Kuvumilia Matendo Mabaya Kwaleta Utukufu
JE! MTU akitukanwa, kutemewa mate, kuchapwa makofi au kupigwa, anapata utukufu? Kwa kawaida matendo ya namna hiyo huaibisha anayetendwa hivyo. Lakini hakuna aibu kuvumilia matendo hayo mabaya ikiwa unatendwa hivyo kwa sababu ya kuwa mwanafunzi mshikamanifu wa Yesu Kristo. Mtume Petro alionyesha waamini wenzake hilo, akisema: “Lakini ikiwa [anateswa] kwa sababu ni Mkristo asione haya, bali amtukuze Mungu katika jina hilo.”—1 Pet. 4:16.
Yaliyompata Paulo yaonyesha mateso ambayo yaweza kupata Mkristo naye aeleza sababu mambo hayo hayakumwaibisha.
Wakati Paulo alipokuwa akitimiza agizo lake kama mtume kwa mataifa, alivumilia mambo mengi—kutiwa gerezani, kupigwa na kukaribia kufa. Karibu na mwaka wa 55 W.K. aliwaandikia Wakristo Korintho akawaambia: “Kwa Wayahudi mara tano nalipata mapigo arobaini kasoro moja. Mara tatu nalipigwa kwa bakora; mara moja nalipigwa kwa mawe; mara tatu nalivunjikiwa jahazi; kuchwa kucha nimepata kukaa kilindini; katika kusafiri mara nyingi; hatari za mito; hatari za wanyang’anyi; hatari kwa taifa langu; hatari kwa mataifa mengine; hatari za mjini; hatari za jangwani; hatari za baharini; hatari kwa ndugu za uongo; katika taabu na masumbufu; katika kukesha mara nyingi; katika njaa na kiu; katika kufunga mara nyingi; katika baridi na kuwa uchi.”—2 Kor. 11:24-27.
Hapa mtume alieleza sehemu tu ya mateso yaliyokuwa yamekwisha mpata karibu miaka mitano au sita kabla hajaandikia Wakristo katika Efeso. Paulo alipojua kwamba Wakristo wengine wa Efeso wangeweza kuogopa wakijua dhiki yote iliyompata alipokuwa ametiwa gerezani Rumi, aliwatia moyo hivi: “Naomba msikate tamaa kwa sababu ya dhiki zangu kwa ajili yenu, zilizo utukufu kwenu.”—Efe. 3:13.
Mtume Paulo alighadhibikiwa na wananchi wenzake kwa sababu ya kufanya kazi sana kati ya watu wasio Wayahudi akiwa mwanafunzi wa Yesu Kristo. Mwishowe jambo hilo lilimfanya atiwe gerezani Rumi. Kwa sababu hiyo angeweza kusema kwamba alitaabikia “Mataifa.” Yeye alikuwa ‘mfungwa wake Kristo Yesu kwa ajili yao.’—Efe. 3:1.
Je! waamini wenzi wa Paulo walipaswa kuogopa au kuaibika kwa sababu ya dhiki iliyompata? Sivyo, bali kudhikishwa kwake kulikuwa utukufu kwao. Kwa njia gani? Kwanza, upendo wa Paulo ulikuwa mwingi sana hata alikuwa amekuwa na nia ya kuwatumikia bila kujali magumu yo yote ambayo yangempata akifanya hivyo. Ni mahali gani pengine katika ulimwengu ambapo waamini hao wangeweza kuonyeshwa upendo mzuri hivyo?
Tena, nia ya mtume ya kuvumilia dhiki ilionyesha Waefeso kwamba mambo waliyokuwa nayo wakiwa Wakristo yalikuwa yenye thamani sana. Walistahili kutaabika, naam, kufa kwa ajili ya tumaini lao na uhusiano wao pamoja na Yehova Mungu na Yesu Kristo. Kama Paulo angalikubali kushindwa alipopatwa na dhiki, angalifanya ionekane kwamba Ukristo haukuwa jambo la maana. Lakini, uvumilivu wake wa uaminifu ulitukuza ukaheshimu Ukristo, kwa maana ulionyesha kwamba watu wangeona kuwa mwanafunzi wa Yesu Kristo kama jambo lenye thamani kuu, linalostahili kuwafanya wajinyime. Hivyo dhiki ya Paulo ilikuwa “utukufu” kwa waamini wenzake.
Ndivyo ilivyo leo. Mateso makali sana yanayowapata wanafunzi wa Yesu Kristo walio washikamanifu yanaletea ushirika mzima wa ndugu utukufu katika dunia yote. Bila shaka, ni jambo lenye kuhuzunisha kusikia kwamba Wakristo waaminifu wamepigwa vibaya sana, wakatendwa vibaya katika viungo vyao vya uzazi na watu wenye ghasia au wakatendwa mabaya mengine. Hata hivyo, uvumilivu wao wa uaminifu unafanya washinde kwa kufuata adili wanapoteswa na watesi wao. Ushindi huo unaongeza fahari na uangavu wa ibada ya kweli. Unatukuza sana Ukristo wa kweli machoni pa watu wenye akili ‘wasioandamana na mkutano kutenda uovu’ bila kufikiri. (Kut. 23:2) Kwa upande mwingine, mtu akikubali kushindwa na watesi, Ukristo unaonekana ni jambo ovyo tu.
SABABU GANI WANATESWA
Wakati mtu anapotaabika au anaposikia wengine wanapata dhiki, huenda akauliza upesi hivi, ‘Sababu ni nini?’ Ndivyo alivyojiuliza Daudi wa kale aliyekuwa mtumishi wa Mungu. Alipozungukwa na maadui, alidhani Mungu alikuwa amemwacha. Kwa sababu alijisikia hakuwa na hatia, aliuliza hivi: “Mungu wangu, Mungu wangu, mbona umeniacha? Mbona U mbali na wokovu wangu?”—Zab. 22:1.
Hata mtu anapojua sababu ya mateso, kuongezeka sana kwa magumu huenda bado kukamfanya aulize, “Sababu gani?” Kwa hiyo ni jambo la maana sana tuwe na maoni yanayofaa juu ya dhiki au mateso. Ama sivyo huenda kuharibika sana kwa hali fulani kukatufanya tufikie maamuzi mabaya.
Wanafunzi waliojitoa wa Yesu Kristo wasishangae wakilazimika kuteseka kwa sababu ya kushikamana kwa uaminifu na Maandiko Matakatifu. “Wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu [watateswa].” (2 Tim. 3:12) Yesu Kristo mwenyewe aliteswa vikali na mwishowe akauawa juu ya mti wa kufishia. Aliwaambia wanafunzi wake hivi: “Ikiwa waliniudhi mimi, watawaudhi ninyi.”—Yohana 15:20.
Sababu ya watumishi wa kweli wa Mungu kuchukiwa sana ni kwamba wanadamu wengine wote wanaongozwa na mungu mwingine, Shetani Ibilisi. Biblia yatuambia hivi: “Dunia yote pia hukaa katika yule mwovu.” (1 Yohana 5:19) Kwa habari ya mtumishi mwaminifu wa Mungu, Ayubu, “mwovu” huyo alidai hivi: “Yote aliyo nayo mtu atayatoa kwa ajili ya uhai wake.” (Ayubu 2:4) Hivyo ndivyo Ibilisi anavyoshikilia kwa habari ya wote wanaotaka kumtumikia Yehova Mungu. Shetani anashikilia kwamba hakuna mtu ye yote anayeongozwa na upendo, bali kwamba wote wanaongozwa na mapendezi yao wenyewe na wanaweza mwishowe kushawishwa wamwache Muumba. Yehova Mungu ameruhusu Shetani awe na wakati wa kuhakikisha dai lake. Adui huyo ametumia mateso, pamoja na tisho la kifo chenye jeuri, ili kujaribu kuvunja ukamilifu wa watumishi wa Mungu.
Kwa kuendelea kuwa waaminifu yajapokuwapo mateso, watu wa Mungu wameshiriki kuhakikisha kwamba adui huyo ni mwongo. Naam, wameweza kuendeleza ukamilifu wao kwa kufahamu suala linalohusika na kumtegemea Yehova awatie nguvu. Wanajua kwamba hata wakiuawa, wanadamu hawawezi kamwe kuzuia wasifufuliwe. Hilo, pamoja na msaada wa roho ya Mungu, limewasaidia watende kupatana na maneno ya Yesu: “Yeye aipendaye nafsi yake ataiangamiza; naye aichukiaye nafsi yake katika ulimwengu huu ataisalimisha hata uzima wa milele.”—Yohana 12:25.
FURAHA WAKATI WA MATESO
Bila shaka, mateso makuu hayaleti furaha. Kunakuwa na huzuni nyingi nyumba zinapoteketezwa kwa moto, shamba linaponyang’anywa, watoto wanapotenganishwa na wazazi wao na wakati wanaume na wanawake wanapotendwa kinyama na hata kuuawa. Hata hivyo mtu aweza kuwa na furaha nyingi ya ndani.
Kuna furaha ya kujua kwamba mtu anafanya yaliyo haki, kushikamana na Mungu wake. Mtu akiendelea kuwa na dhamiri safi ateswapo, anakuwa na uhakikisho kwamba amekubaliwa na Mwenye Nguvu Zote. Mtume Petro alieleza hilo alipoandika hivi: “Mkilaumiwa kwa ajili ya jina la Kristo ni heri yenu; kwa kuwa [roho ya utukufu na ya] Mungu [i]nawakalia.”—1 Pet. 4:14.
Kuamini sana kwamba Mungu “huwapa thawabu wale wamtafutao” kwa bidii kunasaidia sana pia kuongeza furaha ya wale wanaoteswa kwa ajili ya haki. (Ebr. 11:6) Kutumainia thawabu hiyo kunaweza kuleta furaha nyingi sana hata mateso yaliyo makali zaidi yaonekane si kitu. Ndivyo Maandiko yanavyoeleza: “Maana dhiki yetu nyepesi, iliyo ya muda wa kitambo tu, yatufanyia utukufu wa milele uzidio kuwa mwingi sana.”—2 Kor. 4:17.
Ndivyo Yesu Kristo alivyoifikiria thawabu. Mfano wake waweza kututia moyo kweli kweli tuvumilie kwa uaminifu. Biblia yatusihi ikisema, “Na tupige mbio kwa saburi katika yale mashindano yaliyowekwa mbele yetu, tukimtazama Yesu, mwenye kuanzisha na mwenye kutimiza imani yetu; ambaye kwa ajili ya furaha iliyowekwa mbele yake aliustahimili [mti wa mateso] na kuidharau aibu, naye ameketi mkono wa kuume wa kiti cha enzi cha Mungu. Maana mtafakarini sana yeye aliyeyastahimili mapingamizi makuu namna hii ya watendao dhambi juu ya nafsi zao, msije mkachoka, mkizimia mioyoni mwenu.”—Ebr. 12:1-3.
Kama vile katika habari ya Yesu Kristo, hakuna kitu kinachoweza kuzuia Yehova Mungu asithawabishe mtu mwaminifu, hata mtu huyo akifa. Mtume Paulo aliwaandikia Wakristo katika Rumi akawaambia, “Nimekwisha kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.” (Rum. 8:38, 39) Upendo wa Mungu waonekana anaposaidia watumishi wake sasa, na utaonekana pia atakapowapa thawabu iliyo kubwa zaidi ya zote—uzima wa milele wakiwa watu wanaokubaliwa naye. Ni furaha gani nyingine inayoweza kuzidi hiyo! Je! hatupaswi kuvutwa na furaha hiyo tuendelee kuwa waaminifu hata tupatwapo na mateso makali sana?
Tuwe ni sisi wenyewe tunaoteswa au wawe ni wengine, yatupasa tukumbuke sana suala halisi linalohusika. Tusiogope kamwe kiasi cha kusimama upande wa adui kwa kuvunja ukamilifu. Bali, sikuzote na tufahamu kwamba kuvumilia kwa uaminifu tunapoteswa kwaletea jina la Yehova utukufu na kuunga mkono upande wake wa suala linalohusika. Kwaletea ushirika mzima pia wa ndugu utukufu. Tukivumilia, tunaweza kwa uhakika na furaha kutazamia thawabu tukufu—uzima wa milele tukiwa watumishi waliokubaliwa wa Yehova Mungu na wanafunzi washikamanifu wa Mwanawe.