Wakati Ni Nini?
NI SAA ngapi? Ni mara ngapi wewe umeuliza hivyo? Labda unaposoma ukurasa huu unajisikia ukitaka kuangalia saa yako ya mkononi au kutazama ya ukutani. Kwa sababu gani? Kwa sababu mwanadamu anajali sana kupita kwa wakati, kama kwamba hawezi kuishi bila kufikiria wakati kwa njia fulani.—Zaburi 90:12; Mhubiri 3:11.
Kila siku walio wengi kati yetu wanaongozwa na saa yenye mikono. Tunalala, tunaamka, tunakula, tunafanya kazi na kufurahisha watu kwa starehe mbalimbali wakati tunapoongozwa na mikono ya saa, wala si kila mara tunapofanya hivyo kwa kuongozwa na hisi zetu tu. Na ajabu ni kwamba, wakati tunapotazama saa, huenda tukakosa hamu ya kujua ni saa ngapi lakini tutake zaidi kujua ni wakati gani tumebaki nao wa kufanya jambo hili au lile.
Vitu vyote vilivyo hai vinaelekea kuwa vina saa fulani ndani ya miili yavyo. Kwa mfano, mimea mingi na wanyama wengi wana vichocheaji vyenye kupima wakati barabara wa kuchanua (kama ni mimea) na wa kuhamia eneo jingine (kama ni wanyama). Bila sisi kujua, kemikali zilizo ndani yetu zinaachiliwa zisafiri mwilini kisha utendaji mbalimbali wa mwili unaendeshwa na saa za miili yetu zenye kuchochea utendaji kama kwamba zinatokeza-tokeza milio ya nukta za saa. Je! jambo hilo halitukumbushi ule usemi wa mithali ya kwamba, “Kwa kila jambo kuna majira yake”?—Mhubiri 3:1.
Kama ungeombwa utoe maelezo ya kuonyesha wakati ni nini, wewe ungesemaje? Watu wengine wangesema kwamba wakati ni njia fulani ya kufikiria mambo au ni umbali ulio kati ya tukio moja na jingine. Basi, kama hakungekuwa kamwe na matukio, hakungekuwa na wakati. Hata hivyo kueleza maana ya wakati ni jambo lenye kutatiza sana kama vile lilivyo tatizo kueleza ukubwa wa eneo lote la anga.
Mambo ya Hakika Juu ya Wakati
Tunajua namna wakati unavyosonga—unasonga ukielekea mbele. Unaelekea upande mmoja tu. Mambo ya zamani yanakuwa yamekwisha kupita, yasirudiwe tena kamwe. Makosa yetu yanakuwa yameacha alama zisizoweza kufutwa kwa sababu wakati haurudi nyuma. Ndivyo na matendo yetu mema. Sikuzote tunaishi katika wakati uliopo kisha tunasonga mbele kuelekea wakati ujao, lakini hatuwezi kamwe kurudisha wakati nyuma ili tufute makosa yetu yaliyokwisha kufanyika. Kwa hiyo, ni jambo bora sana tufanye maamuzi mema wakati wa sasa ili tuweze kufurahia wakati ujao ulio bora badala ya kuwa na wakati wenye majuto siku zinazokuja.—Mithali 3:1, 2.
Tunajua namna ya kupima wakati. Zamani za kale mwanadamu alitosheka kwa kuliacha jua, mwezi na nyota zimpimie wakati uliopita. Kwa watu wengi, wakati jua lilipochomoza asubuhi, huo ulikuwa wakati wa kazi, na wakati jua liliposhuka jioni, huo ulikuwa wakati wa kwenda kulala.
Shughuli za watu zilipozidi kuwa ngumu na za haraka-haraka, mwanadamu alijishughulisha zaidi kupima wakati. Basi kukawa na mavumbuzi yenye akili nyingi za mwanadamu ya kupima wakati, kama vile saa-ya-duara jua (chombo cha mviringo chenye kijiti ambacho kivuli chake chenye kuletwa na jua kilisaidia kujua wakati), kuchoma mishumaa, kutumia shisha (chupa yenye mchanga ya kuhesabia saa). Walitumia pia saa ya kutiwa majira na, leo, wanatumia saa ya atomi (yenye kwenda kwa kutegemea mivumo ya umeme). Saa zote hizo zinakuwa vipimo vya kupimia kitu fulani kirefu kisichoonekana kinachoitwa wakati. Kwa sababu ya mwanadamu kushughulisha akili zake na kufanya mambo kwa wakati barabara, watu wengi zaidi wameacha kufikiria sana utimizaji wa madaraka yao wakawa wenye kujali wakati zaidi.
Lakini kwa sababu gani nyakati nyingine wakati unaelekea kupita mbio na nyakati nyingine unajikokota tu? Ni kwa sababu wakati unaweza kupimwa kwa matukio. Kipindi cha kutokuwa na utendaji kinaonekana kuwa kirefu kuliko kipindi cha utendaji, na kadiri tunavyozidi kupendezwa na tunalofanya ndivyo wakati unavyoelekea kupita mbio zaidi. Tukijisikia tumechoshwa na kazi fulani kwa sababu ya kutopendezwa nayo, wakati unaonekana kuwa mrefu mno. Je! wewe umepata kuketi na kumngoja mtu fulani? Saa moja yenye kutumiwa kwa njia hiyo inaelekea kuwa na urefu usiofikia mwisho linakuwa ni tukio moja tu. Lakini ingekuwaje kama katika saa iyo hiyo moja ungefanya kazi nyingi sana zenye mafanikio, kama vile kutayarisha chakula kwa ajili ya wageni wasiokuwa wametazamiwa (kumenya viazi, kuoka, kupika Mboga, kuandaa meza, kupangusa-pangusa vumbi upesi katika nyumba na kubadili mavazi yako ya jikoni ili uketi ukiwa na sura nzuri pamoja na wageni hao)? Hapo saa hiyo ingeonekana ikienda mbio ajabu, kwa kuwa imekuwa na matukio mengi sana ya kuijaza.
Kujua kwetu matukio ya zamani, ya sasa na ya wakati ujao kunatutofautisha na wanyama. Wanyama wanaendelea kuishi maisha ya wakati uliopo daima, lakini ingawa wanadamu wanaishi maisha ya sasa, wao wanaweza kufikiria matukio ya zamani ili wajue mambo wanayopaswa kutazamia wakati ujao. Na kadiri miaka inavyoendelea kupita nasi tunazidi kuwa na maono mengi sana ya maisha, ndivyo wakati unavyoonekana kutushinda mbio. Basi, je! tunapozidi kuwa wazee na kuhuzunikia zaidi jambo la kwamba sisi ni watu wanaoweza kufa, haitupasi kufikiria maisha kwa njia nzuri zaidi na kuangalia tunayaishi namna gani?—Zaburi 90:10.
Maelezo ya Mshairi Henry Austin Dobson juu ya wakati ni ya kweli sana:
“Ati wakati wapita kasi?
Haupiti! Wapitao ndisi.”
Lakini ni lazima iwe hivyo sikuzote’ Haitakuwa hivyo ikiwa tunajua kweli kweli ni “wakati” gani sasa (au ni saa ngapi).