Sehemu ya 8
Ishi Milele Juu ya Dunia-paradiso
1 Maisha yatakuwaje wakati Mungu atakapoondoa uovu na kuteseka duniani na kuleta ulimwengu mpya chini ya udhibiti wenye upendo wa Ufalme wake wa kimbingu? Mungu aahidi ‘kuufumbua mkono wake na kutosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.’—Zaburi 145:16, NW.
2 Tamaa zako zinazofaa ni zipi? Je! si ni kupata maisha yenye furaha, kazi yenye kufaa, wingi wa vitu vya kimwili, mazingira yenye kupendeza, amani kati ya watu wote, na uhuru pasi na ukosefu wa haki, magonjwa, kuteseka, na kifo? Na namna gani kuhusu hali ya kiroho yenye shangwe? Mambo hayo yote yatatimizwa karibuni chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu. Angalia yale ambayo unabii mbalimbali wa Biblia husema kuhusu baraka nzuri ajabu zitakazoujia ulimwengu mpya huo.
Ainabinadamu Yakaa kwa Amani Kamilifu
3 “[Mungu] avikomesha vita hata mwisho wa dunia; avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari [ya vita].”—Zaburi 46:9.
4 “Nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Isaya 2:4.
5 “Wenye upole watairithi nchi [dunia, NW], watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.
6 “Dunia yote inastarehe na kutulia. [Watu wamekuwa wenye uchangamfu kwa vilio vya shangwe, NW].”—Isaya 14:7.
Amani Kati ya Binadamu na Wanyama
7 “Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza. Ng’ombe na dubu watalisha pamoja; watoto wao watalala pamoja; na simba atakula majani kama ng’ombe. Na mtoto anyonyaye atacheza penye tundu la nyoka, na mtoto aliyeachishwa atatia mkono wake katika pango la fira. Hawatadhuru wala hawataharibu.”—Isaya 11:6-9.
8 “Nami siku hiyo nitafanya agano na wanyama wa mashamba kwa ajili yao, tena na ndege wa angani, tena na wadudu wa nchi . . . nami nitawalalisha salama salimini.”—Hosea 2:18.
Afya Kamili, Uhai wa Milele
9 “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”—Isaya 35:5, 6.
10 “Naye [Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:4.
11 “Wala hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24.
12 “Nyama ya mwili wake itakuwa laini kuliko ya mtoto; huzirudia siku za ujana wake.”—Ayubu 33:25.
13 “Karama ya Mungu ni uzima wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu.”—Warumi 6:23.
14 “Kila mtu amwaminiye . . . , [atapata] uzima wa milele.”—Yohana 3:16.
Wafu Warudishwa Kwenye Uhai
15 “Kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki [waadilifu, NW] na wasio haki [wasio waadilifu, NW] pia.”—Matendo 24:15.
16 “Saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini [katika ukumbuko wa Mungu] wataisikia sauti yake. Nao watatoka.”—Yohana 5:28, 29.
17 “Bahari ikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake; na Mauti [kifo, NW] na Kuzimu [Hadesi, NW, yaani kaburi] zikawatoa wafu waliokuwamo ndani yake.”—Ufunuo 20:13.
Dunia, Paradiso Yenye Ufanisi
18 “Yatakuwako manyunyu ya baraka. Na mti wa kondeni utazaa matunda yake, nayo ardhi itatoa mazao yake, nao watakuwa salama katika nchi yao.”—Ezekieli 34:26, 27.
19 “Nchi imetoa mazao yake; MUNGU, Mungu wetu, ametubariki.”—Zaburi 67:6.
20 “Nyika na mahali palipo ukiwa patafurahi; jangwa litashangilia na kuchanua maua kama waridi.”—Isaya 35:1.
21 “Milima na vilima vitatoa nyimbo; na miti yote ya kondeni itapiga makofi. Badala ya michongoma utamea msunobari, na badala ya mibigili, mhadesi.”—Isaya 55:12, 13.
22 “Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.”—Luka 23:43, NW.
Nyumba Nzuri kwa Wote
23 “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake . . . Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine; . . . Wateule wangu wataifurahia kazi ya mikono yao muda wa siku nyingi. Hawatajitaabisha kwa kazi bure, wala hawatazaa kwa taabu.”—Isaya 65:21-23.
24 “Bali wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.”—Mika 4:4.
Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso
25 Ni taraja zuri ajabu kama nini kwa wakati ujao! Maisha zaweza kuwa na kusudi halisi sasa kama nini zinapotegemezwa na tumaini hakika kwamba katika ulimwengu mpya wa Mungu matatizo yote ya leo yatakuwa mambo yaliyokwisha kupita! “Mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.” (Isaya 65:17) Na inafariji kama nini kujua kwamba wakati huo uhai utakuwa wa milele: “[Mungu atameza] mauti hata milele.”—Isaya 25:8.
26 Je! wewe wataka uishi milele katika ulimwengu huo mpya wa Paradiso ulio karibu sana sasa? Huenda ukauliza hivi: ‘Ningehitaji kufanya nini ili kupata upendeleo wa Mungu kwenye mwisho wa ulimwengu huu na kuendelea kuishi katika ulimwengu wake mpya?’ Wahitaji kufanya yale ambayo Yesu alionyesha katika sala kwa Mungu hivi: “Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na Yesu Kristo uliyemtuma.”—Yohana 17:3.
27 Kwa hiyo, jipatie Biblia, na uhakikishe yale ambayo umesoma katika broshua hii. Watafute-tafute wengine wanaojifunza na kufundisha kweli hizi za Biblia. Jitenge na dini zenye unafiki zinazofundisha na kufanya mambo yaliyo kinyume cha Biblia. Jifunze jinsi wewe, pamoja na mamilioni ya wengine ambao tayari wanafanya mapenzi ya Mungu, waweza kushiriki katika kusudi la Mungu ili wanadamu waishi milele juu ya dunia-paradiso. Na zingatia moyoni yale ambayo Neno lililopuliziwa la Mungu hujulisha kuhusu wakati ujao ulio karibu: “Dunia [ulimwengu, NW] inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.”—1 Yohana 2:17.
[Maswali ya Funzo]
1, 2. Maisha yatakuwaje chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu?
3-6. Tuna uhakikishio gani kwamba wanadamu watakuwa na amani katika ulimwengu mpya?
7, 8. Kutakuwa na amani gani kati ya watu na wanyama?
9-14. Eleza jinsi hali ya afya itakavyokuwa katika ulimwengu mpya.
15-17. Kuna tumaini gani kwa wale ambao tayari wamekufa?
18-22. Dunia nzima itabadilishwa kuwa nini?
23, 24. Tuna uhakikishio gani kwamba kutakuwa na nyumba nzuri za kutosha kwa wote?
25. Tuna taraja gani zuri ajabu kwa wakati ujao?
26. Ni nini ulio ufunguo wa kuishi milele katika ulimwengu mpya wa Mungu?
27. Ni lazima ufanye nini ili ushiriki katika kusudi la Mungu?
[Picha katika ukurasa wa 31]
Kusudi la Mungu la kurudisha paradiso ya kidunia litatimizwa hivi karibuni