Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • g91 6/8 kur. 10-13
  • Ulimwengu Mpya Usio na Taabu

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ulimwengu Mpya Usio na Taabu
  • Amkeni!—1991
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Hayo Yalitangulia Kutolewa Kivuli Katika Unabii Mbalimbali
  • Yaliyopita Hayatadhuru
  • Utawala Tofauti
  • ‘Viumbe Vyawekwa Huru’
  • ‘Wakati Uliowekwa’
  • “Ridhaa”
  • Maoni Yenye Kufikia Mbali
  • Wewe Utachagua Nini?
  • Muda Ambao Mungu Ameruhusu Kuteseka Wakaribia Kwisha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2001
  • Kuteseka Kote Kutaisha Karibuni!
    Kuteseka Kote Kutaisha Karibuni
  • Ule Ulimwengu Mpya Mzuri Ajabu Wenye Kufanyizwa Na Mungu
    Je, Kweli Mungu Anatujali?
  • Yatakayofanywa na Ufalme wa Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2000
Pata Habari Zaidi
Amkeni!—1991
g91 6/8 kur. 10-13

Ulimwengu Mpya Usio na Taabu

“Mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini furahini, mkashangilie daima, kwa ajili ya hivi niviumbavyo.”—Isaya 65:17, 18.

MANENO hayo ya kiunabii yalipuliziwa na Mungu zaidi ya miaka 2,700 iliyopita. Yanaeleza, kwa sehemu, maisha yatakavyokuwa duniani wakati ujao. Wakati gani? Baada ya Mungu kumaliza mfumo wa mambo uliopo sasa. Unabii mwingi mbalimbali wa Biblia huonyesha wazi kwamba ni kusudi la Mungu kuondoa mfumo huu wa mambo uliopo baada ya muda mfupi na mahali pake pachukuliwe na ulimwengu mpya usio na taabu.

Jinsi maisha yatakavyokuwa tofauti katika ulimwengu huo mpya yakilinganishwa na maisha wakati wa historia yote ya kibinadamu iliyopita! Neno la kiunabii la Mungu latuambia kwamba yatakuwa huru kabisa na vita, uhalifu, umaskini, na ukosefu wa haki. Ugonjwa na kifo vitakuwa vimeondolewa kwa umilele. Hakutakuwako tena serikali, dini, au mifumo ya kiuchumi yenye kugawanya ambayo imethibitika kuwa imepungukiwa sana. Machozi ya furaha tele yatachukua mahali pa huzuni kwa sababu uovu na taabu vitakuwa vimeondolewa milele.

Hayo Yalitangulia Kutolewa Kivuli Katika Unabii Mbalimbali

Angalia jinsi hali hizo zilivyotangulia kutolewa kivuli katika unabii huu mbalimbali wa Biblia wa kuonja-onja:

Vita Hakuna Tena: “Avikomesha vita hata mwisho wa dunia.” (Zaburi 46:9) “Taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine.”—Isaya 2:4.

Haki kwa Kila Mmoja: “Nami nitafanya hukumu [haki, NW] kuwa ndiyo kanuni, na haki [uadilifu, NW] kuwa ndiyo timazi.”—Isaya 28:17.

Uhuru Bila Hofu: “Wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.” (Mika 4:4) “Nao watakuwa salama katika nchi yao.”—Ezekieli 34:27.

Njaa Hakuna: “Na uwepo wingi wa nafaka katika ardhi juu ya milima.” (Zaburi 72:16) “Na mti wa kondeni utazaa matunda yake, nayo ardhi itatoa mazao yake.”—Ezekieli 34:27.

Hakuna Uzee wala Ugonjwa Tena: “Nyama ya mwili wake itakuwa laini kuliko ya mtoto; huzirudia siku za ujana wake.” (Ayubu 33:25) “Hapana mwenyeji atakayesema, Mimi mgonjwa.”—Isaya 33:24.

Kifo, Maombolezo, na Maumivu Vimetoweka Milele: “[Mungu] atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena; wala maombolezo, wala kilio, wala maumivu hayatakuwapo tena; kwa kuwa mambo ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:4.

Yaliyopita Hayatadhuru

Ulimwengu mpya unaokuja wenye kufanyizwa na Mungu utaridhisha sana hivi kwamba kufurahiwa kwa maisha na wakaaji wa dunia hakutazuiwa, hata na kumbukumbu zozote zisizopendeza za taabu ya wakati uliopita. Yale mawazo na utendaji mbalimbali mwingi wenye kujenga ambao utakuwa maisha ya kila siku ya watu katika kipindi hicho kipya yatafuta polepole kumbukumbu mbaya za wakati uliopita. Ahadi ya Mungu ni hii: “Mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.” Watu ‘watashangilia daima’ ambacho Mungu ataanzisha duniani pote. “Dunia yote inastarehe na kutulia; hata huanzilisha kuimba.”—Isaya 65:17, 18; 14:7.

Leo, “kilichotarajiwa kikikawia kuja, moyo huugua,” kama isemavyo Biblia. Lakini hali hiyo itageuzwa katika ulimwengu mpya huo. Wakati huo “haja ya mtu [itakuwa], ni mti wa uzima.” (Mithali 13:12) Mioyo haitahuzunishwa tena na taabu wala matumaini yasiyotimizwa. Badala yake, itajazwa na uradhi na shangwe kwa sababu ya mambo mengi mazuri ajabu ambayo Mungu ataipa familia ya kibinadamu.

Utawala Tofauti

Badala ya kuwa na utawala wa kibinadamu usioridhisha ambao hautegemei Mungu, ulimwengu huo mpya utakuwa na utawala ulio tofauti kabisa. Mamlaka ya kutawala itaondolewa mikononi mwa wanadamu. Hawataruhusiwa tena kamwe watawale bila ya kutegemea Mungu.

Unabii wa Biblia wasema hivi: “Katika siku za wafalme hao [watawala walio katika mamlaka sasa] Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [katika mbingu] ambao hautaangamizwa milele, wala watu wengine hawataachiwa enzi yake [hakutakuwako tena utawala wa kibinadamu]; bali utavunja falme hizi zote [zilizopo sasa] vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.

Yesu alifundisha wafuasi wake wasali kwa ajili ya utawala mpya wa dunia aliposema hivi: “Ufalme wako uje, mapenzi yako yatimizwe, hapa duniani kama huko mbinguni.”—Mathayo 6:9, 10.

Huo utakuwa ndio utawala mpya wa ainabinadamu—utawala wa kimbingu wa Mungu kupitia Ufalme wake ukiwa mikononi mwa Kristo. Na juu ya dunia, watumishi wa kibinadamu wa Mungu walio waaminifu-washikamanifu watasimamia mambo kwa kulingana na uelekezi wa Mungu. (Isaya 32:1) Mtume Petro alisema juu ya mpango huo kuwa “mbingu mpya na nchi [dunia, NW] mpya, ambayo haki yakaa ndani yake.” (2 Petro 3:13) Utawala huo wa Ufalme ndio fundisho kuu la Biblia.

‘Viumbe Vyawekwa Huru’

Utawala huo mpya utaongoza kikamili pia nguvu za asili za dunia. ‘Vitendo vya asili’ kama matetemeko ya dunia, vimbunga, mafuriko, wala ukame havitaleta dhiki tena. Yesu mwenyewe alionyesha uwezo wake katika kuamuru nguvu hizo. Kwa kielelezo, katika pindi moja, wakati mashua ambayo Yesu na wanafunzi wake walikuwa ndani yake ilipokaribia kuzama katika tufani, yeye alituliza upepo na bahari. Wanafunzi waliostaajabu walijulisha rasmi hivi: “Huyu ni mtu wa namna gani hata pepo na bahari zamtii?”—Mathayo 8:23-27.

Kwa hiyo dunia, na pia viumbe vya kibinadamu, vitapata uhuru usio na kifani. “Viumbe vyenyewe navyo vitawekwa huru na kutolewa katika utumwa wa uharibifu, hata viingie katika uhuru wa utukufu wa watoto wa Mungu. Kwa maana twajua ya kuwa viumbe vyote pia vinaugua pamoja, navyo vina utungu pamoja hata sasa.”—Warumi 8:21, 22.

Je! twaweza kuwa na uhakika kwamba utawala wa kibinadamu karibuni utamalizika na kwamba serikali mpya ya Mungu itatwaa mamlaka ya kuelekeza mambo yote ya dunia? Hakika ndivyo, kwa sababu Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima ameahidi: “Shauri langu litasimama, nami nitatenda mapenzi yangu yote. . . . Nimenena, nami nitatekeleza; nimekusudia, nami nitafanya.”—Isaya 46:10, 11.

‘Wakati Uliowekwa’

Hayo yatatokeaje? Yatatukia lini? Neno la Mungu lasema hivi: “Kwa kila jambo kuna majira yake [wakati uliowekwa, NW].” (Mhubiri 3:1) Hiyo ni kutia ndani wakati uliowekwa wa Mungu kusema ‘basi!’ na kumaliza uovu na taabu. Danieli alitaja juu ya “wakati wa mwisho ulioamriwa [uliowekwa, NW].” (Danieli 8:19) Yesu pia alisema juu ya “wakati uliowekwa.”—Marko 13:32, 33, NW.

Ndiyo, Mungu ameweka wakati kamili wa kujiingiza katika mambo ya kibinadamu na kuondoa jaribio lenye kuhuzunisha la utawala wa kibinadamu usiomtegemea. “Mungu atawahukumu wenye haki na wasio haki; kwa kuwa kuna wakati huko kwa kila kusudi na kwa kila kazi.” (Mhubiri 3:17) Na uthibitisho wa utimizo wa unabii wa Biblia waonyesha kwamba karibuni wakati uliowekwa wa Mungu kuruhusu taabu utamalizika. Kipimo hicho cha wakati kiishapo, yeye ataponda-ponda usiwepo tena mfumo wa utawala wa kibinadamu usioridhisha ambao kwa maelfu ya miaka umeleta taabu nyingi kwa familia ya binadamu.—Mathayo 24:3-14; 2 Timotheo 3:1-5, 13; Ufunuo 19:11-21.

Mungu atekelezapo hukumu zake, angalia yatakayowapata wale wanaonyenyekea utawala wake, tofauti na wale wasiofanya hivyo: “Maana bado kitambo kidogo asiye haki hatakuwapo, . . . bali wapole watairithi nchi, watajifurahisha kwa wingi wa amani.” “Bali mzao wa wasio haki ataharibiwa. Wenye haki watairithi nchi, nao watakaa humo milele.” “Umwangalie sana mtu mkamilifu, umtazame mtu mnyofu, maana mwisho wake mtu huyo ni amani. Wakosaji wataangamizwa pamoja, wasio haki mwisho wao wataharibiwa.”—Zaburi 37:10, 11, 28, 29, 37, 38; ona pia Mithali 2:21, 22; Mathayo 5:5.

Lakini vipi juu ya maelfu ya mamilioni ya watu ambao tayari wamekufa? Wao watafaidikaje na ulimwengu mpya? Kupitia ufufuo, kurudishwa kwenye uhai papa hapa duniani. Watatoka kaburini na kupewa nafasi ya kufurahia uhai milele. Neno la Mungu latoa uhakikisho huu: “Kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” (Matendo 24:15) Na Yesu alionyesha hilo kwa kufufua wafu, kama vile Lazaro na mwana wa yule mjane wa Naini.—Yohana 11:38-44; Luka 7:11-16.

“Ridhaa”

Inatia moyo kama nini kujua kwamba kusudi la Mungu ni kumaliza taabu na kuingiza ulimwengu mpya wenye uadilifu! Ebu fikiria juu ya mamilioni ya miaka—kwa kweli, milele—na afya kamili na furaha katika mazingira ya kiparadiso, ambapo uovu na taabu yatakuwa mambo ya wakati uliopita milele!

Je! wewe hungekubali kwamba “ridhaa” hiyo kutoka kwa Mungu kwa ainabinadamu—kwa umilele wote—kwa kulinganisha inazidi sana ile miaka maelfu machache ambayo Mungu ameruhusu taabu? Na pia je! haizidi sana ile miaka ya taabu 70 au 80—au michache—ambayo yawezekana kuwa sisi binafsi tumevumilia wakati wa maisha yetu?

Maoni Yenye Kufikia Mbali

Katika maoni yake ya mambo yenye kufikia mbali, Muumba ajua kwamba ni muhimu kwanza kusuluhisha yale mambo ya lazima ya haki yake ya utawala akiwa Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote Mzima na haki ya utawala wake. Na ilikuwa muhimu kusuluhisha lile jambo la matumizi yanayofaa na yasiyofaa ya uhuru wa kuchagua. Pia ilikuwa lazima kuonyesha kwamba uumbaji wake ni mkamilifu kwa njia ya kwamba wanadamu wanaojinyenyekeza kwa sheria zake za uadilifu wanaweza kuendeleza ukamilifu kwake chini ya mnyanyaso na mtihani wa watawala wa ulimwengu, kielelezo chenye kutokeza cha hilo kikiwa ni Mwana wake mwenyewe, Yesu, alipokuwa duniani.

Akiwa amemaliza masuala yote, Mungu hataruhusu uovu na taabu vitokee tena ili kuharibu ulimwengu wote mzima wenye amani. “Mateso hayatainuka mara ya pili.”—Nahumu 1:9.

Katika umilele wote utakaokuja, Mungu aweza kutumia yale yaliyotukia wakati wa maelfu haya ya miaka iliyopita kama kwamba ni mtihani wa kesi iliyoamuliwa katika mahakama kuu. Kitangulizi chayo chaweza kutumiwa wakati wowote ujao, popote katika ulimwengu wote mzima, endapo maswali hayo yatatokezwa tena kuhusiana na enzi kuu ya Mungu au matumizi yanayofaa ya hiari.

Wewe Utachagua Nini?

Leo tuna uchaguzi. Twaweza kutumia hiari yetu katika moja ya njia mbili: Twaweza kuchagua kupuuza makusudi ya Mungu, kuridhika na utawala wa kibinadamu usiokamilika na kuyashiriki yale yatakayoupata, au twaweza kutumia uhuru wetu wa kuchagua kujifunza makusudi ya Mungu juu ya tunachohitaji kufanya ili tumpendeze tukiwa raia waliojitoa wa Ufalme wake.

Yesu alimwambia Mungu katika sala hivi: “Na uzima wa milele ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli na Yesu Kristo uliyemtuma.” (Yohana 17:3) Kwa hiyo ikiwa twataka uhai katika ulimwengu mpya wa Mungu, twahitaji kufanya jitihada ya kujifunza kweli juu ya Mungu, makusudi yake, na matakwa yake. Angalia jinsi Biblia inavyolisema hilo: “BWANA [Yehova, NW] yu pamoja nanyi, mkiwa pamoja naye; nanyi mkimtafuta ataonekana kwenu; lakini mkimwacha atawaacha ninyi.”—2 Mambo ya Nyakati 15:2.

Wakati wa ulimwengu huu wa kale unakwisha; mwingine mpya uko njiani ukija: “Dunia [ulimwengu, NW] inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele.” (1 Yohana 2:17) Utachagua nini—ulimwengu wa kale unaoondoka au ule mpya unaokuja?

Neno la Mungu lasema hivi: “Nimekuwekea mbele yako uzima na mauti, baraka na laana; basi chagua uzima ili uwe hai, wewe na uzao wako; kumpenda BWANA [Yehova, NW], Mungu wako, kuitii sauti yake, na kushikamana naye; kwani hiyo ndiyo uzima wako, na wingi wa siku zako.”—Kumbukumbu la Torati 30:19, 20.

Je! ni tamaa yako kufurahia mibaraka ambayo Mungu ameweka akiba kwa ajili ya wale wanaopatanisha mapenzi yao na yake? Watangazaji wa gazeti hili au Mashahidi wa Yehova mahali popote ulimwenguni watafurahi kukusaidia, bila malipo, upate kujifunza mengi juu ya hilo.

[Blabu katika ukurasa wa 12]

Wafu watapata nafasi ya kuishi katika ulimwengu mpya wa Mungu kwa kufufuliwa kutoka kaburini

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki