Je! Mungu Anajali?
1, 2. (a) Je! maulizo yaliyoandikwa katika fungu la kwanza ni yale ambayo wewe umepata kuuliza? (b) Ni hali gani zinazofanya watu waulize maulizo hayo?
IKIWA Mungu ni Mwenye Nguvu Zote, sababu gani ameruhusu mambo mengi yaliyo mabaya sana? Ikiwa kweli anatujali sisi, sababu gani anaruhusu uovu na kuteseka kuendelee?
2 Kila mahali watu wenye kufikiri wanauliza maulizo hayo. Na wana sababu nzuri ya kuuliza hivyo, maana kwa karne nyingi jamaa ya kibinadamu imeteswa sana na vita vibaya sana, upungufu wa chakula, umaskini, uhalifu na magonjwa. Udhalimu na uonezi umesababisha huzuni nyingi pia. Vivyo hivyo na misiba kama vile mafuriko na matetemeko ya ardhi. Mara nyingi, watu wasio na hatia wanateseka. Je! yote hayo ni ushuhuda wa kwamba Mungu hajali yanayotupata? Je! kuna tumaini lo lote la kweli la kuwa na ulimwengu bora, ulimwengu ambamo tunaweza kufurahia kabisa uzima duniani, pasipo taabu zote hizo?
3. Kwa nini ni jambo la busara kuweza kupata majibu ya maulizo hayo?
3 Maulizo hayo yanataka majibu ya kweli na yenye kuridhisha. Lakini si kweli, wala hairidhishi, kuambiwa “Mungu anataka tuteseke ati,” au, “Hayo ni mambo tusiyoweza kufahamu.” Ikiwa Mungu aliuumba ulimwengu mzima huu ulio mkubwa mno na wa utaratibu hivyo, bila shaka lazima awe na sababu nzuri ya kuruhusu wanadamu wavurugike hivyo. Je! Muumba kama huyo hawezi kujali sana uumbaji wake wa kibinadamu hata atuambie sababu iliyomfanya aruhusu uovu? Je! yeye hangeona ni jambo la busara kuondoa hali mbaya hizo katika wakati wake ikiwa ana uwezo wa kufanya hivyo? Baba ye yote mwenye upendo angefanyia watoto wake hivyo ikiwa angeweza. Hakika Muumba mwenye uwezo wote, hekima yote na upendo, hangekosa kufanyia hivyo watoto wake wa kidunia.
Nani Anaweza Zaidi Kujibu?
4. Ni nani anayeweza zaidi kutuambia sababu iliyomfanya Mungu aruhusu uovu?
4 Nani anaweza zaidi kuyajibu maulizo yale juu ya Mungu kuruhusu uovu? Haya, ikiwa ungeshtakiwa kosa fulani, je! ungetaka watu wasikilize yanayosemwa na wengine tu? Au ungetaka ujisemee mwenyewe ili uondoe shaka lililo katika akili za ye yote ambaye angetaka kujua kwa unyofu wa moyo? Ni Mungu anayeshtakiwa kosa la kuruhusu uovu. Kwa kuwa yeye ndiye anajua zaidi sababu ya kuuruhusu, je! haingefaa kumwacha ajisemee mwenyewe? Kutumaini kupata majibu kwa wanadamu hakutaridhisha kamwe, maana mara nyingi wana mawazo yanayopingana juu ya mambo hayo.
5. Je! ni jambo la busara kuamini kwamba Mungu ndiye alitunga Biblia? (2 Petro 1:21; Habakuki 2:2)
5 Mungu anatoa majibu wapi? Kuna chanzo kimoja tu ambacho Muumba anadai amekiruhusu kituambie lililotendeka na sababu gani lilitendeka. Chanzo hicho ni ile Biblia, inayosema: “Maandiko yote matakatifu yameandikwa kwa uongozi wa Mungu.” (2 Timoteo 3:16, HNWW) Hilo lisishangaze, kwa sababu ikiwa Mungu alikuwa na uwezo wa kuumba ulimwengu mzima wenye kustaajabisha, bila shaka angeweza kuwa mtungaji wa kitabu. Wanadamu wa vivi hivi wanaweza kupeleka sauti na mawazo, hata picha, katika radio au televisheni yako kupitia mawimbi ya upepo yasiyoonekana. Basi haingekuwa kazi kubwa kwa Muumba mwenye nguvu zote kupelekea waandikaji waaminifu wa kibinadamu mawazo yake na kuhakikisha wameyaandika kwa usahihi. Ndiyo sababu mtume Paulo aliweza kusema akiwa na hakika: “Mlipopata lile neno la ujumbe la Mungu mlilolisikia kwetu, mlilipokea si kama neno la wanadamu, bali kama neno la Mungu; na ndivyo lilivyo kweli kweli.”—1 Wathesalonike 2:13.
6. Historia ya Biblia inarudi nyuma mpaka wapi, na kwa sababu hiyo, ni habari gani tunayoweza kupewa na Biblia? (Luka 1:1-4; angalia Luka 3:23-38.)
6 Labda hujapata kuichunguza Biblia. Hata hivyo huenda ukapendezwa kujua kwamba hiyo ndiyo yenye habari za kihistoria na tarehe zilizo kamili zaidi ya zote zinazopatikana leo. Kwa kweli, Luka, mwanahistoria na daktari wa karne ya kwanza, aliweza kufuatia ukoo wa Yesu wa Nazareti wenye muda wa miaka 4,000 ya historia, hatua kwa hatua, jina kwa jina, mpaka kurudi kwa yule mtu wa kwanza. Kwa kuwa Biblia inarudia mwanzo wenyewe wa kuwako kwa wanadamu, inaweza kutuambia mtu anayefaa kulaumiwa kwa sababu ya uovu, sababu Mungu ameuruhusu, na utakavyoondolewa.
Je! Mungu Ndiye wa Kulaumiwa?
7. Makosa yanapofanywa, ni nani anayepaswa kulaumiwa?
7 Kama mtu mwingine angefanya uhalifu fulani, ungeonaje ikiwa ni wewe ungelaumiwa kuwa umeufanya? Ungeliona jambo hilo kuwa la udhalimu sana. Haki yataka mwenye hatia aadhibiwe na yule asiye na hatia aondolewe lawama. Ikiwa dereva wa motokaa anapuza ishara inayosema simama penye barabara-panda yenye magari mengi, na basi anapata aksidenti mbaya, hilo si kosa la sheria hiyo. Ikiwa mtu anakuwa mlafi kisha anakuwa mgonjwa kwa kula kupita kiasi, hilo si kosa la mkulima aliyelima chakula hicho. Ikiwa, ajapopewa malezi mazuri, kijana anaondoka nyumbani, anapuza shauri zuri la baba yake kisha anaumia, baba siye wa kulaumiwa. Basi kwa nini yule Baba wa kimbingu, Mungu, alaumiwe wakati wanadamu wanapofanya makosa? Je! si inafaa mwenye hatia ndiye alaumiwe?
8. Ni kupingana gani kwa maneno kunakotokea ikiwa tunamlaumu Mungu kwa sababu ya mabaya?
8 Pia, kuna jambo jingine la kufikiria. Ikiwa tunamlaumu Mungu kwa sababu ya mambo kama vile kufa njaa kwa kupungukiwa na chakula, basi tutasema ni nani anayefanya mashamba ya nafaka na ya matunda yatoe mazao mengi hivyo katika nchi nyingi? Tukimlaumu Mungu kwa sababu ya magonjwa, basi tutasema ni nani aliyeufanya mwili kuwa na mifumo ya ajabu ya kuponesha magonjwa? Ikiwa tunamlaumu Mungu kwa sababu ya mitaa yenye nyumba chafu-chafu mjini, basi tutasema ni nani aliyefanya milima yenye fahari, maziwa yenye maji safi sana, maua yenye kupendeza na miti mizuri? Kwa wazi, tukimlaumu Mungu kwa sababu ya taabu za ulimwengu kisha tuseme ndiye anayetoa vitu vizuri vya dunia hii, tunapinganisha maneno. Mungu mwenye upendo hawezi kuendeleza mema na mabaya wakati ule ule.
9. Je! ni jambo la akili kusema kwamba hakuna Mungu kwa sababu tu wanadamu wanafanya mabaya? (Isaya 45:18)
9 Kusema kwamba hakuna Mungu ni kufanya tatizo liwe kubwa zaidi. Kuamini kwamba dunia hii na namna zake za ajabu za uhai zilijitokeza zenyewe ni kupuza mambo ya hakika. Ukweli ni kwamba dunia hii ina vitu vya kuendeleza uhai kuliko nyumba yo yote, na hali kila nyumba ina mbuni na mjenzi mwenye akili. Basi namna gani sayari hii yenye mifumo ya hewa, ardhi na maji ya kuendeleza uhai, mifumo iliyo bora kupita yote? Biblia inasema hivi kwa kufaa: “Kila nyumba imejengwa na mutu; lakini yeye aliyejenga vitu vyote ni Mungu.” (Waebrania 3:4, ZSB) Kweli, watu fulani wanakata shauri kwamba kwa kuwa wanadamu wanafanya mabaya, hakuna Mungu. Walakini, hiyo ni kama kusema kwamba kwa kuwa watu wanaoishi katika nyumba wanafanya mabaya, basi nyumba hazina wabuni wala wajenzi. Pia ingekuwa kama kusema kwamba kwa kuwa mtu anafanya kosa fulani, yeye hajapata kamwe kuwa na baba-mzazi.
10. Ni nani tunayepaswa kulaumu zaidi kwa sababu ya uovu?
10 Basi, ni nani wa kulaumiwa kwa mabaya makubwa sana ambayo yameipata jamaa ya kibinadamu? Sehemu kubwa ya lawama lazima iwakalie watu wenyewe. Udanganyifu na kuvurugika akili kwa wanadamu husababisha uhalifu. Kiburi na choyo cha kibinadamu kinasababisha ndoa zenye kuvunjika, chuki na ubaguzi wa rangi. Makosa ya wanadamu na kutojail kwao husababisha uchafu na takataka. Majivuno ya kibinadamu na upumbavu wao husababisha vita. Na mataifa mazima yanapofuata viongozi wa kisiasa kwa upofu katika vita hivyo, ni lazima washiriki lawama la hali za kuteseka zinazotokea. Njaa na umaskini zinatokea hasa kwa sababu ya kutojali na pupa ya wanadamu. Ebu fikiri: sasa ulimwengu huu unapoteza madola zaidi ya bilioni 200 ya fedha kila mwaka ili kuunda au kununua silaha. Kama fedha zote hizo zingetumiwa vizuri kwenye kilimo na kugawia watu wote chakula kwa usawa na kuondoa nyumba zisizofaa, fikiria mambo ambayo yangeweza kutimizwa!
11. Kwa kuwa makasisi wanatoa sala kwa ajili ya majeshi ya mataifa yao, je! Mungu ndiye wa kulaumiwa kwa vita vinavyopigwa na majeshi hayo? (Isaya 1:15: Mithali 28:9)
11 Wala Mungu si wa kulaumiwa kwa mabaya yanayotendwa kwa kutumia dini. Kwa mfano, makasisi wanasali Mungu abariki vita vya mataifa yao. Hata hivyo, mara nyingi, katika pande tofauti, wale askari wanaouana ni wa dini moja! Mungu hawezi kulaumiwa kwa jambo hilo, kwa sababu yeye anapinga sana wanayofanya, akisema kwamba ni lazima wale wanaomtumikia kweli kweli ‘wapendane’ (Yohana 13:34, 35) lkiwa hawana upendo huo, basi Mungu anasema wao ni “kama Kaini alivyokuwa wa yule mwovu, akamwua ndugu yake.” (1 Yohana 3:10-12) Kuua watu kwa kutumia jina la Mungu, iwe ni wakati wa kutesa wenye kuanzisha dini mpya au katika vita, ni sawa na lile zoea la kale la kutoa watoto wawe sadaka kwa miungu ya uongo, jambo ambalo Mungu Mwenye Nguvu Zote anasema ‘hakuliagiza wala halikuingia moyoni mwake.’—Yeremia 7:31.
12. Kwa nini makasisi wa kidini wanaitwa “wanafiki” katika Biblia? (Mathayo 15:7-9)
12 Kujiingiza kwa makasisi katika siasa, kuunga mkono vita, na mafundisho yao ya uongo kama kusema kwamba Mungu ndiye analeta mateso hayo ya ulimwengu, au kwamba hata anachoma watu milele katika moto halisi, yanachukiza sana watu wenye kufikiri, na Mungu pia. Viongozi wa kidini wanaofundisha na kuzoea mambo yanayopingana na Mungu wanaitwa “wanafiki” katika Neno la Mungu, linalowaambia hivi pia: “Mko kama makaburi yaliyopakwa chokaa ambayo kwa nje yanaonekana kuwa mazuri lakini ndani yamejaa mifupa ya maiti na kila namna ya uchafu.” (Matayo 23:27, 28, HNWW) Kwa kweli, Yesu alisema hivi juu ya viongozi wa kidini wenye unafiki: “Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi.”—Yohana 8:44.
13. (a) Basi, Mungu alaumiwe wakati wanadamu, hata viongozi wa kidini, wanapofanya mabaya? (b) Hata hivyo, ni maulizo gani ambayo huenda bado yakaulizwa?
13 La, Mungu si wa kulaumiwa kwa makosa hayo ambayo wanadamu wenyewe wanafanya. Na si wa kulaumiwa kwa makosa yale yanayobarikiwa na makasisi wanaojidai kumtumikia Mungu na kumbe hawaisemi kweli wala kuizoea. Basi, sasa, je! Mungu alifanya wanadamu wakiwa na kasoro fulani? Je! aliipa jamii ya kibinadamu mwanzo mbaya?
Mwanzo Mkamilifu
14. Eleza mwanzo ambao Mungu aliwapa wazazi wetu wa kwanza ulikuwa namna gani. (Mwanzo 1:26-31: 2:7-9, 15)
14 Mtu anaposoma zile sura mbili za kwanza za kitabu cha Mwanzo, inakuwa wazi sana kwamba Mungu alipomwumba mwanamume na mwanamke aliwapa mwanzo mkamilifu. Aliwaumba wakiwa na milli na akili kamilifu, hivi kwamba magonjwa na kifo hayangewasumbua kamwe. Makao yao yalikuwa bustani yenye kupendeza sana, mfano wa shamba lenye maua mazuri, majani mabichi yaliyo laini na miti yenye kuzaa matunda. Hakukuwa na ukosefu wa cho chote. Bali, kulikuwako wingi wa vitu. Pia, Mungu aliweka mbele ya wazazi wetu wa kwanza kazi yenye kupendeza na miradi yenye kusisimua. Aliwaagiza wazipanue hali zilizo kama shamba za paradiso hiyo zienee katika dunia nzima. Baadaye wangesaidiwa kufanya hivyo na watoto wengi wakamilifu ambao wangezaa. Hivyo, mwishowe, jamaa ya kibinadamu ingekuwa jamii ya watu iliyo kamilifu, yenye kukaa katika paradiso ya kidunia, wakifurahia uzima milele, na hata kutawala wanyama kwa upendo.
15. Ukamilifu wa kibinadamu unamaanisha nini, na haumaanishi nini?
15 Lakini sababu gani mambo yakageuka vibaya sana? Je! kweli ni kwa sababu hapo mwanzoni Mungu hakuumba wanadamu wakiwa wakamilifu? Sivyo hata, maana andiko la Kumbukumbu la Torati 32:4 linasema hivi juu ya Mungu, “Kazi yake ni kamilifu.” Walakini, ukamilifu wa kibinadamu haukuwa na maana ya kwamba wale watu wawili wa kwanza walijua kila jambo, au wangeweza kufanya kila jambo, au hawangeweza kufanya kosa. Hata viumbe vikamilifu vina mipaka. Kwa mfano, kulikuwako mipaka ya kimwili. Kama hawangekula chakula, wanywe maji na kuvuta hewa, wangekufa. Wala hawangeweza kuivunja sheria ile ya uvutano kwa kuruka chini kutoka mahali palipo juu sana wakitazamia kwamba hawataumia. Pia, walikuwa na mipaka ya akili. Kwa wazi, Adamu na Hawa walikuwa na mengi ya kujifunza, maana hawakuwa na ujuzi. Lakini hata kama wangejifunza mambo mengi namna gani, hawangeweza kamwe kujua mengi kama Muumba wao. Kwa sababu hiyo, wajapokuwa wakamilifu, walikuwa na mipaka kwa maana walikuwa katika makao ya kibinadamu. Ukamilifu ulimaanisha kwamba walikuwa timamu, kwamba miili na akili zao hazikuwa na kasoro yo yote.
16. Uhuru wa kibinadamu ulikusudiwa ufae zaidi ukiwa katika mipaka gani? (1 Petro 2:16)
16 Pia, Mungu aliumba wanadamu wakiwa viumbe vilivyo huru kuchagua mema na mabaya, si vyenye kuongozwa na tabia ya asili kama wanyama. Na bila shaka wewe unathamini uhuru huo. Hungetaka ye yote awe akikuamuru kila dakika ya maisha yako jambo unalopaswa kufanya. Walakini, uhuru huo haukuwa bila mipaka, bali ulikuwa uhuru wa kiasi. Ulitakwa utumiwe bila kuruka mipaka ya sheria za Mungu. Sheria nzuri hizo zingekuwa chache na rahisi, zenye kusudi la kupatia jamaa nzima ya kibinadamu ile furaha iliyo kubwa kuliko zote. Upendo wa Mungu kwa wanadamu ulionyeshwa kwa kuwataka watii sheria zake, maana yeye alijua kwamba kuheshimu sheria hizo kungewaletea faida zisizo na ukomo. Kutokuheshimu Mungu na sheria zake kungeharibu furaha yao. Hakungewaletea jambo zuri hata moja. Kwa kweli, kungeleta msiba, kwa sababu Mungu alionya Adamu na Hawa kwamba kama wangemwacha ‘wangekufa hakika.’ (Mwanzo 2:17) Basi ili waendelee kuishi, walihitajiwa si kula chakula, kunywa maji na kuvuta hewa tu, bali pia kuongozwa na Mungu na sheria zake.
17. Ni sababu gani nyingine ya maana sana inayofanya wanadamu wahitaji kumtegemea Mungu? (Zaburi 146:3; Yeremia 17:5-9)
17 Kuna sababu nyingine iliyo ya maana sana iliyowahitaji wazazi wetu wa kwanza waendelee kumtegemea Mungu. Sababu hiyo ni ya kwamba wanadamu hawakuumbwa wasimamie mambo kwa kufanikiwa pasipo kumtegemea Mungu. Mungu hakuwapa haki wala uwezo wa kufanya hivyo. Kama Biblia inavyosema: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” (Yeremia 10:23) Ndiyo sababu Biblia inatangaza hivi: “Mwenye kujitumainia moyo wake ni mjinga.”—Mithali 28:26.
Uovu Ulianza Namna Gani?
18. Kulitokea kasoro gani kwa wazazi wetu wa kwanza? (Yakobo 1:14, 15; Zaburi 36:9)
18 Mwanzo ukiwa mzuri namna hiyo, kasoro ilikuwa nini? Ni hii: wazazi wetu wa kwanza, Adamu na Hawa, walitumia vibaya uhuru wao. Waliamua kufuata njia yao wenyewe badala ya kutii sheria ya Mungu. Kwa kweli, yule mwanamke akafikiri ati wangeweza kuwa ‘kama Mungu, wakijua mema na mabaya.’ (Mwanzo 3:5) Walitaka kujiamulia yaliyokuwa sawa na yaliyokuwa makosa, wakitegemea kufikiri kwao wenyewe. Hawakutangulia kuona hasara kubwa mno ambayo ingetokana na kufikiri huko. Lakini ndivyo ikatukia, maana ‘Mungu hawezi kusema uongo.’ (Tito 1:2) Walipojiondoa mbali na utawala wa Mungu, yaliyotokea, katika maana kubwa, ni kama yale yanayotokea unapochomoa plagi ya feni ya umeme (upepeo wa hewa). Inapokatwa mbali na chanzo chake chenye kuendeleza umeme, feni hiyo inapepea polepole na hatimaye inasimama kabisa. Hali kadhalika, watu wa kwanza wawili walipojiondoa mbali na kile Chanzo cha uzima, yaani, Yehova Mungu, hatimaye walizorota wakafa, kama Mungu alivyoonya.
19. Sababu gani jamii nzima ya kibinadamu ilizaliwa ikiwa si kamilifu? (Warumi 5:12)
19 Kwa kuwa wazazi wetu wa kwanza walimwasi Mungu kabla ya kuzaa watoto, kutokamilika kulianza kabla ya kuzaliwa kwa mtoto wao wa kwanza. Adamu na Hawa wakawa kama kiolezo kilicho na kasoro. Kila kitu kilichofanyizwa kutokana nao kilikuwa na kasoro pia. Wangeweza kupitisha kwa watoto wao kile tu ambacho sasa wao wenyewe walikuwa nacho, yaani, miili na akili zenye kasoro. Hawakuwa tena wakamilifu kwa sababu walikuwa wamejiondoa kwa kile Chanzo kinachoendeleza ukamilifu na uzima, yaani, Yehova Mungu. Basi kupatana na inavyosema Biblia katika Warumi 5:12, kila mtu ambaye amezaliwa tangu wakati huo amezaliwa katika kutokamilika, na ni mwenye kuelekea kuwa mgonjwa, kuzeeka na kufa. Lakini Mungu hawezi kulaumiwa kwa hilo. Andiko la Kumbukumbu la Torati 32:5 linasema: “Wametenda mambo ya uharibifu, hawawi watoto wake, hii ndiyo ila yao.” Andiko la Mhubiri 7:29, NW linasema: “Mungu wa kweli alifanya wanadamu wakiwa wanyofu, lakini wao wenyewe wametafuta mipango mingi.”
20. Makosa ya watu wachache yanaweza kuletaje umizo kwa watu wengi sana?
20 Lakini, ni jambo la busara kwamba kutokutii kwa watu wawili tu kungepasa kutokezee kila mtu mabalaa makubwa namna hiyo? Tunajua kwamba uzembe wa kibinadamu wa mtu mmoja tu katika kushughulika na kifaa kidogo cha usalama katika ujenzi wa jengo fulani unaweza kutokeza balaa ambalo huenda likahasirisha maisha za watu wengi. Kutojali kuangalia sehemu fulani kama hiyo katika boma la maji kungeweza kuleta mpasuko na furiko ambalo lingeweza kusababisha uharibifu mkubwa sana. Tendo moja la ufisadi lenye kufanywa na mtawala huenda likafungulia mfululizo wa kufanya makosa katika serikali, kisha umizo kubwa lipate mamilioni ya watu. Katika jamaa, baba na mama wanapofanya chaguo baya, watoto wao wanaweza kupatwa na mabaya makubwa. Wazazi wetu wa kwanza walifanya chaguo baya. Basi, jamaa nzima ya kibinadamu ilitumbukizwa katika kutokamilika na maafa.
21. Sababu gani Mungu alifikiliza ile adhabu ya kifo, hata hivyo rehema yake ilionyeshwaje?
21 Kwa kuwa sheria ya Mungu ilihusika, hata ukamilifu wake, yeye hangeweza kuachilia tu uhalifu huo kwa kutofikiliza sheria hiyo. Kama hangefanya lo lote, watu wangemheshimuje yeye au sheria yake? Je! leo tunaheshimu watawala wasiotii sheria zao wenyewe, au wanaoruhusu watu fulani wazivunje makusudi bila kuadhibiwa? Kwa sababu hiyo, Mungu alitekeleza adhabu aliyosema angetoa kwa sababu ya kutokutii, nayo ilikuwa kifo. Lakini kwa rehema aliwaruhusu watu wale wawili wa kwanza wapate watoto, jambo ambalo imetupasa tushukuru, ama sivyo tusingalizaliwa kamwe. Na tujapokuwa wasiokamilika kwa sababu ya kosa la Adamu na Hawa, je! hatuoni ni afadhali kuwa hai kuliko kuwa wafu?
22. Nani mwingine analaumika sana kwa sababu ya uovu? (Mathayo 4:1-11; Waefeso 6:12)
22 Je! ndiyo kusema kwamba uovu ulianza na wanadamu tu? Sivyo, kuna zaidi. Mungu hakuumba wanadamu peke yao wawe viumbe wenye akili. Katika mbingu alikuwa amekwisha kuumba wana wengine wenye akili wasiohesabika, yaani, viumbe wa kiroho. Ijapokuwa wao pia waliumbwa wawe na uhuru wa kuchagua mema na mabaya, wao pia wangelazimika kutii sheria za Mungu zilizo njema na za kiasi ili waendelee kuishi. Walakini, mmoja wa viumbe hao wa kiroho alitafakari mawazo mabaya. Na mtu anapotafakari jambo baya, linaweza kuwa kubwa kiasi cha kumfanya atende jambo baya analofikiria. Ndivyo na kiumbe huyo wa kiroho. Alikuza tamaa ya makuu ndani yake mwenyewe mpaka ikamwongoza apinge matendo ya Mungu. Alimwambia Hawa, mke wa Adamu, kwamba wangemwasi Mungu na hata hivyo, akasema, “Hakika hamtakufa.” (Mwanzo 3:4) Alitilia mashaka uhitaji wao wa kumtegemea Muumba ili waweze kuendelea kuwa na uzima na furaha. Kwa kweli aliwaambia kwamba hakika kutokutii kungewafanyia mambo yawe bora, wawe kama Mungu. Kwa njia hiyo akatilia mashaka ukweli wa Mungu. Na kwa kuzitilia mashaka sheria za Mungu, alishuku njia ya Mungu ya kutawala—ndiyo, aliishuku haki ya Mungu ya kutawala. Kwa sababu hiyo akaitwa Shetani, maana yake mpingaji, na Ibilisi, maana yake mchongezi.
Sababu Gani Umeruhusiwa kwa Muda Mrefu Sana?
23, 24. Kwa nini yale masuala yangechukua wakati kabla ya kujibiwa?
23 Kwa kuwa Mungu ni mwenye nguvu zaidi sana, yeye angaliweza kwa vyepesi kufagilia mbali waasi hao wa kibinadamu na wa kiroho pale pale mwanzoni. Lakini kufanya hivyo hakungalimaliza mambo kwa njia yenye kuridhisha. Sababu gani sivyo? Kwa sababu si nguvu za Mungu zilizotiliwa mashaka. Yale masuala yaliyotokezwa yalikuwa ya wema na ubaya. Na suala la maana sana kati ya hayo lilikuwa hili: Je! njia hiyo ya uasi ingefaulu? Je! utawala ambao haukumjali Mungu ungeweza kuiletea jamaa nzima ya wanadamu faida zenye kuendelea? Je! utawala wa Mungu juu ya watu ungekuwa bora kwao, au utawala wa wanadamu ungekuwa bora? Katika hekima yake, Mungu alijua kwamba suala hilo, na mengine makuu yaliyotokezwa, lingechukua wakati kumalizwa. Kwa hiyo akaruhusu kipindi maalumu cha wakati ambacho kingewapa wanadamu nafasi tele ili wakifikie kilele cha kutimiza mambo yao ya kisiasa, kijamii, ki-viwanda na kisayansi.
24 Kipindi hicho cha wakati hakingeweza kuwa siku chache wala miaka michache tu. Vizazi vingi vingehitajiwa ili jibu lionyeshwe kwa njia isiyoweza kutiliwa mashaka. Kesi za mahakamani zinaweza kuchukua majuma mengi au miezi mingi hata ikiwa ni watu wawili tu wanaohusika na kesi. Yale masuala makubwa yaliyotokezwa kuhusiana na utawala wa Mungu yanataka kujibiwa kikamili, si nusu-nusu. Kwa njia hiyo kujibiwa kwa masuala hayo hakungehitaji kurudiwa kamwe wakati wo wote ujao. Mungu mwenye upendo angeweza kukubali jibu kamili tu. Na sisi tunaweza kufurahi kwamba ndivyo ilivyo, kwani ni jibu la namna hiyo tu linaloweza kufungua njia ya kupata amani na usalama usiokwisha kwa jamaa yote ya ulimwengu mzima ya Mungu, mbinguni na duniani.
25. Ijapokuwa kuna maendeleo ya kimwili, je! kujitegemea kwa mwanadamu pasipo Mungu kumeleta amani na furaha ya kweli?
25 Sasa miaka 6,000 imepita tangu masuala hayo yalipotokezwa kwanza. Matokeo ya kutokutegemea utawala wa Mungu yamekuwa nini? Kumetokea aina zote za serikali, aina zote za taratibu za kijamii, aina zote za mifumo ya kiuchumi. Na aina zote za dini zenye madhehebu mbalimbali zimejaribiwa. Lakini hakuna ambayo imeleta amani ya kweli, usalama wa kweli, afya na furaha yenye kuendelea. Je! ye yote anaweza kujivunia maendeleo ya kimwili na hali Vita ya Ulimwengu ya Pili pekee iliua watu zaidi ya milioni 50? Je! ni maendeleo kutuma watu kwenye mwezi na huku maroketi yenye kubeba makombora ya nyukilia yangeweza kuangamiza kabisa wanadamu, na huku mamia ya mamilioni ya watu duniani wanateswa na njaa na umaskini wakati ule ule ambao watu wanatua kwenye mwezi? Kuna faida gani kuwa na nyumba yenye vifaa vingi huku jamaa nyingi zikitenganishwa na magomvi, huku idadi ya talaka ikizidi kuongezeka, woga wa kutendwa uhalifu katika ujirani ukienea, huku uchafuzi na mitaa yenye nyumba chafu-chafu ikiongezeka, kuzorota kwa uchumi kukiachisha mamilioni ya watu kazi, huku ghasia, vita vya wenyewe kwa wenyewe na kupinduliwa kwa serikali nyingi yakiwa ni mambo yanayotukia kila mwaka, yakitaka kuharibu makao na njia ya maisha ya wanadamu?
26. Ule wakati ulioruhusiwa umefunua nini juu ya kujitegemea kwa mwanadamu pasipo Mungu? (Zaburi 127:1)
26 Kweli ni kama aliyekuwa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Kurt Waldheim alivyokubali: “Ijapokuwa kumekuwako maendeleo ya kimwili, uhai wa kibinadamu haujapata kuwa na ukosefu mkubwa wa usalama kama ulivyo leo.”a Kile kitabu kinachoitwa Environmental Ethics (Maadili ya Kimazingira) kilieleza hivi pia: “Ingawa mwanadamu aliumbwa avute hewa safi, anywe na kufurahia maji safi, afurahie mazingira yake, amebadili mazingira hayo na anaona hawezi kujirekebisha. Anatayarisha mauaji ya kuangamiza watu kama mainzi, mauaji ya kujifanyia mwenyewe.”b Kweli kweli ile ruhusa ya muda mrefu ya uovu imetosha kuonyesha watu wote wenye akili nzuri kwamba wanadamu hawakuumbwa wakiwa na uwezo wa kufaulu kuelekeza mambo yao pasipo mwongozo wa Mungu. Kwa kuwa miaka elfu sita ya kushindwa kwa wanadamu inashuhudia hivyo, hakuna ye yote anayeweza kamwe kumshtaki Mungu kwa haki aseme hakuruhusu wanadamu wakati wa kutosha wafanye majaribio. Ule wakati ulioruhusiwa umetosha kuonyesha kwamba ile njia ya kumwasi Mungu imekuwa balaa kabisa kabisa.
Karibuni Uovu Utakwisha
27. Mungu amekusudia kuwe na badiliko kubwa kadiri gani? (Mithali 2:21, 22; Warumi 16:20)
27 Jamaa ya kibinadamu inahitaji sana badiliko la mambo bora. Kwa kweli, sisi tunahitaji mfumo ulio mpya kabisa. Kama vile alivyokiri Erich Fromm msosholojia, yale maovu yaliyo katika jamii yanaweza kusahihishwa “ikiwa tu ule mfumo mzima ambao umekuwako wakati wa ile miaka 6,000 iliyopita ya historia unaweza kubadilishwa ili badala yake ukae ulio tofauti kabisa kabisa.”c Hilo ndilo Mungu anakusudia hasa! Kitakapokwisha kipindi cha wakati wake alioweka, Mungu ametoa uhakikisho wa kwamba atauponda-ponda kabisa huu mfumo mzima wa mambo usiwepo, pamoja na wale wanaoupendelea. “Waovu wote atawaharibu.”—Zaburi 145:20, ZSB.
28. Wakati tunamoishi unaitwa wakati gani na Biblia, na kwa nini? (2 Timotheo 3:1-5, 12, 13; Mathayo 24:3-14)
28 Hilo litatukia wakati gani? Upesi sana, kwa sababu Neno la Mungu linaonyesha kwamba zile taabu zisizo na kifani ambazo zimeipata jamaa ya kibinadamu tangu vita ya ulimwengu ya kwanza ilipoanza mwaka wa 1914 zinajumlika kuwa ishara ya kutambulisha siku zinazoitwa katika Biblia “siku za mwisho.” Biblia ilitabiri kwamba katika hizo “siku za mwisho” kungekuwa na vita vya ulimwengu, uhalifu wenye kuongezeka, njaa, magonjwa ya kipuku, utafutaji mwingi wa anasa kwa upande wa walio wengi, kuacha kumwamini Mungu, unafiki na upotovu wa kidini, na matukio mengine mengi. Matukio hayo yangekuwa kama ile mistari inayofanyiza alama ya vidole, yenye kutambulisha kwa uhakika kizazi chetu kuwa ndicho kizazi cha mwisho ambacho Mungu angevumilia hali hizo mbaya. Yesu alitabiri kwamba katika wakati wetu ndipo mwisho wa mfumo wa mambo unaotawala dunia sasa ungetokea.
29. Twajuaje kwamba mwisho wa mfumo huu ni karibu?
29 Pia juu ya kizazi cha watu walioona mwanzo wa zile “siku za mwisho” katika mwaka wa 1914, Yesu alisema: “Amin, nawaambia, Kizazi hiki hakitapita, hata hayo yote yatakapotimia.” (Mathayo. 24:34) Maana yake ni kwamba baadhi ya watu waliokuwa hai wakati Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilipoanza mwaka wa 1914 wangekuwa bado hai wajionee mwisho wa huu mfumo wa mambo. Kizazi hicho cha wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza kinazeeka sana sasa, na huo ni ushuhuda wenye nguvu kwamba mwisho wa uovu unakaribia haraka sana.
30. Ni nini kitakacholpata mifumo yote ya utawala wa kibinadamu inayosimamia dunia sasa? (Sefania 3:8; Isaya 1:28)
30 Mwisho huo utakapokuja, Mungu ataonyesha nguvu za uweza wake mwingi na kuingilia moja kwa moja mambo ya wanadamu. Mifumo yote ya kibinadamu inayompinga itapondwa-pondwa. Ule unabii wa Danieli sura ya 2, mstari wa 44, unasema hivi juu ya jambo hilo: “Katika siku za hao wafalme yule Mungu wa mbingu atasimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe, wala enzi kuu ya huo haitaachwa kwa taifa jingine. Utavunja-vunja falme hizo zote vipande-vipande na kuzikomesha, nao utasimama milele.” (Revised Standard Version) Mifumo yote ya kibinadamu yenye kuumiza ikiisha kuondolewa, utawala wa Mungu juu ya dunia utaanza tena usimamizi kamili.
31. Ni serikali gani ambayo Mungu atawapa wanadamu wote? (Mathayo 6:9, 10)
31 Kwa sababu hiyo, utawala wa Mungu utaongozwa na serikali mpya, serikali ya kimbingu, ule ufalme wa Mungu. Hiyo ndiyo ile serikali ambayo Yesu Kristo alifanya iwe jambo kuu la mafundisho yake. Naye alitabiri kwamba hiyo pekee ndiyo ingesimamia dunia nzima katika wakati wake. Kwa kuwa Ufalme huo utatawala kutoka mbinguni, ukielekezwa na Mungu, hakutakuwa na nafasi ya Ufalme huo kuchafuliwa na wanadamu wenye choyo. Kwa hiyo uwezo wa kutawala utakuwa pale ulipokuwa mwanzoni, yaani, mikononi mwa Mungu, mbinguni. Utawala wa Mungu utakapokuwa ukisimamia dunia, ahadi yake ni kwamba “uadilifu ndio wakazi wa nchi inayozaa watajifunza hakika.” (Isaya 26:9, NW) Wala hakuna mtu atakayepotezwa na dini ya uongo, kwa kuwa dini ya uongo haitakuwapo hata moja. Kila aishiye atafundishwa ile kweli juu ya Mungu na juu ya makusudi yake, hivi kwamba, katika maana iliyo kamili zaidi, “dunia itajaa hakika maarifa ya kumjua Yehova kama maji yanavyoifunika bahari yenyewe.”—Isaya 11:9, NW.
Taratibu Mpya Yenye Uadilifu
32. Chini ya ule utawala wa ufalme wa Mungu, amani itaenea kwa kadiri gani? (Isaya 2:2-4)
32 Chini ya utawala wa ufalme wa Mungu, jamii ya kibinadamu iliyo mpya kabisa itasitawi, jamii ya watu wenye kumwogopa Mungu. Katika hiyo taratibu mpya, Mungu ataonyesha kwa matendo yake kwamba anatujali sana. Kwanza, vita havitaharibu tena amani na furaha ya wanadamu. Sababu gani? Kwa sababu wote watakaouokoka mwisho wa ulimwengu mbovu wa sasa watakuwa wamekwisha kuelimishwa katika njia za amani, hivi kwamba ile jamii mpya ya kibinadamu itakuwa imekuwa na mwanzo wenye amani. Kisha, wote watakaoishi katika hiyo taratibu mpya wataendelea kupokea elimu ile ile ya kufanya mapenzi ya Mungu. Ndiyo sababu ahadi ya Biblia itatimizwa hakika kwamba Mungu “anafanya vita vikome mpaka kwenye ncha ya dunia.” (Zaburi 46:8, 9, NW) Amani hiyo itakuwa kamili namna gani? Neno la Mungu la unabii lasema: “Wenye upole watairithi [dunia], watajifurahisha kwa wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.
33. Dunia itakuwa na badiliko gani?
33 Kwa kuongezea, wale watakaokuwa wakiishi katika hiyo taratibu mpya wataigeuza dunia iwe paradiso ambayo Mungu alikusudia mwanzoni. Hiyo itakuwa kazi yenye kuridhisha wanadamu wee! Na paradiso ikiwa imerudishwa, watu watakuwa na uwezo wa kufurahia kikamili maziwa ya maji, mito na zile bahari kuu; vilima, milima, nyanda na mabonde; maua yenye kupendeza, mimea na miti; vilevile wanyama wenye kufurahisha. Wala hautatokea tena upungufu wa chakula, maana “dunia yenyewe hakika itatoa mazao yake; Mungu, Mungu wetu, atatubariki.” Ndiyo, “Kutakuwako na nafaka tele juu ya dunia; na juu ya milima kutakuwako mfuriko.”—Zaburi 67:6; 72:16, NW.
34. Ni kuponeshwa gani kwa mwili kutakakotokea?
34 Afya bora na yenye uchangamshi itafuatana na amani yenye kudumu na wingi wa chakula. Kwa kuwa Mungu alimwumba mwanadamu, yeye anajua sana kuliko daktari ye yote jambo la kufanya hasa ili kuponesha viwete, kufanya vipofu waone na viziwi wasikie, na namna ya kuondoa magonjwa yote, uzee na kifo. Uwezo huo wa Mungu wa kufanya hivyo ulionyeshwa na Yesu Kristo kwa kiasi kidogo, alipokuwa hapa duniani. Biblia inatuambia hivi: “Watu wengi sana wakamjia wakiwaleta vilema, vipofu, viwete, bubu na wengine wengi waliokuwa wagonjwa, wakawaweka mbele ya miguu yake, naye Yesu akawaponya. Umati ule wa watu ulishangaa sana ulipoona bubu wakiongea, waliokuwa wamelemaa wamepona, viwete wakitembea na vipofu wakiona.”—Matayo 15:30, 31, HNWW.
35, 36. Watu watapatiwaje nafasi ya kuishi katika taratibu mpya ya Mungu? (Yohana 5:28, 29; Luka 7:11-15)
35 Yesu alielekeza kwenye Paradiso hiyo ya kidunia alipomwambia hivi yule mwanamume aliyetundikwa kando yake: “Utakuwa pamoja na mimi katika Paradiso.” (Luka 23:43, NW) Lakini mwanamume huyo alikufa. Basi angeweza kuingiaje katika Paradiso? Kupitia mpango mwingine wa ajabu unaoonyesha jinsi Mungu anavyojali sana—kupitia ufufuo kutoka kwa wafu. Biblia yasema hivi katika Matendo 24:15: “Kutakuwa na ufufuo wa wafu, wenye haki na wasio haki pia.” Alipokuwa hapa duniani, Yesu alifufua wafu ili aonyeshe uwezo wa Mungu wa kufanya hivyo chini ya utawala wa ufalme wake.
36 Je! wewe unaona wazo la ufufuo kuwa gumu kuamini? Hata hivyo, sasa hivi unaweza kutazama vipindi vya televisheni vyenye watu ambao walikufa zamani. Unasikia sauti zao, unatazama matendo yao na kuona tabia zao. Ikiwa mwanadamu wa vivi hivi anaweza kuhifadhi vitu hivyo katika kanda za televisheni, haingekuwa vigumu kwa Mungu Mwenye Hekima Yote kutunza katika kumbukumbu lake alama yenye mambo mbalimbali ya utu na tabia za kila binadamu ambaye angetaka kuumba upya. Amekwisha kutunza kumbukumbu hilo, naye atawafufua wafu hao waishi tena. Kwa njia hiyo, wao pia watakuwa na nafasi ya kufurahia uzima katika taratibu mpya ya Mungu. Na kwa kuyafanya makaburi yawe matupu, kuponesha watu magonjwa waliyorithi, kuondoa uzee na kifo, Mungu “hakika atameza kifo milele.” (Isaya 25:8, NW) Kwa njia hiyo, watu wataweza kuishi milele!
37. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba Mungu atalipia kiasi kinachoizidi sana hasara yo yote ambayo watu wamepokea bila kuistahili?
37 Kupitia ufalme wake, Mungu atabadili kabisa ile hali ambayo imekuwapo kwa muda mrefu sana! Katika umilele wote ataonyesha anatujali sana kwa kumimina baraka nyingi zitakazolipia kiasi kinachoizidi sana hasara yo yote ambayo tumepokea zamani. Itakuwa shida sana kuzikumbuka zile taabu za zamani ambazo tumepata katika mfumo huu. Ahadi ya Mungu ni kwamba: “Mimi ninaumba mbingu mpya [serikali mpya ya kimbingu juu ya wanadamu wote] na dunia mpya [jamii ya kibinadamu yenye uadilifu], na maneno ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni. Lakini mufurahi, na mushangilie daima, kwa ajili ya hivi ninavyoumba.”(Isaya 65:17, 18, ZSB) Kwa sababu ya hizo baraka za ajabu zinazokuja, unaweza kufahamu kwa nini Biblia inasema kwamba Mungu, “atapangusa kila chozi katika macho yao.” Na kwa nini asifanye hivyo? Maana “mauti haitakuwa tena; wala maombolezo, wala kilio, wala uchungu hautakuwa tena; kwa manna maneno ya kwanza yamekwisha kupita.”—Ufunuo 21:4, ZSB.
Mungu Anajali—Je! Sisi Tunajali?
38. Ni watu wa aina gani ambao Mungu anataka katika taratibu mpya yake? (Zaburi 37:37, 38)
38 Uhakika wa kwamba karibuni Mungu atakomesha uovu na kuleta upesi taratibu mpya yenye kupendeza unaonyesha kwamba anatujali sisi kweli kweli. Lakini, je! sisi tunamjali? Ikiwa tunajali, tunahitaji kuonyesha hivyo. Ni lazima tufanye nini? Biblia inasema: “Ulimwengu unapita na ndivyo na tamaa yake, lakini yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” (1 Yohana 2:17, NW) Aina ya watu ambao Mungu anataka katika taratibu mpya yake ni wale wanaofanya mapenzi yake na kutii utawala wake wenye uadilifu. Hao ndio aina ya watu watakaotii sheria zake na kushiriki kuifanya ile “dunia mpya” iwe mahali pazuri pa kuishi. Watu wanaopinga utawala wa Mungu watakuwa wenye kufanya matata tu, kwa hiyo hawataruhusiwa waishi humo.
39. Ikiwa unataka uzima wa milele, ni lazima ufanye uchunguzi gani? (Mithali 2:1-6)
39 Je! wewe wataka kuishi katika taratibu mpya ya Mungu yenye uadilifu? Basi jambo la kwanza ni kujifunza matakwa ya Mungu ya uzima. Je! kukuomba utimize matakwa hayo ni kukudai mno? Kama ungeambiwa utapewa nyumba nzuri katika mazingira yaliyo kama shamba zuri, bila malipo, je! hungetumia wakati ujue namna ungeweza kustahili kuishi humo? Neno la Mungu linatutolea kilicho bora hata zaidi—uzima wa milele katika dunia-paradiso—ikiwa tutachunguza tujue anayotaka tufanye, kisha tuyafanye. Biblia inasema: “Hii ndiyo maana ya uzima wa milele, wapate maarifa ya kukujua wewe, Mungu wa kweli mmoja tu, na ya yeye uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3, NW.
40. Biblia inatoa faida gani za ziada sasa? (2 Timotheo 3:16, 17)
40 Kujifunza Biblia kutakupa pia wewe na jamaa yako ule mwongozo unaofaa ambao ni wa lazima sana kwa maisha ya kila siku katika nyakati hizi zenye msukosuko. Kwa kuongezea, Biblia inampa mtu amani ya kweli ya akili, kwa kuwa inatuambia ni kwa sababu gani hali ni mbaya sana na ni mambo gani yaliyoko wakati ujao. Jambo la maana zaidi, itakuwezesha usitawishe upendo wa kweli kwa Mungu, uone kwamba yeye “huwapa thawabu wale wamtafutao” kwa bidii.—Waebrania 11:6.
41. Ni msaada gani ambao Mashahidi wa Yehova watakupatia bila malipo?
41 Mashahidi wa Yehova watatoa wakati wao kwa furaha na bila malipo wakusaidie ujifunze mengi zaidi juu ya maandalizi ya Mungu ya uzima katika taratibu mpya yake. Bila shaka, pia, kuna maulizo mengine uliyo nayo juu ya Mungu na Biblia. Mashahidi wa Yehova watafurahi kuyazungumza pamoja nawe katika nyumba yako mwenyewe, wakitumia Biblia yako mwenyewe. Kisha, badala ya kufuata mwendo wa kujitegemea au wa kutegemea fikira za wanadamu wasiokamilika, utaongozwa na ile habari yenyewe iliyo bora kuliko zote inayopatikana leo. Kwa sababu hiyo, kukiwa kungali na wakati unasihiwa ufanye kama linavyosema shauri la Neno la Mungu lililoongozwa na roho yake: “Kwa hiyo, jinyenyekezeni chini ya mkono wenye nguvu wa Mungu, . . . kwa sababu yeye anawajali ninyi.”—1 Petro 5:6, 7, NW.
[Maelezo ya Chini]
a New York Times. Novemba 6, 1972, uku. 5.
b Environmental Ethics kilichohaririwa na Donald R. Scoby, 1971. uku. 17.
c New York Post, Machi 30, 1974, uku. 35.
[Chati katika ukurasa wa 22]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
YOTE HAYA KATIKA KIZAZI KIMOJA
Mwaka wa 1914
Vita vya Ulimwengu
Njaa Nyingi Sana
Magonjwa ya Kipuku
Uhalifu wa Kijeuri
Uchafuzi wa Dunia
Mwisho wa Mfumo Huu
[Picha katika ukurasa wa 6]
Ikiwa Mungu anashtakiwa kwa sababu ya umaskini wa kibinadamu na mitaa yenye nyumba chafu-chafu . . .
[Picha katika ukurasa wa 7]
. . . itasemwa ni nani aliyefanya uzuri wa dunia na mashamba yake yenye mazao?
[Picha katika ukurasa wa 9]
Dunia ina vitu vingi vya kuendeleza uhai kuliko nyumba yo yote
[Picha katika ukurasa wa 9]
Kwa kuwa kila nyumba ina mjenzi, ni wazi zaidi kwamba dunia iliumbwa na mtu fulani!
[Picha katika ukurasa wa 13]
Biblia inaonyesha kwanba kusudi la Mungu lilikuwa kuifanya dunia nzima iwe shamba zuri, parasido, ili wanadamu waifurahie milele
[Picha katika ukurasa wa 14]
Feni (upepeo wa hewa) inapochomolewa kutoka chanzo chake cha umeme, inapepea polepole na kusimama. Hali kadhalika, wanadamu walipojiondoa mbali na Mungu, matokeo yakawa ni kuzorota
[Picha katika ukurasa wa 16]
Kifaa kidogo cha usalama kinapokosa kuangaliwa, hata boma kubwa la maji laweza kubomoka. Wazazi wetu wa kwanza walipovunja sheria ya Mungu, furiko la uovu na kuteseka likaanza
[Picha katika ukurasa wa 19]
Kesi mahakamani inaweza kuchukua majuma mengi hata ikiwa ni watu wawili tu wanaohusika. Yale masuala yanayohusu utawala wa Mungu lazima yamalizwe kabisa, milele, na hiyo inataka wakati wa kutosha
[Picha katika ukurasa wa 24]
Vita haitakuwa katika taratibu mpya ya Mungu, maana yeye “anafanya vita vikome”
[Picha katika ukurasa wa 25]
Wanadamu hawatateswa tena kamwe na njaa
[Picha katika ukurasa wa 25]
Dunia itazaa kwa wingi kwa baraka ya Mungu
[Picha katika ukurasa wa 26]
Wazee watarudishiwa nguvu za uchangamshi zinazotokana na ujana na afya kamilifu
[Picha katika ukurasa wa 27]
Wafu wote wanaokumbukwa na Mungu watarudishwa kwenye uzima waunganishwe na wapendwa wao
[Picha katika ukurasa wa 29]
Chini ya utawala wa ufalme wa Mungu, maisha yatapendeza sana hata yalipie kiasi kinachoizidi hasara yo yote ambayo tumepata sasa bila kuistahili
[Picha katika ukurasa wa 31]
Ikiwa uzima katika mazingira yenye kupendeza ungekuwa ukitolewa bila malipo, je! wewe hungetaka kujua jinsi ya kustahili uzima huo? Taratibu mpya ya Mungu inatutolea kilicho bora hata zaidi, lakini ni lazima tutumie wakati kujifunza jinsi ya kustahili kukipata