Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w85 11/15 kur. 12-16
  • Je! Wewe Unaweza Kujitayarisha Sasa kwa Ajili ya Mateso?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Wewe Unaweza Kujitayarisha Sasa kwa Ajili ya Mateso?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Tayarisha Akili na Moyo Wako
  • Wewe Unashughulikaje na Watu?
  • Wewe Unauonaje Utumishi wa Shambani?
  • Wewe Unategemeka?
  • Wewe Unachukulianaje na Watu?
  • Je! Wewe Unadadisi (Unachungua-chungua) Mambo ya Watu?
  • Je! Wewe Ni Mwanafunzi wa Biblia?
  • Wewe Unasali?
  • Je! Wewe Unawatumaini Wenye Mamlaka?
  • Unaweza Kuwa Mshindi
  • Kuvumilia kwa Furaha Ijapokuwa Mateso
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
  • Wakristo Wanaelekeana na Mateso kwa Uvumilivu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Unaweza Kuvumilia Mateso
    Furahia Maisha Milele!—Masomo ya Kujifunza Biblia
  • ‘Ninyi ni Wenye Furaha Wakati Watu Wanawatesa Ninyi’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1982
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
w85 11/15 kur. 12-16

Je! Wewe Unaweza Kujitayarisha Sasa kwa Ajili ya Mateso?

“Ikiwa wamenitesa mimi, watawatesa ninyi pia.”​—YOHANA 15:20, Biblia ya New World Translation.

1, 2. Ni hatua gani isiyokuwa imetazamiwa ambayo serikali Fulani zimechukulia Mashahidi wa Yehova?

JIWAZIE ukiwa unapumzika kitandani mapema asubuhi moja. Kwa sababu ya usingizi unafikiri-fikiri, niamke mara hii ama niendelee kulala, nistarehe kidogo. Lakini kwanza, unafungulia redio usikie habari za asubuhi. Kwa ghafula, msoma-habari anakugutusha mpaka usingizi wote unakutoka. Anatangaza hivi: “Kulingana na amrisho la serikali, ile madhehebu inayoitwa Mashahidi wa Yehova imepigwa marufuku katika nchi yote.” Sasa hakuna cha kujistarehesha!

2 Jambo hilo, au jingine la namna hiyo, ndilo limewapata Wakristo katika nchi fulani-fulani nyakati za kisasa. Mara nyingi, kumekuwa na maonyo juu ya jambo linaloweza kutukia. Lakini nyakati nyingine marufuku imekuwa isiyotazamiwa kabisa. Je, jambo hilo litushangaze?

3. Ni mambo gani yenye kutofautiana yaliyompata Yesu mwaka 33 W.K.?

3 Hata kidogo. Mambo kama hayo yalitukia katika karne ya kwanza. Kumbuka jinsi Yesu Kristo, mwanzoni mwa masika ya 33 W.K., aliyopanda kuingia Yerusalemu akiwa juu ya punda. Watu walimshangilia kwa vifijo, wakatandaza mavazi yao barabarani mbele yake. Lakini ni jambo gani lililotukia siku chache baadaye? Yesu alisimama mbele ya Pontio Pilato ajaribiwe, kisha watu wenye ghasia wa mji huo huo wakapiga makelele kwa kutaka damu imwagike: “Atundikwe mtini!. . . Atundikwe mtini!” (Mathayo 21:6-9; 27:22, 23, NW) Hali ilikuwa imebadilika kwa ghafula.

4. Inatupasa tutazamie kutendwaje sisi tulio wafuasi wa Yesu?

4 Kwa hiyo, tusishangae ikiwa hali itabadilika katika nchi fulani-fulani leo kisha mateso yatokee bila kutazamiwa. Kumbuka, ikiwa sisi ni wafuasi wa Yesu kweli kweli tunapaswa kutazamia mateso. (Yohana 15:20) Jambo hilo linakazia umaana wa maneno ya Yesu, “Kesheni.”—Mathayo 24:42.

5. Sasa ni maulizo gani yanayostahili tuyafikirie?

5 Tunaweza kufanyaje hivyo? Je, kuna njia ambayo tunaweza kujitayarisha iwapo ubaya usiotazamiwa unatukia?

Tayarisha Akili na Moyo Wako

6, 7. (a) Kwa sababu gani ni vigumu kufanya matayarisho ya kimwili kwa ajili ya mateso? (b) Ni matayarisho gani yaliyo ya maana zaidi yanayoweza kufanywa kwa ajili ya mateso?

6 Ni vigumu kujitayarisha mwili kwa ajili ya mateso kwa sababu hujui ni hali gani hasa itakayotokea. Kabla marufuku haijatukia, hujui itafikilizwa kwa dhati sana au ni kwa ulegevu tu, wala hata hujui kitakachopigwa marufuku ni nini. Labda ni kazi ya kuhubiri nyumba kwa nyumba tu itakayokatazwa, au labda mikutano ya kidini. Nyakati nyingine, tengenezo lililoandikishwa kisheria la Mashahidi wa Yehova ndilo linalovunjwa, au watu fulani-fulani wanafungwa gerezani mara hiyo. Tunaweza kukumbuka kuweka akilini sehemu mbalimbali ambako vitabu vingeweza kufichwa iwapo uhitaji utatokea. Lakini zaidi ya jambo hilo, hakuna mengi tunayoweza kufanya katika kujitayarisha kimwili.

7 Lakini, wewe unaweza kutayarisha akili na moyo wako, na hilo ndilo jambo la maana zaidi. Kaza akili yako juu ya sababu inayofanya mateso yaruhusiwe na sababu inayofanya wewe uweze kusukumwa mbele ya watawala. “Ili kuwa ushuhuda,” akasema Yesu. (Mathayo 10:16-19, NW) Yehova anaweza kufunua jinsi ilivyo hekima kutenda wakati uhitaji unapotokea, ikiwa moyo wako umetayarishwa kabisa kubaki katika uaminifu, hata kutokee nini. Kwa hiyo, tunaweza kujitayarishaje kiroho kwa ajili ya mateso?

Wewe Unashughulikaje na Watu?

8. Kwa sababu gani Paulo aliweza kusema kwamba ‘alipendezwa na kutendwa ufidhuli’?

8 Mtume Paulo alisema: “Napendezwa na udhaifu, na ufidhuli, na misiba, na adha, na shida, kwa ajili ya Kristo.” (2 Wakorintho 12:10) Je, Paulo alifurahia kutendwa ufidhuli? Bila shaka sivyo. Lakini mara nyingi mateso yanatia ndani kutendwa ufidhuli. Na kama ilihitajiwa atendwe hivyo ndipo jina la Mungu liweze kupata sifa, basi Paulo alifurahi kuvumilia.

9. Tunaweza kujitayarishaje sasa ili tuvumilie kutendwa “ufidhuli. . . kwa ajili ya Kristo”?

9 Sisi, pia, tunaweza kuwa na uhakika kwamba wakati fulani tutalazimika kuvumilia “ufidhuli . . . kwa ajili ya Kristo.” Huenda tukatendwa vibaya kwa maneno au hata kimwili. Je, tutavumilia? Haya basi, wakati wa sasa sisi tunajionaje? Je, tunajichukua kuwa watu wa maana sana na kufanya haraka ya kuchukulia watu hatua wakati tunapotendwa kikweli mambo ya ufidhuli au tunapowazia tu kwamba wametutenda hivyo? Ikiwa ndivyo, sababu gani tusijitahidi kusitawisha “ustahimilivu, . . . upole, kujiweza”? (Wagalatia 5:22, 23, NW) Hayo yatakuwa mazoezi mazuri sana kwa maisha ya Kikristo sasa, na yangeweza kuokoa uhai wako nyakati za mateso.

Wewe Unauonaje Utumishi wa Shambani?

10. Kulingana na Maandiko inafaa kutendaje wakati kazi yetu ya kuhubiri inapopigwa marufuku?

10 Mara nyingi, jambo linalokuwa la kwanza kuzuiwa chini ya marufuku ni kazi ya kuzihubiri waziwazi “habari njema.” Hata hivyo kuhubiri na kufanya wanafunzi ni mambo yanayohitajiwa kabisa katika hizi siku za mwisho. Kama sivyo watu watajifunzaje juu ya Ufalme wa Mungu? Kwa hiyo, tendo linalofaa itokeapo marufuku ya namna hiyo ni lile lililoonyeshwa na mitume, wakati viongozi wa kidini Wayahudi walipojaribu kuupiga marufuku utendaji wao wa kuhubiri. (Matendo 5:28, 29) Kunapokuwa na marufuku, huenda njia fulani za kuhubiri zikafungwa. Lakini ni lazima kazi ifanywe kwa njia fulani. Je, wewe ungekuwa na nguvu za kuendelea kuhubiri chini ya mkazo wa mateso?

11, 12. Unaweza kuamuaje kama ungekuwa na nguvu unazohitaji ili uhubiri nyakati za mateso?

11 Basi, je, wewe unaionaje kazi ya kuhubiri sasa? Je,unaruhusu vipingamizi vidogo vikuzuie na kukufanya usiye wa kawaida katika utumishi wa shambani? Ikiwa ndivyo, ungefanya nini ukiwa chini ya marufuku? Je, sasa unaogopa wanadamu? Je, ungali una moyo wa kupenda kuhubiri nyumba kwa nyumba katika eneo unaloishi? Je, unaogopa kufanya kazi peke yako? Katika nchi fulani-fulani, mara nyingi watu wawili wakifanya kazi pamoja wanavuta mno fikira za wenye kuwaangalia. Kwa hiyo, sababu gani sasa usifanye kazi ukiwa peke yako mara kwa mara, mahali ambapo ni salama kufanya hivyo? Hayo yatakuwa ni mazoezi mazuri.

12 Je, wewe unaishiriki kazi ya barabarani ya magazeti? Je, una ushujaa na akili ya kuchukua hatua ya kwanza ili ufanyize nafasi za kutolea ushuhuda wa vivi hivi? Je, wewe unafanya kazi katika maeneo ya kibiashara? Je, unaogopa kuwafikia matajiri au watu mashuhuri? Ikiwa unashiriki katika aina fulani tu za kuhubiri, utafanya nini utakapokuwa chini ya marufuku isiwezekane tena kuendelea na aina hiyo ya kuhubiri?

13. Unaweza kufanya nini sasa na huduma yako ili ujitayarishe vizuri zaidi kuhubiri nyakati za mateso?

13 Je, wewe unatambua kwamba una udhaifu katika upande fulani? Sasa ndio wakati wa kuutengeneza. Jifunze kumtegemea Yehova na kusawazika pande zote ukiwa mhudumu. Ndipo utakapokuwa umetayarishwa vizuri zaidi kuhubiri sasa na kuvumilia katika nyakati za mateso.

Wewe Unategemeka?

14, 15. (a) Ni Wakristo wa namna gani katika karne ya kwanza ambao bila shaka walikuwa nguvu za kuimarisha wengine mateso yalipotokea?

14 Katika sehemu zote za Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, watu mmoja mmoja wanatajwa ambao walikuwa minara yenye nguvu kundini. Kwa mfano, Onesiforo alimsaidia Paulo kwa ushujaa wakati alipokuwa gerezani Roma. (2 Timotheo 1:16) Fibi alipendekezwa kwa sababu ya kazi yake ya bidii katika kundi lililokuwa Kenkrea. (Warumi 16:1, 2) Bila shaka wanaume na wanawake hao walikuwa nguvu imara yenye kuimarisha wengine wakati mateso yalipotokea. ‘Walikesha, wakasimama imara katika imani, wakafanya kiume.’

15 Wakristo wote, hasa wazee, wanapaswa wajaribu kufanya maendeleo na kuwa kama watu hao. (1 Timotheo 4:15) Ujue jinsi ya kutofunua mambo yanayopasa kubaki yakiwa siri. Jifunze jinsi ya kufanya maamuzi yanayotegemea kanuni za Kimaandiko. Jizoeze kutambua sifa za Kikristo katika wengine ili ujue ni nani atakayekuwa mtu wa kutegemeka chini ya mkazo. Kwa nguvu za Yehova, jitahidi kuwa nguzo katika kundi lenu, uwe mtu anayesaidia wengine badala ya wewe mwenyewe kuwa unahitaji msaada sikuzote.​—Wagalatia 6:5.

Wewe Unachukulianaje na Watu?

16, 17. Kuyafuata sasa yale yanayosemwa na Wakolosai 3:12, 13 kunaweza kukusaidiaje ujitayarishe kwa ajili ya mateso?

16 Mtume Paulo alitutia moyo hivi: “Jivikeni wenyewe shauku nyororo za huruma, fadhili, udhalili wa akili, upole, ustahimilivu. Endeleeni kuchukuliana mmoja na mwenzake na kusameheana kabisa mmoja na mwenzake.” (Wakolosai 3:12, 13, NW) Je, ni jambo jepesi kwako kufanya hivyo? Au wewe unaudhika-udhika bure tu kwa sababu ya hali za wengine za kutokamilika? Je, unachukizwa upesi au kuvunjika moyo? Ikiwa ndivyo, hiyo ni sehemu nyingine ambayo unaweza kufanyia matayarisho.

17 Katika nchi ambako mikutano imepigwa marufuku? Wakristo wanakutana kwa ukawaida katika vikundi vidogo. Katika hali za namna hiyo, makosa ya kupungukiwa kwao yanaonekana wazi hata zaidi. Sababu gani basi usijizoeze sasa kuchukuliana na udhaifu mbalimbali wa wengine, sawa na vile ambavyo bila shaka wanachukuliana na wako? Usilaumu-Iaumu wengine na hivyo uwavunje moyo sana. Pia, jizoeze wewe mwenyewe na watoto wako kuheshimu mali za wengine unapohudhuria mafunzo ya kitabu ya kundi. Chini ya mateso, heshima hiyo itaendeleza uhusiano wenye amani.

Je! Wewe Unadadisi (Unachungua-chungua) Mambo ya Watu?

18. Kwa sababu gani nyakati nyingine ni salama zaidi kujua habari zile tu unazohitaji kujua?

18 Kwa kuzaliwa, wengine wetu ni wadadisi sana (tunataka kujua-jua sana mambo). Tunashindwa kuvumilia tusipojulishwa mambo yote. Je, ndivyo ulivyo wewe? Ikiwa ndivyo, fikiria hili: Nyakati nyingine, wakati kazi ya Mashahidi wa Yehova inapokuwa imepigwa marufuku, wenye mamlaka wanajaribu kugundua mipango yao ya kitengenezo na majina na waangalizi wenye madaraka. Kama wewe ungekuwa mtu anayejua hayo, wangeweza kukutesa-tesa kimwili kwa jitihada ya kukulazimisha uyafunue wazi mambo hayo. Na kama kweli ungeyafunua, kazi ya ndugu zako ingeweza kupatwa na matokeo mazito. Kwa hiyo, nyakati nyingine ni salama zaidi kujua kiasi cha habari zile tu unazohitaji kujua, na basi.

19. Ni nini kinachoweza kukusaidia sasa uje kuepuka kufunua mambo ya siri wakati wa kuteswa?

19 Je, wewe unaweza kujizoezea jambo hilo sasa? Ndiyo. Kwa mfano, ikiwa kuna kesi ya halmashauri ya hukumu katika kundi, watu mmoja mmoja wanapaswa waridhike na habari zo zote ambazo wazee wanaona zinafaa kufunuliwa wala haiwapasi kuchungua-chungua ili wajue mambo kwa urefu. Wake na watoto wa wazee hawapaswi wajaribu kuwakazakaza ili wafunue mambo ya siri. Katika kila njia, inatupasa tujifunze ‘kutojiingiza katika mambo yasiyotuhusu.’​—2 Wathesalonike 3:11, NW.

Je! Wewe Ni Mwanafunzi wa Biblia?

20, 21. Kujifunza Biblia kwa bidii sasa kutakusaidiaje kazi ikipigwa marufuku?

20 Biblia ndiyo msingi wa nguvu za kiroho za Mkristo. Inampa majibu kwa maulizo yake yaliyo ya maana sana na kumwezesha apate hekima ya Mungu mwenyewe. (2 Timotheo 3:14-16) Wakristo wote wanaitambua kanuni ya kwamba ndivyo Biblia ilivyo, lakini je, kwa kweli wewe unaiacha iwe na sehemu gani katika maisha yako? Je, unajifunza hiyo kwa ukawaida na kuiacha ikuongoze katika kila jambo unalotenda?​—(Zaburi 119:105).

21 Mara nyingi, inakuwa vigumu sana kuweza kupata vitabu vyetu vya Kibiblia wakati kazi inapopigwa marufuku, Nyakati nyingine, hata Biblia zenyewe zinapatikana kwa shida. Chini ya hali kama hizo, roho takatifu itakukumbusha mambo ambayo umejifunza nyakati zilizopita. Lakini haitakukumbusha mambo ambayo hukujifunza! Basi, kadiri unavyozidi kujifunza sasa, ndivyo utakavyozidi kuhifadhi akilini na moyoni mwako habari za kukumbushwa na roho takatifu katika nyakati za uhitaji.​—Marko 13:11.

Wewe Unasali?

22. ‘Kudumu katika sala’ kunaweza kusaidiaje katika kujitayarisha kwa ajili ya mateso?

22 Hilo ni ulizo la maana tunapofikiria mateso. Biblia inashauri hivi: “Dumuni katika sala.” (Warumi 12:12, NW) Sala ni kupashana habari na Yehova Mungu kwa njia ya moja kwa moja. Kupitia hiyo tunaweza kuomba nguvu za kuvumilia magumu na kufanya maamuzi yanayofaa, na pia kujenga uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova Mungu. Hata kama wapinzani wanachukua vitabu vyetu, Biblia zetu, na kutuzuia tusishirikiane na Wakristo wale wengine, hawawezi kulichukua pendeleo letu la sala. Akiwa katika gereza lililojengwa imara kuliko magereza yote, Mkristo anaweza kupashana habari na Mungu. Basi, kujifaidi kikamili na pendeleo la sala ni njia nzuri ya kujitayarisha kwa ajili ya mambo yo yote yanayoweza kutokea wakati ujao.

Je! Wewe Unawatumaini Wenye Mamlaka?

23. Kwa sababu gani ujenge hali ya kuwatumaini wazee waliowekwa rasmi na pia “mtumwa mwaminifu mwenye akili”?

23 Ni jambo la maana kujenga hali hiyo ya kutumaini. Wazee katika kundi ni sehemu ya uandalizi wa Mungu wa kutulinda. Wazee wanahitaji kutenda kwa njia inayostahili watumainiwe, na wale wengine kundini wanahitaji kujifunza kuwatumaini. (Isaya 32:1, 2; Waebrania 13:7, 17) Jambo la maana zaidi ni kwamba inatupasa tujifunze kumtumaini “mtumwa mwaminifu mwenye akili.”​—Mathayo 24:45-47.

24. Ni nini linaloweza kufanywa ili kujitayarisha kupinga mashambulio ya uwongo yanayofanywa na adui za watu wa Mungu?

24 Huenda adui wakaeneza habari za uwongo juu ya tengenezo la Mungu. (1 Timotheo 4:1, 2) Katika nchi moja, Wakristo fulani walidanganywa waamini kwamba Baraza Linaloongoza la Mashahidi wa Yehova lilikuwa limeuacha Ukristo, lakini ni wao peke yao walioendelea kuufuata. Njia nzuri ya kujitayarisha kupinga mashambulio yaliyo kama hilo ni kujenga upendo wenye nguvu kwa ajili ya ndugu zetu na kujifunza kuutumaini mpango wa mambo ulioandaliwa na Yehova.​—1 Yohana 3:11.

Unaweza Kuwa Mshindi

25. Ni nini kitakachotusaidia tushinde tunapoteswa?

25 Yohana mtume aliyezeeka alituambia hivi baada ya kupatwa na mateso: “Kila kitu kilichozaliwa na Mungu huushinda ulimwengu; na huku ndiko kushinda kuushindako ulimwengu, hiyo imani yetu.” (1 Yohana 5:4) Huwezi kuushinda kwa nguvu zako mwenyewe. Shetani na ulimwengu wake ni wenye nguvu kuliko wewe. Lakini si wenye nguvu kuliko Yehova Mungu. Kwa hiyo, tukitii amri za Mungu, kusali tupewe roho yake itusaidie kisha tumtegemee yeye kabisa atupe nguvu za kuvumilia, hapo tunaweza kushinda.​—Habakuki 3:13, 18; Ufunuo 15:2; 1 Wakorintho 15:57.

26. Hata ikiwa sasa hupatwi na mateso, inakupasa ufanye nini?

26 Katika nchi zote, kuna Wakristo wengine wanaoteswa, ama na wenzi wa ndoa wanaopinga au kwa njia nyingine. Katika nchi fulani-fulani, watumishi wote wa Mungu wanataabika kwa sababu ya hatua rasmi zilizochukuliwa na serikali ya huko. Lakini hata kama wewe mwenyewe hupatwi sasa hivi na upinzani au magumu yasiyo ya kawaida, kumbuka kwamba yanaweza kutokea wakati wo wote yakupate. Yesu alisema kwamba mateso ya Wakristo yangekuwa sehemu ya ishara ya wakati wa mwisho; kwa hiyo, inatupasa sikuzote tuyatazamie. (Mathayo 24:9) Sababu gani basi usijitayarishe sasa kwa ajili ya mateso hayo? Piga moyo konde iwe kwamba, hata kuje kutokea nini wakati ujao, sikuzote mwenendo wako utamletea sifa Baba yako wa kimbingu, Yehova Mungu.​—Mithali 27:11.

Majibu Yako Ni Nini?

◻ Ni matayarisho ya aina gani ambayo wewe unaweza kufanya sasa kwa ajili ya mateso?

◻ Wewe unaweza kufanya nini sasa usitawishe nguvu unazohitaji ili uendelee kuhubiri unapoteswa?

◻ Kufuata sasa Wakolosai 3:12,13 kunaweza kukusaidiaje mateso yakitokea?

◻ Kwa sababu gani ujenge hali ya kuwatumaini wazee waliowekwa rasmi na pia “mtumwa mwaminifu mwenye akili”?

◻ Unaweza kuwaje mshindi unapoteswa?

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki