Maswali Kutoka kwa Wasomaji
■ Kwenye Wafilipi 2:9 Paulo anasema hivi juu ya Yesu: “Mungu . . . akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina.” Ni katika maana gani Yesu alipewa “Jina lile lipitalo kila jina”?
Katika maana ya kwamba alikabidhiwa na Yehova cheo au mamlaka ya juu kuliko aliyopewa kiumbe mwingine ye yote. Huenda wengine wakawa na maoni ya kwamba ni Mungu Mwenye Nguvu Zote peke yake anayeweza kuwa na “Jina lile lipitalo kila jina.” Kwa hiyo huenda wakawaza kwamba andiko hilo linathibitisha Yesu yuko sawa na Yehova Mungu, au hata wao ni mtu yule yule mmoja. Lakini, uchunguzi wa uangalifu wa andiko hilo hauungi mkono wazo hilo.
Habari inayozunguka maneno ya Wafilipi 2:9 inaonyesha kwamba Yesu alipokea “jina” hilo baada ya kifo na ufufuo wake. Kwa hiyo, kabla ya wakati huo hakuwa na “Jina lile lipitalo kila jina.” Kupewa kwake jina hilo kulionyesha cheo chake kilikuwa kimebadilika. Je! kuna njia yo yote ambavyo cheo cha Yehova kingeweza kubadilika wakati wo wote? Hapana. Sikuzote yeye amekuwa mkuu kupita wote. Hivyo, kupewa kwa Yesu jina la juu zaidi kunathibitisha kwamba yeye si mtu mmoja na Yehova, wala hayuko sawa naye.
Angalia, pia, kwamba jina hilo ‘lilikirimiwa’ kwa Yesu na Yehova. Kwa wazi, ikiwa Mungu anaweza kuchagua kumpa Yesu Mwanaye jina kama hilo, basi lazima Baba awe ndiye mkubwa zaidi, na Yesu awe ndiye mdogo. (1 Wakorintho 11:3) Kwa njia hiyo ni kwamba heshima yo yote inayomwendea Yesu kwa sababu ya pendeleo kubwa hilo inakuwa “kwa utukufu wa Mungu Baba.”—Wafilipi 2:11.
Kwa hiyo, Yesu alipewa jina lililo juu zaidi ya alilopewa ye yote wa viumbe wa Mungu. Lakini kwa wazi kupokea kwake jina hilo hakukumfanya sawa na Mungu. Linganisha na 1 Wakorintho 15:27, panaposema kwamba Mungu alitiisha vitu vyote chini ya miguu ya Yesu lakini yeye mwenyewe hakutiishwa chini ya Yesu.
Jina la juu zaidi alilopewa ni jina gani? Nabii Isaya anatusaidia kujibu. Akinena juu ya Yesu, anasema hivi: “Uweza wa kifalme utakuwa begani mwake; naye ataitwa jina lake, Mshauri wa ajabu, Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani.” (Isaya 9:6, 7) Andiko hilo linaonyesha kwamba uwezo wa juu, cheo au mamlaka ya juu—katika pande zote zilizotajwa na Isaya—ambao Yesu amepewa ili atimize mapenzi ya Yehova.
Yesu alionyesha kadiri ya mamlaka yake ya ukuu alipowaambia wanafunzi wake hivi: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” (Mathayo 28:18) Tumaini la peke yake la wanadamu kwa wakati ujao linategemea cheo cha juu alichokabidhiwa Yesu, na ndiyo sababu unabii wa Isaya unatumiwa kumhusu. “Na jina lake Mataifa watalitumainia.”—Mathayo 12:21.
Mtume Paulo alisema kwamba ‘kwa jina la Yesu kila goti linapasa kupigwa.’ (Wafilipi 2:10) Hilo si jambo linalofanywa juu-juu tu. Yesu alionya kwamba wengi wangedai kufanya kazi za ajabu kwa “jina” lake, lakini yeye hangewatambua. (Mathayo 7:21-23) ‘Kupiga goti’ kikweli kwa jina la Yesu kunamaanisha kutambua cheo chake na kujitiisha kabisa kwenye mamlaka yake. Leo, hiyo maana yake ni kujitiisha kwake akiwa Mfalme, kushiriki katika kazi ya kutangaza habari njema za Ufalme na kutokuwamo katika mambo ya falme za kidunia,—Mathayo 24:14.
Kufanya hivyo kunachochea upinzani kutoka wafalme wa kilimwengu. Yesu alionya hivi: “Mtakuwa watu wa kuchukiwa na mataifa yote kwa ajili ya jina langu.” (Mathayo 24:9) Lakini kwa wale ‘wanaopiga goti’ hivyo, jina la Yesu lina uwezo kweli kweli.
Mtume Petro alitangaza hivi: “Hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.” (Matendo 4:12) Kabla ya hapo, Petro alikuwa ameambia mwanamume kiwete hivi: “Kwa jina la Yesu Kristo wa Nazareti, simama uende.” Kisha mwanamume huyo akatembea. (Matendo 3:6) Yesu aliambia wafuasi wake kwamba wanapaswa kusali ‘kwa jina lake.’ (Yohana 14:14) Tunapotumia jina la Yesu katika sala zetu, hatuwi tukifuata mtindo fulani tu wa kutaja mambo. Bali, tunaomba kwamba uwezo na mamlaka ya juu ya Yesu Kristo itumiwe kwa ajili yetu.
Kwa kuonyesha utukuzo na heshima inayofaa kwa “jina” la Yesu, yaani, cheo au mamlaka yake ya juu, tunapata kuwa kati ya wale ambao inasemwa hivi juu yao: ‘Kila ulimi ukiri ya kuwa Yesu Kristo ni Bwana, kwa utukufu wa Mungu Baba.’—Wafilipi 2:11.