Tunaweza ‘Kuvumilia Mpaka Mwisho’
“Yeye ambaye avumilia kwa saburi mpaka ule mwisho, ataokolewa.”—MATHAYO 24:13, THE EMPHATIC DIAGLOTT.
1. (a) Kwetu sisi mmoja mmoja, huenda “mwisho” uliotajwa na Yesu ukawa nini, kama ulivyoandikwa kwenye Mathayo 24:13? (b) Ni nini kinachohitajiwa sana ili kupata wokovu?
YESU KRISTO, katika unabii ule mkuu unaohusu “kuwapo” kwake, alisema maneno haya yenye kutia watu tumaini: “Yeye ambaye amevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 24:3,13, NW) Kwetu sisi mmoja mmoja, huenda “mwisho” ukawa ama ni “umalizio wa mfumo wa mambo” ama kifo chetu, labda baada ya kujaribiwa muda mrefu kwa njia yenye kutatiza. Hata hivyo, uvumilivu wa uaminifu unahitajiwa sana ili tuweze kupata wokovu hatimaye.—1 Petro 1:8, 9.
2, 3. (a) Kwa sababu gani tunaweza kuwa na uhakika kwamba tunaweza kupata wokovu tungawa tu watu wasio wakamilifu? (b) Sasa tutaangalia nini?
2 Yesu alituwekea mfano mkamilifu wa uvumilivu. (Waebrania 12:1-3) Lakini sisi wanadamu wasio wakamilifu tunaweza kuwa waaminifu kwa Mungu tujapopatwa na taabu nyingi sana na mateso “kwa ajili ya uadilifu.” (Mathayo 5:10, NW) Ndiyo, kwa fadhili zisizostahilika za Yehova tunaweza kupata wokovu hata tuwe na uzima wa milele kupitia dhabihu ya ukombozi ya Mwanaye mpendwa, Yesu Kristo.—Yohana 3:16; 1 Yohana 2:1, 2.
3 Ingawa mtume Paulo alikuwa mwanadamu asiye mkamilifu, yeye ni mfano mwema kwetu wa kuwa na uvumilivu unaoongoza kwenye wokovu. Tulipokuwa tukiangalia kisehemu cha maneno yake ya utetezi yaliyoandikwa kwenye 2 Wakorintho 11:23-27 (NW), tumejifunza kwamba katka kazi ngumu-ngumu na taabu yeye alikuwa ‘mhudumu wa Kristo hata zaidi’ ya wale “mitume walio bora zaidi” ati wa Korintho. Kama tutakavyoona, yeye aliwashinda akiwa ‘mhudumu wa Kristo’ katika safari pia, katika hatari na magumu mbalimbali.
Safari Zenye Hatari kwa Kusudi la Kusogeza Mbele Habari Njema
4. Mtume Paulo alimaanisha safari gani alipoonyesha kwamba ‘alisafiri mara nyingi’?
4 Katika safari mara nyingi: Paulo alisafiri mara nyingi kuzitangaza habari njema, akawapita kwa mbali wapinzani wake wa Korintho katika jambo hilo. (Mistari 23, 26) Bila shaka, alikabili hatari zilizokuwa kawaida ya wasafiri katika maeneo ya Kiroma. Lakini safari zake zilikuwa ndefu sana na za kuchosha sana. Safari zake zilimfikisha kwenye miji kama Antiokia katika Pisidia, Ikonio, Listra, Derbe, Filipi, Thesalonike, Beroya, Athene na Korintho.—Matendo 13:14-14:26; 16:11-18:17.
5. Ni nini kilichofanya safari za Paulo zitatize zaidi na kuwa zenye hatari, naye angewezaje kuvumilia safari hizo zenye kumtoa jasho?
5 Safari za mtume zilikuwa zenye matatizo na hatari nyingi zaidi pia kwa sababu alikuwa ‘kitu cha kuchukiwa kwa sababu ya jina la Kristo.’ (Mathayo 10:22, NW) Hata hivyo, Yehova alimpa Paulo nguvu na ushujaa aliouhitaji katika safari zake zenye kuchosha sana. (Isaya 40:28-31) Kwa uhakika, mtume aliwekea Mashahidi wa Yehova wa kisasa mfano mwema wa kuendeleza faida za Ufalme kwa sababu alikuwa mhudumu mwenye bidii.—Mathayo 6:33.
Kuvumilia Hatari Nyingi kwa Uaminifu
6. Inaweza kuwa mtume alikuwa akimaanisha hatari gani kwa kusema “hatari kutokana na mito”?
6 Katika hatari kutokana na mito: Kwa sababu siku hizo madaraja hayakuwa mengi kama leo, bila shaka maisha ya Paulo yaliingia hatarini alipokuwa akivuka mito yenye mafuriko kwa kutembea ndani. Kwa mfano, wakati wa ziara yake ya kwanza ya umisionari, ya kwenda na kurudi, alipitia Pisidia, ambako mito ya milimani yenye kutelemka mbio ilikuwa hatari sana. (Matendo 13:13, 14; 14:21, 24) Mashahidi wa Yehova, na hasa wamisionari na wahudumu wengine walio katika maeneo ya huko ndani-ndani mbali na miji, wanaweza kupata kitia-moyo kutokana na uvumilivu wa Paulo akiwa chini ya hali za namna hiyo.
7. (a) Ni ‘hatari gani kutokana na wakora wa njiani’ zilizomwelekea Paulo? (b) Mashahidi leo wanaweza kuvumiliaje hatari kama hizo?
7 Katika hatari kutokana na wakora wa njiani: Mfano wa Yesu wa yule Msamaria mwenye huruma ya kijirani unaonyesha kwamba msafiri wa karne ya kwanza angeweza ‘kuangukia kati ya wanyang’anyi, ambao wangeweza kumvua nguo, wamtie jeraha na kwenda zao kwa kumwacha akiwa karibu ya kufa.’ (Luka 10:25-37) Waviziaji wenye silaha walikuwa wengi katika maeneo mengi aliyopitia Paulo. Kwa mfano, wakati yeye na Barnaba waliposafiri kuelekea kaskazini kutoka Perga na kufika Antiokia katika Pisidia, walipitia eneo la milima-milima lililojaa waviziaji (waoteaji). (Matendo 13:13, 14) Wahalifu hao hatari walikuwa wakizingira wapitaji katika maeneo yasiyo na watu na kuwatenda jeuri moja kwa moja. Inaweza kuwa kwamba Paulo mwenyewe alishambuliwa na wakora wa njiani. Mashahidi wa Yehova wa kisasa huenda wakakabili hatari kama hizo na wanahitajiwa watumie hadhari. Walakini, kama mtume wanaweza kuvumilia kwa uaminifu, wasishindwe na woga bali wawe na uhakika watapata ulinzi wa Yehova.—Linganisha Zaburi 56:4.
8. Kwa sababu gani Paulo alichukiwa hata akataka kuuawa na Wayahudi wenzake?
8 Katika hatari kutokana na mbari ya wangu mwenyewe: Paulo alikuwa akihubiri habari za Masihi aliyetundikwa na kufufuliwa, ambaye alikataliwa na wananchi wenzake kwa ujumla. (1 Wakorintho 1:22-24; 2:2) Kuongezea hilo, yeye alifundisha kwamba mtu angetangazwa kuwa mwadilifu, si kwa kutegemea kazi za Sheria ya Musa, bali kupitia imani katika Yesu Kristo. (Warumi 3:20; 5:18-21; 6:14, NW) Kwa hiyo, Wayahudi wenzake walimchukua Paulo kuwa mwasi-imani, wakamchukia, wakampiga na hata wakataka kumwua. (Matendo 9:23-25) Hata wale wa mbari yake mwenyewe walichukizwa kwa sababu alikuwa akisadikisha watu fulani wa Mataifa ambao Wayahudi walikuwa wamejaribu kuwaongoa wafuate dini yao wenyewe.—Mathayo 23:15; Matendo 17:1-10.
9. Ni ‘hatari gani kutokana na mataifa’ alizokabili mtume, lakini je! hatari hizo zilimnyamazisha?
9 Katika hatari kutokana na mataifa: Mataifa, au watu wa mataifa, walimtesa Paulo hata wao. (Matendo 19:11-41) Kwa kweli, adui zake wa Kiyahudi walichochea Mataifa nyakati nyingine wamtende jeuri mtume huyo. (Matendo 14:1-7, 19, 20) Walakini, hatari hizo kutoka kwa Wayahudi na Mataifa hazikunyamazisha mtangazaji huyo wa Ufalme asiyeogopa. Vivyo hivyo, mashahidi Wakristo wa Yehova wanaoteswa leo wanahubiri bila woga kati ya watu wa mbari yao wenyewe na kati ya wengineo.—Matendo 17:30; linganisha Zaburi 59:1-4.
10. Paulo alitiwaje hatarini ‘katika mji’?
10 Katika hatari mjini: Kwa njia fulani-fulani, Paulo aliteswa katika miji kama Dameski, Yerusalemu, Listra na Efeso. (Matendo 9:23-30; 14:19; 19:29-31) Wapinzani wa Mataifa wa huko Filipi walisema kwamba Paulo na Sila walikuwa ‘wanachafua sana mji wao.’ Basi, waeneza evanjeli hao walitendwa jeuri na kundi la watu wenye ghasia, wakapigwa-pigwa na kufungwa gerezani. (Matendo 16:16-24) Lakini jambo hilo halikuwakomesha watangazaji hao wa Ufalme. Vivyo hivyo, jeuri ya namna hiyo haijanyamazisha Mashahidi wa Yehova katika siku zetu.
11. “Hatari za jangwani” ambazo zingeweza kumpata ni nini?
11 Katika hatari za jangwani: Mtume hakufanya utendaji na safari zake kwenye maeneo yenye watu wengi na kwenye njia zenye kupitiwa na watu wengi peke yazo. Alipitia pia mikoa yenye wakazi wachache, hata katika “mapori.” (Today’s English Version) . Akiwa huko Paulo alikabili kwa ushujaa uwezekano wa kufa-njaa, kupigwa na pepo (tufani) kali, kupotea njia, kunyemelewa na wanyama-mwitu na kuzingirwa na waviziaji wenye silaha.
12. Paulo alikabili “hatari huko baharini” za namna gani, na je! zilimzuia asiendeshe huduma yake?
12 Katika hatari huko baharini: Wakati kueneza habari njema au kusaidia waamini wenzao kulipohitaji asafiri ‘kwenye mawimbi makubwa ya bahari iliyochafuka’ (TEV), zilikuwako hatari za kupigwa dhoruba na maji, na vilevile uwezekano wa kuvunjikiwa merikebu. Lakini Paulo hakuacha hatari hizo zimzuie kuendesha huduma yake. Ndivyo wengi wa Mashahidi wa Yehova katika wakati wetu wanavyovumilia kishujaa hatari kama hizo wanaposafiri ili kuendeleza faida za Ufalme.
Akatiwa Hatarini na “Ndugu za Uongo”
13, 14. (a) Ni nani waliokuwa “ndugu za uongo”? (b) Kwa sababu gani hao “ndugu za uongo” ndio waliokuwa hatari zaidi? (c) Mashahidi wa Yehova wameimarishwaje kiroho wajikinge na “ndugu za uongo” ambao huenda wakajipenyeza ndani ya makundi?
13 Katika hatari kutokana na ndugu za uongo: Jambo lililomtia Paulo katika hatari kubwa zaidi ya zote, na bila shaka likamjaribu vikali sana, ni “ndugu za uongo” wenye hila au “ndugu za bandia.” (The Kingdom Interlinear Translation of the Greek Scriptures) Watu wa namna hiyo wamepatikana kati ya wafuasi wa Kristo tangu wakati wa Yuda Iskariote aliyekuwa msaliti. Katika siku za Paulo huenda wale “mitume walio bora zaidi” wa Korintho wakawa walikuwa miongoni mwa hao “ndugu za uongo.” “Ndugu za uongo” walikuwa hatari zaidi kwa sababu walijifanya kwa hila kuwa rafiki na kumbe walikuwa wasaliti wasio washikamanifu. Watu wa namna hiyo walikuwa wakijaribu kupata jambo la kumshtakia Paulo.—2 Wakorintho 11:5, 12-14; linganisha Danieli 6:4, 5.
14 Kati ya “ndugu za bandia” walikuwako wale wenye kutenda kazi katika “makundi ya Galatia.” Lakini Paulo haukukubali kushindwa kamwe na watu hao, “ili ile kweli ya habari njema iweze kuendelea kuwa na” waamini wenzake. (Wagalatia 1:1, 2; 2:4, 5, NW; linganisha Yuda 3, 4.) Kama vile Yehova alivyomsaidia Paulo, Yeye amewaimarisha kiroho mashahidi wake wa kisasa hivi kwamba “ile kweli ya habari njema” imeendelea kuwa nao. Katika maandiko yaliyoongozwa na Mungu kama zile barua walizoandikiwa waamini Wakorintho na Wagalatia, mashahidi wa kisasa wanapata msaada wa kiroho unaohitajiwa ili kujikinga na “ndugu za uongo” ambao huenda wakajipenyeza katika makundi.
Kuvumilia Magumu Katika “Utumishi Mtakatifu”
15. Paulo alikuwa akimaanisha nini aliposema kwamba alikuwa mhudumu wa Kristo ‘hata zaidi katika kazi ngumu na kutoa jasho’?
15 Katika kazi ngumu na kutoa jasho: Ndipo Paulo alipotaja magumu yaliyomfanya awe ‘mhudumu wa Kristo hata zaidi’ kuwapita wapinzani wake. (Mistari 23, 27) “Kazi ngumu na kutoa jasho” kunakotajwa hapa kunaweza kuwa kunahusu kazi ya mikono yenye kumchosha Paulo, aliyoifanya ili kujipatia riziki katika huduma. (Matendo 18:1-4; 1 Wakorintho 4:11, 12; 2 Wathesalonike 3:7, 8) Lakini kila jambo alilofanya mtume liliutegemea utumishi wa Yehova. Kwa hiyo, bila shaka hii “kazi ngumu na kutoa jasho” ilitia ndani jitihada kubwa zake na uchovu alioupata kwa sababu ya safari zenye kumkakamua, hali mbaya za hewa, ukosefu wa mahitaji ya maisha na magumu mengine aliyovumilia katika “utumishi mtakatifu” aliomtolea Yehova.—Warumi 12:1, NW.
16. Ni nini kilichosababisha Paulo awe na “nyakati za usiku za kukosa usingizi” mara nyingi?
16 Katika nyakati za usiku za kukosa usingizi, mara nyingi: Kwa sababu Paulo alitaka sana kuepuka kuwa mzigo wa kipesa juu ya wale aliowahubiri habari njema, yeye alifanya kazi ngumu ya mikono “usiku na mchana,” labda akiwa anakosa usingizi mara nyingi sana. (1 Wathesalonike 2:9, NW) Bila shaka, hayo yote yalihusika katika utendaji wa mtume akiwa ‘mhudumu wa Kristo.’ ‘Nyakati za usiku alizokosa usingizi’ hazikusababishwa na hangaiko juu ya mahitaji ya vitu vya kimwili, kwa maana Yehova anahakikisha kwamba watumishi Wake wanavipata. (Mathayo 6:25-34) Lakini huenda ikawa kwamba nyingine za hizo nyakati za kukesha usiku zilitumiwa katika sala au katika kuwafikiria sana waamini wenzake. (Linganisha Luka 6:12-16; 2 Wakorintho 11:28, 29.) Wakati mmoja aliona ni lazima ahutubie ndugu waliokusanyika “mpaka usiku wa manane” ndiyo, usiku wote “mpaka mapambazuko.” (Matendo 20:7-12, NW) Kuongezea hilo, bila shaka nyingi za hizo nyakati za usiku za kukosa usingizi zilitokana na kujisikia vibaya mwilini, zikatokana na hatari mbali-mbali na magumu mengine yaliyovumiliwa na mtume alipokuwa akifanya huduma yake.
17. Ni wakati gani huenda mtume akawa aliona “njaa na kiu”?
17 Katika njaa na kiu: Inaweza kuwa kwamba Paulo aliona “njaa na kiu” alipokuwa akisafiri katika mikoa isiyo na watu au katika maeneo ya majangwa yenye joto jingi. Huenda nyakati nyingine akawa aliona njaa na kiu kwa sababu ya kuwategemea watu wasiojuana naye au kwa sababu ya vyakula vya kiasi cho chote alichoweza kupata kutokana na kazi zake mwenyewe katika maeneo ya ugenini. Hata hivyo sikuzote Yehova alihakikisha Paulo ameendelea kuwa hai, ingawa vyakula vilikuwa haba nyakati nyingine. Kwa njia kama hiyo, “Mungu wa faraja yote” anawapa chakula watumishi wake wa kisasa.—Zaburi 37:25; Luka 11:2, 3.
18. “Kujiepusha na chakula mara nyingi’’ kungeweza kuwa kunahusiana na nini?
18 Katika kujiepusha na chakula mara nyingi: Hapa (mstari 27) huenda ikawa Paulo alikusudia kutofautisha “njaa ya kiu” inayoonwa bila kukusudia na “kujiepusha na chakula [kwa halisi, kufunga kula] mara nyingi” kunakofanywa kwa makusudi. Nyakati fulani huenda akawa alifunga kwa kutaka mwenyewe, kama wakati alipokuwa akijiwekea kando wakati wa kusali au kutimiza mambo mazito sana ya kiroho. (Linganisha Matendo 13:3; 14:23.) Lakini ikiwa alikuwa akitaja magumu tu hapa, basi alimaanisha kukaa bila kula pasipo kukusudia, labda kwa sababu ya ugonjwa, kama wa kuhara damu, au kukosa mahitaji ya maisha katika huduma yake. (Linganisha 2 Wakorintho 6:5.) Bila shaka, wakati Paulo alipofunga safari fulani za kihuduma huenda akawa alijua kwamba chakula na maji yangekuwa haba au yasingepatikana. Lakini hakuacha jambo hilo limzuie kusogeza mbele faida za Kikristo.—Wafilipi 4:12.
19. Ni chini ya hali gani huenda Paulo akawa alivumilia “baridi na uchi”?
19 Katika baridi na uchi: Magumu ya baridi na hali ya kuwa “uchi” akilinganishwa na watu wa siku hizo, yalivumiliwa na mtume pia. Lakini ‘hakuvaa isivyotosha’ kwa sababu ya uvivu. Paulo alifanya kazi kujitimizia mahitaji yake. (1 Wakorintho 4:11, 12; linganisha Matendo 20:33, 34.) “Baridi na uchi” ni magumu ambayo mtume aliyavumilia akiwa amevaa isivyotosha wakati wa mateso, alipokuwa akisafiri katika hali ya hewa yenye upepo mkali na baridi nyingi au alipokuwa akifanya huduma akiwa chini ya hali zenye kutatiza.
‘Vumilia Mpaka Mwisho’!
20, 21. (a) Kwa sababu gani ungesema kwamba Paulo hakuwa ngome ya kibinadamu yenye nguvu? (b) Mashahidi wa Yehova leo wanaweza kulinganishwaje na mtume Paulo?
20 Baada ya mtu kuangalia nyingine za kazi ngumu-ngumu za mtume Paulo, taabu zake, safari zake, hatari na magumu, huenda akamchukua kuwa ngome ya kibinadamu yenye nguvu. Walakini, yeye alikuwa mwanadamu asiye mkamilifu kama kila mmoja wetu. (Warumi 7:21-25) kwa kweli, wapinzani wake Wakorintho walimdharau, wakisema: “Nyaraka zake ni nzito, hodari; bali akiwapo mwenyewe mwilini ni dhaifu, na maneno yake [kuhutubu kwake] si kitu.” (2 Wakorintho 10:10) Kuongezea hilo, Paulo alikuwa na “mwiba katika mwili”—labda ugonjwa wa macho.—2 Wakorintho 12:7; Matendo 23:1-5; Wagalatia 4:15; 6:11.
21 Vivyo hivyo, sisi Mashahidi wa Yehova wa kisasa ni watu wasio wakamilifu, ingawa kama Paulo tunajitahidi sana kumpendeza Mungu. (1 Wakorintho 9:24-27) Ulimwengu unatudharau kama wengine walivyomdharau mtume, ingawa tunahangaikia sana masilahi ya kiroho wanadamu wenzetu. (Mathayo 22:39) Kama Paulo, wengi wetu wana ugonjwa fulani unaowasumbua. Lakini hiyo inatufanya tutegemee zaidi nguvu za Mungu, na katika udhaifu wetu uwezo wake unadhihirishwa zaidi kati ya wale tunaowahubiri.—2 Wakorintho 12:7-10.
22. (a) Tukitakwa tutaabike “kwa ajili ya uadilifu,” tunafarijiwa namna gani na Yehova? (b) Ni kwa njia gani tu tunaweza ‘kuvumilia mpaka?
22 Hakuna shaka kwamba uwezo kutoka juu ulimsaidia Paulo moja kwa moja mpaka kifo chake akiwa mtumishi wa Yehova asiye mkamilifu lakini mwaminifu. (2 Wakorintho 4:7; 2 Timotheo 4:6-8) Kwa kulinganishwa na hali, ni kwa nguvu za Mungu tu sisi tunaweza ‘kuvumilia mpaka mwisho’ wa mfumo huu mbovu wa mambo mpaka tukafe tukiwa na uaminifu. (Zaburi 29:11; Mathayo 10:28; 24:3, 13; Marko 13:13) Tukitakwa tutaabike “kwa ajili ya uadilifu,” tunafarijiwa sana na roho takatifu ya Yehova, ahadi zake zenye thamani kubwa na majibu yake kwa sala zetu. Mambo ya namna hiyo yanatupa uhakika wa kwamba Mungu wa faraja yote” yuko pamoja nasi. Kama mtume Paulo huenda sisi ‘tukatatanishwa sana, lakini tusikose kabisa njia ya kutokea, tukateswa, lakini tusiachwe tukiwa hoi kabisa, tukatupwa chini, lakini tusiangamizwe.’ (2 Wakorintho 4:8, 9, NW) Mungu wetu anatupa uwezo wa kuzitangaza habari njema bila woga kwa kukabili mateso na magumu. Na, kwa uhakika, kwa nguvu za Yehova sisi tunaweza ‘kuvumilia mpaka mwisho.’—Kutoka The Watchtower, December 1, 1982.
Je! unaweza kujibu maulizo haya?
◻ Ni nini maana ya ‘kuvumilia mpaka mwisho’?
◻ Mtume Paulo alimaanisha safari za namna gani aliposema “katika safari mara nyingi”?
◻ Mtume alitiwaje hatarini na “ndugu za uongo,” na Mashahidi wa Yehova wa kisasa kiroho waweze kujikinga na watu wa namna hiyo?
◻ Ni chini ya hali gani Paulo aliona “njaa na kiu,” na pia akapatwa na “baridi na uchi”?
◻ Ingawa sisi ni watu wasio wakamilifu, kama Paulo alivyokuwa, inawezekanaje ‘kuvumilia mpaka mwisho’?
[Picha katika ukurasa wa 15]
Katika safari zake za kihuduma, Paulo alikuwa mara nyingi katika hatari kutokana na wakora wa njiani
[Picha katika ukurasa wa 17]
Paulo alikuwa katika hatari za kutokana na mataifa, kwa mfano katika Listra