko lenye kuanza kipindi cha mambo mapya. Kwa kweli, “nyakati za mataifa zilizowekwa” zilikwisha mwaka huo. (Luka 21:24-28, NW) Yehova hangeruhusu tena mamlaka za Mataifa yasiyo ya Kiyahudi zitawale kama zilivyotaka. Kwa hiyo unabii huu ulitimizwa kuelekea Bwana Yesu: “[Yehova] atainyosha toka Sayuni [“Yerusalemu wa mbinguni,” ule ufalme wa kimasihi] fimbo ya nguvu zako [akisema,] Uwe na enzi kati ya adui zako.” (Zaburi 110:2) Huyo mfalme aliyeketishwa kwenye enzi alitii na akatupa Shetani na magenge yake ya kishetani yatoke mbinguni na kushuka kwenye ujirani wa dunia. Kwa hiyo, kwa “wakati mchache,” ni “ole wa nchi.” (Ufunuo 12:7-12) Sasa, tangu mwaka wa 1914 na kuendelea, unabii mkubwa wa Yesu wa Mathayo sura ya 24 na 25 unatimizwa duniani pote.
11. Wewe mwenyewe umeona nini katika utimizo wa unabii mkubwa wa Yesu?
11 Je! sisi sote hatukuwa mashahidi wenye kujionea kwa macho yetu wenyewe ile “ishara . . . ya umalizio wa mfumo wa mambo”? Je! sisi wenyewe hatukuona vile vita vikubwa, upungufu mwingi wa chakula, magonjwa ya kipuku, matetemeko ya ardhi na ‘maono mengine ya kutia hofu ambayo Yesu alitabiri? Je! sisi hatukujionea mateso ya Wakristo, na kushiriki katika kuzihubiri “habari njema hizi za ufalme . . . katika dunia yote inayokaliwa na watu kwa ushuhuda kwa mataifa yote”? Kwa kweli wengi wetu tumejionea hayo! (Mathayo 24:3-14, NW; Luka 21:10-12) Lakini namna gani maneno ya Yesu, kwenye Mathayo 24:15, 16, NW, juu ya kile “kitu chenye kuchukiza chenye kuharibu”?
Utimizo wa Duniani Pote
12. “Dhiki kubwa” itatofautiana namna gani na uharibifu wa Yerusalemu?
12 Utimizo wa karne ya kwanza wa unabii huu unaweka kielelezo kwa jambo tunaloweza kutazamia leo. Lakini kuna mambo fulani madogo-madogo yasiyopatana kwa ulinganifu kabisa. Kwa mfano, kwenye mistari 21 na 22 Yesu anasema: “Wakati huo kutakuwapo dhiki kubwa, ambayo haijatokea namna yake tangu mwanzo wa ulimwengu hata sasa, wala haitakuwapo kamwe. Na kama siku hizo zisingalifupizwa, asingeokoka mtu ye yote [au, mwili wo wote, NW]; lakini kwa ajili ya wateule zitafupizwa siku hizo.” Hiyo “dhiki kubwa” yenye kufikia upeo haitapata Yerusalemu tu wala mji wo wote mmoja mwingine. Hayo yatakuwa ndiyo maafa makubwa zaidi ambayo yamepata kupiga dunia yetu, nayo yatakuwa ya duniani pote.—Yeremia 25:30-33; Mathayo 24:30.
13. Tofauti na “mwili” uliookoka uharibifu wa Yerusalemu, ni “mwili” gani utakaookolewa uipite “dhiki kubwa”?
13 Tena, “mwili” utakaookoka hautakuwa wa Wayahudi wachache wenye kuasi imani, wenye kukusudiwa kupelekwa utumwani, kama ilivyokuwa kwenye uharibifu wa Yerusalemu wa kidunia. Bali, utakuwa “mwili” wa “wateule” (wachaguliwa), wale wanaowakilisha duniani ule “Yerusalemu wa mbinguni,” pamoja na “mwili” wa wenzao wa lile “kundi kubwa” kutoka mataifa yote, ambao juu yao Ufunuo 7:14 unasema hivi: “Hao ndio wanatoka katika dhiki ile iliyo kuu, nao wamefua mavazi yao, na kuyafanya meupe katika damu ya Mwana-Kondoo.” Basi, tutaielewaje Mathayo 24:15, 16 katika utimizo wake wa kisasa?
“Msomaji na Atumie Ufahamu”
14, 15. Ni nini mengine ya mambo ambayo ‘msomaji anaweza kufahamu’ kwa kuchunguza Danieli sura ya 7 na 8?
14 Hapa Yesu anamtaja “Danieli nabii,” kisha anaongezea kusema: “Msomaji na atumie ufahamu.” “Katika mwaka wa kwanza wa Belshaza, mfalme wa Babeli” ndipo Danieli alipopewa njozi ya Mzee wa Siku, Yehova Mungu, na ya kuhukumu kwake mataifa ya kilimwengu kupitia ufalme wa Kimasihi. Jambo hilo lingetukia ‘majira yakiwadia watakatifu waumiliki ufalme.’—Danieli 7:1, 9-14, 21, 22, 27.
15 Danieli aliona njozi zaidi katika mwaka wa tatu wa uufalme wa Belshaza. Hapa, katika Danieli 8:3-9, nabii anatumia usemi wa mfano katika kusimulia mfuatano wa ‘wanyama-mwitu’ na “pembe” zenye nguvu nyingi zinazoota kutokana na vichwa vya hao ‘wanyama.’ Danieli 8:20-25 inatusaidia kutambua wanyama hao kuwa ni mamlaka za ulimwengu za miaka 2,500 iliyopita, kuanza na Mwungano wa Wamedi na Waajemi, kisha Ugiriki, Rumi na mwishowe Milki ya Uingereza ikiwa kama ‘pembe ndogo iliyokua sana’ ikawa hodari kwa uwezo. Baadaye jamhuri ya Amerika ilikuja kushirikiana na milki hiyo. Kwa njia hiyo ikasimamishwa mamlaka ya ulimwengu yenye sehemu mbili.
16. (a) ’Majira yaliyowadia’ ni majira gani, na ni jambo gani lililotukia kuhusu “watakatifu”? (b) Kwa sababu gani matoleo ya Juni 1938 ya Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) yalikuwa ya maana kwa watu wa Mungu?
16 Mwaka wa 1918 WK ‘majira barabara yaliwadia’ “watakatifu” waupokee ufalme. Tangu mwaka wa 1919 “watakatifu” waliokuwa wangali wamebaki duniani walipangwa kwa namna ya tengenezo ili watoe tangazo kuu la duniani pote juu ya ufalme uliosimamishwa wa Masihi. (Mathayo 24:14) Baada ya muda mfupi wakajulikana ulimwenguni pote kuwa “Mashahidi wa Yehova” na “kundi kubwa” la wafanya kazi wenzao likaanza kujiunga nao. (Isaya 43:10, 12; Ufunuo 7:9, NW) Walakini, wakati wa miaka ya 1930 mawingu meusi ya mateso yalikusanyika pamoja. Yehova aliwaimarisha watu wake wakutane na tisho hilo kwa kuwapanga upya kitengenezo kwa njia ya kitheokrasi. Matoleo ya Mnara wa Mlinzi ya Juni 1 na 15, 1938 (Kiingereza), yalikuwa na makala za kujifunza juu ya “Tengenezo.” Ziliwajulisha watu wa Mungu umbo la kitheokrasi ambalo lingekuwa msingi wa utendaji wao wakati wa vita ya ulimwengu ya pili.—Isaya 60:17.
17. Sasa Danieli 8:10, 11 ilitimizwa kuelekea nani?
17 Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili ndipo Danieli 8:10, 11 ilipotimizwa. Ile “pembe ndogo” ilimkaidi (ikampinga) Yehova Mungu, ‘Mkuu wa jeshi.’ Na ni “jeshi” gani hilo? Je! ni jeshi la wenye kufuata sana madhehebu nyingi sana za kidini za Jumuiya ya Wakristo? Hapana. Madhehebu hizo ‘hazichukiwi,’ kwa maana zinajifanya sehemu ya ulimwengu wa Shetani. (Mathayo 24:9; Yohana 15:18-20) Hapa Danieli anamaanisha jeshi dogo zaidi, linalolinganika na kikosi cha pigano cha Gideoni kilichokuwa kidogo sana kikilinganishwa na makundi ya askari wa Midiani. (Waamuzi 7:8, 12) Mabaki walio duniani wa lile “jeshi” la “watakatifu” 144,000 ndio jeshi linalotajwa hapa. Ni hao watakaotawala pamoja na Mwana-Kondoo, Kristo Yesu, juu ya Mlima Sayuni wa “Yerusalemu wa mbinguni.”—Ufunuo 14:1-5.
Kuchukua Msimamo “Mahali Patakatifu”
18. (a) Maandiko yanaonyesha “mahali patakatifu’’ pako wapi? (b) Kulingana na Danieli 8:12, ni nini kinachotukia mahali hapo?
18 Leo hawa waliobaki wanachukua msimamo “mahali patakatifu,” na wanawakilisha duniani ule “Yerusalemu wa mbinguni” na mpango wake wa hekalu. Danieli anapaeleza (katika mstari wa 11) kuwa “mahali pa patakatifu pake [Yehova]” hapa kwenye “kibago (au kiti) cha kuwekea miguu” yake, hapa duniani. (Isaya 66:1, NW) Yeye anasema: “Ikamwondolea [Yehova] sadaka ya kuteketezwa ya daima, na mahali pa patakatifu pake pakaangushwa chini. Na jeshi likatolewa kwake pamoja na sadaka ya kuteketezwa ya daima, kwa sababu ya makosa; nayo ikaiangusha kweli hata chini; ikatenda ilivyopenda, na kufanikiwa.” (Danieli 8:11, 12) Hayo yalitimizwa namna gani?
19. (a) Tunaelewa nini hapa kutokana na ‘makosa ya ile pembe ndogo’? (b) Pembe hiyo iliendelea namna gani ‘kuiangusha kweli hata chini’?
19 Haya basi, ni jambo gani lililowapata wanafunzi wa Biblia waaminifu—Mashahidi wa Yehova—wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili? Ni mateso makali sana! Mateso hayo yakawa ni “makosa,” jitihada ya kuifanya ukiwa jamii ya Mungu ya “patakatifu,” na kwa njia hiyo kumnyang’anya Yehova ile “sadaka ya kuteketezwa ya daima,” ya kuabudu wazi-wazi kila siku. Jambo hilo lilianza katika nchi za Unazi na Ufasisti (zenye kufuata maongozi ya kiongozi mmoja mwenye mamlaka kamili kabisa yenye ukatili). Lakini baada ya muda mfupi ‘kweli ikawa ikiangushwa hata chini’ katika milki ile kubwa sana ya hiyo ‘pembe ndogo iliyokua sana’ katika nguvu zake. Lile “jeshi” la watangazaji wa Ufalme na kazi yao ya kuhubiri kweli ya ufalme likapigwa marufuku katika karibu sehemu zote za Jumuiya ya Madola ya Uingereza. Wakati mataifa hayo yalipoandikisha majina ya watu wao katika majeshi yao, walikataa kuwapa Mashahidi wa Yehova ruhusa ya kutokuandikishwa, maana hawakukubali wao walikuwa wahudumu (maminista wa kidini); hawakuonyesha heshima yo yote juu ya kuwekwa kwa Mashahidi kwa njia ya kitheokrasi wawe wahudumu wa Mungu. Katika United States (Amerika) watumishi waaminifu wa Yehova walitendwa jeuri nyingi na makundi ya watu wenye ghasia na kufanywa mambo mengine ya kuwavunjia heshima.
20. (a) Danieli 8:14 inatupa uhakikisho gani? (b) Pale ‘mahali patakatifu palitokea kwa ushindi’ kwa njia gani? (c) Wakati Vita ya Ulimwengu ya Pili ilipokuwa ikikaribia kumalizika kulikuwa na matukio gani katika tengenezo la Yehova?
20 Walakini, kulingana na Danieli 8:13, 14, baada ya kipindi cha ‘siku elfu mbili na mia tatu’ (miaka sita, miezi minne na siku 20), “patakatifu” pangerudishwa tena “ndani ya hali yake inayofaa,” NW, ‘pangejitokeza kwa njia ya ushindi’ (New English Bible). Kwa kweli, Mashahidi wa Yehova wameteswa vikali sana kwa sababu ya kudumu ‘wakitii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’ (Matendo 5:29, NW) Lakini wakati wa miezi ya mwisho-mwisho ya Vita ya Ulimwengu ya Pili walikaza upya nia yao ya kutukuza utawala wa Yehova na kuushika sana ndani ya tengenezo lao. Kwa kusudi hilo, kupangwa upya kwa kazi na umbo la usimamizi wa Mashahidi wa Yehova kulianzwa mwaka wa 1944. Kichwa cha Mnara wa Mlinzi wa Oktoba 15, 1944 (gazeti la Kiingereza) kilikuwa “Kapangwa Kitengenezo kwa Kazi ya Mwisho.” Makala hiyo na nyingine zenye kukazia utumishi katika kipindi icho hicho zilionyesha kwamba “mahali patakatifu” palikuwa pamerudia ‘hali yake inayofaa’ kwa maoni ya Yehova.a
21. Kufikia hapo, ufalme ulikuwa umefaulu kwa njia gani?
21 Jaribio la adui lenye madhara la kutaka kupafanya ukiwa na kupaharibu “mahali patakatifu” lilikuwa limeshindwa kabisa. Wale “watakatifu” waliokuwa wamebaki duniani, pamoja na wenzi wao wa lile “kundi kubwa,” walikuwa wamejipatia ushindi. Ule ufalme wa Aliye Mkuu Kupita Wote, Yehova, na wa Kristo wake, ulikuwa umefaulu! Sasa ingekuwaje, kulingana na neno la kiunabii la Yehova? Tutaona.
[Maelezo ya Chini]
a Ili upate habari zenye maelezo marefu juu ya Danieli sura ya 7 na 8 angalia Mnara wa Mlinzi, Aprili 1, 1972, kurasa 149-165.
WEWE ‘UNAFAHAMU’ NINI KUTOKANA NA—
Danieli 7:22: “majira yakawadia”?
Danieli 7:27: “watakatifu,” “ufalme”?
Danieli 8:9: “pembe ndogo”?
Danieli 8:10: “jeshi la mbinguni”?
Danieli 8:11: ‘Mkuu wa jeshi’?
Danieli 8:12: “Ikaiangusha kweli hata chini”?
Danieli 8:14, NEB: “pale Mahali Patakatifu patatokeza kwa ushindi”?
[Sanduku katika ukurasa wa 12]
Mwaka wa 1965 Chansela Konrad Adenauer wa Ujeremani alitangaza hivi: “Mawazo na picha zinakuja kwenye akili yangu . . . mawazo ya kabla ya mwaka wa 1914 wakati kulipokuwa na amani halisi, utulivu na usalama juu ya dunia hii—wakati ambao hatukujua hofu. . . . Usalama na utulivu umetoweka katika maisha za wanadamu tangu mwaka wa 1914.”
[Sanduku katika ukurasa wa 13]
Mwaka wa 1980 aliyekuwa waziri mkuu wa Uingereza, Harold Macmillan alisema: “Kila kitu kilikuwa kikizidi tu kuwa kizuri zaidi. Huo ndio ulimwengu nilimozaliwa. . . . Kwa ghafula, bila kutazamiwa, asubuhi moja katika mwaka wa 1914 mambo yote hayo yalikoma.”