Maswali kutoka kwa Wasomaji
◼ kwa sababu gani nyakati nyingine wasikilizaji wanakaribishwa wasimame kwa ajili ya wimbo na sala kwenye mikutano na makusanyiko ya Kikristo?
Wimbo na sala ni mambo ambayo kwa muda mrefu yamekuwa sehemu ya ibada ya kweli. (1 Mambo ya Nyakati 16:7-9; Mathayo 26:26-30; Yakobo 5:13, 14) Hivyo, ni mambo ya kawaida na ni sehemu ya maana ya ibada kwenye mikutano ya kundi au kwenye makusanyiko ya Mashahidi wa Yehova.
Nyimbo nyingi ziko katika namna ya sala au sifa zenye kuelekezwa kwa Mungu. Wakati watu wengi wanaposimama kwa umoja kwa ajili ya wimbo na sala, jambo hilo linaweza kuchukuliwa kwamba ni kuonyesha heshima kwa kuja mbele za Mungu wakiwa na shukrani.—1 Wafalme 8:14, 22, 23.
Hata hivyo, inapasa kufahamiwa kwamba Biblia inaonyesha kusali au kuimbia Mungu sifa kunaweza kufanywa mtu akiwa katika hali ya kikao cho chote. (Linganisha Luka 22:39-41; Matendo 16:24, 25.) Kwa hiyo hakuna sheria katika habari hii. Ikiwa afya au hali za mtu zinafanya iwe vizuri zaidi awe ameketi wakati kundi linapoimba au sala inapotolewa, si kosa kufanya hivyo. Mara nyingi Wakristo wanakuwa wameketi wakati wa kusali kwenye Mafunzo ya Kitabu ya Kundi yaliyo madogo kuliko mikutano ile mingine. Wanafanya hivyo pia kwenye mafunzo ya nyumbani ya Biblia na nyakati za vyakula.