Je! Watoto Wanataka Amri?
“HATA mtoto awe anaonekana kinje-nje amekomaa namna gani,” ndivyo anavyosema Dakt. Harry Mendelsohn, kiongozi wa utibabu wa jamaa kwenye Hospitali na Makao ya Utibabu Montefiore, New York, “bado yeye ni mtoto.” Na bado amri zitahitajiwa. Yeye anaeleza hivi: “Lazima mzazi mmoja achukue usimamizi. Jamaa si demokrasia, ingawa maoni kutoka kwa kila mtoto yanapasa kutiwa moyo. Lakini hatimaye maamuzi yote yapasa kuwa juu ya wazazi. Amri zapasa kufanywa, zapasa kuwa wazi na kurudiwa-rudiwa. Haiwapasi watoto kuwa na daraka la kujifanyia amri zao wenyewe.”—New York Daily News, Septemba 13, 1981.
“Watoto ni mafundi wa kupinga amri,” ndivyo anavyosema mkuu mmoja wa makao ya vijana. “Wanakana wanataka amri, lakini ukiwalainisha, unakuta sivyo. Uhakika ni kwamba wanafikiri amri za kufaa ni ishara ya upendo.”
Je! watoto wanakubaliana na hayo? Kutoka kwa fungu la “Amri kwa Wazazi Kupitia wavulana katika Shule ya Kurekebisha Tabia,” haya ni baadhi ya mambo wanayosema:
“Tusumbueni kidogo. Mshikilie sana nidhamu na kuitoa bila kubadilika-badilika. Tuonyesheni ni nani mkubwa. Kujua tuna utegemezo wenye nguvu kunatufanya tuhisi salama.
“Toeni mwangaza; tuonyesheni njia. Tuambieni Mungu hajafa, hajalala, au hayuko likizoni. Tunahitaji kuamini mtu mkubwa zaidi na mwenye nguvu zaidi yetu.
“Mkitugundua tunadanganya, tunaiba au kuwa wakatili, tujulisheni kwa sababu gani tuliyofanya ni kosa. Tunapohitaji adhabu itoeni, lakini tujulisheni mngali mnatupenda.
“Tuambieni tunapojifanya. Msiwe wenye kubadilika-badilika kwa urahisi na msiogopeshwe na vitisho vyetu kwamba tutaacha shule au tutatoroka nyumbani. Simameni imara. Hakika watoto hawataki kila kitu wanachoomba.”
Yote hayo yanasemwa kwa maneno machache yaliyoandikwa na mzazi mwenye hekima zaidi ya wote, msimamizi mkubwa zaidi ya wasimamizi wa masilahi ya watoto, Yehova Mungu. Katika Neno lake lililoongozwa kwa roho yake, Biblia, inasemwa hivi: “Ninyi, akina baba, msiwe mkiwaudhi watoto wenu, bali endeleeni kuwalea katika nidhamu na rekebisho akilini la Yehova.” (Waefeso 6:4, NW) Muumba anafahamu si yale tu watoto wanahitaji bali pia yale wazazi wanahitaji. Uwe kijana au mzazi, kaza fikira kwenye mambo yenye kusaidia katika makala mbili zinazofuata.