Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 4/15 kur. 3-5
  • “Mahali Patakatifu Paharibiwa—Maana ya Jambo Hilo Leo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • “Mahali Patakatifu Paharibiwa—Maana ya Jambo Hilo Leo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • ‘Kimbieni Kwenda Kwenye Milima’
  • Utimizo wa Karne ya Kwanza
  • Yerusalemu Waachwa Ukiwa
  • “Mwacheni Msomaji Atumie Ufahamu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Ule Ufalme na “Mahali Patakatifu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Je, Utaokolewa Mungu Atendapo?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Kukimbilia Usalama Kabla ya “Dhiki Kubwa”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 4/15 kur. 3-5

“Mahali Patakatifu Paharibiwa​—Maana ya Jambo Hilo Leo

“MAJENGO YA MAKANISA NA WAHEKALU KATIKA NCHI YOTE YAHARIBIWA KATIKA FUJO ZA WENYE KUPINGA DINI!”

Loo! watu wengi wangeshtuka kama nini magazeti au radio zikitangaza siku kwamba jambo hilo limetokea! Hata hilo si jambo linaloweza kusemwa labda litatokea; litatokea bila kuepukika!

Inawezaje kuwa hivyo? Ni kwa sababu unabii wa Biblia unaonyesha waziwazi kwamba hivyo ndivyo itakavyotukia karibu sana katika nchi moja baada ya nyingine. Kwa mfano, unabii ulio katika sura ya 24 unataja kuachwa kwa mahali “patakatifu.” Ingawa lilitimizwa katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu, lina utimizo mkubwa zaidi katika siku zetu.

Kwanza unabii huo ulitolewa kuhusu Yerusalemu na hekalu lake lenye uzuri mwingi ajabu, lililotumiwa na Wayahudi ibada yao. Safari moja Yesu Kristo alipokuwa akisema na wanafunzi wake alinena hivi juu ya majengo ya hekalu:“Hamyaoni haya yote? Amin, nawaambieni, Halitasalia hapa jiwe juu ya jiwe ambalo halitabomoshwa.”​—Mathayo 24:2.

Kwa sababu gani Mungu angeleta hukumu kali hivyo juu ya hekalu hilo ‘takatifu’ la karne ya kwanza pamoja na mfumo wa kidini uliowakilishwa na hekalu hilo? Ni kwa sababu Wayahudi walikuwa wamegeuka wakawa waasi imani. Walikuwa wameacha sheria za Mungu walizopewa kupitia Musa. Isitoshe. Walikuwa wamewakataa wajumbe wa Mungu waliotumwa kuwaonya, hata wakamwaga damu yao. Ndiyo sababu Yesu alisema: “Ee Yerusalemu, Yerusalemu, uwauaye manabii, na kuwapiga kwa mawe wale waliotumwa kwako! . . . Angalieni, nyumba yenu mmeachiwa hali ya ukiwa.”​—Mathayo 23:37, 38.

‘Kimbieni Kwenda Kwenye Milima’

Yesu alielekeza maneno haya kwa wale waliomwabudu Mungu kwa unyofu wa moyo: “Kwa hiyo, mwonapo lile chukizo kuu lenye kufanyiza uharibifu, kama lilivyosemwa kupitia kwa Danieli nabii, likisimama katika mahali patakatifu, (Msomaji na atumie ufahamu,) basi walio Yudea na waanze kukimbia kwenye milima. Mtu aliye juu ya paa ya nyumba asije chini kuchukua bidhaa kutoka nyumba yake; na mtu aliye katika shamba asirudi kwenye nyumba kuokota vazi lake la nje. Ole wao wanawake wenye mimba na wale wanaonyonyesha kitoto katika siku hizo!”​—Mathayo 24:15-19, NW.

Kwa sababu gani Yesu akawahimiza wafuasi wake wafanye haraka hivyo katika ‘kukimbia kwenda kwenye milima’? Yeye alisema: “Kwa maana wakati huo kutakuwako dhiki kuu ya namna ambayo haijatukia tangu mwanzo wa ulimwengu mpaka sasa, la, wala haitatukia tena. Kwa kweli, kama siku hizo zisingekatwa ziwe fupi, hakuna mwili ambao ungeokoka; lakini kwa ajili ya waliochaguliwa siku hizo zitakatwa ziwe fupi.”​—Mathayo 24:21, 22, NW.

Lakini Yesu alikuwa na maana gani hasa wakati alipolitaja “lile chukizo kuu lenye kufanyiza uharibifu . . . likisimama katika mahali patakatifu”? Alikuwa na maana gani kwa kusema “dhiki kuu,” na “mwili” ambao ungeokolewa? Kwa sababu gani ni “kwa ajili ya waliochaguliwa” dhiki hiyo ‘ingekatwa iwe fupi’?

Utimizo wa Karne ya Kwanza

Ni utimizo gani hasa wa unabii huu uliotokea katika karne ya kwanza? Kwanza kabisa, liangalie onyo la haraka la kukimbilia kwenye milima “mwonapo lile chukizo kuu lenye kufanyiza uharibifu . . . likisimama katika mahali patakatifu.”

Kitu hicho chenye kuchukiza chenye kuharibu kilikuwa nini? Historia inatueleza ni kitu gani hasa kilicholeta uharibifu wa Yerusalemu: Kilikuwa ni majeshi ya Milki ya Rumi. Wakati majeshi hayo yalipojitokeza mara ya kwanza kwa nguvu kwa kuzingira Yerusalemu, hicho kilikuwa ndicho kiishara kwa mtu ‘mwenye ufahamu’ aondoke katika eneo hilo. Na ndivyo ilivyokuwa mwaka wa 66 WK. Wakati huo, majeshi ya Kirumi yakiwa chini ya Jemadari Sesho Gallo yaliuzingira Yerusalemu na hata yakashambulia ukuta wa hekalu, yakaufukua yakitaka kuubomoa. Yangaliweza kwa urahisi kuuteka mji mzima.

Basi, hayo yalikuwa ni majeshi ya Kirumi yakiwa yamesimama katika ule “mji mtakatifu.” (Linganisha Mathayo 4:5; 27:53.) Hata Wayahudi wenye kuasi imani waliufikiria Yerusalemu na mazingira yake kuwa “patakatifu.” Kuwapo kwa majeshi hayo katika hapo “mahali patakatifu” kulikuwa jambo la kuchukiza sana Wayahudi.

Lakini, kwa sababu fulani isiyoeleweka vizuri na wanahistoria, ndipo Jemadari Gallo alipoondosha majeshi yake wakarudi walikotoka. Hicho ndicho kiishara ambacho Yesu alikuwa ametabiri. Wakati ulikuwa umewadia wafuasi wake, “waliochaguliwa,” waanze kukimbia. Kwa kutambua uharaka wa nyakati, walifanya upesi wakaondoka Yerusalemu na Yudea yote, kama Yesu alivyokuwa ameelekeza. Mwanahistoria Eusebio anataja kwamba walikimbia wakavuka Mto Yordani na kuufikia ujirani wa Pella katika mkoa wa Gileadi wenye milima-milima.

Yerusalemu Waachwa Ukiwa

Miaka michache baadaye, katika mwaka wa 70 WK, majeshi ya Kirumi yakiwa chini ya Jemadari Tito yalirudi yakaingia Yudea kisha yakauzunguka Yerusalemu. Lakini kufikia wakati huo “waliochaguliwa” wote, yaani, Wakristo, walikuwa wamekwisha kupaondoka “mahali patakatifu.” Basi, Warumi walipouzingira Yerusalemu wakati huo, hakukuwa tena na nafasi ya mtu awaye yote kukimbia akapate usalama.​—Luka 19:43, 44.

Baada ya mazingiwa mafupi ya miezi minne na siku 25, majeshi ya Rumi yaliubomoa mji kabisa na hekalu. Mwana historia Yosefo, shahidi aliyejionea tukio hilo kwa macho yake mwenyewe, anasema hesabu ya waliouawa ni 1,100,000 na wenye kutekwa wakawa 97,000. Hesabu hizo zilikuwa kubwa kwa sababu Wayahudi wasio waaminifu hawakutii onyo la Yesu la kukimbia. Walitenda kinyume. Wakati wa sherehe ya kidini walimiminika wakiingia Yerusalemu kisha wote wakanaswa mtegoni wakati Warumi walipouzunguka mji kwa ghafula.

Uhakika wa kwamba Wakristo “waliochaguliwa” hawakuwa tena katika Yerusalemu ulimaanisha kwamba Mungu asingepaswa kuhangaikia usalama wao. Wao walikuwa wamekwisha kukimbia. Basi Mungu angeweza kuruhusu Warumi waingie Yerusalemu na kufikiliza hukumu Yake mbio-mbio juu ya mji huo. Kwa hiyo kwa ajili ya kuwa Wakristo waliochaguliwa walikuwa wamekwisha kutoka Yerusalemu, siku hizo za dhiki zilifikia kikomo upesi zaidi, zikawa ‘zimekatwa zikawa fupi.’ Jambo hilo liliruhusu “mwili” fulani, yaani wale 97,000, uokoke.

Hiyo “dhiki kuu” katika mwaka wa 70 WK ndiyo msiba mbaya kabisa uliopata kuujilia Yerusalemu. Iliukomesha ndi! ule mji uliojengwa na Wayahudi, ukakomesha hekalu lake na mfumo wa kidini uliolitegemea.

Lakini historia hiyo ya kale inahusianaje na sisi tunaoishi katika karne hii ya 20? Tunahusika sana.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki