Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • dg seh. ya 10 kur. 22-28
  • Ule Ulimwengu Mpya Mzuri Ajabu Wenye Kufanyizwa Na Mungu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ule Ulimwengu Mpya Mzuri Ajabu Wenye Kufanyizwa Na Mungu
  • Je, Kweli Mungu Anatujali?
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Uadilifu Wachukua Mahali pa Uovu
  • Afya Kamilifu Yarudishwa
  • Wafu Warudi
  • Ulimwengu Wenye Amani Kweli Kweli
  • Dunia Yageuzwa Sura Kuwa Paradiso
  • Kubatilisha ya Wakati Uliopita
  • Ishi Milele Juu ya Dunia-paradiso
    Ni Nini Lililo Kusudi la Uhai?
  • Ulimwengu Mpya Usio na Taabu
    Amkeni!—1991
  • Baada ya Har-Magedoni, Dunia-Paradiso
    Unaweza Kuishi Milele Katika Paradiso Duniani
  • Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani
    Uzima Katika Ulimwengu Mpya Wenye Amani
Pata Habari Zaidi
Je, Kweli Mungu Anatujali?
dg seh. ya 10 kur. 22-28

Sehemu ya 10

Ule Ulimwengu Mpya Mzuri Ajabu Wenye Kufanyizwa Na Mungu

1, 2. Kutatukia nini baada ya vita ya Har–Magedoni yenye kusafisha?

BAADA ya vita yenye kusafisha ya Mungu ya Har–Magedoni, ndipo nini? Ndipo enzi mpya tukufu itaanza. Waokokaji wa Har–Magedoni, wakiwa wamekwisha thibitisha uaminifu-maadili wao kwa utawala wa Mungu, wataingizwa ndani ya ulimwengu mpya. Kitakuwa kipindi kipya chenye kusisimua kama nini cha historia huku manufaa nzuri ajabu zikimiminikia familia ya kibinadamu kutoka kwa Mungu!

2 Chini ya mwelekezo wa Ufalme wa Mungu, waokokaji wataanza kusitawisha paradiso. Nishati zao zitatolewa kwa mifuatio isiyo na ubinafsi itakayonufaisha wote walio hai wakati huo. Dunia itaanza kugeuzwa sura iwe makao yenye kuvutia, yenye amani, yenye kuridhisha kwa ajili ya ainabinadamu.

Uadilifu Wachukua Mahali pa Uovu

3. Ni kitulizo gani cha mara hiyo kitakachohisiwa baada tu ya Har–Magedoni?

3 Yote hayo yatafanywa yawezekane kwa kuharibiwa kwa ulimwengu wa Shetani. Hakutakuwako tena dini bandia, mifumo ya kijamii, au serikali zenye kugawanya. Hakutakuwako tena propaganda za kishetani ili kudanganya watu; vyombo vyote viitokezayo vitaharibiwa pamoja na mfumo wa Shetani. Ebu fikiri tu: Hewa yote yenye sumu ya ulimwengu wa Shetani ikiwa imeondolewa mbali! Kitakuwa kitulizo kama nini!

4. Eleza badiliko ambalo litatukia katika mafundisho.

4 Ndipo badala ya mawazo yenye kuharibu ya utawala wa kibinadamu kutakuwako mafundisho yenye kujenga yatokayo kwa Mungu. “Watoto wako wote watafundishwa na BWANA [Yehova, NW].” (Isaya 54:13) Maagizo hayo yenye kujenga yakiwapo mwaka baada ya mwaka, “dunia itajawa na kumjua BWANA [Yehova, NW], kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Isaya 11:9) Watu hawatajifunza tena yaliyo mabaya, bali “uadilifu ndio wakaaji wa bara lizaalo watajifunza hakika.” (Isaya 26:9, NW) Mawazo na vitendo vyenye kujenga vitakuwa ndivyo tabia ya kawaida ya watu.—Matendo 17:31; Wafilipi 4:8.

5. Itakuwaje na uovu na watu wote waovu?

5 Hivyo, hakutakuwako tena uuaji wa kukusudia, jeuri, kulalwa kinguvu, unyang’anyi, au uhalifu mwingine wowote. Hakuna mtu ambaye atalazimika kuteseka kwa sababu ya vitendo viovu vya wengine. Mithali 10:30 husema hivi: “Mwenye haki hataondolewa milele; bali wasio haki hawatakaa katika nchi.”

Afya Kamilifu Yarudishwa

6, 7. (a) Ni magumu gani ya maisha yenye kutaabisha ambayo utawala wa Ufalme utakomesha? (b) Yesu alionyeshaje jambo hilo alipokuwa duniani?

6 Katika ulimwengu mpya, matokeo mabaya yaliyoletwa na uasi wa kwanza yataondolewa. Kwa mfano, utawala wa Ufalme utaondolea mbali magonjwa na uzee. Leo, hata kama wafurahia kadiri fulani ya afya njema, uhakika ni kwamba uzidivyo kuzeeka, macho yako hufifia, meno yako huchakaa, masikio yako huwa mazito kusikia, ngozi yako hukunjamana, viungo vyako vya ndani huharibika, mpaka hatimaye unakufa.

7 Hata hivyo, matokeo hayo yenye kutaabisha tuliyorithi kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza karibuni yatakuwa kitu cha wakati uliopita. Je! wakumbuka jambo ambalo Yesu alionyesha kuhusu afya alipokuwa duniani? Biblia husimulia hivi: “Wakamwendea makutano mengi wakimletea viwete, vipofu, mabubu, vilema, na wengine wengi, wakawaweka miguuni pake; akawaponya; hata ule mkutano wakastaajabu, walipowaona mabubu wanasema, vilema wanakuwa wazima, viwete wanakwenda, na vipofu wanaona.”—Mathayo 15:30, 31.

8, 9. Eleza furaha ambayo itakuja katika ulimwengu mpya wakati afya kamilifu inaporudishwa?

8 Itakuja furaha kuu kama nini katika ulimwengu mpya magonjwa yetu yote yaondolewapo! Kuteseka kulikotokana na afya mbaya hakutatutesa tena kamwe. “Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.” “Ndipo macho ya vipofu yatafumbuliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Ndipo mtu aliye kilema ataruka-ruka kama kulungu, na ulimi wake aliye bubu utaimba.”—Isaya 33:24; 35:5, 6.

9 Je! haitasisimua kuamka kila asubuhi na kujua kwamba sasa wafurahia afya yenye nguvu? Je! haitaridhisha watu wazee-wazee kujua kwamba wamerudishwa kwenye nguvu kamili ya ujana na kwamba watafikia ukamilifu ambao Adamu na Hawa walifurahia mwanzoni? Ahadi ya Biblia ni: “Nyama ya mwili wake itakuwa laini kuliko ya mtoto; huzirudia siku za ujana wake.” (Ayubu 33:25) Itachangamsha kama nini kuweza kutupilia mbali miwani hiyo, vidude vya kusaidia kusikia, mikongojo, viti vya vilema, na madawa! Mahospitali, madaktari, na waganga wa meno hawatahitajiwa tena kamwe.

10. Itakuwaje na kifo?

10 Watu wanaofurahia afya hiyo yenye kusisimua hawatataka kufa. Na haitakuwa lazima wafe, kwani ainabinadamu haitakuwa tena ikishikwa na kutokamilika na kifo kilichorithiwa. Kristo ‘sharti amiliki hata Mungu awaweke maadui wake wote chini ya miguu yake. Adui wa mwisho atakayebatilishwa ni mauti.’ “Karama ya Mungu ni uzima wa milele katika Kristo Yesu Bwana wetu.”—1 Wakorintho 15:25, 26; Warumi 6:23; ona pia Isaya 25:8.

11. Ufunuo hutoaje muhtasari wa manufaa za ulimwengu mpya?

11 Kikitoa muhtasari wa manufaa ambazo zitamiminikia familia ya kibinadamu katika Paradiso kutoka kwa Mungu, kitabu cha mwisho cha Biblia husema hivi: “Naye [Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:3, 4.

Wafu Warudi

12. Yesu alionyeshaje uwezo aliopewa na Mungu wa kufufua?

12 Yesu alifanya zaidi ya kuponya wagonjwa na viwete. Alirudisha watu pia kutoka kaburi. Akaonyesha hivyo ule uwezo wa ajabu wa kufufua ambao Mungu alikuwa amempa. Je! wewe wakumbuka pindi ile Yesu alipokwenda kwenye nyumba ya mtu ambaye binti yake alikuwa amekufa? Yesu alimwambia msichana huyo aliyekufa: “Msichana, nakuambia, Inuka”! Matokeo yakawa nini? “Mara akasimama yule kijana, akaenda.” Kwa kuona hivyo, watu hao “wakashangaa mshangao mkuu.” Ilikuwa vigumu kuzuia furaha yao!—Marko 5:41, 42; ona pia Luka 7:11-16; Yohana 11:1-45.

13. Ni aina gani za watu watakaofufuliwa?

13 Katika ulimwengu mpya, “kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15) Wakati huo Yesu atatumia uwezo wake aliopewa na Mungu kuinua wafu kwa sababu, kama alivyosema, “Mimi ndimi huo ufufuo, na uzima. Yeye aniaminiye mimi, ajapokufa, atakuwa anaishi.” (Yohana 11:25) Alisema pia: “Wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake [Yesu] nao watatoka.”—Yohana 5:28, 29.

14. Kwa sababu kifo hakitakuwapo tena, ni vitu gani vitakavyoondolewa?

14 Shangwe itakuwa kuu duniani pote wakati kikundi baada ya kikundi cha watu wafu warudipo kwenye uhai kujiunga na wapendwa wao! Hakutakuwako tena safu za majina ya wafu magazetini kuleta huzuni kwa waliofiwa. Badala ya hivyo, yaelekea sana kutakuwako kinyume kabisa: matangazo ya waliofufuliwa karibuni kuleta shangwe kwa wale waliowapenda. Hivyo hakutakuwako tena maziko, mioto ya kuchomea maiti, mahali pa kuchomea maiti, au makaburi!

Ulimwengu Wenye Amani Kweli Kweli

15. Unabii wa Mika utatimizwaje katika maana kamili?

15 Amani ya kweli katika maeneo yote ya maisha itapatikana. Vita, wachochezi wa vita, na watengenezaji wa silaha watakuwa vitu vya wakati uliopita. Kwa nini? Kwa sababu masilahi yenye kugawanya ya kitaifa, kikabila, na kijamii yatatoweka. Ndipo, katika maana kamili, “taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”—Mika 4:3.

16. Mungu atahakikishaje kwamba haitawezekana kupigana vita?

16 Huenda hilo likaonekana kuwa jambo lenye kushangaza kwa sababu ya historia ya mwanadamu ya kutaka kumwaga damu katika vita vya daima. Lakini imekuwa hivyo kwa sababu ainabinadamu imekuwa chini ya utawala wa kibinadamu na wa roho waovu. Katika ulimwengu mpya, chini ya utawala wa Ufalme, hili ndilo litakalotukia: “Njoni myatazame matendo ya BWANA [Yehova, NW] . . . Avikomesha vita hata mwisho wa dunia; avunja uta, akata mkuki, achoma moto magari [ya vita].”—Zaburi 46:8, 9.

17, 18. Ni uhusiano gani utakaokuwapo kati ya wanadamu na wanyama katika ulimwengu mpya?

17 Wanadamu na wanyama watakuwa pia na amani, kama walivyokuwa katika Edeni. (Mwanzo 1:28; 2:19) Mungu husema: “Nami siku hiyo nitafanya agano na wanyama wa mashamba kwa ajili yao, tena na ndege wa angani, tena na wadudu wa nchi; nami . . . nitawalalisha salama salimini.”—Hosea 2:18.

18 Amani hiyo itaenea kadiri gani? “Mbwa-mwitu atakaa pamoja na mwana-kondoo, na chui atalala pamoja na mwana-mbuzi; ndama na mwana-simba na kinono watakuwa pamoja, na mtoto mdogo atawaongoza.” Wanyama hawatakuwa tena kamwe tisho kwa mwanadamu au kwa wao wenyewe. Hata “simba atakula majani kama ng’ombe”!—Isaya 11:6-9; 65:25.

Dunia Yageuzwa Sura Kuwa Paradiso

19. Dunia itageuzwa sura iwe nini?

19 Dunia yote itageuzwa sura kuwa makao ya paradiso kwa ajili ya ainabinadamu. Ndiyo sababu Yesu angeweza kumwahidi mwanamume aliyemwamini: “Wewe utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” Biblia husema hivi: “Nyika na mahali palipo ukiwa patafurahi; jangwa litashangilia na kuchanua maua kama waridi. . . . Maana katika nyika maji yatabubujika; na vijito jangwani.”—Luka 23:43, NW; Isaya 35:1, 6.

20. Kwa nini njaa haitasumbua ainabinadamu tena kamwe?

20 Chini ya Ufalme wa Mungu, njaa haitasumbua mamilioni tena kamwe. “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.” “Na mti wa kondeni utazaa matunda yake, nayo ardhi itatoa mazao yake, nao watakuwa salama katika nchi yao.”—Zaburi 72:16; Ezekieli 34:27.

21. Itakuwaje na ukosefu wa makao, mitaa michafu-michafu, na mitaa-jirani mibaya?

21 Hakutakuwapo tena umaskini, watu wasio na makao, mitaa michafu-michafu, au mitaa-jirani iliyojaa uhalifu. “Nao watajenga nyumba, na kukaa ndani yake; watapanda mizabibu, na kula matunda yake. Hawatajenga, akakaa mtu mwingine ndani yake; hawatapanda, akala mtu mwingine.” “Wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.”—Isaya 65:21, 22; Mika 4:4.

22. Biblia huelezaje baraka za utawala wa Mungu?

22 Wanadamu watabarikiwa na vitu hivyo vyote, na zaidi, katika Paradiso. Zaburi 145:16 husema: “[Wewe Mungu] waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.” Si ajabu unabii wa Biblia hujulisha wazi hivi: “Wenye upole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani. . . . Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.”—Zaburi 37:11, 29.

Kubatilisha ya Wakati Uliopita

23. Ufalme wa Mungu utabatilishaje kuteseka kote ambako tumepata?

23 Utawala wa Ufalme wa Mungu utabatilisha madhara yote ambayo familia ya kibinadamu ilitendewa kwa miaka elfu sita iliyopita. Shangwe za wakati huo zitazidi sana kuteseka kokote ambako watu walipata. Maisha hayatasumbuliwa na kumbukumbu mbaya za kuteseka kwa wakati uliopita. Yale mawazo yenye kujenga na utendaji ambao utakuwa maisha ya kila siku ya watu utafuta polepole kumbukumbu zenye kuumiza.

24, 25. (a) Isaya alitabiri kungetukia nini? (b) Kwa nini tunaweza kuwa na hakika kwamba kumbukumbu za kuteseka kwa wakati uliopita zitafifia?

24 Mungu mwenye kujali ajulisha wazi hivi: “Mimi naumba mbingu mpya [serikali mpya ya kimbingu juu ya ainabinadamu] na nchi mpya [jamii ya kibinadamu yenye uadilifu], na mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo.” “Dunia yote inastarehe na kutulia; hata huanzilisha kuimba.”—Isaya 65:17, 18; 14:7.

25 Hivyo kwa njia ya Ufalme wake, Mungu atapindua kabisa ile hali mbaya ambayo imedumu muda mrefu sana. Muda wote wa umilele ataonyesha kutujali sana kwa kumimina chini baraka ambazo zitalipia na kuzidi dhara lolote ambalo tulipata wakati wetu uliopita. Taabu za wakati uliopita ambazo tumepata zitafifia wakati huo, na kuwa kumbukumbu hafifu ikiwa kwa vyovyote tutataka kuzikumbuka.

26. Kwa nini Mungu atatulipia kwa sababu ya kuteseka kokote kwa wakati uliopita?

26 Hivyo ndivyo Mungu atatulipia kuteseka ambako huenda tukawa tulivumilia katika ulimwengu huu. Yeye ajua kwamba halikuwa kosa letu kwamba tulizaliwa tukiwa tusiokamilika, kwa kuwa tulirithi kutokamilika kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza. Si kosa letu kwamba tulizaliwa katika ulimwengu wa kishetani, kwa kuwa badala ya hivyo, kama Adamu na Hawa wangalikuwa waaminifu, sisi tungalizaliwa katika paradiso. Hivyo kwa huruma kuu Mungu atatimiza mengi hata zaidi ya kulipia tu wakati mbaya uliopita tulioletewa.

27. Ni unabii gani mbalimbali utakaopata utimizo wao mzuri ajabu katika ulimwengu mpya?

27 Katika ulimwengu mpya, ainabinadamu itapata uhuru uliotabiriwa kwenye Warumi 8:21, 22: “Viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu. Kwa maana twajua ya kuwa viumbe vyote pia vinaugua pamoja, navyo vina utungu pamoja hata sasa.” Ndipo watu wataona utimizo kamili wa ile sala: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.” (Mathayo 6:9, 10) Zile hali nzuri ajabu katika dunia-Paradiso zitaonyesha jinsi hali zilivyo mbinguni.

[Picha katika ukurasa wa 23]

Katika ulimwengu mpya, wazee-wazee watarudia nguvu za ujana

[Picha katika ukurasa wa 24]

Magonjwa na kutojiweza kote kutaondolewa mbali katika ulimwengu mpya

[Picha katika ukurasa wa 25]

Katika ulimwengu mpya, wafu watafufuliwa waje kwenye uhai

[Picha katika ukurasa wa 26]

‘Hawatajifunza vita tena’

[Picha katika ukurasa wa 27]

Wanadamu na wanyama watakaa katika amani kamili katika Paradiso

[Picha katika ukurasa wa 27]

‘Mungu atafumbua mkono wake na kushibisha matakwa ya kila kilicho hai’

[Picha katika ukurasa wa 28]

Ufalme wa Mungu utatimiza mengi zaidi ya kulipia tu kuteseka kote ambako tumevumilia

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki