Kuvumilia kwa Furaha Ijapokuwa Mateso
“Na tushangilie tunapokuwa katika dhiki, kwa kuwa tunajua kwamba dhiki inatokeza uvumilivu; nao uvumilivu, hali inayokubalika; nayo hali inayokubalika, tumaini, na tumaini haliongozi kwenye kukata tamaa.”—Warumi 5:3-5, NW.
1. Kama matokeo ya mateso ya Wakristo katika hizi “siku za mwisho” ni jambo gani linaloonekana wazi?
MAMBO ambayo yamewapata watu wa Yehova katika hizi “siku za mwisho” kwa hakika yamethibitisha maneno ya Yesu ni ya kweli: “Ninyi ni wenye furaha wakati wo wote watu wanapowachukia, na wakati wo wote wanapowakataa na kuwasuta na kulitupilia mbali jina lenu kuwa ni ovu kwa ajili ya Mwana wa mtu. Furahini katika siku hiyo na kuruka, kwa maana, tazama! zawadi yenu ni kuu katika mbingu, kwa maana ayo hayo ndiyo mambo babu zao walikuwa wakiwatenda manabii.” (Luka 6:22, 23, NW; 2 Timotheo 3:1) Ndiyo, watumishi wa Mungu wanaweza kuvumilia kwa uaminifu namna zote za mateso, na kufanya hivyo kwa furaha.
2. (a) Je! wale wanaopatwa na mateso zaidi wanapokea zawadi kubwa zaidi? (b) Ni nini baadhi ya matokeo yenye faida ya kuvumilia mateso kwa kufaulu?
2 Si kwamba tunafurahia kuteswa, kwa maana mateso hayapendezi na mara nyingi ni yenye uchungu. Si mateso yenyewe, bali matokeo yake ndiyo yanatupa sababu ya kufurahi. (Yakobo 1:2, 3) Wakristo hawataki kuteswa. Hawajaribu kuwa wafia-imani, na kufikiri kwamba kwa kadiri wanavyovumilia mateso mengi ndivyo watakavyokuwa na sifa nyingi machoni pa Baba yao wa kimbingu. Wale wanaopatwa na mateso zaidi hawapokei zawadi kubwa zaidi, wala kwa lazima wao si waaminifu zaidi ya wale ambao wamepatwa na mateso madogo zaidi. Lakini ebu angalia mfuatano wa mambo yanayotokea wakati Mkristo anavumilia dhiki kwa kufaulu: “Dhiki inatokeza uvumilivu; nao uvumilivu, hali inayokubalika; nayo hali inayokubalika, tumaini, na tumaini haliongozi kwenye kukata tamaa.”—Warumi 5:3-5, NW.
3. (a) Kama inavyoonyeshwa katika Warumi 5:3, dhiki inatokezaje uvumilivu? (b) Jambo hilo linaletaje matokeo yenye kutia nguvu imani yetu? (Waebrania 10:38, 39)
3 Tunaposoma juu ya mateso ambayo Wakristo wenzetu wanapata katika sehemu fulani, huenda tukataka kujua hivi, “Mimi ningeweza kuvumilia hayo?” Lakini, wakati upinzani au majaribu yanatujia kwa ghafula, na tukimgeukia Mungu atupe msaada, mahali pa kushindwa au kuacha kumtumikia yeye, tunaona kwamba yeye anajibu sala zetu, na tunajionea jinsi dhiki inavyotokeza uvumilivu. Halafu hatujiulizi-ulizi tena kama tungeweza kuyavumilia; tunajua tunaweza, kwa nguvu za Yehova. Huenda jaribu likawa halikuwa kali sana, lakini hata hivyo imani yetu imejaribiwa, na inakuwa yenye nguvu zaidi ya jaribu la namna hiyo. Huenda jaribu linalofuata likawa gumu zaidi, lakini imani yetu pia ina nguvu zaidi kwa sababu hatukushindwa na lile la kwanza. Kwa hiyo kwa nguvu za Yehova tunaweza kweli kweli kukabili jaribu lo lote la imani yetu tukijua kwamba yeye hataruhusu tujaribiwe kupita yale tunayoweza kuvumilia; wala hatatuacha “bila msaada.”—1 Wakorintho 10:13; 2 Wakorintho 4:8-10, NW.
4. Baada ya kuvumilia kwa kufaulu jaribu au mateso, tunakuwa na sababu gani halisi za kufurahi?
4 Kweli kweli kuvumilia dhiki ni sababu ya kushangilia. Tunaweza kuwa wenye furaha kwamba hatukushindwa na jaribu bali tulishikilia imara yaliyo haki. Tunajua hayo ndiyo Mungu anakubali, kwa hiyo uvumilivu wetu uliofaulu umetuleta karibu zaidi naye, na hiyo ni sababu zaidi ya kufurahi, kama inavyoonyeshwa wazi sana katika Yakobo 1:12.
Mateso ni ya Namna Nyingi
5. Katika nchi nyingi hali ikoje kwa habari ya mateso na kutaabishwa-taabishwa kwa ndugu zetu? Kwa sababu gani iko hivyo? (Amosi 7:10-17)
5 Leo kazi ya Mashahidi wa Yehova iko chini ya vizuizi katika nchi zaidi ya 40, na katika nyingi ya sehemu hizo watu wa Mungu wamelazimika kuvumilia majaribu na mateso makali sana kwa sababu tu wameazimia kumtumikia Mungu wao, Yehova, kwa uaminifu. Katika visa vingi marufuku imechochewa na viongozi wa kidini, ambao wamesingizia kutojiingiza kwetu katika siasa ili kukomesha kazi yetu ya kuhubiri. Maofisa wanaojua mambo yalivyo, wanafahamu kwamba Mashahidi wa Yehova hawana nia ya kupindua wala si hatari kwa Serikali katika njia yo yote. Maofisa wa serikali wenye ufahamu wanajua Mashahidi ni raia waaminifu wenye kutii sheria ambao wanafanya yote wawezayo kutegemeza na kutii sheria za nchi. Hata hivyo, kwa habari ya Mashahidi wa Yehova, utii kamili kwa Mungu ndilo jambo la kwanza. Kwa hiyo, hawashiriki katika siasa za nchi yo yote. Kwa hiyo kukiwako kupingana na sheria za Mungu, wao, kama mitume, ‘wanatii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’—Matendo 5:29, NW.
6. (a) Ni baadhi ya mifano gani ya mateso ambayo Mashahidi wa Yehova wamelazimika kuvumilia? (b) Je! unaweza kusimulia juu ya hali kama hizo katika wakati huu?
6 Vikundi vya watu wenye kufanya ghasia wasiofuata sheria, nyakati nyingine wakiwa wanaongozwa na viongozi wa kidini au watu wenye kufuata siasa bila kufikiri, wametendea watu wa Yehova kwa uonezi mahali kwingi. Wengi wa ndugu zetu wa kiroho wamelazimishwa waache nyumba zao na mali zao na kukimbia ili waokoe maisha zao, kama ilivyotokea katika miaka ya karibuni katika Malawi na Ethiopia. Wengine wameachishwa kazi zao au kufukuzwa katika mahali pao pa kazi, na wengine wamelazimishwa kufunga biashara zao kwa sababu tu wao ni Mashahidi wa Yehova. (Ufunuo 13:16, 17) Mikutano yao ya Kikristo ya kujifunza Biblia imeingiliwa na kusimamishwa; msako umefanywa katika nyumba zao na Biblia na vitabu vya Biblia vimetwaliwa. Maogopesho na vitisho vimetumiwa ili kujaribu kuwatia woga, na wengi wamekamatwa na kufungwa gerezani, hata wengine wameuawa. Mateso yalikuwa makali sana hasa wakati wa vile vita vya ulimwengu, lakini hata sasa hivi yanaendelea katika nchi nyingi.
7. Hata katika nchi ambazo hakuna mateso yanayoletwa na serikali, watu wengi wa Mungu wamelazimika kuvumilia hali gani?
7 Vilevile duniani pote, maelfu ya ndugu na dada zetu wanalazimika kukabili upinzani na mateso kila siku kutoka kwa jamaa zao na watu wao wa ukoo kwa sababu ya kutaka kumtumikia Yehova wakiwa wanafunzi wa Yesu Kristo. Ni kama alivyotabiri Yesu: “Na adui za mtu [watakuwa] wale wa nyumbani mwake.”—Mathayo 10:35, 36.
Lengo la Mateso
8. Je! Mashahidi wa Yehova wanateswa kwa sababu wao ni wahalifu?
8 Watesi wa watu wa Mungu wanatumaini kutimiza nini? Je! wao wanawatesa mashahidi wake kwa sababu wao ni watenda maovu au ni wahalifu? La, hasha. Mashahidi wa Yehova wanatambuliwa ulimwenguni pote kuwa watu wenye kutii sheria ambazo ni zenye adili. Wao ni wafanya kazi wazuri, wanapendeza, ni wenye urafiki, ni wenye fadhili na wenye kujadilika nao hawatendi kama watu wenye kufuata dini bila kufikiri. Kwa kweli, wao ni watu bora wa kuwa jirani. (Tito 2:6-10; Wagalatia 6:9, 10) Ujumbe wao ni wa amani, wenye kufariji wale wanaotaabika na kuomboleza. Wanahubiri “habari njema” kwamba ufalme wa Mungu karibuni utawaondoa waonezi wote na kuleta mfumo mpya wa haki.—Mathayo 6:9, 10; Zaburi 37:10, 11.
9. Wapinzani wanataka kukomesha utendaji gani wetu, na kwa sababu gani?
9 Hata hivyo, kuhubiri kwa hizi “habari njema” kunafunua kwamba viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo hawana ujumbe wa tumaini wo wote wa kuwapa watu. Kwa hiyo wanajaribu kuwanyamazisha wale wanaouhubiri! Ingawa viongozi wengine wa serikali wana nia ya kuruhusu watu wa Yehova waamini wanayotaka, wao pia wanakataa wakihubiri wengine. Kama vile viongozi wa kidini Wayahudi ambao walikuwa wanakabili utendaji wa juhudi wa Wakristo wa kwanza, ni kama kwamba wanasema: “Na tuwatishe wasiseme tena na mtu awaye yote kwa jina hili [la Yesu].” (Matendo 4:17,18) Ndiyo, wanataka kukomesha kuhubiri kwetu.—Ona pia Matendo 5:28, 40.
10. (a) Licha ya kujaribu kukomesha kazi yetu ya kuhubiri, Shetani anataka kutimiza jambo gani? (b) Jambo hilo linaonyeshwaje na namna ya marufuku ambayo mara nyingi inawekwa juu ya utendaji wetu?
10 Kumbuka pia, kwamba mchochezi halisi wa mateso ni Shetani Ibilisi. (1 Petro 5:8) Yeye anataka kukomesha kuhubiri kwetu na pia anataka kudhoofisha imani yetu na kutufanya tuvunje ukamilifu wetu kwa Mungu, kwa njia hiyo atufanye tupoteze uzima wa milele. Kwa hiyo lengo jingine la mateso ni kututenganisha na chakula cha kiroho na ushirikia wa ndugu zetu kwenye mikutano yetu. Hivyo, utendaji wetu unapopigwa marufuku, kwa ujumla kuhubiri kwetu na mikutano yetu ndiyo inayowekewa vizuizi. Mara nyingi tunaambiwa, “Mwaweza kuwa Mashahidi wa Yehova lakini msihubiri wala kufanya mikutano yo yote.” Hata hivyo tusipohubiri wala kufanya mikutano, sisi hatungekuwa mashahidi wa Yehova Mungu wala Kristo Yesu, kwa kuwa shahidi asiyesema jambo lo lote si shahidi wa kweli hata kidogo.(Isaya 43:10, 12; Matendo 1:8) Na ingekuwaje kwa imani yetu kama hatungetii tena amri ya Mungu ya kukutana pamoja?—Waebrania 10:24, 25.
Kuvumilia Chini ya Mateso
11. Wakristo waaminifu wametendaje kuhusiana na mateso mengi sana ambayo yameelekezwa juu yao?
11 Watumishi wa Mungu wa kisasa wametendaje chini ya mateso mengi ambayo yameelekezwa juu yao? Kama Wakristo wa kwanza, hawajakuwa na woga bali wameendelea kujikaza kwa ujasiri katika kazi ya kuhubiri ijapokuwa marufuku na vitisho. Wao, kama Paulo, wana sababu ya ‘kufurahi.’ Msimamo wao imara katika upande wa Yehova wa suala lile unathibitisha Ibilisi ni mwongo. Ni pendeleo kama nini kuweza kushiriki kulitukuza jina la Yehova!—Wafilipi 2:17, 18; 2 Wathesalonike 1:4.
12. Je! kuna sababu yo yote ya kuogopa yale ambayo watesi huenda wakatisha kutufanya?
12 Kwa kweli hakuna sababu ya kuwaogopa wale wanatutesa. Paulo aliwaandikia hivi Wafilipi: “Lakini mwenendo wenu na uwe kama inavyoipasa Injili . . . wala [kutowaogopa] adui zenu, katika neno lo lote; [kwa ninyi kutowaogopa] kwao hao ni ishara mathubuti ya kupotea, bali kwenu ni ishara ya wokovu, huo utokao kwa Mungu.”—Wafilipi 1:27, 28.
13, 14. (a) Maofisa wenye kupinga katika nchi moja walifanya nini hivi karibuni katika jitihada ya kuwaogopesha Mashahidi wa Yehova? (b) Mambo hayo yaliyoonwa yanaonyesha nini hasa?
13 Hivi karibuni, katika nchi moja ya Ulaya ambako kazi ya Mashahidi wa Yehova haitambuliwi kisheria, ndugu mmoja alikamatwa kwa ajili ya kutoa hotuba fupi yenye kufariji ya Biblia katika mazishi. Vilevile yule ndugu aliyetoa sala alikamatwa. Maofisa wa mahali hapo walisema kwamba ni watu waliopewa mamlaka na Serikali peke yao wanaoweza kuzungumza kwenye mazishi, na kwamba sala hairuhusiwi “kwa sababu sala inaweza kutumiwa kwa kusudi la kufundisha.” Ndugu mwingine katika eneo hilo hilo alikamatwa kwa sababu alikuwa akiisomea jamaa yake mwenyewe Biblia. Ndugu hao hawakufanyiwa mashtaka yo yote. Walizuiliwa kwa muda mfupi kisha wakaachiliwa. Kwa wazi lengo lilikuwa kuwafanya waogope na kuacha.
14 Lakini kwa kweli wenye woga ni kina nani? Ikiwa maofisa wa mahali hapo wanatishwa na mtu anayesomea jamaa yake Biblia au na ndugu anayetoa hotuba au kutoa sala kwenye mazishi, lazima wawe wanaogopa sana sana ujumbe wa Biblia na wale wanaouhubiri! Kwa hiyo kwa sababu gani tuwaogope? Kama Paulo alivyoonyesha, umoja na ujasiri wetu “kwao hao ni ishara mathubuti ya kupotea, bali kwenu ni ishara ya wokovu.”—Wafilipi 1:28.
15. Jinsi tunavyotenda tunapotishwa inawezaje kuwa na matokeo juu ya kuendelezwa kwa mateso?
15 Katika sehemu fulani wahubiri wa “habari njema” wanaitwa kwenye stesheni za polisi kila baada ya juma chache ili watolewe hotuba, na mara nyingi wanatishwa watapewa adhabu kali sana wasipoacha kuzungumza juu ya ufalme wa Mungu. Lakini mara nyingi ndugu na dada hao wanapopuza vitisho hivyo na kuendelea na kazi hiyo bila woga, maofisa hao wanakubali kushindwa na kuwaacha. Hata hivyo, wakiona ushuhuda wo wote wa kudhoofika upande wa wahubiri wa Ufalme huo, wataendelea na jitihada zao za kuwaogopesha.
Kuendelea Chini ya Marufuku
16, 17. (a) Ni jitihada gani zilizofanywa za kuwafikishia ndugu chakula cha kiroho katika sehemu ambazo kazi imepigwa marufuku, na kwa wale walio gerezani? (b) Kwa sababu gani hilo ni jambo la maana?
16 Mashahidi katika nchi zile ambazo kazi imepigwa marukufu na uenezaji wa vitabu vyao umewekewa vizuizi wanathamini umaana wa kupokea chakula cha kiroho kwa ukawaida. Kwa kuwa Mnara wa Mlinzi na vichapo vingine vya Mashahidi wa Yehova haviwezi kuchapishwa kisheria na kupelekwa kupitia posta katika nchi fulani, mipango mingine inafanywa kuhakikisha kwamba chakula cha kiroho kinafikia kila mtu. Katika Ujeremani, wakati wa mateso yenye kuongozwa na Hitler, makala za kujifunza zilinakiliwa kwa mashine, zikapigwa chapa kwa taipuraita na, katika visa vingine, hata zikanakiliwa kwa mkono. Inakuwa lazima kufanya hilo pia katika mahali kwingi leo. Ikiwa nakala za kutosha haziwezi kutengenezwa ili kila mmoja awe na yake, wanazipokezana ili kila mmoja apate nafasi ya kusoma habari hiyo. Jambo la maana ni kutwaa chakula cha kiroho kwa ukawaida.—Mathayo 4:4.
17 Mambo yaliyoonwa yameonyesha kwamba sikuzote Yehova ameongoza mambo ili chakula cha kiroho kipate njia ya tuingia, hata katika hali ngumu sana. Njia mbalimbali zimetumiwa kukiingiza katika magereza na kambi za mateso. Nacho kimekuwa chenye kuwatia nguvu kama nini wale waliofungiwa humo!
18. Kwa sababu gani ni jambo la maana kuzungumza juu ya chakula cha kiroho pamoja na wengine kwa ukawaida, na jambo hilo lawezaje kufanywa hata chini ya hali ngumu?
18 Ikiwezekana, watumishi waaminifu wa Mungu wanakula chakula cha kiroho pamoja kwa ukawaida—hata ingawa mikutano imepigwa marufuku, hata ingawa wanafungwa gerezani. Kuzungumza andiko moja la Biblia kila siku, pamoja na wengine iwapo jambo hilo laweza kufanywa, kunakaza akili kwenye mambo ya kiroho. Hata mazungumzo mafupi kila siku yanatia nguvu nyingi za kiroho.—Zaburi 1:2; Matendo 17:11.
Umaana wa Mikutano
19. (a) Ni jambo gani lisilotazamiwa ambalo liliwapata ndugu wengi wetu katika Liberia? (b) Kulingana na ripoti ya Kitabu cha Mwaka cha 1977 (Kiingereza) ilisemekana ni nini kilichowasaidia waaminifu wavumilie?
19 Katika Machi 1963, huko Gbarnga, Liberia, karibu watu 400 waliokuwa wakihudhuria kusanyiko la wilaya la Mashahidi wa Yehova walikamatwa na kuzuiwa kwa siku nne bila chakula kwenye uwanja wa jeshi. Ikiwa ni jitihada ya kuwalazimisha wakane imani zao za kidini na kupigia saluti (kusalimu) bendera ya Liberia, Mashahidi hao walitendwa vibaya na mali zao zilitwaliwa. Ingawa katika kisa hicho wengi zaidi ndio waliokubali kushindwa wakaikana imani, bado kikundi kikubwa kiliendeleza ukamilifu wacho. Angalia maelezo yaliyotolewa katika Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1977 (Kiingereza): “Walikuwa wa aina zote, wasiojua kusoma na wenye elimu nyingi. Wale waliokuwa katika kikundi cha washikamanifu walikuwa wamekuwa wahudhuriaji waaminifu wa mikutano.”
20. Wengi wanajitahidije sana ili ‘wasiache kukusanyika pamoja,’ na ijapokuwa hatari gani?
20 Neno la Mungu aliloliongoza linatushauri tusiache kukusanyika pamoja. (Waebrania 10:24, 25) Umaana wa jambo hilo haupungui wakati wa mateso. Huenda ikawa lazima kufanyia mikutano katika vikundi vidogo vidogo katika nyumba za kibinafsi; mahali na saa huenda zikabadilishwa-badilishwa na huenda sikuzote zisiwafae, mikutano mingine ikiwa inafanywa usiku sana. Hata hivyo, ijapokuwa hatari hizo, ndugu na dada zetu waaminifu wanatia kila jitihada wahudhurie kila mkutano. Na ndugu wana nia ya kukubali nyumba zao zitumiwe kwa mikutano hiyo, hata ingawa wakigunduliwa huenda wakafungwa.
21. (a) Kuna nafasi gani za kufaidika kikamilifu kutokana na chakula cha kiroho chini ya hali hizo? (b) Ni maandiko gani yanayoonyesha umaana wa kukusanyika kwa ukawaida na kushiriki katika mikutano hiyo?
21 Pengine huenda mikutano katika vikundi vidogo vidogo isiwawezeshe wote kufaidika kutokana na walimu bora katika kundi, lakini kuna nafasi kubwa zaidi kwa kila mmoja kushiriki na kwa njia hiyo kufaidika sana na mikutano hiyo. Nyakati nyingi, vikundi vikubwa zaidi vyaweza kukusanyika kwa namna ya pikiniki (mandari), matembezi ya nje, au pindi kwa pindi, kwa namna ya mwaliko wa kibinafsi. Kuhudhuria mikutano yote kwa ukawaida ni jambo la maana katika ‘kushikamana kwao na mwanzo wa uthabiti wao kwa nguvu mpaka mwisho,’ ili waendeleze ukamilifu wao na kuona utimizo wa ahadi hizo kwa ‘kutokuacha.’—Waebrania 3:14; 10:36; Wagalatia 6:9, NW.
Kuhubiri Chini ya Marufuku
22. (a) Kwa sababu gani leo watu wa Mungu hawawezi kuacha kuzungumza juu ya mambo ambayo wameona na kusikia? (b) Jambo hilo linatimizwaje katika sehemu fulani?
22 Kama mitume, leo watu wa Yehova ‘hawawezi kuacha kuyanena mambo waliyoyaona na kuyasikia.’ (Matendo 4:20) Yesu alisema kwamba “sharti Injili ihubiriwe kwanza katika mataifa yote,” na hakuna mwanadamu au wakili ye yote shetani awezaye kuzuia jambo hilo. (Marko 13:10) Katika sehemu fulani, hata ingawa utendaji huo wa Mashahidi wa Yehova umepigwa marufuku, inawezekana kwenda nyumba kwa nyumba ukiwa mtu binafsi, kwa kutumia Biblia peke yake.
23, 24. (a) Katika sehemu ambazo si jambo la hekima kufanya kazi ya nyumba kwa nyumba, kazi ya kuhubiri inafanywaje? (b) Je! unaweza kusimulia mambo yo yote yaliyoonwa yanayoonyesha kwamba matokeo mazuri yamepatikana katika njia hiyo?
23 Mahali ambako si jambo la hekima kwenda nyumba kwa nyumba, “habari njema” zaweza kuhubiriwa katika njia nyingine. Pengine ziara za mbalimbali zaweza kufanywa katika sehemu tofauti tofauti za eneo, kwa kusudi la kutokueneza majengo yo yote katika njia ya mfululizo. Lakini si lazima tungojee mpaka watu wawe ndani ya nyumba. Ndugu zetu katika nchi nyingi wanafaulu sana katika kuzungumza na watu po pote wanapopatikana—barabarani, katika makaburi na bustani, au wanaposafiri. Hata wengine wameenda kama watalii katika maeneo yasiyo na Mashahidi, na huko wanaanzisha mazungumzo pamoja na watu po pote inapowezekana. Kwa vyo vyote adui hawana njia ya kutuzuia kuzungumza katika njia hizo tofauti, maadamu tuna pumzi na kuna watu tunaoweza kuzungumza nao.
24 Kupitia mazoezi, watu wa Yehova wamekuwa stadi kuanzisha mazungumzo ya kirafiki juu ya vichwa vya mazungumzo mbalimbali, ambavyo kwa kufaa vinaongoza kwenye mazungumzo ya Biblia. Shahidi mmoja katika nchi moja aliwafikia wenzi wa ndoa vijana katika bustani walipokuwa wakinywa maji katika kijito. Shahidi huyo akauliza kama wangependa kujua mahali yalipokuwa maji mazuri zaidi. Ndipo alipoanza kuwaambia juu ya maji yenye kutoa uzima katika Paradiso inayokuja, na wakawa na mazungumzo yaliyochukua saa tatu. Jambo hilo likatokeza funzo la Biblia, na baada ya miezi mitatu wenzi hao wakaanza kushiriki katika huduma ya shambani. Mwaka mmoja baadaye, wote wawili walibatizwa, na baadaye mwanamume huyo akatumika akiwa mtumishi wa huduma katika kundi.—Linganisha Yohana 4:7-15.
25. Tunapaswa kujaribu kuepuka nini, hasa mahali ambapo kuhubiri kumepigwa marufuku?
25 Katika kufanya utendaji huo wote ni jambo la hekima kuepuka pambano la moja kwa moja na wapinzani. Pia, tunahitaji kujihadhari tusiwape adui habari za kuarifu wanapojaribu kutufanya tujiunge nao kwa kuzungumza nasi kirafiki na kutusifu-sifu isivyo kweli. Tunataka kukumbuka shauri la Yesu: “Angalieni, mimi nawatuma kama kondoo kati ya mbwa-mwitu; basi iweni na busara kama nyoka, na kuwa watu wapole kama hua.” (Mathayo 10:16) Vilevile Paulo anashauri hivi: “Kadiri inavyowezekana, kwa upande wenu, muwe na amani na watu wote.”—Waroma 12:18, HNWW.
Matokeo Mazuri ya Kuendeleza Ukamilifu
26. Ni nini baadhi ya matokeo mazuri ya kuendeleza ukamilifu ijapokuwa mateso makali sana?
26 Ushahidi mzuri kama nini umetolewa wakati wa vizazi vyote na wale ambao wameshikilia kwa uthabiti ukamilifu wao ijapokuwa mateso makali sana! Jitihada zote za Ibilisi na mawakili wake za kuzuia kutolewa kwa ushuhuda zinatokeza tu ushuhuda mkubwa zaidi unaoletea jina la Yehova heshima. Na wale maelfu wote, ndiyo mamilioni, ambao wameendeleza (na wangali wanaendeleza) ukamilifu wao chini ya mateso, kwa njia hiyo wakaonyesha Ibilisi ni mwongo na wakathibitisha imani yao isiyoweza kuvunjwa katika Yehova Mungu na upendo kwake, wameshiriki jambo zuri sana kama nini!
27. Tunapata faida gani za kibinafsi kwa kuvumilia majaribu na mateso kwa uaminifu?
27 Tunapovumilia kwa uaminifu, tunakuwa na dhamiri njema, na kujua kwamba tumefanya yaliyo haki na kwamba tuna kibali ya Yehova. Jambo hilo linaimarisha tumaini letu, ambalo, nalo, linaongeza furaha yetu. Imani yetu ilijaribiwa, na, kwa kuwa hatukushindwa wala kukimbia mateso hayo, Yehova alitusaidia kuvumilia. Kama matokeo, imani yetu sasa ni yenye nguvu zaidi. Huo ‘ubora wa imani yetu uliojaribiwa’ unatufanya tuwe katika hali bora zaidi ya kukabili majaribu ya wakati ujao.—1 Petro 1:6, 7.
28. (a) Yule dada wa Finland aliyetangulia kutajwa ana sababu gani za kufurahi? (b) Na anaweza kuendelea kutumaini nini?
28 Dada aliyetajwa mwanzoni mwa makala iliyotangulia ndivyo alivyojionea ukweli wa hayo. Kwa mara nyingine anaishi katika mji wa kwao, ambako amekuwa akitumikia akiwa painia wa kawaida (mtangazaji wa Ufalme wa wakati wote) kwa muda fulani sasa. Ingawa watoto wake wachanga watatu hawako chini ya uangalizi wake, yeye anaruhusiwa kuwaona mara tatu kwa mwezi, naye ameweza kushiriki “habari njema” pamoja nao, na kuwa na matokeo yenye kutia moyo. Na ni nani ajuaye matokeo ya mwisho yatakuwa nini? Kumekuwako visa vingi sana, ambapo wapinzani na watesi wenye kutumia jeuri wamevutiwa sana na msimamo wa uaminifu waliochukua ndugu na dada zetu hata wakachochewa kujichunguzia Biblia, na hatimaye wengine wamekuwa waabudu wa Yehova.
29. Sisi sote tuna kitia-moyo gani kingine cha kuendelea kuwa waaminifu na wenye furaha ijapokuwa mateso?
29 Yakobo aliandika hivi: “Ndugu, chukueni manabii kuwa kielelezo cha kutaabishwa na uovu na wonyesho wa saburi, ambao walizungumza katika jina la Yehova. Tazama! Tunawatangaza wale ambao wamevumilia kuwa wenye furaha.” (Yakobo 5:10, 11, NW) Na, kupitia mifano myema mingine ya Wakristo wa karne ya kwanza na wale wa nyakati za sasa, sisi sote tunatiwa moyo sana kuwa wenye furaha ijapokuwa mateso.—Kutoka The Watchtower, April 15,1982.
[Picha katika ukurasa wa 14]
Yesu alisema: “Na adui za mtu [watakuwa] wale wa nyumbani mwake”
[Picha katika ukurasa wa 17]
Hata chini ya marufuku Mashahidi wa Yehova hawaachi kuhubiri