Neno la Mungu Li Hai
Kifo cha Yesu Kina Maana Gani Kwetu?
BAADA ya Yesu Kristo kufa, wasafiri Kleopa na rafiki yake walisimama njiani bila kutembea, wakiwa “wamekunja nyuso zao.” (Luka 24:17) Kifo ni adui, kwa hiyo si ajabu kwamba kinaleta huzuni. Hata hivyo watu hao wangeweza kuwa wenye furaha kwamba Yesu alikuwa amekufa, na hata sisi pia. Unajua sababu?
Biblia inaeleza hivi: “Kristo alikufa kwa ajili ya dhambi zetu.” “Alikufa kwa ajili yetu, ili tuishi.” (1 Wakorintho 15:3; 1 Wathesalonike 5:10) Ndiyo, Yesu alitumwa duniani kutuokoa. Yeye mwenyewe alisema hivi: “Mwana wa Adamu alikuja . . . kutoa nafsi yake [au, uhai wake] ukombozi badala ya wengi.” (Mathayo 20:28) Lakini maana yake nini kwamba Yesu alitoa uhai wake uwe “ukombozi”? Ukombozi ni nini?
Mara nyingi neno “ukombozi” linatumiwa wakati mtu fulani ametoroshwa. Baada ya mtoroshi (mficha-watu) anapoteka mtu, huenda akasema atarudisha mtu huyo ikiwa kiasi fulani cha pesa kitalipwa kiwe ukombozi. Kwa hiyo ukombozi ni kitu kinachofanya mtu aliyeshikwa mateka akombolewe. Ni kitu kinacholipwa ili mtu huyo asipoteze uhai wake. Uhai wa Yesu wa kibinadamu uliokuwa mkamilifu ulitolewa ili kufanya wanadamu wafunguliwe katika utumwa kwa dhambi na mauti. (1 Petro 1:18, 19; Waefeso 1:7) Kwa sababu gani kufunguliwa kwa namna hiyo kulihitajiwa?
Kulihitajiwa kwa sababu Adamu, babu yetu, alimwasi Mungu. (Mwanzo 2:17; 3:11, 12) Kwa njia hiyo tendo lake la kutokufuata sheria lilimfanya mtenda dhambi, kwa kuwa Biblia inaeleza kwamba “dhambi ni uasi.” (1 Yohana 3:4; 5:17) Basi ikawa kwamba hakustahili kupokea zawadi ya Mungu ya uzima wa milele. (Warumi 6:23) Kwa hiyo Adamu alijipotezea uhai mkamilifu wa kibinadamu katika dunia-paradiso. Pia alipotezea watoto ambao wangezaliwa naye tumaini hilo zuri sana la kupata uzima wa milele. Lakini huenda wewe ukauliza, ‘Sababu gani watoto wake walazimike kufa, hali ni Adamu aliyetenda dhambi?’
Hiyo ni kwa sababu wakati Adamu alipokuja kuwa mtenda dhambi alipitishia watoto wake dhambi na mauti, kutia ndani wanadamu wote walio hai sasa. (Ayubu 14:4; Warumi 5:12) Kwa hiyo wanadamu wamekuwa wakifa kwa sababu ya dhambi waliyorithi kwa Adamu. Basi, iliwezekanaje kifo cha Yesu kuwaweka watu wote huru watoke katika utumwa kwa dhambi na mauti?
Kanuni halali katika sheria ambayo Mungu alitolea taifa la Israeli inahusika. Kanuni hiyo inataja kwamba ‘uhai utozwe kwa uhai.’ (Kutoka 21:23) Kwa kutokutii kwake, Adamu mkamilifu alijipotezea mwenyewe na watoto wake wote uhai mkamilifu katika dunia-paradiso. Yesu Kristo alitoa uhai mkamilifu wake mwenyewe ili kununua arudishe kile kilichopotezwa na Adamu. Kama Biblia inavyoeleza, Yesu “alijitoa mwenyewe kuwa ukombozi unaolingana kwa ajili ya wote.”—1 Timotheo 2:5, 6, NW.
Ebu fikiria jambo hilo lina maana gani kwetu! Lina maana ya kwamba Yesu alimwaga damu ya uhai wake katika mauti ili sisi tuweze kuwa na nafasi ya kuishi milele chini ya utawala wa ufalme wa Mungu. Je! wewe utaonyesha shukrani zako kwa kutumia maisha yako utumikie Mungu na Mwana wake wa kimbingu, Yesu Kristo?—2 Wakorintho 5:14,15.
[Picha katika ukurasa wa 21]
‘Pesa za ukombozi’ zinaweza kutusaidiaje tuelewe ukombozi uliotolewa na Yesu?
[Picha katika ukurasa wa 22]
Kwa kuwa Yesu alikuwa mtu mwenye kulingana na Adamu mkamilifu, jambo hilo lina maana gani?
Kutokutii kwa Adamu kulimletea yeye na jamii yote ya kibinadamu matokeo gani?