Uchaguzi Ulio Bora—Maisha Katika Dunia ya Paradiso
Kuchagua maisha haya ya sasa kunaweza kuwa uchaguzi mbaya kwa sababu ya taabu nyingi zilizopo. Hata hivyo watu wengi wangali wakiyashikilia maisha ya sasa kweli kweli, wasitake kuponyokwa nayo. Ingawa ni maisha yenye taabu nyingi, ni afadhali kuwa na hayo kuliko kuwa bila, kuliko kuwa na patupu. Walakini, sasa watu wanaweza kuchagua paradiso isiyo na taabu itakayokuwa hapa duniani wakitaka.
KAZI NZURI SANA
Ikiwa ungependa kuitunza dunia, uigeuze iwe mashamba yenye kuzaa chakula au iwe bustani za kupendeza zinazozaa maua malidadi, ufanye majangwa yachanue, badala ya miiba na michongoma uone wanja zenye nyasi za kupendeza sana na misitu, ulinde maeneo fulani yenye vichaka na milima yawe makao ya wanyama-mwitu ili yawe yakimtolea Muumba sifa kwa uzuri wayo—ikiwa ungependa kushiriki katika kazi hii ya kupamba dunia, basi wewe ungependa kuishi katika hiyo dunia ya paradiso. Kuona mema kutokana na kazi hiyo “ni karama ya Mungu.”—Mhubiri 3:13.
AMANI PAMOJA NA WANYAMA
Ikiwa ungependezwa na kutawala wanyama, si kwa kutumia bunduki wala viboko wala fito za chuma, bali kwa upendo na kuaminiana; ikiwa unatamani sana kuuona wakati ambao dubu na ndama (mtoto wa ng’ombe) watalala pamoja, chui na mtoto wa mbuzi walishe pamoja, wakati ambao simba atakula nyasi kavu kama ng’ombe, na ikiwa ungependa kuiona siku ambayo wanyama wote hawa watafanya upole wafuate uongozi wa kitoto kidogo, basi wewe ungeipenda ile dunia ya paradiso. “Hawatadhuru wala hawataharibu katika mlima wangu wote mtakatifu,” ndivyo anavyoahidi Yehova.—Isaya 11:9.
AFYA NA UZIMA
Ikiwa unatumaini kwa moyo kuiona siku ambayo viwete wataruka-ruka kama ayala (mnyama kama paa), kuusikia ulimi wa mabubu ukiimba, kuyaona macho ya vipofu yakifunguka, kutazama masikio ya viziwi yakizibuliwa, kushuhudia miguno ya maumivu na vilio vya watu vikigeuka viwe vicheko kisha machozi na maombolezo yawe kicheko cha sauti kubwa na maumivu na kifo viachie nafasi afya na uzima wa milele, basi wewe hutaruhusu kitu cho chote kikuzuie kuingia katika ile dunia ya paradiso yenye mibaraka ambamo mtakuwa hali za namna hiyo milele. Hiyo, pia, ni ahadi ya Mungu. “Yeye atayafuta machozi yao yote; maana hakutakuwako tena na kifo, wala uchungu, wala kilio, wala maumivu.”—Ufunuo 21:4, Habari Njema kwa Watu Wote.
HAKUNA VITA TENA
Ikiwa moyo wako unauma ukitamani sana wakati ambao panga zitapigwa-pigwa ziwe plau (majembe) za kulimia na mikuki iwe makasi ya kufyekea majani na mimea mingineyo, wakati ambao hakutakuwako shule za kijeshi, kusiwe na masomo ya vita, makombora yasitengenezwe, wenye kuchochea vita wasiwepo, basi wewe utampigia Mungu asante kwa ajili ya taratibu mpya yake ambamo yote hayo yatatukia. Yehova anatoa uhakikisho wa mambo hayo kwa kusema: “Avikomesha vita hata mwisho wa dunia.”—Zaburi 46:9.
MWISHO WA UONEZI
Ikiwa unataka sana kuuona wakati ambao utawala wa kisiasa wenye uonezi utatokomea kisha pupa ya kibiashara isiwepo tena, wakati ambao wanadamu watajenga nyumba wazikae wakiwa na amani, wakati dunia itakapojawa na kicheko chenye shangwe hata iwe na nderemo kwa sababu ya nyimbo za kuvutia sana za ndege, na wakati ambao hewa iliyosafishwa itajawa na manukato ya maua, basi utafurahi unapoelezwa juu ya uzima katika dunia ya paradiso. Ahadi hii ndiyo wanayopewa watu wa Mungu: “Wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi.”—Isaya 65:22.
SI HADITHI TAMU TU ISIYO YA KWELI
Je! labda msomaji fulani anaona mashaka juu ya mambo hayo, au kuyafanyia mzaha kweli kweli? Dunia hii iwe paradiso ati? Je! hivyo ndivyo anavyowaza akitia shaka? Si ajabu kwamba anaweza kuwa na mashaka, kwa kuwa sote tumekuwa tukipatwa na taabu tu katika maisha haya ya sasa. “Mshahara wa dhambi ni kifo,” na wanadamu wamekuwa wakitenda dhambi na kujiokotea mshahara wa dhambi zao. (Waroma 6:23, HNWW) Walakini, Neno la Mungu linaahidi kwamba ‘ulimwengu unapita,’ lakini “mtu atendaye atakalo Mungu, anahisi milele.”-—1 Yohane 2:17, HNWW.
AHADI ZENYE KUAMINIKA
Ahadi hizi za dunia ya paradiso zimefokana na Yehova Mungu, “asiyeweza kusema uongo.” (Tito 1:2) Taifa la Israeli lilikumbushwa jambo hili: “Halikuwapungukia ninyi hata neno moja katika mambo hayo mema yote aliyoyanena [Yehova], Mungu wenu.” (Yoshua 23:14) Hata mpinzani wa Mungu alilazimika kusema: “Mungu si mwanadamu kwamba yeye apaswe kusema mambo ya uongo. . . . Je! yeye mwenyewe amesema hilo na yeye asifanye hilo?”—Hesabu 23:19, NW.
Uzima wa milele katika dunia ya paradiso—hilo ndilo lililokuwa kusudi la Mungu la kwanza kabisa kwa ajili ya dunia hii na wanadamu wanaoikaa. Hayo ndiyo maisha (uzima) ambayo msomaji anaweza kuchagua, akitaka. Yehova Mungu halioni jambo hili kuwa ndoto lisiweze kutimizwa, kwa hiyo msomaji ye yote asilione kuwa ndoto tu. Yehova anawaza kwamba taratibu hii ya sasa imekuwa mbaya mno isiweze kuendelea kuwapo, nawe kwa uhakika unakubaliana naye. Hata sasa anaagiza watu wachague ama uzima wa milele katika paradiso ama kifo cha milele pamoja na ulimwengu huu wa kale.
Watu wanaonyeshaje sasa uchaguzi walioufanya? Wewe unaweza kuuonyeshaje uchaguzi wako? Iangalie habari inayofuata.