”Mungu wa Faraja Yote” Yuko Pamoja Nasi
“Awe mbarikiwa . . . Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote.”—2 Wakorintho 1:3, 4, NW.
1, 2. Kwenye 2 Wakorintho 1:3-7, mtume Paulo alisema nini juu ya faraja katika nyakati za dhiki?
YEHOVA ndiye “Mungu wa faraja yote.” Mtume Paulo alijua jambo hilo kutokana na ujuzi wake wa mambo aliyojionea mwenyewe. Hivyo, ili kuwatia moyo Wakristo wenzake, aliandika maneno haya:
2 “Awe mbarikiwa . . . Baba wa rehema pole na Mungu wa faraja yote, ambaye hutufariji katika dhiki yetu yote. . . . Sasa kama tuko katika dhiki, jambo hilo ni kwa ajili ya faraja na wokovu wenu; au kama tunafarijiwa, jambo hilo ni kwa ajili ya faraja yenu inayotenda kazi kuwafanya mvumilie taabu zile zile ambazo sisi tunataabika pia. Na kwa hiyo tumaini letu kwa ninyi si la kuyumba-yumba, tukijua kama tunavyojua kwamba, sawa na vile ninyi ni washiriki wa taabu hizo, kwa njia iyo hiyo ninyi mtashiriki pia ile faraja.”—2 Wakorintho 1:3-7, NW.
3. (a) Kwa sababu gani Paulo alimjua Yehova kuwa “Mungu wa faraja yote”? (b) Ni juu ya msingi gani Mashahidi wenzetu wanaweza kufarijiwa na kutiwa moyo wavumilie dhiki?
3 Ndiyo, Paulo alimjua Yehova kuwa “Mungu wa faraja yote.” Yeye alikuwa ameona Baba yake wa kimbingu akimfanyia mambo kwa njia yenye faraja na rehema pole, hasa wakati alipokuwa akitaabika “kwa ajili ya uadilifu.” (Linganisha Mathayo 5:10, NW) Basi, mtume angeweza kufariji wengine na kuwatia moyo wavumilie dhiki. Kwa uhakika, kupitia mfano wao wa uaminifu na maonyesho yao ya kumtumaini Yehova, mashahidi Wakristo wa Yehova ambao wamevumilia dhiki wanawapa waamini wenzao kitiamoyo kinachowachochea waendelee kuwa waaminifu kwa Mungu. Na katika kuvumilia taabu Paulo alikuwa mfano mwema.
Kumbukumbu la Uvumilivu wa Uaminifu
4, 5. (a) Ni wakati gani Paulo alipoandika Wakorintho wa Pili? (b) Paulo alikuwaje sawa na “mitume walio bora zaidi” wa Korintho, lakini ni kwa njia gani yeye alikuwa mkuu kuliko wao?
4 Karibu na mwaka wa 55 W.K. Paulo aliandika barua yake ya pili yenye kuogozwa na Mungu kwa Wakristo waliokuwa katika mji wa Korintho. Huko alipingwa na wale aliowaita kwa dhihaka “mitume walio bora zaidi.” Alikitetea kwa ushujaa cheo chake cha kimtume, si kwa ajili yake mwenyewe, bali “kwa ajili ya Mungu,” yaani, ili kuliokoa kundi lililo mali ya Yehova. (2 Wakorintho 11:5, 12-14; 12:11; 5:12, 13, NW) Mtume alionyesha kwamba kulingana na ukoo wa vizazi yeye alikuwa sawa na wapinzani wake, kisha akaonyesha kwamba alikuwa mkuu kuliko wao katika kufanya kazi ngumu-ngumu, kupatwa na taabu, katika safari zake, hatari na magumu yaliyompata akiwa ‘mhudumu wa Kristo.’ Aliandika hivi:
5 “Je! wao [yaani, wapinzani wake] ni wahudumu wa Kristo? Najibu kama mwenda-wazimu, mimi niko hivyo hata zaidi: katika kazi ngumu-ngumu kwa utele zaidi, katika magereza kwa utele zaidi, katika dharuba za kupita kiasi, katika hali za kukaribia kifo, mara nyingi. Kupitia Wayahudi mimi nilipokea mara tano viboko arobaini kasoro kimoja, mara tatu nilipigwa kwa fito, mara moja nilipigwa kwa mawe, mara tatu nilivunjikiwa merikebu, usiku mmoja nimekesha na mchana mmoja nimeshinda nikiwa katika kilindi; katika safari mara nyingi, katika hatari kutokana na mito, katika hatari kutokana na wakora wa njiani, katika hatari kutokana na mbari ya watu wangu mwenyewe, katika hatari kutokana na mataifa, katika hatari mjini, katika hatari za jangwani, katika hatari huko baharini, katika hatari kutokana na ndugu za uongo, katika kazi ngumu na kutoa jasho, katika nyakati za usiku za kukosa usingizi, mara nyingi, katika njaa na kiu, katika kujiepusha na chakula mara nyingi, katika baridi na uchi.”—2 Wakorintho 11:21-27, NW.
6. (a) Ni wapi tunapoona kumbukumbu la sehemu fulani za maisha ya Kikristo ya Paulo kabla hajaandika Wakorintho wa Pili? (b) Tutafaidikaje kwa kulifikiria kumbukumbu la Paulo la uvumilivu wa uaminifu?
6 Kitabu cha Biblia cha Matendo ya Mitume (9:3 mpaka karibu na 20:4) kinataja mengine ya mambo yaliyotangulia kutajwa ya maisha ya Paulo, tangu alipokuwa Mkristo mpaka alipoandika Wakorintho wa Pili. Sasa acheni tulifikirie kumbukumbu lake la uvumilivu wa uaminifu. Bila shaka litatutia moyo tuvumilie dhiki tukiwa na uhakika wa kwamba “Mungu wa faraja yote” yuko pamoja nasi.
‘Kazi Ngumu-Ngumu na Kufungwa Gerezani kwa Utele Zaidi’
7. (a) Ni kazi gani inayomaanishwa na ‘kazi ngumu-ngumu za utele zaidi’ za Paulo? (b) Kulingana na maneno ambayo mtume aliwaambia “wanaume wazee’’ wa kundi la Efeso, yeye aliendeshaje huduma yake? (c) Ni nini kilichomchochea Paulo aendelee na kazi ngumu za kujikaza kwa ajili ya habari njema na faida za Ufalme?
7 Katika kazi ngumu-ngumu kwa utele zaidi: Akiwa mtangazaji wa “habari njema,” Paulo ‘alifanya kazi kwa bidii zaidi ya’ wapinzani wake. (2 Wakorintho 11:23, Today’s English Version) Bila shaka, yeye alikuwa amefanya kazi ya kuhubiri kwa muda mrefu kuliko wao na mara nyingi alifanya hivyo akiwa katika eneo lenye magumu mengi. Kwa mfano, katika Efeso ambako mungu-mke wa kipagani Artemi aliabudiwa, Paulo alitendwa jeuri na kundi la watu wenye ghasia. Huko jitihada zake katika huduma na kwa ajili ya waamini wenzake zilikuwa za kujikaza sana, nyakati nyingine hata zikawa zinataka kupasua moyo wake. Lakini matunda mazuri ya kiroho yalipatikana. Baadaye, angeweza kuwaambia “wanaume wazee” wa kundi la Efeso maneno haya: “Sikujiepusha kuwaambia ninyi lo lote la mambo yaliyokuwa yenye faida wala kuwafundisha waziwazi na nyumba kwa nyumba. Lakini nilitoa ushuhuda kikamilifu kwa wote Wayahudi na Wagiriki juu ya toba kwa Mungu na kumwamini Bwana yetu Yesu.” (Matendo 20:17, 20, 21, 31, NW; 19:1-41) Basi, kabla wanaume hao waliokuwa wazee hawajawa Wakristo, mtume Paulo alikuwa amewafundisha kweli zile za msingi za Ukristo katika utendaji wa kuhubiri “nyumba kwa nyumba.” Utendaji wa Neno la Yehova na roho takatifu juu ya moyo wa Paulo ndio uliomchochea afanye kazi ngumu kwa kujikaza akizieneza habari njema na kuendeleza faida za Ufalme. (Isaya 61:1, 2; Warumi 10:8-10) Katika utendaji huo wa kujikaza sana mtume aliwekea Wakristo wa karne ya 20 mfano bora kabisa.
8. (a) Kwa sababu gani Paulo angeweza kusema alikuwa amekuwa “katika magereza kwa utele zaidi” ya wale “mitume walio bora zaidi”? (b) Bila shaka, Paulo na Sila walipata faraja katika nini walipokuwa wamefungwa gerezani huko Filipi, nao walifanya nini walipowekwa huru na tetemeko la ardhi? (c) Ni kitiamoyo gani kinachoweza kupatikana kutokana na yaliyompata Paulo gerezani huko Filipi?
8 Katika magereza kwa utele zaidi: Klementi wa Roma, ambaye aliandika kuelekea mwisho wa karne ya kwanza W.K., anasema kwamba Paulo alikuwa amefungwa gerezani mara kadha. Kabla ya kuandika Wakorintho wa Pili alikuwa tayari amekwisha kuwa gerezani mara nyingi kuliko wale “mitume walio bora zaidi.” Maandishi katika Matendo yanaeleza juu ya kifungo kimoja kati ya hivyo—katika mji wa Filipi wa Kimakedonia. Ni wazi kwamba Paulo na Sila walifurahi kutaabika “kwa ajili ya uadilifu,” kwa maana walipokuwa wangali wamefungwa gerezani walimpelekea Mungu sala na wakamsifu kwa wimbo. Walipata faraja kwa kuyafikiria Maandiko na vilevile kwa kujua kwamba Mungu alisikia sala zao na alikuwa akiwajibu. (Zaburi 65:2; 119:52) Walipowekwa huru na tetemeko la ardhi, hawakutoroka mbio-mbio, bali ‘walinena neno la Yehova kwa mtunza gereza pamoja na wote wale waliokuwa katika nyumba yake.’ Matokeo yakawa nini? Mtunza gereza na watu wa nyumba yake wakawa Wakristo! (Matendo 16:16-40, NW) Kwa kweli masimulizi hayo yanawatia moyo Mashahidi wa Yehova waliofungwa gerezani leo wakubali mateso kwa furaha ya kimungu, wawe wenye kusali, walitafakari Neno la Mungu na kunena habari zalo kwa ujasiri!—Matendo 4:29-31.
Hakuvunjwa Moyo na Mapigo na Hali za Kukaribia Kifo
9. Ni nini kinachoonyeshwa na maneno “dharuba za kupita kiasi”?
9 Katika dharuba (mapigo) za kupita kiasi: Paulo alikuwa amepigwa kupita kiasi. Imesemwa pia kwamba mara nyingi alikuwa “kwenye mlango wa kifo.” (Mstari 23, The Twentieth Century New Testament) Huenda hilo likawa na maana ya kwamba wakati wa mapigo fulani dharuba alizopata zilikuwa kali sana hata akawa mahututi, karibu na kifo.
10. (a) Paulo alikuwa amepatwaje na “hali za kukaribia kifo”? (b) Inaelekea ni nini kilichomtegemeza mtume alipokuwa “kwenye mlango wa kifo”?
10 Katika hali za kukaribia kifo, mara nyingi: Si lazima jambo hili liwe linahusu mapigo fulani tu. Mapema katika barua ii hii Paulo alikuwa amesema: “Sikuzote twachukua katika mwili kuuawa kwake Yesu.” (2 Wakorintho 4:10, 11) Mtume alikuwa amekuwa katika hatari yenye kuelekea kumaliza uhai wake au hata akawa na maumivu yaliyokaribia kumwua akiwa huko Dameski, Antiokia ya Pisidia, Ikonio, Listra, Thesalonike na Beroya. (Matendo 9:23-25; 13:49-51; 14:1-6, 19, 20; 17:1, 5-9, 13, 14) Kwa kweli, huenda akawa alikuwa katika hali ya kupatwa na hatari za kifo za michezo ya Kirumi kwa sababu anataja kwamba ‘alipigana na wanyama-mwitu huko Efeso.’ (1 Wakorintho 15:32, NW; linganisha Matendo 19:23-41; 2 Wakorintho 1:8-11.) Kwa sababu ya uhai wake kuwa hatarini mara nyingi hivyo, kwa uhakika mtume angeweza kusema hivi: “Kila siku nakabili kifo’ (1 Wakorintho 15:31, NW) Bila shaka msaada wa roho takatifu ya Yehova na imani ya Paulo katika ahadi za Mungu zenye thamani ni mambo yaliyomtegemeza mtume alipokuwa “kwenye mlango wa kifo” mara nyingi—2 Wakorintho 1:20- 22.
11. Mapigo ambayo Paulo alipata kwa Wayahudi yalikuwa ya namna gani?
11 Kupitia Wayahudi mimi nilipokea mara tano viboko arobaini kasoro kimoja: Paulo alionyesha kwamba mapigo aliyopigwa nyakati tano “kwa ajili ya uadilifu’ yalifanywa na Wayahudi, labda katika masinagogi yao. (Mstari 24; Mathayo 10:17) Sheria ya Musa iliruhusu kupiga mtu kwa fimbo au ufito, na waamuzi ndio walioamua hesabu ya viboko ambavyo mtu angepata kulingana na ubaya wake. Lakini kwa huruma za kibinadamu adhabu hiyo haingeweza kupita viboko 40, nao Wayahudi walipunguza hesabu ya viboko ikawa 39 wasije wakapitisha hesabu iliyowekwa kisheria kwa sababu ya kukosea bila kujua. (Kumbukumbu la Torati 25:1-3) Mapigo hayo yalikuwa yenye maumivu makali. Lakini “Mungu wa faraja yote” alimtia nguvu Paulo avumilie tendo hilo kwa uvumilivu wa uaminifu.
12. (a) Inaelekea kuwa wazi kwamba mtume alimaanisha kutendwa namna gani aliposema “mara tatu nilipigwa kwa fito”? (b) Ni kwa msaada gani mapigo “kwa ajili ya uadilifu” yanaweza kuvumiliwa?
12 Mara tatu nilipigwa kwa fito: Inaelekea kuwa wazi kwamba mapigo makali hayo yalifanywa na maafisa Waroma wenye kuwa na fito. (Mstari 25) Mapigo hayo ya kutumia ufito yalikuwa yakifanywa baada ya mpigwa kuvuliwa mavazi yake ya nje. Paulo hangeweza kupokea mapigo ya namna hiyo kulingana na sheria kwa sababu alikuwa raia Mroma. Walakini, jambo hilo halikumwokoa yeye wala Sila asipokee “dharuba nyingi” kabla hawajafungwa gerezani wakiwa watangazaji wa habari njema huko Filipi. (Matendo 16:19-24, 33, 35-40, NW) Nyakati nyingine mapigo kama hayo yangeweza kuwa ya ukatili sana, lakini kwa msaada wa roho ya Mungu Paulo aliuvumilia kwa uaminifu ukatili huo “kwa ajili ya uadilifu.” Nao Wakristo wengi wa kisasa wamedumisha ukamilifu kwa Mungu wajapotendwa vibaya kimwili kwa njia inayolinganika na hiyo. Wameweza kufanya hivyo kwa sababu ya tegemezo lile lile la kimungu.
13. Paulo alipigwa kwa mawe akiwa wapi, lakini Je! jambo hilo lilikomesha huduma yake?
13 Mara moja nilipigwa kwa mawe: Huko Listra Wayahudi wenye kushikilia mno maoni yao ‘walimpiga Paulo kwa mawe na wakamburuta nje ya mji, wakiwaza alikuwa amekufa.’ Bila shaka, kusudi la kumpiga kwa mawe lilikuwa ni kumwua. (Linganisha Mambo ya Walawi 20:2; Matendo 7:58-60.) Lakini “wakati wanafunzi walipomzunguka, yeye aliinuka na kuingia ndani ya mji,” akaanza tena safari zake za kuhudumu siku ile ile iliyofuata.—Matendo 14:19-22, NW.
Kuvunjikiwa Merikebu na Kuwa Hatarini Katika Bahari
14. Paulo alitaja visa gani vya kuvunjikiwa na merikebu, na visa hivyo vilikuwa na matokeo gani juu ya safari alizofunga kwa ajili ya habari njema?
14 Mara tatu nilivunjikiwa merikebu: Kitabu cha Matendo kimeandika habari za kisa kimoja tu cha kuvunjikiwa merikebu, nacho kilitukia baada ya Paulo kuwaandikia Wakorintho. Kilitukiwa Paulo akiwa katika safari ya kuelekea Roma. (Matendo, sura ya 27) Walakini, kabla ya hapo mtume alisafiri mara nyingi akiwa katika vyombo vya baharini, na halikuwa jambo lisilo la kawaida merikebu kuvunjika katika safari za pwani. Kwa hiyo, ingawa Maandiko hayatoi maelezo juu ya visa vitatu vya kuvunjikiwa merikebu vilivyotajwa hapa, ni wazi kwamba balaa za safari za Bahari ya Kati hazikumfanya Paulo akatishe safari alizokuwa akifunga kwa ajili ya habari njema.
15. (a) Paulo alikuwa na maana gani aliposema “usiku mmoja nimekesha na mchana mmoja nimeshinda nikiwa katika kilindi”? (b) “Mungu wa faraja yote’’ alimsaidiaje Paulo katika kisa hicho kilichotajwa, na jambo hilo linapasa kutupa uhakika gani?
15 Usiku mmoja nimekesha na mchana mmoja nimeshinda nikiwa katika kilindi: Bila shaka, mtume hakusema kwamba alivumilia kimwujiza akiwa chini ya maji kwa muda wa saa 24. Kwa kuvunjikiwa merikebu, huenda ikawa alitumia saa hizo zenye hatari akiogelea kwa shida nyingi katika maji yenye machafuko au akiwa ameshikilia sana ubao wenye kuelea au mabaki ya chombo kilichovunjwa-vunjwa. Hata kama alikuwa juu ya chelezo, tukio hilo lenye kumkera (kumsumbua) mawazo (lisilotajwa mahali penginepo katika Maandiko) lilimhitaji awe na uvumilivu wenye ushujaa mpaka mtume huyo aokolewe au afaulu kufikia nchi kavu. Kwa uhakika, ‘alimlilia Yehova akipaza sauti katika taabu yake kuu, na katika mikazo iliyokuwa juu yake Mungu alimtoa.’ (Linganisha Zaburi 107:23-31.) Uyo huyo “Mungu wa faraja yote” anaweza kujibu sala zetu pia.—Linganisha 1 Yohana 5:13-15.
Mungu Wetu Anatupa Faraja Isiyokwisha
16, 17. Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba msaada wa roho takatifu ya Yehova ni wenye thamani kubwa sana tunapotaabika “kwa ajili ya uadilifu”?
16 Tumeona vingine vya vyanzo vya faraja vilivyomsaidia Paulo aendelee kuwa mwaminifu kwa Yehova ijapokuwako dhiki. Vyanzo hivyo vinastahili kukaziwa, kwa maana vitasaidia Mashahidi wa Yehova wa kisasa wavumilie taabu nyingi “kwa ajili ya uadilifu.”
17 Msaada wa roho takatifu ya Yehova ni wenye thamani kubwa sana. Hasa wakati wa dhiki tunapaswa kuiomba roho, tukubali mwelekezo wake na kudhihirisha matunda yake. (Luka 11:13; Zaburi 143:10: Wagalatia 5:22, 23, NW) Roho ya Yehova ikitenda kazi juu ya mioyo yetu inatufanya tuukumbuke upendo wake, na uhakikisho huo wenye kufariji utatusaidia tuvumilie dhiki.—Warumi 5:3-5; 8:35-39; 2 Wathesalonike 3:5.
18. Sisi Wakristo tunapopatwa na dhiki, imani katika ahadi za Mungu zenye thamani inaweza kutufariji namna gani?
18 Imani katika ahadi za Mungu zenye thamani, ambazo zimeonyeshwa katika Maandiko, itatufariji pia. (Warumi 15:4) Kumbuka kwamba “kwa ajili ya furaha ambayo iliwekwa mbele yake [Yesu Kristo] yeye alivumilia mti wa mateso.” (Waebrania 12:1, 2, NW) Hata tukitaabika kufikia kiasi cha kuupitia “mlango kifo,” kuna lile faraja zuri ajabu la ufufuo na uzima usiokwisha katika taratibu mpya ya Mungu, yawe matumaini yetu ni ya kimbingu au ya kidunia. (Mathayo 10:28; Luka 23:43, NW; Yohana 5:28, 29; 17:3; 1 Wakorintho 15:53; 2 Petro 3:13) Dhiki inakuwa ‘nyepesi na ya muda wa kitambo tu’ tunapoutazamia umilele!—2 Wakorintho 4:16-18.
19. Sala inatuleteaje faraja katikati ya dhiki nyingi?
19 Kupewa kwetu na Mungu amani ya akili na nguvu kwa kujibu sala zetu ni chanzo kikuu pia cha faraja wakati wa dhiki. (Angalia Luka 22:32; Matendo 4:23-31; Yakobo 5:16-18.) Yesu alifanya dua kwa bidii na akamwomba Yehova, ‘aliyeweza kumwokoa na kumtoa katika mauti, naye akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu.’ Ndiyo, Yehova alituma malaika akamtie Yesu nguvu wakati wa jaribu. (Waebrania 5:7; Luka 22:43) Kwa uhakika, tunapoona kwamba Yehova anajibu sala zetu katikati ya dhiki nyingi, tunafarijiwa.
20. Ni njia gani nyingine Paulo aliwashindia wale “mitume walio bora zaidi” wa Korintho tutakazoziangalia?
20 Ikiwa tunajitahidi kwa bidii kuvumilia kiuaminifu tukiwa mashahidi Wakristo wa Yehova, “Mungu wa faraja yote” atakuwa pamoja nasi, sawa na alivyokuwa pamoja na mtume Paulo. Kufikia hapo, tumeangalia kazi ngumu-ngumu za Paulo na taabu zake. Lakini utetezi wake akiwa ‘mhudumu wa Kristo’ unaonyesha kwamba aliwapita pia wale “mitume walio bora zaidi” wa Korintho katika safari, hatari na magumu. Tunaweza kujifunza nini kutokana na mambo hayo yaliyompata?
Je! wewe unakumbuka mambo haya?
◻ Kwa sababu gani mtume Paulo alimjua Yehova kuwa “Mungu wa faraja yote”?
◻ Wakristo ambao wamevumilia dhiki wanawezaje kuwatia moyo waamini wenzao waendelee kuwa waaminifu kwa Yehova?
◻ Ni kazi gani iliyotiwa ndani ya ya ‘kazi ngumu-ngumu za utele zaidi’ za mtume?
◻ Tunaweza kufaidikaje na yaliyompata Paulo gerezani?
◻ Ni nini nyingine za njia ambazo Yehova Mungu anawapa watu faraja isiyokwisha?
[Picha katika ukurasa wa 8]
Mara nyingi Paulo alifungwa gerezani, kama wakati yeye na Sila walipofungwa katika Filipi
[Picha katika ukurasa wa 11]
Mara nne wakati wa huduma ya Paulo, yeye alivunjikiwa merikebu