Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w84 5/15 kur. 20-23
  • Mrudishie Yehova Moyo Wako

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mrudishie Yehova Moyo Wako
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Moyo Wenye Kutanga-tanga
  • Moyo—“Hakuna Kitu Kinginecho Chenye Udanganyifu Mwingi Hivyo”
  • Moyo Wako Unaweza Kubadilishwa
  • Jihadhari na Washirika Wako
  • ‘Mungu Ni Mkuu Kuliko Moyo Wako’
  • Yehova Atatoa Msaada
  • Jipatie Moyo Unaompendeza Yehova
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Kumwendea Daktari wa Moyo Aliye Hodari Kupita Wote Nyakati Zetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1978
  • Kuazimia Kumtumikia Yehova kwa Moyo Kamili
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1986
  • Linda Moyo Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
w84 5/15 kur. 20-23

Mrudishie Yehova Moyo Wako

Je! wewe ulilelewa na wazazi walio Mashahidi wa Yehova? Hata hivyo, sasa umepunguza bidii yako katika njia ya ule ukweli? Ikiwa ndivyo, habari inayofuata itakufaa wewe kwa njia ya pekee.

MAWAZO mengi ya moyoni yenye kupingana yanasukasuka moyo wa kijana. Kwa mfano, huenda ukataka kuwa na hali ya kujitegemea. Unaelekeana nyakati zote na mitindo ya maisha inayoonekana kuwa ya kusisimua ambayo huenda ikapingana na mambo uliyofundishwa. Nyakati nyingine watu hawajali mambo bora waliyofundishwa utotoni. Labda jambo hilo limekupata wewe, hata kama wazazi wako ni watumishi wa Yehova Mungu.

Hapa na pale, vijana wanapeperuka na kuliacha kundi la Kikristo. Ikiwa ndivyo wewe umefanya, bila shaka unakumbuka mengine ya mambo uliyojifunza juu ya Yehova. Huenda ikawa wakati fulani ulikuwa ukijisikia umemkaribia Mungu na ukawa ukimpelekea sala kwa ukawaida. Bila shaka, Yehova alikujali wewe sawasawa na vile alivyowajali watu wake wa kale, Waisraeli. Akililinganisha taifa hilo na mtoto mdogo, Yehova alisema hivi: “Nalimfundisha Efraimu [yaani, Waisraeli] kwenda kwa miguu; naliwachukua mikononi mwangu... Naliwavuta kwa kamba za kibinadamu, kwa mafungo ya upendo.”​—Hosea 11:3, 4.

Ni jambo lenye kugusa moyo kama nini! Mtoto mdogo sana mwenye kutikisika-tikisika akisaidiwa atembee kwa kuongozwa na kamba zilizoshikwa na mzazi mwenye upendo! Kwa kuzishikilia, mtoto huyo angeweza kupata tegemezo na kuepuka anguko. Sasa, je! hangaikio ambalo Yehova alikuonyesha wewe halikuwa na wororo uo huo? Kwa uhakika upendo wake ulionekana wazi katika uangalizi uliopokea ama kutoka kwa wazazi wenye kumcha Mungu ama kutoka kwa wengine kwenye Jumba la Ufalme. Je! si uangalizi huo unaweza kufananishwa na kuongozwa kwako kwa “mafungo ya upendo”? Ni wazi kwamba wazazi wako na wazee wa kundi walitaka sana kukusaidia uepuke kujiumiza kimoyo, kimwili na kiroho. Walitaka wewe ubaki katika njia ya ule ukweli.​—Linganisha 3 Yohana 2-4.

Sasa huenda hayo yote yakaelekea kuwa yamekwisha kumalizika na kupita. Unapotazama nyuma, huenda ukafikiria sababu kadha zilizokufanya ukapeperuka na kuiacha njia ya ule kweli.

Moyo Wenye Kutanga-tanga

Kwa sababu gani wengi sana kati ya Waisraeli wa kale walipeperuka wakaiacha ibada ya kweli? Ni kwa sababu “mioyo yao haikuwa thabiti” kwa Yehova. (Zaburi 78:37) Mambo mengine yanayopendwa kwa shauku yanaweza kuusonga sana upendo kwa Mungu hata usionyeshwe vizuri. Kulingana na Yesu Kristo, mahangaikio ya ulimwengu huu, uwezo wa mali na “anasa za maisha haya” ni mambo yanayoweza kulisonga neno la Mungu ambalo wakati mmoja lilikuwa limepandwa moyoni.​—Luka 8:14; Marko 4:19.

“Anasa za maisha haya” zinafanywa zionekane zenye kuvutia sana na wanashule wenzako, na pia na vyombo vya utangazaji wa habari na vya kufurahisha watu. Kwa mfano, kijana mmoja wa kike, ambaye wazazi wake walikuwa wamemfundisha Neno la Mungu tangu utoto mchanga, alipeperuka akaiacha njia ya ule ukweli alipofikia umri wa miaka kumi na tisa. Yeye alikiri ya kwamba, “Nilitaka kuonja nione maisha yako namna gani na kufanya mengine ya mambo ambayo vijana wale wengine walikuwa wameyaonyesha kuwa yenye kufurahika sana. Kwa hiyo nikahama na kwenda kukaa katika chumba changu mwenyewe na kuanza kufanya matembezi na wavulana na kwenda kwenye karamu ili tu nione msisimuko. Muda mwingi haukupita kabla sijaacha kufuata maadili ya Biblia.”

Bila shaka, si wote wanaopeperuka na kuuacha ule ukweli wanaohusika katika makosa. Wengine ni kwamba tu wanaacha kupendezwa na kumwabudu Yehova. Huenda ikawa hakuna hata siku moja walipouthamini ule ukweli kwa nafsi yao wenyewe. Labda jambo lililoshiriki katika kuwafanya wasiuchukue ukweli kwa uzito ni kuwekewa mfano mbaya na wazazi au kutokujali kwa wazazi wenyewe. Sasa huenda mambo kama matatizo ya kijamaa, kujitafutia riziki, au tamaa kubwa ya kutaka kufanikiwa katika kazi ya kibinafsi ya maisha huenda yakajaza mioyo yao.

Lakini je! unaweza kuwa mwenye furaha ikiwa humjali zaidi Mfanyi wako kuliko unavyojali mambo mengine? Je! utapata furaha ya kweli kwa kufuata tamaa za moyo wako?

Moyo—“Hakuna Kitu Kinginecho Chenye Udanganyifu Mwingi Hivyo”

“Moyo ni mudanganyifu kuliko vyote, una ugonjwa wa hatari; nani anayeweza kuujua?” (Yeremia 17:9, ZSB) Ndiyo, moyo wako una uwezo wa kukupoteza wewe​—hata upatwe na madhara wewe mwenyewe. Ndivyo ilivyotukia kwa yule kijana mwanamke aliyetangulia kutajwa. Yeye alikiri hivi: “Mara ya kwanza nilipokuwa nikifanya lo lote nililotaka kufanya, lilikuwa jambo la kufurahisha. Lakini baada ya muda kidogo kupita, ingawa bado nilikuwa nikisisimuka kabisa, sikuelekea kuwa na furaha yo yote ya ndani. Jambo fulani lilielekea kuwa limekosekana. Furaha yangu ilikuwa ya kijuujuu tu. Nikawa mwenye huzuni nyingi.”

Wengi ambao wamepeperuka wamekiri pia kwamba walipata ‘furaha ya kijuujuu tu.’ Kwa sababu ya maumivu na utupu wa kindani uliotokana na kufuata moyo wao wenye upotovu, sasa wanajua kwamba “hakuna kitu kinginecho chenye udanganyifu mwingi hivyo.”​—Today’s English Version.

Wakati unapotazama maisha yako mwenyewe, je! unajisikia ukiwa na maoni ayo hayo? Je! mambo ambayo wakati mmoja uliyafikiria kuwa upendezi wa moyo wako yamekufanya ujisikie kweli kweli ya kwamba umetimiza jambo fulani? Je! mwendo wako wa maisha umekuletea amani ya akili na hali ya kujiheshimu?

Wakati unapokuwa hauko kwenye amani pamoja na nafsi yako mwenyewe, huwezi kuwa na furaha kikweli. Ikiwa moyo wako uko “katika maumivu,” hakuna kicheko kitakachouponya hata kiwe ni kingi namna gani. (Mithali 14:13, NW) Kwa mfano, kijana mwingine wa kike alipofika umri wa miaka kumi na minane aliviacha viwango vya Biblia alivyokuwa amefundishwa muda wote wa maisha yake. Hata hivyo, alipokuwa akifuatia “maisha ya kutokujali na ya kusisimua,” yeye anakumbuka kwamba: “Nilianza kufikiri juu ya wakati ujao. Ningepatwa na nini muda wa miaka mitano iliyokuwa ikija kama ningeendelea kufuata mwendo wangu? Nilishindwa kabisa kuendelea kujisadikisha nilikuwa mwenye furaha ati. Kwa kukosa tumaini lo lote nikajisikia kama msichana aliye mwenye huzuni zaidi ya wote katika ulimwengu!”

Kwa hiyo, basi, ikiwa wewe umeiacha njia ya ukweli, unaweza kupataje tena furaha ya kweli? Mtunga zaburi Daudi alitoa kielekezi wakati alipomwomba Mungu hivi: “Unipe mafundisho, Ee Yehova, juu ya njia yako. Mimi nitatembea katika ukweli wako. Unganisha moyo wangu uwe kitu kimoja ili kuogopa jina lako.” (Zaburi 86:11, NW) Daudi alijua kwamba moyo wenye kugawanyika katika shauku mbalimbali ulikuwa hatari kuu. Basi, ni lazima moyo wako urekebishwe ili nguvu zao zote ziweze kukazwa kwenye jambo moja​—“utumishi mtakatifu” kwa Yehova na kicho cha moyo wote kwa Mungu wetu. (Warumi 12:1, 2, NW) Lakini hali hiyo ya kutamanika ya moyoni inaweza kuletwaje?

Moyo Wako Unaweza Kubadilishwa

Kwanza kabisa, ni lazima wewe utambue kwamba moyo​—moyo wako​—unaweza kubadilishwa. Kwa habari ya watu wake wapotovu, Yehova alisema: “Mimi nitawapa moyo mmoja [wenye kuungana], na roho mpya nitatia ndani yao; na mimi kwa uhakika nitauondoa moyo wa jiwe kutoka mwili wao na kuwapa moyo wenye nyama, ili wao wapate kutembea katika maagizo yangu mwenyewe na kushika maamuzi ya hukumu yangu mwenyewe na kwa uhakika wayatimize; na wapate kweli kweli kuwa watu wangu na mimi mwenyewe nipate kuwa Mungu wao.” (Ezekieli 11:19, 20, NW) Lo! fadhili za upendo wa kimungu kama nini! Na ebu wazia​—mioyo isiyoitikia sawasawa na jiwe ikiwa myororo, yenye wepesi wa kuitikia, yenye nia ya kupokea mawazo ya kiroho.

Lakini, je! ni kupitia mwujiza fulani kwamba Yehova anatimiza badiliko hilo? Au, wewe unashiriki sehemu fulani katika kulitimiza? Ni lazima wewe utie jitihada ya kupanga katika moyo wako mambo unayokumbuka juu ya Yehova. (Mithali 16:1) Fikiria sana habari hii. Kisha ongeza maarifa juu ya kufikiri kwako. Ni wakati gani uliokuwa mara yako ya mwisho kuchukua Biblia au kitabu cha kusaidia kujifunza kinachotolewa na tengenezo la Yehova? Bila shaka una vingine vya vichapo hivyo nyumbani kwenu au unajua unakoweza kuvipata. Sababu gani usianze kuvisoma kwa moyo mweupe? Kutenda kupatana na maarifa sahihi ya Biblia kunaweza kubadili moyo wako na mwendo wako katika maisha.​—Mithali 2:10-14.

Katika kuisoma Biblia yenyewe, huenda ukaiona Zaburi 25 hasa kuwa yenye kufariji. Fikiria sana maombi yale yanayoelekezwa kwa Yehova, kama lile linalosema “usiyakumbuke makosa ya ujana wangu” na “unisamehe uovu wangu, maana ni mwingi.” Kisha fikiria namna lilivyo jambo la kufariji kujua kwamba “siri ya [ Yehova] iko kwao wamchao.”​—Zaburi 25:7, 11, 14.

Lakini, ni lazima kujifunza Biblia hivyo kuwe ni zaidi ya kujaza mambo akilini tu. Tunahitaji kuwa na nia ile ile ya mtunga zaburi, aliyesema hivi: “Katika moyo wangu mimi nimeweka kama hazina usemi wako [Yehova], ili kwamba mimi nisipate kutenda dhambi juu yako.” (Zaburi 119:11, NW) Unaweza ‘kuliweka kama hazina’ neno la Yehova kwa njia gani? Baada ya kuisoma Biblia na vichapo vinavyohusiana na Biblia vya “mtumwa mwaminifu mwenye akili,” jiulize mwenyewe hivi: Shauri hili ni lenye kuthaminika kwa kadiri gani hasa? Je! lingenisaidia mimi nimpendeze Yehova na kuepuka maumivu ya moyoni yasiyo na sababu? Naweza kulitumiaje? Je! shauri hili lenye mafaa halionyeshi kwamba Baba yangu wa kimbingu anajua jambo linalonifaa mimi zaidi ya mambo mengineyo yote?​—Mathayo 24:45-47.

Ukiingiza sheria ya Mungu ndani ya moyo wako, hatua zako ‘hazitatikisika-tikisika.’ (Zaburi 37:31, NW) Lakini, ili umrudishie Yehova moyo wako, kwa kawaida utahitaji kupata msaada wa upendo kutoka kwa shahidi aliyekomaa wa Yehova. Ndiyo, huenda ukahitaji mtu wa kuanza kukufundisha “kutoka mwanzo” yale ‘mambo ya msingi wa matamko matakatifu ya Mungu.’ (Waebrania 5:12, NW) Wazee wa kundi watafurahi kukusaidia. Sababu gani usiwafikie?

Jihadhari na Washirika Wako

Watu wanaweza vyepesi ‘kugeuza moyo wako’ uwe ama mwema ama mbaya. (Linganisha 1 Wafalme 11:3, 4.) Huenda ikawa mambo yaliyokufanya upeperuke na kuuacha ukweli ni mavutano ya tabia za upotovu na majisifu ya wenzi wako. Huenda watu wa namna hiyo wakasema hivi kwa mkazo: ‘Hakuna mtu anayeniambia mimi jambo la kufanya! Mbona ujiwekee vizuizi vikali namna hiyo?’ Lakini je! kweli wao wako huru? Namna gani nyingine za zile tabia zisizo za Kikristo ambazo huenda zikawa zimewafanya watumwa wazo? (Linganisha 2 Petro 2:18, 19.) Je! watu hao mmoja mmoja wanakusaidia wewe ufanye mambo yatakayoleta faida ya kudumu? Hapana, wanakuzuia wewe. Kwa hiyo jitenganishe na washirika wabaya hao uwe huru kisha utafute watu waliokomaa, wale “wenye hekima” machoni pa Mungu!—Mithali 13:20, UV; 1 Wakorintho 15:33, NW.

‘Mungu Ni Mkuu Kuliko Moyo Wako’

Kijana mmoja aliyekuwa amehusika katika tabia zisizo za Kikristo akiwa na umri wa miaka kumi na minane alisema hivi: “Sababu kubwa iliyofanya iwe vigumu sana kwangu kuurudia ukweli ni kwamba nilijisikia sistahili. Nilidhani kwamba mambo yote niliyokuwa nimefanya yalikuwa mabaya sana hivi kwamba Yehova hangenisamehe kamwe wala hangekubali nimrudie.” Ingawa moyo wa kijana huyo ulimlaumu, baadaye alipata kuona rehema ya Mungu. Katika hali hizo, maandiko kama 1 Yohana 3:19, 20 yanaweza kuwa yenye kufariji kama nini! Hapo tunasoma hivi: “Katika hili tutafahamu ya kwamba tu wa kweli, nasi tutaituliza mioyo yetu mbele zake, ikiwa mioyo yetu inatuhukumu; kwa maana Mungu ni mkuu kuliko mioyo yetu naye anajua yote.”

Ni kweli kwamba huenda mioyo yetu ikatulaumu. Hata hivyo Yehova anaona mambo mengine mengi, wala haoni dhambi zetu tu. Yeye anaona “siri za moyo.” (Zaburi 44:21) Ukuu wa maarifa yake unamwezesha yeye kusikia kwa huruma sala zetu za bidii za kuomba msamaha. Tukiungama dhambi zetu na kubadili mwendo wetu, Mungu ana nia ya kupenda kufuta kabisa hata dhambi nzito kwa kutegemea msingi wa dhabihu ya ukombozi ya Yesu. Uhakika wa kwamba mtu anajisikia akiumwa sana moyoni unaonyesha kwamba yeye (awe ni mwanamume au mwanamke) hajapita kiasi cha kutokuweza kupona. Lakini ili mtu apate msaada na mapono ya kiroho, anahitaji pia kupata msaada wa Kimaandiko kutoka kwa wazee wa kundi. (Isaya 1:18; 1 Yohana 2:1, 2; 3:21; Yakobo 5:13-16) Ikiwa wewe umepeperuka ukauacha ukweli, je! utachukua zile hatua zinazohitajiwa kabisa ili upone? Sisi tunakutia moyo ufanye hivyo.

Yehova Atatoa Msaada

Kwa hiyo wewe ‘ongoza moyo wako,’ badala ya kuuacha ukuongoze wewe vibaya. Kuza woga unaofaa juu ya Yehova. “Ikiwa hivyo,” inasema Biblia, “kutakuwako wakati ujao, na tumaini lako mwenyewe halitakatiliwa mbali.” (Mithali 23:17-19, NW) Tena kuna tumaini bora kama nini​—wakati ujao usio na mwisho katika dunia mpya yenye kufanywa ifikie uzuri wa kiparadiso na utawala wa ufalme wa Mungu! Ebu wazia kuacha kusumbuliwa-sumbuliwa na maelekeo ya moyo wenye dhambi. Zaidi ya hilo, hali za ulimwengu zinaonyesha kwamba sasa sisi tumeingia sana katika siku za mwisho na kwamba karibuni tumaini hilo litakuwa limetimizwa. Kwa uhakika inastahili kujitahidi kufikia tumaini hilo!—Mathayo 24:7-14, 34; 2 Timotheo 3:1-5; 2 Petro 3:13; Luka 23:43, NW; Ufunuo 21:3, 4.

Uhakika wa kwamba Yehova anatutolea sisi wakati ujao ulio mzuri sana na kututia nguvu tuufikie unapasa kutufanya tumkaribie yeye. Uhusiano huo wa kirafiki ni thawabu kubwa hata ukiwa peke yake. Baada ya yule kijana mwanamke aliyetangulia kutajwa kupona, yeye alisema hivi: ‘Mimi najisikia ni kama Yehova amekuwa tena Baba yangu.’ Uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu unaleta dhamiri safi, amani ya kindani na hali ya kujiheshimu. Tena, kwa kurudia Yehova na tengenezo lake, utafurahia tena urafiki wa kweli kutoka kwa watu mbalimbali.

Bila shaka, si jambo jepesi kubadili moyo. Hata hivyo, Yehova atabariki jitihada zako. Roho yake itakusaidia ‘ufanywe imara kwa nguvu katika utu wa ndani.’ (Waefeso 3:16) Utaona kwamba unapoendelea kuwa katika sala na katika mafunzo ya mambo ya kiroho, kushirikiana na Mashahidi wa Yehova na kuutia adabu moyo wako, pambano litakuwa rahisi zaidi. Moyo utaanza kuwa na tamaa ya kutaka yaliyo mema. Moyo huo utataka kurudia Yehova.

“Usiogope, kwa maana mimi ni pamoja nawe,” anasema Yehova. “Usifadhaike, kwa maana mimi ni Mungu wako; nitakutia nguvu, naam, nitakusaidia.” (Isaya 41:10) Hivyo ndivyo Yehova atakavyofanyia wale wanaompenda kweli kweli. Ikiwa wewe umepeperuka ukauacha ukweli lakini moyo wako unakusukuma ufanye mema, kweli Mungu ‘atakusaidia’ kwa roho takatifu yake na kupitia watu mmoja mmoja wenye madaraka katika kundi la Kikristo. Kwa kusudi hilo, wazee waliowekwa wanafurahi kutoa usaidizi wa kiroho. (1 Wathesalonike 5:12; Waebrania 13:7) Tumia kwa faida msaada wao wa upendo. Mbona usiutafute moja kwa moja bila kukawia?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki