‘Ninyi ni Wenye Furaha Wakati Watu Wanawatesa Ninyi’
“Ninyi ni wenye furaha wakati watu wanawashutumu na kuwatesa ninyi na kwa uongo kuwasemea kila jambo ovu kwa ajili yangu. Furahini na kuruka kwa furaha, kwa kuwa zawadi yenu ni kuu katika mbingu.”—Mathayo 5:11, 12, NW.
1-4. Ni jambo gani lililoonwa linaloweza kutokeza maulizo akilini mwetu kuhusu kufurahi chini ya mateso?
JE! KWELI unaweza kuwa mwenye furaha watu wanaposema mambo ya uongo juu yako na kujaribu kukutenda madhara ya namna zote? Ebu kifikirie kisa cha mwanamke kijana katika Finland aliyeanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova miaka michache iliyopita. Upesi akawa anafurahia mambo mazuri aliyokuwa akijifunza juu ya kusudi la Yehova kwa wanadamu, na akaja kuthamini sana wema na upendo wake.
2 Lakini ndipo mume wake alipoanza kumpinga asijifunze Biblia, na alipokataa kuacha kujifunza, mumewe alianza kumtenda jeuri. Mwishowe yeye aliiandikia mahakama iwape amri ya kutengana. Karibuni mwanamke huyo akafukuzwa nyumbani mwake na kulazimishwa kuwaacha watoto wake wachanga watatu, kutia kitoto kinachozidi kidogo tu umri wa mwaka mmoja, kwa kuwa mahakama hiyo iliwaweka chini ya uangalizi wa baba. Kwa sababu gani? Je! mwanamke huyo alikuwa amepuza wajibu wa kuwatunza? Hapana, kwa maana funzo lake la Biblia lilikuwa linamfundisha hasa kuwa mke na mama bora.
3 Juma chache baadaye mumewe alifanya achukuliwe kwa nguvu kutoka mahali pake pa kazi akapelekwa kwenye makao ya kuangalia afya ili akapewe cheti cha kuonyesha yeye ni mwenda wazimu ndipo akabidhiwe kwa hospitali ya akili. Hapo kwanza daktari aliyekuwa akimchunguza alikataa kutoa amri ya namna hiyo, lakini, baadaye, kwa kukazwa na mume, alitoa amri ya kwamba mwanamke huyo akabidhiwe kwa hospitali ya akili. Kufikia hapo mwanamke huyo kijana, ambaye sasa alikuwa amebatizwa akawa mmoja wa Mashahidi wa Yehova alikuwa amekwisha kwenda kwenye mji mwingine, ambako alimwendea daktari mwingine. Baada ya kumchunguza, mara moja daktari huyo alimpa cheti cha kushuhudia yeye ana akili timamu.
4 Lakini hiyo haikubatilisha amri ya kwanza ya daktari yule. Kwa hiyo alipaswa kujificha kwa juma kadha mpaka tarehe za amri hiyo zimalizike. Zilipokwisha, yule daktari alikataa kutoa amri mpya; kwa hiyo dada huyo akaweza kurudi kwenye mji wa kwao. Punde si punde mume wake akaruhusiwa kumpa talaka kwa msingi wa ile amri waliyopewa ya kutengana, na mahakama ikawaweka watoto chini ya uangalizi wa baba.
5, 6. (a) Jambo hilo au jambo jingine kama hilo laweza kuwa sababu ya kufurahi? Kwa sababu gani? (Marko 10:29, 30) (b) Kama inavyoonyeshwa katika maandiko yaliyotajwa, Ayubu alikuwa na sababu gani za kufurahi baada ya mateso yake?
5 Je! wewe ungeweza kukiona kisa hicho kuwa sababu ya kufurahi? Bila shaka hukuna mke wala mama ye yote angefurahi kufukuzwa nyumbani mwake na kunyang’anywa watoto wake. Wala hangefurahi ikiwa wapendwa wangejaribu kufanya apelekwe kwenye hospitali ya akili ati kwa sababu tu alitaka kujifunza Biblia na kufuata kanuni zayo. Lakini angalia sababu anayotoa Yesu ya kufurahi chini ya hali hizo: “Furahini na kuruka kwa furaha, kwa kuwa zawadi yenu ni kuu katika mbingu.”—Mathayo 5:12, NW.
6 Ndiyo, ikiwa kweli sababu ya kuteswa ni ile ambayo Yesu alisema katika mstari unaotangulia, “kwa ajili yangu,” tunaweza kufurahia kuwa na nafasi ya kuonyesha ukamilifu wetu kwa Yehova na kushiriki katika kuliondolea lawama jina lake, kama alivyofanya Yesu. Kwa njia hiyo tunamthibitisha Ibilisi kuwa mwongo anapodai anaweza kuwaondoa watu wote kwa Mungu. Kusimama upande wa Yehova Mungu kwa njia hiyo kunampendeza, na, kama inavyoonyeshwa na kisa cha Ayubu, kutatokeza zawadi.—Ayubu 1:9,10; 42:10-16; 1 Petro 2:19, 20.
Mateso ni ya Kutazamiwa
7. (a) Kwa sababu gani Wakristo wanaweza kutazamia kuteswa? (b) Je! jambo hilo linawahusu Wakristo wote, au ni baadhi yao tu?
7 Lakini kwa sababu gani mtu ye yote ateswe kwa sababu tu anataka kujifunza Neno la Mungu, Biblia, na kuwa Mkristo? Yesu alijibu ulizo hilo kwa njia hii: “Iwapo ulimwengu ukiwachukia, mwajua ya kuwa umenichukia mimi kabla ya kuwachukia ninyi. Kama mngekuwa wa ulimwengu, ulimwengu ungewapenda walio wake; lakini kwa kuwa ninyi si wa ulimwengu, bali mimi naliwachagua katika ulimwengu, kwa sababu hiyo ulimwengu huwachukia. Likumbukeni lile neno nililowaambia, Mtumwa si mkubwa kuliko bwana wake. Ikiwa waliniudhi mimi, watawaudhi ninyi; ikiwa walilishika neno langu watalishika na lenu. Lakini haya yote watawatenda kwa ajili ya jina langu, kwa kuwa hawamjui yeye aliyenipeleka.” (Yohana 15:18-21) Kama mtume Paulo alivyotaja katika barua yake ya pili iliyoongozwa na Mungu aliyomwandikia Timotheo, Wakristo wanapaswa kutazamia mateso. Yeye aliandika hivi: “Wote wapendao kuishi maisha ya utauwa katika Kristo Yesu wataudhiwa.”—2 Timotheo 3:12.
8. Ni nani hasa anayetokeza mateso ya Wakristo, na lengo lake ni nini?
8 Na tusisahau kwamba mwenye kutokeza mateso hayo si mwingine ila ni yule mpinzani mkuu, Shetani Ibilisi. Msimamo wako imara ukiwa Mkristo na upendo wako kwa Yehova Mungu unathibitisha Ibilisi kuwa mwongo, kwa kuwa yeye anadai kwamba hakuna mtu anayempenda Mungu kikweli, na kwamba mtu ye yote akimtumikia Yeye, ni kwa sababu tu ya yale anayofaidika nayo kwa kufanya hivyo. Shetani alijidai kwamba akiruhusiwa kufanya atakavyo, angeweza kumgeuza Ayubu kutoka kwa Mungu, na kwa njia hiyo akadokeza angeweza kuwafanya vivyo hivyo wanadamu wote. (Ayubu 1:8-11; 2:3-5) Ingawa alishindwa kuvunja ukamilifu wa Ayubu, Ibilisi bado hajakubali kushindwa.—2 Wakorintho 4:4.
Wakristo wa Kwanza Waliteswa
9. Toa mifano kutoka katika Maandiko inayoonyesha namna namna za mateso ambayo Wakristo wa kwanza walilazimika kuvumilia.
9 Kwa kupatana na onyo la Yesu, Wakristo wa kwanza walipatwa na mateso ambayo yalikuwa makali sana nyakati nyingine. Wengi walifukuzwa kutoka nyumbani mwao na kulazimishwa wakimbilie sehemu nyingine, kama ilivyokuwa kwa kundi la Yerusalemu. (Matendo 8:1) Wengine, kama mtume Yohana, walihamishwa. (Ufunuo 1:9) Mtume Paulo na wale waliokuwa wakifanya kazi pamoja naye katika huduma mbele ya watu wote walipigwa kwa mawe na kwa mijeledi (Matendo 14:19; 16:22) Wengi kati ya Wakristo wa kwanza walifungwa gerezani wengine walinyang’anywa mali zao na hata wengine wakauawa. (Wakolosai 4:3; Filemoni 9, 10; Waebrania 10:34; 13:3; Matendo 12:1, 2) Walakini waliweza kufurahi, kwa sababu walifahamu kabisa sababu gani walikuwa wakiteswa.
10. Ni jambo gani linaloonyesha kwamba wafuasi wa Kristo katika karne ya kwanza hawakutishwa na mateso?
10 Je! mateso hayo yaliisimamisha au hata kuipunguza kazi ya ‘kuzungumza juu ya Mungu na kumshuhudia Yesu’? La sivyo, kwa maana Wakristo wa kwanza walikataa kutishika. Masimulizi katika Matendo 5:40-42, NW, yanatuambia kwamba maofisa wa Sanhedrini (Mahakama Kuu) ya Kiyahudi ‘waliwaita mitume, wakawapiga mijeledi, na kuwaamuru waache kusema juu ya jina la Yesu, na kuwaacha waende zao.’ Halafu Wakristo hao walifanya nini? “Kwa hiyo, wao, wakaenda zao kutoka mbele ya Sanhedrini, wakifurahi kwa sababu walikuwa wamehesabiwa wanastahili kuvunjiwa heshima kwa ajili ya jina lake. Na kila siku katika hekalu na kutoka nyumba kwa nyumba wakaendelea bila kuacha kufundisha na kuzitangaza habari njema juu ya Kristo, Yesu.”
11. Petro na Yohana walijibuje walipotishwa?
11 Mapema, mitume Petro na Yohana walikuwa wamekuwa mbele ya Sanhedrini kwa sababu walikuwa wamemponya mtu aliyelemaa na kwa sababu ya kufundisha kwa msingi wa jina la Yesu. Masimulizi hayo yanatuambia hivi: “[Watawala na wanaume wazee] wakawaita, wakawaamuru wasiseme kabisa wala kufundisha kwa jina la Yesu. Petro na Yohana wakawajibu wakawaambia, Kwamba ni haki mbele za Mungu kuwasikiliza ninyi kuliko Mungu, hukumuni ninyi wenyewe; maana sisi hatuwezi kuacha kuyanena mambo tuliyoyaona na kuyasikia. Nao walipokwisha kuwatisha tena wakawafungua, wasione njia ya kuwaadhibu, kwa sababu ya watu.”—Matendo 4:18-21.
12. Mitume na wanafunzi waliomba msaada gani kutoka kwa Yehova kwa njia ya sala walipokuwa chini ya mateso?
12 Hawakuogopeshwa na vitisho hivyo. Maandishi yanaonyesha kwamba mitume na wanafunzi walisali inavyofaa, si kwamba Yehova aondoe mateso hayo bali awape nguvu kupitia roho yake waendelee kuzungumza neno lake kwa ujasiri. Naye alifanya hivyo.—Matendo 4:29, 31.
13. Kulingana na yale ambayo Paulo aliwaandikia Wafilipi, kufungwa kwake Roma kulileta faida gani?
13 Kufungwa kwa Paulo katika Roma kulikuwa na matokeo mazuri, kama alivyoeleza katika barua yake aliyowaandikia Wafilipi: “Lakini, ndugu zangu, nataka mjue ya kuwa mambo yote yaliyonipata yametokea zaidi kwa kuieneza Injili; hata vifungo vyangu vimekuwa dhahiri katika Kristo, miongoni mwa askari, na kwa wengine wote pia. Na wengi wao hao ndugu walio katika Bwana, hali wakipata kuthibitika kwa ajili ya kufungwa kwangu, wamezidi sana kuthubutu kulinena neno la Mungu pasipo hofu.” (Wafilipi 1:12-14) Ndiyo, kuteswa kwa Paulo kulitokeza ushuhuda mkubwa zaidi, si kwa sababu tu ya namna alivyotangazwa sana na nafasi alizokuwa nazo za kutolea ushuhuda maofisa wa mahakama, bali pia kwa sababu Wakristo wengine walitiwa moyo kwa njia hiyo wazidishe utendaji wao.
Mateso Katika “Siku za Mwisho”
14. Yesu alisema ni sababu gani za sisi kuteswa leo?
14 Kama vile manabii wa Mungu wa nyakati za kale na kama vile Yesu Kristo na mitume na wanafunzi wake katika karne ya kwanza walivyopatwa na mateso, ndivyo Wakristo katika hizi “siku za mwisho” za hii taratibu ya mambo wanavyoweza kutazamia kulazimika kuvumilia mateso. Yesu alitabiri hilo kuwa sehemu ya ile “ishara” (NW) yenye mambo mengi ya mwisho wa hii taratibu ya mambo. Yeye alisema hivi: “Wakati huo watawasaliti ninyi mpate dhiki, nao watawaua; nanyi mtakuwa watu wa kuchukiwa na mataifa yote kwa ajili ya jina langu.”—Mathayo 24:9.
15, 16. (a) Ni unabii gani zaidi unaohusu wakati wetu unaoonyesha kwamba tunaweza kutazamia mateso kwa sababu ya kutoa ushuhuda? (b) Ni maulizo gani yanayotokezwa sasa ili tuyachunguze?
15 Baadaye, Yesu alimdokezea mtume Yohana yale ambayo wafuasi wake duniani wangeweza kutazamia baada ya kuzaliwa kwa ufalme wa kimbingu. Akizungumza kwa lugha ya mfano, yeye alisema hivi: “Na joka yule [anayetambulishwa katika mstari wa 9 kuwa “nyoka wa zamani, aitwaye Ibilisi na Shetani”] alipoona ya kuwa ametupwa katika nchi, alimwudhi mwanamke yule [tengenezo la Mungu la ulimwengu wote wa juu na chini] aliyemzaa mtoto mwanamume [ufalme ambao Mfalme wake ni Kristo]. . . . Joka akamkasirikia yule mwanamke, akaenda zake afanye vita juu ya wazao wake waliosalia, wazishikao amri za Mungu, na kuwa na ushuhuda wa Yesu.”—Ufunuo 12:13, 15-17.
16 Je! hilo limetimia katika hizi “siku za mwisho”? Wakristo wa kweli wamelazimika kuvumilia mateso kwa njia gani katika wakati wetu, na wamewezaje kufurahi ijapokuwa hayo? Mateso yamekuwa na matokeo gani juu yao na juu ya wengi wenye kutazama wakiteswa? Maulizo hayo yatachunguzwa katika makala inayofuata.
[Picha katika ukurasa wa 9]
Wale wanaomthibitisha Ibilisi kuwa mwongo, kama alivyofanya Ayubu, watapewa zawadi
[Picha katika ukurasa wa 11]
Petro, Yohana na Wakristo wengine wa kwanza walikataa kutishwa na maofisa ambao waliipinga kazi yao waliopewa na Mungu
[Picha katika ukurasa wa 12]
‘Joka akakasirika akaenda zake afanye vita na wale wanaomtolea Yesu ushuhuda.’—Ufunuo 12:15-17