Filemoni—Ushuhuda wa Ukristo Wenye Matendo
TENDA kama unavyohubiri! Yesu anakazia sana jambo hilo anapotangaza ubaya wa viongozi wa kidini wa siku zake! (Mathayo, sura ya 23) Lakini namna gani walimu katika kundi la kwanza la Kikristo? Je! wao walitenda mambo waliyoyahubiri? Kitabu cha Biblia cha Filemoni kinaonyesha kwamba walifanya hivyo.
Barua kwa Filemoni ilielekezwa kwa mtu mmoja hasa, si kwa kundi, nayo inashughulikia jambo la kibinafsi. Kinachoongezea hali ya barua hiyo kuwa ya kibinafsi ni uhakika wa kwamba Paulo aliiandika kwa mkono wake mwenyewe, badala ya kutumia mwandishi.
Sababu ya Paulo kumpelekea Filemoni barua hiyo ya kibinafsi ilikuwa nini? Ilikuwa hii: Paulo alikuwa anakaribia kumrudishia Filemoni mtumwa wake, Onesimo. Onesimo alikuwa amekimbia, labda hata akamwibia Filemoni pesa ili afunge safari yake ya kwenda Roma. Kwa njia fulani Onesimo alikuwa ameonana na Paulo katika Roma, akasikiliza mahubiri yake kisha akawa Mkristo. Basi alikuwa mwenye mafaa sana katika kumhudumia Paulo, naye mtume alikuwa amekwisha kumpenda sana. Lakini Paulo hakutaka Onesimo aendelee kukaa huko pamoja naye bila ruhusa ya Filemoni. Kwa hiyo, Paulo alikuwa sasa anamrudisha kwa Filemoni, naye Onesimo akawa amekubali jambo hilo—si akiwa mtumwa tu, bali pia ndugu mpendwa katika Bwana.
Jambo la kwamba sasa Onesimo alikuwa ndugu mwenye kuthaminiwa na kutumainiwa inaonyeshwa pia na kukabidhiwa kwake, pamoja na Tikiko mwenzi wake, barua za Paulo kwa makundi ya Efeso na Kolosai. (Waefeso 6:21,22; Wakolosai 4:7-9) Katika barua zote hizo mbili Paulo anatoa mawazo ya kwamba watumwa wawe watiifu kwa mabwana wa kazi. (Waefeso 6:5-7; Wakolosai 3:22, 23) Kwa hiyo, kwa kumrudishia Onesimo, Paulo alikuwa akitenda kupatana na shauri alilotoa. Yeye aliheshimu mali ya wengine na akaishi kwa kufuata mawazo aliyotolea wengine kwamba wawe watiifu kwa mpango uliopo wa kiserikali.—Warumi 13:1-7; 1 Wakorintho 7:20-24.
Pia Paulo aliweka mfano wenye kutimiza shauri alilolitoa yeye mwenyewe la kunyenyekea, kupenda na kuhangaikia wengine. (Waefeso 4:1-3; Wafilipi 2:3, 4; Wakolosai 3:12-14) Badala ya kumlazimisha Filemoni kwa kutumia uzito wa mamlaka yake ya kimtume ili amsamehe Onesimo na kumpokea kuwa ndugu, Paulo alitumia unyenyekevu akamsihi kwa msingi wa upendo wa Kikristo na urafiki wao wa kibinafsi. (Filemoni 8, 9,17) Hakika huo ni mfano mwema sana kwa waangalizi Wakristo leo!
Filemoni alikuwa na deni kwa Paulo, kwa maana ni kupitia Paulo yeye alikuwa amezijua habari njema na akawekwa huru aache kuwa katika utumwa wa upagani. Hata hivyo, kulingana na sheria bado angeweza kumtenda Onesimo vibaya na kwa ukali. Na kwa uhakika yeye alikuwa na sababu kamili ya kumkasirikia. Si kwamba tu Paulo alimtia Filemoni moyo aonyeshe fadhili, msamaha na rehema, bali mtume mwenyewe pia alikuwa na nia ya kufanya hivyo “Kama [Onesimo] amekukosea, ao kuwa na deni,” akaandika Paulo, “uandike hii juu yangu. . . . nitalipa.”—Filemoni 18,19, ZSB
Kwa uhakika, kama inavyoonyeshwa na kitabu cha Filemoni, waandikaji na walimu wa zamani wa Ukristo waliishi wenyewe kwa kufuata kanuni za Kikristo. Waliyatenda mambo waliyoyahubiri.