Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 7/15 kur. 4-7
  • Je! Mungu Anakuhesabu Wewe Kuwa Mtu wa Maana?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Je! Mungu Anakuhesabu Wewe Kuwa Mtu wa Maana?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ni Uhusiano wa Namna Gani Unaowezekana?
  • Ni Tangu Lini Mwanadamu Amehesabiwa na Mungu Kuwa wa Maana?
  • Je! Kristo Alikazia Jambo la Kwamba Baba Yake Anajali Watu?
  • Je! Leo Mwanadamu Anahesabiwa na Mungu Kuwa wa Maana?
  • Je! Wakati Ujao wa Mwanadamu Unahesabiwa na Mungu Kuwa wa Maana?
  • Je! Wafu Wanahesabiwa na Mungu Kuwa wa Maana?
  • Yehova Ni Mchungaji Wetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • “Yehova Ni Mchungaji Wangu”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2011
  • Mahali pa Kupata Faraja
    Jifunze Kutoka kwa Mwalimu Mkuu
  • Mchungaji Mwenye Upendo
    Kumsikiliza Mwalimu Mkuu
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 7/15 kur. 4-7

Je! Mungu Anakuhesabu Wewe Kuwa Mtu wa Maana?

JE! WEWE umewahi kuutazama ulimwengu wa juu wakati wa usiku? Je! umewahi kujiuliza macho yako yanafika umbali gani hasa katika anga, au ni nyota ngapi unazoweza kuona kwa macho yako mwenyewe, bila kutumia darubini? Basi, uliposhangazwa kabisa na fahari kubwa sana ya mbingu, je! umewahi kujiuliza ya kwamba, Mwanadamu aliye kitu duni tu anahesabiwa na Mungu kuwa wa maana? Je! Mungu ananijali mimi kweli nikiwa binafsi?

Miaka elfu tatu iliyopita mfalme-mshairi aliyekuwa Mwebrania, Daudi wa Yuda, alistaajabu akisema maneno yanayofuata: “Nikiziangalia mbingu zako, kazi ya vidole vyako, mwezi na nyota ulizoziratibisha; mtu ni kitu gani hata umkumbuke, na binadamu hata umwangalie?” (Zaburi 8:3, 4) Ndiyo, ingawa Daudi hakuwa anajua, macho yake yasiyotumia darubini yalikuwa yakiangalia ndani ya ulimwengu wa juu wenye umbali wa miaka ya nurua ipatayo 600,000. Alishangazwa na jambo la kwamba Muumba wa anga hiyo iliyo kubwa sana anamkumbuka hata mwanadamu na kumhesabu kuwa wa maana.

Daudi alitaja wazo linalolingana na hilo katika Zaburi 144, ambapo tunasoma: “Ee [Yehova], mtu ni kitu gani hata umjue? Na binadamu hata umwangalie? Binadamu amefanana na ubatili, siku zake ni kama kivuli kipitacho.” (Mistari 3, 4) Hata hivyo, Daudi alijua kwamba Mungu anamhesabu mwanadamu kuwa wa maana angawa yeye ni kitu duni na ni wa kitambo tu akilinganishwa na Mungu. Aliwezaje kuwa sana na uhakika wa jambo hilo? Ni kwa sababu yeye mwenyewe alikuwa amekuza uhusiano wa kibinafsi pamoja na Yehova.

Ni Uhusiano wa Namna Gani Unaowezekana?

Tunajuaje kwamba Daudi alikuwa na uhusiano wa kibinafsi pamoja na Mungu? Kutupia jicho yo yote ya zaburi za Daudi au nyimbo za kishairi, kunatosha kutusadikisha alikuwa nao. Kwa mfano, na tuchukue Zaburi 23 kisha tuyaangalie maneno yayo yaliyoandikwa kwa njia nyepesi kufahamika tujaribu kuuona uhakika kamili ambao Daudi alikuwa nao katika Mchungaji wake, Yehova Mungu.

“[Yehova] ndiye mchungaji wangu,

Sitapungukiwa na kitu.

Katika malisho ya majani mabichi hunilaza,

Kando ya maji ya utulivu huniongoza.

Hunihuisha nafsi yangu; na kuniongoza

Katika njia za haki kwa ajili ya jina lake.

Naam, nijapopita kati ya bonde la uvuli wa mauti,

Sitaogopa mabaya;

Kwa maana Wewe upo pamoja nami,

Gongo lako na fimbo yako vyanifariji.”​—Zab 23 Mistari 1-4.

Hapa, kina cha uhusiano wa Daudi pamoja na Mungu kinaonekana wazi kwa njia yenye mng’ao. Zaburi hiyo inakufanya wewe uwe namna gani? Je! unauona mwungano wa kutumainiana kati ya yule “kondoo” Daudi asiyekuwa na ulinzi na Mchungaji wake mwenye kumlinda, Yehova? Bila shaka hata moja, Daudi aliujua uhakika wa kwamba ingawa mwanadamu anafanana na “ubatili” (“mpumuo tu,” NW), yeye binafsi alihesabiwa kuwa mtu wa maana na Mungu wake aliyekuwa Mchungaji wake pia. Basi, Daudi angeweza kusema hivi kwa usadiki: “[Yehova] ndiye mchungaji wangu, sitapungukiwa na kitu.” Sasa, wewe unaweza kupataje uhakika wa namna iyo hiyo, tumaini la namna iyo hiyo?

Kwanza, kuna jambo moja la maana kabisa tusiloweza kulipuza. Si shauri la mchungaji pekee kupendezwa na kondoo zake. Kondoo pia wanapaswa kufuata mchungaji wao na kutii sauti yake. Ndiyo kusema, kama tunataka kuhesabiwa na Mungu kuwa watu wa maana, ni lazima sisi wenyewe pia tumhesabu Mungu kuwa anastahili kutegemewa nasi. Kondoo wakitoroka kwenye zizi au wamkatae mchungaji, hapo wanapoteza ulinzi. Uhusiano uliopo unaharibiwa na upotovu wa makusudi wa kondoo wenyewe. Ijapokuwa historia ya mwanadamu imekuwa na upotovu huo, Mungu amewajali wanadamu, si wakiwa wote kwa ujumla tu bali wakiwa watu mmoja mmoja. Tuna ushuhuda gani wa kutufanya tuseme hivyo?

Ni Tangu Lini Mwanadamu Amehesabiwa na Mungu Kuwa wa Maana?

Tangu kule kule kwenye mwanzo wa historia ya kibinadamu, Yehova amedhihirisha kuwa anawajali wanadamu na wakati ujao wao. Wakati uasi wa kichoyo ulipotokea katika Edeni, Mungu hakuitoroka jamaa ya kibinadamu na kuiacha bila tumaini. Aliahidi kutokeza “uzao” wa wakati wa baadaye ambao ungechukua hatua dhidi ya yule aliye adui mkubwa zaidi wa mwanadamu kisha ulete kitulizo kwa kuponda kichwa cha Shetani. (Mwanzo 3:15; Warumi 16:20) Baada ya hapo Yehova aliendelea kushughulika na wanadamu, nyakati nyingine wakiwa watu mmoja mmoja na pindi nyingine wakiwa mataifa mazima-mazima.

Mfano ulio wazi wa kwamba Yehova alijali watu mmoja mmoja katika Isareli wa kale ni ile sheria iliyofanyia yatima na wajane maandalizi, hao wakiwa ni watu hohehahe katika taifa hilo. Kwa mfano, sheria hiyo ilisema wazi kwamba walipaswa kuwa na fungu la ushiriki katika mavuno hata kama hawakuwa na shamba lao wenyewe. Walipewa haki za kuokota masalio ya mavuno yaliyoachwa katika mashamba yaliyovunwa. Kweli mpango huo ulikuwa bora sana kuliko mipango mingi iliyo katika mataifa ya leo ya kuangalia masilahi ya watu! Katika Israeli mtu alibaki na hali yake ya kujiheshimu ajapokuwa na umaskini. Kwa sababu gani? Kwa sababu haikumlazimu aombe-ombe au angoje msaada wa kifedha kutokana na Serikali ya nchi. Alitumia mikono yake mwenyewe kujikusanyia-kusanyia masalio ya mavuno ili ajitimizie mahitaji. Alifanya kazi yenye mafaa na akaonyesha shukrani kwa Mungu wake mwenye ujazi, Yehova.​—Mambo ya Walawi 19:9, 10; Ruthu, sura ya 2.

Je! Kristo Alikazia Jambo la Kwamba Baba Yake Anajali Watu?

Zile Gospeli (Injili) nne zinaonyesha wazi kwamba Yesu Kristo aliwajali watu. Na kwa kuwa yeye alionyesha barabara sifa zile zile za Baba yake, kujali kwake kulikuwa ushuhuda wa wazi kwamba Mungu anahesabu mwanadamu kuwa wa maana. (Yohana 14:9) Mafundisho ya Kristo yalikuwa na maelekezo yenye upendo na mafaa kwa ajili ya maisha yasiyo ya kichoyo. Jambo hilo lilionyeshwa wazi sana wakati wanafunzi wake waliporudi wakiwa wamechoka na kuishiwa na nguvu kutoka shughuli kubwa ya kuhubiri! Yeye alitendaje? Alitenda kwa huruma na kufikiria hali yao. Yesu alifahamu walivyojisikia, akafahamu walihitaji pumziko kabla ya kuendelea tena. “Akawaambia, Njoni ninyi peke yenu kwa faragha, mahali pasipokuwa na watu, mkapumzike kidogo. Kwa sababu walikuwako watu wengi, wakija, wakienda, hata haikuwapo nafasi ya kula.” Basi wote wakaenda wakaingia mashua na kuwa mahali pa upekee ili wapumzike kidogo.

Lakini kundi lile la watu likawafuata. Yesu alitendaje kwa kuona hivyo? Je! alifanya haraka-haraka akakasirika? “Naye aliposhuka mashuani, akaona mkutano mkuu, akawahurumia; kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji; akaanza kuwafundisha mambo mengi.”​—Marko 6:30-34.

Kristo alionyesha hali ya kujali watu kama Baba yake kwa njia ya wazi sana! Alikazia jambo hilo wakati aliposema hivi pia: “Je! mashomoro watano hawauzwi kwa senti mbili? wala hasahauliwi hata mmojawapo mbele za Mungu. Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Msiogope basi, bora ninyi kuliko mashomoro wengi.”​—Luka 12:6, 7.

Kwa uhakika, mtu anayetafuta kumfuata Yesu Kristo hawi kama kitu kidogo tu katikati ya umati mkubwa wa watu, kisichoweza kuonwa na Mungu. Lakini jambo la maana ni la kwamba, Wewe unatafuta kwa bidii kumfuata Yesu Kristo? Je! wewe unaujua uhitaji wa kiroho ulio nao katika jambo hilo? (Mathayo 5:3) Kumbuka kwamba muda mfupi kabla Yesu hajakamatwa na kuuawa halafu, yeye alisali hivi kwa Baba yake: “Wala si hao tu [mitume waaminifu 11 walioshiriki naye kijio cha mwisho chake] ninaowaombea; lakini na wale [wanafunzi wengine] watakaoniamini kwa sababu ya neno lao.” (Yohana 17:20) Yesu alijua kwamba, zaidi ya mitume wake kuhesabiwa na Mungu kuwa watu wa maana, hata wale ambao baadaye wangekuwa waamini kutokana na mahubiri yao wangehesabiwa ivyo hivyo. Hiyo inaonyesha kwamba yule Mchungaji Mkuu, Yehova Mungu, anatoa ruhusa ya kuweza kufikiwa na wote wale wanaodhihirisha nia ya unyenyekevu ya kondoo.​—Zaburi 23:1.

Je! Leo Mwanadamu Anahesabiwa na Mungu Kuwa wa Maana?

Lakini huenda sasa ukauliza, ‘Ikiwa kweli mwanadamu anahesabiwa na Mungu kuwa wa maana, jambo hilo linaonekanaje leo? Mimi naweza kufaidikaje kutokana na kujali kwa Mungu juu ya wanadamu?

Leo Yehova, yule Mchungaji Mkuu, ameandalia watu walio kama kondoo mpango wa kusikia sauti yake kote kote ulimwenguni. Amefanyaje hivyo? Yesu anajibu hivi: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu, asipovutwa na Baba aliyenipeleka.” Hivyo, Yehova anavuta watu wenye mioyo ya unyenyekevu wamwelekee kwa kumtumia “mchungaji mwema” aliyemweka, yaani, Yesu Kristo.​—Yohana 6:44; 10:11, 14-16.

Kazi hiyo ya kuvuta watu inatimizwaje? Ni kupitia utendaji wa kuhubiri wa wafuasi waaminifu wa Kristo ambao ni mashahidi wa yule Mungu wa kweli, Yehova, kama vile Yesu alivyokuwa shahidi. Ndiyo, mashahidi Wakristo wa Yehova wanahubiri ko kote ambako watu wanaweza kupatikana. Wao wanasaidia kila mtu mmoja mmoja anayetaka kumjua Mungu, bila kumtoza malipo. Ikiwa wewe hujachukua hatua ya kwanza ya kuelekea kukuza uhusiano wa kibinafsi pamoja na yule Mchungaji Mkuu, Yehova, je! una nia ya kufanya hivyo? Je! una nia ya kumtafuta Mungu kupitia Yesu Kristo? Kumbuka himizo la Yesu: “Ombeni, nanyi mtapewa; tafuteni, nanyi mtaona; bisheni, nanyi mtafunguliwa.” Kwa kutuma Mwanaye duniani kwa ajili yetu, yule Mchungaji Mkuu amekwisha kuchukua hatua ya kwanza yenye lengo zuri la kukusaidia wewe. Ukiiitikia, karibuni utajigundulia kwamba mwanadamu anahesabiwa na Mungu kuwa wa maana.​—Mathayo 7:7; 1 Yohana 4:7-10.

Je! Wakati Ujao wa Mwanadamu Unahesabiwa na Mungu Kuwa wa Maana?

Uhakika wa kwamba kuwako kwa mwanadamu kunalinganishwa na mpumuo tu, na pumzi ya kawaida tu, unaonyesha maisha ya mwanadamu ni mafupi sana. Hata hivyo, kama wewe ungeweza kufurahia afya na furaha kamili, ungependa kuishi kwa muda mrefu namna gani? Je! umejibu kwa kusema, “Milele”? Hilo hilo ndilo jambo ambalo Yehova ameahidi​—uzima wa milele katika dunia-paradiso. Hivyo, katika barua ambayo Paulo alimwandikia Tito, tunasoma juu ya “tumaini la uzima wa milele, ambao Mungu asiyeweza kusema uongo aliuahidi tangu milele.” (Tito 1:2) Kwa kutegemea ahadi iyo hiyo, Paulo alitolea wengine shauri “watende mema, wawe matajiri kwa kutenda mema, wawe tayari kutoa mali zao, washirikiane na wengine kwa moyo; huku wakijiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao, ili wapate uzima ulio kweli kweli.” Huo “uzima ulio kweli kweli” unaongoza kwenye uzima wa milele.​—1 Timotheo 6:17-19.

Je! Wafu Wanahesabiwa na Mungu Kuwa wa Maana?

‘Lakini,’ huenda ukauliza, ‘namna gani wafu? Je! wanahesabiwa na yule Mchungaji Mkuu kuwa wa maana?’ Hakika wanahesabiwa hivyo! Ndiyo sababu mtume Paulo “alikuwa akihubiri habari [njema] za Yesu na ufufuo.” (Matendo 17:18) Kwa uhakika, ufufuo ni mfano wenye kutokeza wa kuonyesha Yehova anajali mtu mmoja mmoja. Kwa sababu gani? Kwa sababu ufufuo unaonyesha kwamba Yeye ameweka kumbukumbu, hata la vile vijambo vidogo kabisa vinavyohusu utu wa wale watakaorudishiwa uzima. Mwendeshaji Aliye Mkuu Kupita Wote anayeendesha ulimwengu mzima wote, pamoja na mamilioni yao ya magalaksi na nyota, havunjwi moyo na uhitaji wa kukumbuka mambo yote hayo yanayohusu utu wa waliokufa kisha kukaza ndani ya utu huo ubongo na moyo ulioumbwa upya. Basi si ajabu kwamba Yesu alitangaza hivi akiwa na usadiki: “Msistaajabie maneno hayo; kwa maana saa yaja, ambayo watu wote waliomo makaburini wataisikia sauti yake [Yesu]. Nao watatoka.”​—Yohana 5:28, 29.

Ikiwa wewe ungependa uhesabiwe na yule Mchungaji Mkuu, Yehova, kupitia Mwanaye, Yesu Kristo, usisite kuwaomba Mashahidi wa Yehova wakusaidie. Katika faragha ya nyumba yako mwenyewe unaweza kuuliza maulizo yo yote ya Biblia unayotaka kuuliza. Utakuwa na uhakika wa kupata majibu ya kadiri inayofaa. Au unaweza kuandikia wachapishaji wa gazeti hili nao watakusaidia ujithibitishie kabisa kabisa kwamba kwa kweli wewe unaweza kuhesabiwa na Mungu kuwa wa maana sasa na wakati ujao.

[Maelezo ya Chini]

a Mwaka wa nuru ni umbali ambao nuru inasafiri kwa mwaka mmoja kwa mwendo wa maili 186,281 (kilometa 299,338) kwa nukta moja. Hiyo inajumlika kuwa maili 5,878,000,000,000 (kilometa 9,460,000,000,000), huo ukiwa ndio umbali ambao nuru inasafiri kwa muda wa mwaka mmoja. Bila shaka, ulimwengu mzima wote una mapana na marefu yaliyo makubwa kuliko vile macho ya mwanadamu yasiyotumia darubini yanavyoweza kuona.

[Picha katika ukurasa wa 5]

Je! Mungu anatujali sisi?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Yule Mchungaji Mkuu anatunza “kondoo” zake wote kwa upendo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki