Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 10/1 kur. 9-13
  • Wakristo Wanaelekeana na Mateso kwa Uvumilivu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Wakristo Wanaelekeana na Mateso kwa Uvumilivu
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kujitayarishia Mateso
  • Kuelekeana Nayo kwa Uvumilivu
  • Ukatili wa Shetani Ni Kazi-Bure
  • Muumba Wetu Hatakosa Kutusaidia
  • Wenye Furaha Wajapoteswa!
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Kunyanyaswa kwa Ajili ya Uadilifu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Kuvumilia kwa Furaha Ijapokuwa Mateso
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Unaweza Kuvumilia Mateso
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 10/1 kur. 9-13

Wakristo Wanaelekeana na Mateso kwa Uvumilivu

1, 2. Mashahidi washikamanifu wa Yehova wanaelekeanaje na mateso, lakini ni ulizo gani linalotokezwa na jambo hilo?

MASHAHIDI WA YEHOVA hawajitafutii kufia imani. Lakini, wao wanajua kwamba “wale wote wanaotamani kuishi maisha ya utawa katika ushirika pamoja na Kristo Yesu watateswa pia.” (2 Timotheo 3:12, NW) Je! jambo hilo linawashusha moyo?

2 Hapana, kwa maana Wakristo washikamanifu wanaweza ‘kuelekeana na mateso kwa uvumilivu.’ (1 Wakorintho 4:2, The Twentieth Century New Testament, Chapa Iliyosahihishwa) Lakini sisi tunaweza kujitayarishaje kwa taabu za namna hiyo kabla hazijatupata?

Kujitayarishia Mateso

3. Ni nini nyingine za njia za kujitayarishia mateso?

3 Mazungumzo yetu yaliyotangulia yalionyesha njia zinazoweza kutumiwa ili kujitayarishia mateso. Kwa mfano, tunahitaji kukumbuka shabaha ya Ibilisi ni nini​—kuangamiza uhusiano wetu pamoja na Yehova. Kwa fadhili zisizostahilika, tusimruhusu kamwe afanye hivyo! Tunaweza pia kujitayarishia mateso tukifikiria sababu ya Mungu ya kuyaruhusu. Yeye anafanya hivyo kwa sababu hasa ya lile suala la enzi kuu ya ulimwengu mzima, na pia ili kujaribu ushikamanifu wetu. Kwa hiyo, na tuamue mapema kwamba, kwa msaada wa kimungu, tutakuwa wateteaji washikamanifu wa enzi kuu ya Yehova. Tena, tunaweza kuwa tumejitayarishia mateso ikiwa lile tumaini la Ufalme liko ndani ya moyo wetu.

4, 5. Katika kujitayarisha kabla mateso hayajatujia, tunaweza kujengaje imani yetu?

4 Katika kujitayarisha kabla mateso hayajatupata, tunahitaji kila siku kujenga imani yetu, ushujaa na uvumilivu wetu. Lakini, ikiwa tutakuwa na imani ya kweli, ni lazima tumpende Yehova kikweli, na kufanya hivyo kunahitaji tuwe na maarifa sahihi ya kulijua Neno lake. Halafu kufanya hivyo nako kunataka tusome na kujifunza Maandiko kwa ukawaida pamoja na vichapo vya Kikristo vinavyohusiana nayo. Zaidi ya hilo, imani yenye nguvu inahitaji pia tuwe na ushirika pamoja na waamini wenzetu katika ibada na utumishi wa Yehova.​—Waebrania 10:23-25; 12:28; Ufunuo 7:9, 10, 15.

5 Ili kujitayarishia mateso, tunahitaji pia ‘kuendelea kutembea katika ile kweli,’ kuishi kupatana nayo kila siku, sikuzote ‘kupewa mwongozo na ile Kweli.’ (3 Yohana 3, 4, NW; TCNT) Kwa kukubali mwongozo wa Mungu tunapoelekeana na majaribu madogo-madogo siku baada ya siku, tutajenga imani yetu katika Yehova na katika njia zake. Kuukubali nako kutatusukuma ‘tupewe mwongozo na ile Kweli’ wakati tunapoteswa.

6. Sala inaweza kutusaidiaje tujitayarishie mateso?

6 Tukifanya iwe desturi yetu kumpelekea Yehova sala kwa ukawaida tutamkaribia zaidi, nalo hilo litatusaidia pia kujitayarishia mateso. Kadiri tutakavyozidi kumtegemea kwa sala Baba yetu wa kimbingu, ndivyo tutakavyozidi kumtumaini. (2 Wakorintho 1:8-10) Hivyo uhusiano wetu pamoja naye utapata nguvu nyingi sana hata usiweze kuangamizwa na maadui, wa kibinadamu au wa kishetani.​—Linganisha Zaburi 9:1-6; 1 Yohana 2:12-14.

Kuelekeana Nayo kwa Uvumilivu

7. Tunapoteswa, Mungu anaweza kufanya nini ikiwa nguvu zetu wenyewe zimekwisha?

7 Wakati mateso yanapotupata kikweli, hasa yakiwa ya kinyama, ni jambo gani linaloweza kufanywa ili kuelekeana nayo kwa uvumilivu? Nguvu kutoka kwa Yehova zinahitajiwa kabisa! Tunahitaji “uwezo unaozidi ule wa kawaida” kama Paulo, na inatupasa kusali tuupate. (2 Wakorintho 4:7-12, NW) Halafu, tukiwa na tegemeo kamili juu ya Baba yetu wa kimbingu, tunaweza kuwa na tumaini hakika sawa na alilokuwa nalo Paulo alipokuwa akisema hivi: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu [Yehova Mungu].” (Wafilipi 4:13) Hata nguvu zetu wenyewe za kimwili zikiisha, akiba ya Yehova ya nguvu haitamalizika. Yeye anaweza kuwapa na kweli anawapa watu wake uwezo. (Isaya 40:28-31; 45:22-25) Tukimwegemea Yehova, yeye atatupa nguvu zinazozidi zile tunazoweza kutumia nyakati za mkazo. Tena tusiogope. Analoweza kufanya mwanadamu ni kuondoa uhai wetu wa sasa tu, lakini Yehova ana uwezo wa kuturudishia uhai kwa ufufuo.​—Zaburi 46:1, 2; Luka 12:4-7; Yohana 5:28, 29.

8. Kwa sababu gani sala ni ya maana sana katika kuelekeana na mateso kwa uvumilivu?

8 Sala kwa Yehova haiwezi kabisa kuwekwa kando katika kuelekeana na mateso kwa uvumilivu. Yesu, aliyepatwa na mambo mengi ya kumtaabisha, alikaa sikuzote akiwa na uhusiano wa karibu na Babaye kwa sala za kutoka moyoni, kwa maana tunasoma hivi: “Siku hizo za mwili wake, [Kristo] alimtolea yule, awezaye kumwokoa na kumtoa katika mauti, maombi na dua pamoja na kulia sana na machozi, akasikilizwa kwa jinsi alivyokuwa mcha Mungu.” (Waebrania 5:7) Tunahakikishiwa kwamba “Msikiaji wa sala” atatusikia pia kwa sababu ya kicho chetu cha kimungu. (Zaburi 65:2, NW) Wakati wa mateso kuna uhitaji mkubwa sana wa ‘kudumu katika sala,’ ‘kuomba bila kukoma,’ ‘kukesha katika sala.’ (Warumi 12:12; 1 Wathesalonike 5:17; 1 Petro 4:7) Ama sivyo, huenda tukafikiria masumbuko na taabu tunazopata, na huenda tukajilegeza tuvutwe na tamaa ya kutaka faraja, tufuate maelekeo ya mwili kwa kukubali kukana imani yetu.

9, 10. (a) “Amani ya Mungu” inaweza kutusaidiaje tunapoteswa? (b) Tunaweza kujifunza nini kutokana na utulivu wa Stefano wakati alipoelekeana na watesi wake?

9 Tafuta “amani ya Mungu” unapokuwa katika vifungo au unapotendwa jeuri. Ikiwa tumempelekea Yehova sala kila siku, tumeimarisha mfano mzuri maishani na inatupasa kuendelea kumfikia kwa bidii tunapoteswa. Inafaa kusali tupewe “amani ya Mungu inayoshinda mawazo yote.” Hiyo ‘italinda mioyo yetu na nguvu zetu za akili kupitia Kristo Yesu’​—moja kwa moja mpaka kifo cha uaminifu ikiwa lazima.​—Wafilipi 4:6, 7, NW.

10 Kisa cha Stefano mwaminifu, aliyekuwa Mkristo wa kwanza kuuawa kwa sababu ya imani, kinaonyesha kwamba tunaweza kuupata utulivu huo usioshindwa na jambo lo lote. Muda mfupi tu kabla roho takatifu haijamwongoza kutoa ushahidi wa mwisho kwa ushujaa, masimulizi ya Biblia yanasema kwamba: “Wakati wote wale waliokuwa wameketi katika ile Sanhedrini walipomkazia macho, waliona kwamba uso wake ulikuwa kama uso wa malaika.” (Matendo 6:15, NW) Yeye hakuwaonyesha uso wenye kuinama chini kwa sababu ya kutenda kosa, bali aliwaonyesha sura ya malaika, mjumbe wa Mungu, akiwa na uhakika kwamba Yehova alikuwa akimwunga mkono. Stefano alikuwa shujaa na mtulivu. (Linganisha Yohana 14:27.) Baada ya yeye kufunua wazi kwamba walikuwa na hatia katika kumwua Yesu Kristo, mahakimu “wakachomwa mioyo, wakamsagia meno.” Lakini Stefano, ‘akijaa roho takatifu, akakaza macho yake, akitazama mbinguni, akauona utukufu wa Mungu, na Yesu akisimama upande wa mkono wa kuume wa Mungu.’ Kwa kutiwa nguvu na njozi hiyo, Stefano aliweza kuelekeana na mahakimu hao dhalimu akiwa na ushujaa na uhakika wa kwamba alikuwa amefanya mapenzi ya Yehova. (Matendo 7:52-56) Ingawa leo Wakristo hawatazamii kuona njozi kama hiyo, wanaweza kupata utulivu kwa Mungu wanapoelekeana na mateso kwa uvumilivu.

11. Ni kutafakari juu ya nini kunakoweza kusaidia watu wa Yehova wavumilie mateso?

11 Tafakari juu ya Neno la Yehova, matendo na makusudi yake kwa watu. Hata ukinyimwa Biblia na vichapo vinavyoeleza Maandiko, wewe endelea kuweka fikira juu ya Neno la Mungu. Kumbuka mistari na masimulizi ya Biblia, ufanye hivyo mchana kutwa na nyakati za usiku unapokosa usingizi. (Linganisha Zaburi 77:2, 6,11,12.) Fikiria matendo mazuri ajabu ambayo Yehova alitendea watu wake walioteswa na kuonewa zamani zilizopita. Kwa mfano, fikiria vile Mungu alivyowakomboa Waisraeli kutoka utumwa wa Misri, akamsaidia Danieli na washirika wenzake watatu wa Kiebrania katika majaribu yao, akaokoa Wayahudi wasiuawe siku za Mordekai na Esta, na kuwatetea mitume na Wakristo wengine wa kwanza katika taabu walizopata kwa ajili ya uadilifu. (Kutoka 12:1-15:21; Danieli 3:1-30; 6:1-28; Esta 3:1–9:32; Matendo 4:1–5:42; 12:1-17; 14:1-7, 19, 20; 16:16-40; 18:12-17; 19:23-41; 21:26–26:32) Fikiria pia vile Yehova amesaidia watumishi wake wa kisasa katika kambi za mateso za Nazi, katika magereza ya kikomunisti na kadhalika. Wakati waabudu wa Yehova wanapoteswa, wanaweza kuona “mikono ya milele” ya Mungu ikiwategemeza.​—Kumbukumbu la Torati 33:27, An American Translation.

12. Tunapoteswa, tunapaswa kukumbuka nini juu ya kutaabika kwetu, na imetupasa tuwe na tumaini na uhakika gani?

12 Kutaabika kutamalizika. Kukumbuka jambo hilo kutatusaidia pia tuelekeane na mateso kwa uvumilivu. Tena, ‘Mungu atawalipa mateso wale watutesao,’ na kwa upande mwingine atupe sisi faraja. (2 Wathesalonike 1:6-10) Basi, wakati tunapotendwa mambo ya kututaabisha tukiwa Mashahidi wa Yehova, inatupasa tuutazame wakati ujao, tukiwa na uhakika kwamba magumu yetu yatakoma na uaminifu wetu utafanya Baba yetu wa kimbingu atupe baraka nyingi. Kwa mfano, baada ya muda fulani huenda tukafunguliwa gerezani kisha tufurahie tena uhuru wa kumtumikia yeye bila kizuizi tukiwa watangazaji wa Ufalme wenye furaha nyingi. Lakini hata isipofanyika hivyo upesi, kutaabika kwetu hakutaendelea milele. Na tunaweza kuvumilia hali hiyo tukimtumaini kabisa Yehova na kudumisha uhakika wetu katika utimizo wa ahadi yake ya kuleta baraka zisizolinganika katika Taratibu Mpya iliyotabiriwa.​—Ufunuo 21:1-4; linganisha 2 Wakorintho 1:19, 20.

13. Wakati wa mateso, tunaweza kupata faraja gani katika 1 Wakorintho 10:13?

13 Mungu hataturuhUsu tujaribiwe kupita kipimo tunachoweza kuvumilia. Mtume Paulo alitoa uhakikisho huo alipoandika hivi: “Jaribu halikuwapata ninyi, isipokuwa lililo kawaida ya wanadamu; ila Mungu ni mwaminifu; ambaye hatawaacha mjaribiwe kupita mwezavyo; lakini pamoja na lile jaribu atafanya na mlango wa kutokea, ili mweze kustahimili.” (1 Wakorintho 10:13) Si Wakristo wote wanaotakwa kuvumilia hali zenye kutaabisha za namna ile ile. Kwa hiyo, hakuna sababu ya kufikiri kwamba pasipo shaka kila mmoja wetu ataletewa mateso ya kinyama kabisa. Yehova hatakosa kutusaidia wala hataruhusu kitu cho chote kitujie ambacho sisi mmoja mmoja hatuwezi kuvumilia kwa nguvu zake na nguvu za roho takatifu yake. Bila shaka, ni lazima tumtegemee yeye kabisa kabisa na kuamini yanayosemwa na Neno lake. Hata hivyo, tukimtumaini kabisa Yehova tunaweza kweli kuelekeana na mateso kwa uvumilivu.​—Zaburi 9:9, 10.

Ukatili wa Shetani Ni Kazi-Bure

14, 15. Shetani amepingwaje katika majaribio yake ya kumaliza watu wa Yehova kupitia mateso?

14 Kwa sababu mashahidi waaminifu wa Yehova wanaelekezwa na kusaidiwa kwa nguvu nyingi na Mungu wao asiyelinganika na mwenye nguvu zote, Shetani Ibilisi na wajinga wake anaowatumia kuleta mateso hawatawashinda kamwe Wakristo hao wa kweli. Mara nyingi majaribio ambayo Ibilisi amepanga ili awamalize watu wa Yehova kupitia mateso yamezuiwa yakapanguka. Kwa kweli, mara nyingi mateso yameruka yakamrudia huyo Adui mkubwa zaidi wa Yehova na wa watu Wake, kisha mapenzi ya kimungu yakashinda.

15 Kwa kuthibitisha jambo hilo, fikiria ile “adha kuu” iliyolipata kundi katika Yerusalemu mara tu baada ya Stefano kuuawa kwa ajili ya imani. Tunaambiwa hivi: “Wote wakatawanyika katika nchi ya Uyahudi na Samaria, isipokuwa hao mitume.” Lakini wanafunzi waliotawanyika ‘walienda huko na huko wakihubiri’ habari njema za lile neno, na jitihada zao zilibarikiwa. Kwa mfano, kulikuwa na ufanisi wa kiroho katika mji wa Samaria. (Matendo 8:1-8) Wanafunzi wengine waliotawanyika walihubiri katika Foinike, Kipro na Antiokia, Shamu. Ndiyo, katika Antiokia “mkono wa Yehova ulikuwa pamoja nao, na hesabu kubwa ambao walipata kuwa waamini walimgeukia Bwana”! (Matendo 11:19-21, NW) Ni jambo la uhakika kwamba tukio hilo lilileta matokeo tofauti kabisa na yale yaliyotamaniwa na yule Mtesi Mkuu aliyepingwa katika makusudi yake.​—Linganisha Wafilipi 1:12-14.

16. Nyakati nyingine ni nini linalotukia kwa habari ya watesi?

16 Kila wakati shahidi mshikamanifu wa Yehova anapoelekeana na mateso kwa uvumilivu, hiyo inamwongezea Shetani aibu, kuonyesha yeye ni mwongo. Zaidi ya hilo, wakati mtu aliyekuwa mtesi anapokuwa shahidi wa Mungu na Kristo aliye mwaminifu na mwenye kuteswa, kisha mtu huyo anaendelea kuwa shahidi, hapo Ibilisi anakuwa amepata aibu ya kushindwa. Kwa mfano, bila shaka yeye hakupendezwa wakati Sauli wa Tarso aliyekuwa mtesi hapo kwanza alipogeuka akawa mmoja wa wafuasi wa Yesu wenye kuteswa ambao walifanya kazi ngumu kwa bidii sana ya kueneza habari njema kujapokuwako mateso na hali nyingi zenye kutaabisha.​—2 Wakorintho 11:23-27; 1 Timotheo 1:12-16.

17. Inawapasa Mashahidi wa Yehova wenye kuteswa wawe na nia gani kuelekea watesi wao?

17 Basi, ni jambo la maana sana Mashahidi wa Yehova wanaoteswa wawe na nia inayofaa kuelekea watesi wao. Stefano hakujawa na chuki juu ya wale waliomtesa. Kwa kweli, walipokuwa wakimpiga kwa mawe alipiga magoti na, muda mfupi tu kabla hajalala usingizi wa kifo, “alilia kwa sauti yenye nguvu: ‘Yehova, usihesabu dhambi hii juu yao.’ “(Matendo 7:57-60, NW) Zaidi ya hilo, Yesu alisema: “Endeleeni kupenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.”​—Matendo 5:44, NW; Warumi 12:14; 1 Wakorintho 4:11-13.

Muumba Wetu Hatakosa Kutusaidia

18. Ni jambo gani litakalotukia wakati Shetani atakapofanya shambulio lake la mwisho juu ya watu wa Yehova?

18 Sasa sisi tunaishi katika wakati wa hatari iliyo kubwa zaidi ya zote za historia ya kibinadamu. Ni kipindi cha kujaribu na kuchuja (kuchunga) wenye kujiita Wakristo. (Linganisha Luka 22:31, 32; 1 Petro 4:16, 17.) Wakati wa Shetani ni mfupi, na karibuni atafanya shambulio lake la mwisho juu ya watu wa Yehova, akiwa amejikaza kweli kweli. Lakini Mungu atawawezesha waelekeane na mateso hayo kwa uvumilivu, nao watashinda. Kwa mara nyingine tena, hapo Shetani (akiwa Gogu wa Magogu) atakuwa amepingwa katika mipango yake na kupata ushinde wa kugandamizwa kabisa. Tena, katika uteteaji huo wa watu Wake, Mungu ‘atajitukuza na kujitakasa mwenyewe, ajifanye ajulikane mbele ya macho ya mataifa, ili kwamba wapaswe kujua yeye ni Yehova.’ Hapo tena, mambo yatakuwa yamekwenda tofauti kabisa na vile Shetani angetamani yaende.​—Ezekieli 38:14–39:7, NW; Ufunuo 12:12.

19. Kwa msaada wa kimungu, Mashahidi wa Yehova wenye kuteswa watafanya nini?

19 Sisi mashahidi tuliojiweka wakf kwa Yehova tunajua kwamba Shetani anatamani kuangamiza uhusiano wetu na Mungu Mweza Yote. Lakini, kwa fadhili zisizostahilika za Mungu, sisi hatutakubali kukana imani yetu. Bali, tutalikumbuka lile suala kuu na kujaribu kwa kila njia kutetea enzi kuu ya ulimwengu mzima ya Yehova. Tukiwa na uhakika katika lile tumaini la Ufalme, tunaweza kufurahi tujapoteswa. Sisi tuko tayari kuelekeana na mateso kwa uvumilivu, kwa maana tunamtumaini kabisa kabisa “yeye awezaye kufanya mambo ya ajabu mno kuliko yote tuyaombayo au tuyawazayo.”​—Waefeso 3:20, 21.

20. Tunaweza kuwa na tumaini gani hakika katika “Muumba mwaminifu’’ wetu?

20 Basi, acheni sisi tuwe watu wasioogopa adui, tushike ukamilifu, kisha Mungu atapata utukufu na sisi tutajipatia wokovu wetu wenyewe. Na ‘tumtumaini Yehova na kushika njia yake.’ (Zaburi 37:34, NW) Tunapovumilia mateso, na tuonyeshe ile nia inayoonekana wazi katika maneno ya mtume Petro: “Acheni wale wanaotaabika kupatana na mapenzi ya Mungu waendelee kukabidhi nafsi zao kwa Muumba mwaminifu wakati wao wanapotenda mema.” (1 Petro 4:19, NW) “Muumba mwaminifu” wetu hatakosa kutusaidia. Kwa nguvu zake, sisi tunaweza kuwa wenye furaha tujapoteswa na tunaweza kuelekeana na mateso kwa uvumilivu.

Maulizo ya Kujikumbusha

□ Mashahidi wa Yehova wanaweza kujitayarishiaje mateso?

□ Katika kuelekeana na mateso, kwa sababu gani sala ni ya maana sana?

□ “Amani ya Mungu’’ inaweza kutusaidiaje tunapoteswa?

□ Ni faraja gani inayoweza kupatwa katika 1 Wakorintho 10:13?

□ Mashahidi wa Yehova wana nia gani kuelekea watesi wao, na kwa sababu gani?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Stefano hakuchukia watesi wake, na mashahidi wa kisasa wa Yehova hawachukii watesi wao. Baadaye watesi wengine wanakuwa Mashahidi

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki