Kuteseka Kote Kutaisha Karibuni!
Huenda umewahi kujiuliza, ‘Kwa nini wanadamu wanateseka sana?’ Wanadamu wameteseka sana kwa maelfu ya miaka kwa sababu ya vita, umaskini, misiba, uhalifu, dhuluma, magonjwa, na kifo. Wanadamu wameteseka sana katika miaka mia moja iliyopita kuliko wakati mwingine wowote. Je, yote hayo yatapata kwisha?
Inafariji kujua kwamba yatakwisha hivi karibuni! Neno la Mungu, Biblia, linasema: “Mtu mwovu hatakuwako tena . . . Bali wapole wataimiliki dunia, Nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.” Kwa muda gani? “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:10, 11, 29.
Baada ya Mungu kuondoa uovu na kuteseka, dunia itakuwa paradiso. Kisha watu wataishi milele wakiwa na furaha na afya kamili. Neno la Mungu linatabiri: “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena.”—Ufunuo 21:4.
Katika ulimwengu huo mpya, wafu watafufuliwa ili pia wafurahie baraka hizo: “Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.” (Matendo 24:15) Ndiyo sababu Yesu Kristo alimwambia hivi yule mtenda-maovu aliyetubu na kumwamini: “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”—Luka 23:43.
Mwanzo wa Kuteseka
Kwa kuwa Mungu alikusudia wanadamu wawe na maisha mazuri ya wakati ujao, kwa nini hakuzuia kuteseka? Kwa nini ameacha wanadamu wateseke kwa muda mrefu hivyo?
Mungu alipowaumba Adamu na Hawa, walikuwa wakamilifu kimwili na kiakili. Aliwaweka katika paradiso na kuwapa kazi yenye kuridhisha. Biblia inasema: “Mungu akaona kila kitu alichokuwa amefanya na, tazama! kilikuwa chema sana.” (Mwanzo 1:31) Ikiwa wangemtii Mungu, wangezaa watoto wakamilifu, na dunia ingekuwa paradiso, ambamo watu wangeishi milele kwa amani na furaha.
Mungu aliwaumba Adamu na Hawa wakiwa na zawadi nzuri sana ya uhuru wa kuchagua. Hawakutazamiwa watende kama mashine zisizo na akili. Hata hivyo, ili waendelee kuwa na furaha, walihitaji kutumia uhuru wao kwa njia inayofaa, kwa kutii sheria za Mungu. Mungu anasema: “Mimi, Yehova, ni Mungu wako, Yeye anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake.” (Isaya 48:17) Kutumia vibaya uhuru huo kungewaletea msiba, kwa kuwa wanadamu hawakuumbwa wajitegemee. Biblia inasema: “Njia ya mtu wa udongo haimo katika uwezo wake. Mwanadamu anayetembea hana uwezo wa kuongoza hatua yake.”—Yeremia 10:23.
Inasikitisha kwamba wazazi wetu wa kwanza walidhani wangefanikiwa maishani pasipo kumtegemea Mungu. Lakini, walipoukataa utawala wa Mungu, walipoteza kibali chake na ukamilifu wao. Kwa hiyo wakaanza kudhoofika na mwishowe wakazeeka na kufa. Tumerithi kutokamilika na kifo kutoka kwao.—Waroma 5:12.
Ni Nani Aliye na Haki ya Kutawala?
Kwa nini Mungu hakuwaharibu Adamu na Hawa na kuumba wanadamu wengine? Kwa sababu haki ya Mungu ya kutawala ilikuwa imepingwa. Swali lililozuka ni, Ni nani aliye na haki ya kutawala, na ni utawala wa nani unaofaa? Kwa hiyo, Je, wanadamu wangefanikiwa ikiwa hawangekuwa chini ya utawala wa Mungu? Kwa kuwapa wakati wa kutosha na uhuru kamili, Mungu angethibitisha kabisa ikiwa wangefanikiwa wakiwa chini ya utawala Wake au wakijitawala wenyewe. Wanadamu walipewa muda wa kutosha kujaribu mifumo yote ya kisiasa, kijamii, kiuchumi, na kidini pasipo uongozi wa Mungu.
Matokeo yamekuwa nini? Historia imethibitisha kwamba wanadamu wamezidi kuteseka kwa maelfu ya miaka. Katika karne iliyopita wanadamu waliteseka kupindukia. Mamilioni ya watu walikufa katika Vita vya Pili vya Ulimwengu. Zaidi ya watu milioni 100 wameangamia katika vita vinginevyo. Kumekuwa na ongezeko kubwa la uhalifu na jeuri. Dawa za kulevya zinatumiwa kotekote ulimwenguni. Magonjwa ya zinaa yanaendelea kusambaa. Kila mwaka mamilioni ya watu hufa kutokana na njaa na magonjwa. Maisha ya familia na maadili yamezorota kila mahali. Serikali za wanadamu haziwezi kutatua matatizo hayo. Hakuna hata moja imefaulu kuondolea mbali uzee, magonjwa, na kifo.
Hali za wanadamu leo zinapatana na unabii wa Biblia. Neno la Mungu linaziita nyakati zetu “siku za mwisho” za ulimwengu huu, wakati ambapo “kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” Na kama Biblia ilivyosema, ‘watu waovu na wajanja wanaendelea kutoka ubaya mpaka ubaya zaidi.’—2 Timotheo 3:1-5, 13.
Kuteseka Kutaisha Karibuni
Uthibitisho wote unaonyesha kwamba tunakaribia mwisho wa jitihada za wanadamu za kujitegemea ambazo zimeambulia patupu. Imeonekana wazi kwamba wanadamu hawawezi kufanikiwa bila kumtegemea Mungu. Utawala wa Mungu tu ndio unaoweza kuleta amani, furaha, afya kamili, na uzima wa milele. Kwa hiyo, hivi karibuni Yehova hatavumilia tena uovu na kuteseka. Karibuni Mungu ataingilia kati na kuuharibu ulimwengu huu mbovu.
Unabii wa Biblia unasema: “Katika siku za wafalme hao [watawala wa kibinadamu wa leo], Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [mbinguni] ambao hautaharibiwa kamwe. . . . Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote [tawala za sasa], nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” (Danieli 2:44) Biblia inafundisha kwamba Ufalme wa mbinguni wa Mungu utatetea haki ya Yehova ya kutawala. Yesu alipotabiri kuhusu sehemu muhimu ya ishara ya “siku za mwisho” alisema: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.
Ni nani watakaookoka mwisho utakapokuja? Biblia inajibu: “Wanyoofu ndio watakaokaa duniani, na wasio na lawama ndio watakaobaki ndani yake. Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani.” (Methali 2:21, 22) Wanyoofu ni wale wanaojifunza mapenzi ya Yehova na kuyafanya. Yesu Kristo alisema: “Uzima wa milele ndio huu, waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.” (Yohana 17:3) Naam, “ulimwengu unapitilia mbali . . . , lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.”—1 Yohana 2:17.
Isipokuwa imeonyeshwa vingine, manukuu yote ya Maandiko yametoka katika Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.