Kwa Sababu Gani ‘Kuamini Jina‘ la Yesu Kristo Kwaleta Uzima?
“ILI mjue ya kuwa mna uzima wa milele, ninyi mnaoliamini Jina la Mwana wa Mungu.” Ndivyo alivyoandika mtume Yohana kwa wafuasi wenzake wa Yesu Kristo karibu na mwisho wa karne ya kwanza. (1 Yohana 5:13) Mapema zaidi ya nusu karne, mtume Petro alikuwa amekwisha iambia korti kuu ya Kiyahudi au Sanhedrin hivi: “Hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana jina jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo.”—Matendo 4:12.
Kwa sababu gani wokovu wote unaambatishwa na “jina” hili? Je! ni namna fulani ya kanuni ya ajabu yenye kutoa uzima? Nayo maana yake n’nini ‘kuliamini Jina la Mwana wa Mungu’? Je! mtu anayejua jina “Yesu Kristo” peke yake angeweza kuwamo katika hali ya kuitumia imani hiyo yenye kuokoa uhai? Je! kulitumia kwetu mwishoni mwa sala zetu kwatosha kuonyesha kwamba sisi tunayo imani hiyo?
YANAYOTIWA NDANI KATIKA “JINA” HILO
Kwa wazi hatuwezi tukamwamini mtu ikiwa twajua tu jina lake na basi, kama vile tusivyoweza kuamini dawa ya ugonjwa fulani kwa kulijua jina tu la dawa hiyo. Mtume Yohana aonyesha kwamba imani yenye kutoa uzima kwa kweli haitiwi katika maneno tu yanayolifanyiza jina “Yesu Kristo” bali katika mtu ambaye linajulisha juu yake. Ndiyo sababu Yohana anasema juu ya habari zake za Injili, kwamba “zimeandikwa; ili mpate kuamini ya kwamba Yesu ndiye Kristo, Mwana wa Mungu; na kwa kuamini mwe na uzima kwa jina lake.” (Yohana 20:31) Kwa hiyo ujuzi wa Neno la Mungu Biblia na yale yote inayoeleza juu ya Mwanawe, Masihi au Kristo, ni wa lazima ili kuipata imani hiyo yenye kuokoa uhai. Je! wewe unao ujuzi huo?
Kutumia tu jina “Yesu Kristo” hakuhakikishi kwamba mtu anayo imani ya kweli katika hilo, imani ya namna ile inayohakikishia uzima wa milele. Je! Yesu mwenyewe hakusema kwamba, wakati wa kuonyesha hukumu ya Mungu, wengine wangesema: “Bwana, Bwana, hatukufanya unabii kwa jina lako, na kwa jina lako kutoa pepo, na kwa jina lako kufanya miujiza mingi? Ndipo nitawaambia dhahiri, Sikuwajua ninyi kamwe; ondokeni kwangu, ninyi mtendao maovu.” (Mt. 7:21-23) Leo wako viongozi wa dini, wahudumu na wahubiri, na vile vile washiriki wa makundi yao, wanaolitumia jina la Yesu Kristo na wanaojidai kufanya kazi ‘kwa jina lake’ na hali wao ‘hawaliamini Jina lake.’ Kwa sababu gani sivyo?
MAMLAKA YAFANANISHWA
Kwa sababu wao hawatendi wala kuishi kupatana na Neno la Mungu Biblia. Kwa hiyo, “Jina” la Yesu halimsimamii yeye tu, utu wake, lakini vile vile na jambo jingine. Gani? Mamlaka yake ya kutekeleza mapenzi ya Mungu na kusudi kama yalivyoonyeshwa katika Biblia. Twaweza kufahamu hili tukiyakumbuka maneno yanayotumiwa nyakati nyingine na maafisa wa polisi: “Fungua, kwa jina la sheria”; au maneno “kwa jina la Mfalme” yanayoonekana katika amri na maagizo ya kifalme. Hapa maneno “kwa jina la” yamaanisha “kwa mamlaka ya,” yaani, kwa mamlaka ya serikali ambayo sheria yake inafikilizwa au ya mfalme ambaye amri yake yatangazwa.
Ikionyesha kwamba neno la Kigiriki (ὄνομα) kwa “jina” lilitumiwa kwa njia iyo hiyo huko nyuma wakati wa mitume, Expository Dictionary of New Testament Words ya Vine (Kit. cha 3, kur. 99, 100) yasema: “ONOMA (ὄνομα) latumiwa . . . kwa yote yanayomaanishwa na jina, juu ya mamlaka, cheo, daraja, fahari, uwezo, utukufu, n.k., juu ya kila kitu kinachoelezwa na jina hilo.”
Ndiyo, “Jina” la Yesu lasimamia mamlaka kuu ambayo Yehova Mungu amemkabidhi, sawa na vile Yesu alivyowaambia wanafunzi wake alipokwisha kufufuliwa kwamba “nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.” (Mt. 28:18) Kwa hiyo basi ulizo la maana ni: Je! sisi twaamini kwamba yeye anayo mamlaka hiyo na je! twaonyesha hivyo kwa kunyenyekea kwake?
Wakati mitume Petro na Yohana walipofanya kazi ya ajabu ya kuponya, watawala na wazee wa Israeli waliwaleta ndani wapate kuwahoji nao wakawauliza hivi: “Kwa nguvu gani na kwa jina ta nani ninyi mmefanya haya?” Kwa kweli, walikuwa wakiwauliza, ‘N’nani aliyewapa ninyi uwezo wa kufanya kazi hizo, au ninyi mliomba mamlaka ya nani kuweza kufanya mwujiza huo?’ Ndio wakati huo Petro alipoionyesha imani yake kwamba jina la Mwana wa Mungu ndilo ‘jina moja lililo chini ya mbingu’ ambalo kwalo kazi za kuokoa zaweza kutimizwa kwa uthabiti. (Matendo 3:1-10; 4:1-13) Lakini viongozi hao wa kidini hawakuliamini jina hilo. Mapema walikuwa wamekwisha onyesha mahali ilipokuwa imani yao walipokuwa wamepigia kelele Pontio Pilato, “Sisi hatuna mfalme ila Kaisari,” hivyo wakimkataa Mwana wa Mungu. (Yohana 19:13-15) Wao waliliamini jina au mamlaka na uwezo wa Kaisari na serikali yake ya kifalme. Watu wengi wanaolitumia jina la Kristo Yesu na kujidai kuliamini kwa kweli wanalisingizia dai hilo kwa kuweka imani yao katika viongozi wa kibinadamu na serikali za kisiasa za wanadamu zilete amani na hali za haki duniani.
Lakini juu ya Kristo Yesu ilitabiriwa kwamba “ataitwa jina lake. Mshauri wa ajabu. Mungu mwenye nguvu, Baba wa milele, Mfalme wa amani.” (Isa. 9:6) Leo mamia ya maelfu ya watu yanajiepusha na mipango na taratibu za kibinadamu kuja kwenye ufalme wa Mwana wa Mungu kama tumaini lao la kweli nao wanautazamia utawala wake kama yeye aliye na mamlaka na uwezo wa kuwaletea haki na faraja wanayoitaka sana. Kwa njia hii unabii mwingine unatimizwa, kwamba “jina lake Mataifa watalitumainia.”—Mt. 12:18-21; linganisha Isaya 42:4, ambapo Mwebrania analitumia neno “sheria” pahali pa “jina.”
Hii yatusaidia kufahamu kwa sababu gani katika Waefeso 1:21 mtume Paulo anaunganisha ‘majina’ na ‘falme, mamlaka, nguvu na usultani.’ Vile vile twaweza kuona kwamba ni kwa sababu Mungu amemtawaza Mwanawe awe juu ya serikali ya Ufalme na akampa mamlaka yote atimilize mapenzi ya kimungu kwamba Wafilipi 2:9-11 inasema kwamba Mungu “alimwadhimisha mno, akamkirimia Jina lile lipitalo kila jina; ili kwa jina la Yesu kila goti lipigwe, la vitu vya mbinguni, na vya duniani, na vya chini ya nchi; na kila ulimi ukiri ya kuwa YESU KRISTO NI BWANA, kwa utukufu wa Mungu Baba.” Ndiyo, jina la Kristo Yesu limepaswa litutie maono ya heshima na unyenyekevu wa utii upitao ule wa kiongozi ye yote wa kibinadamu duniani na usiolingana na mwingine wo wote ila ule wa Baba yake, Yehova Mungu.
WAKILI MKUU WA MUNGU WA UZIMA
Kristo Yesu alitoa uhai wake kama dhabihu ya ukombozi naye atumikia kama Kuhani Mkuu wa Mungu kwa ajili ya wanadamu. Kwa hiyo, wajapokuwa wengi wanasali kwa Mungu “kwa jina la Yesu,” wengine wanatumia maneno haya bila ya kufahamu maana yake hasa. Wao wanadhani Yesu ni namna ya mtu anayewapitishia maombi yao kwa Mungu kwa wepesi mara tu waombapo.
Kwa hakika, kusali katika jina la Yesu, kama vile yeye mwenyewe alivyofundisha, kwamaanisha kufanya hivyo kupitia kwa vyeo vyake vyema “Wakili Mkuu wa uzima” wa Mungu ambaye, kama Kuhani Mkuu na Mwamuzi aliyewekwa, anasafisha kutoka kwa dhambi na kutoa faida za ukombozi kwa watu mmoja mmoja kulingana na ustahili wao wa kuishi chini ya utawala wake wa Ufalme. (Ebr. 2:10, NW; 6:20; Efe. 1:8-10; Yohana 5:22, 27) Tunaposali kwa “jina” la Yesu, hii basi yamaanisha tunafanya ombi kwa mamlaka yake. Twaomba kwamba uwezo wake na cheo na faida kama Wakili Mkuu wa uzima vitumiwe kwa ajili yetu, vikiifanya sala yetu yenye kukubalika kwa Mtawala Mwenye Enzi Yote, Yehova Mungu.
WAAMINIFU KWA JINA LAKE
Ikiwa twataka kuwamo kati ya wale wanaoonyesha imani katika jina la Kristo Yesu ili aupate kuhakikishiwa uzima wa milele, lazima sisi vile vile tuonyeshe uaminifu kwake. Lazima tumtumikie yeye kama Kichwa cha kundi la Kikristo, kwa uaminifu tukiitegemeza mamlaka yake na faida zake za Ufalme. Lazima tuwe kama wale Wakristo katika kundi la karne ya kwanza katika Pergamo ambao, wakiwamo katika hatari ya kupoteza uhai wao kutokana na wale walioupinga utawala wa Ufalme wa Kristo, walizidi ‘kulishika jina lake wala hawakuikana imani yake,’ na kama wale wa Filadelfia ambao ‘walilitunza neno lake wala hawakulikana jina lake.’ (Ufu. 2:13; 3:8) Mwenendo wetu, kati yetu wenyewe na kwa wale waliomo ulimwenguni vile vile, lazima uwe wa namna ambayo hautakana yanayowakilishwa na jina la Mwana wa Mungu. Sawa na vile Wakristo walivyopatwa na mateso huko nyuma, nasi vile vile twaweza kuyatazamia yale yale leo, kwa maana Yesu alitabiri: “Wakati huo watawasaliti ninyi mpate dhiki, nao watawaua; nanyi mtakuwa watu wa kuchukiwa na mataifa yote kwa ajili ya jina langu.”—Mt. 24:9.
Je! chuki hiyo ya mataifa yote inayajilia matengenezo ya kidini na washiriki wa makanisa wanaojidai tu kumwamini Yesu kama Mkombozi wao anayewakombea katika dhambi? Sivyo, chuki hiyo haiji kwa sababu ya kumkubali tu Kristo Yesu kama “Mwana-kondoo wa Mungu” aliyeimwaga damu yake ya uhai kwa ajili yetu. Inakuja kwa sababu watu ‘wanalishika jina lake’ kama linalowakilisha “mamlaka yote mbinguni na duniani” ambayo ni yake kwa kuagizwa na Mungu. Inakuja kwa sababu ya kumkubali yeye kama Mfalme anayestahili wa dunia yote na serikali yake kama utawala wa pekee wenye kutegemezwa kwa kimungu. Je! ndivyo wewe unavyokubali na je! ndivyo kanisa lako linavyokubali? Au dini yako inajidai kuliamini jina la Yesu na huku ikimtazamamia “Kaisari,” serikali za taratibu iliyopo, kama tumaini lao?
Kwa ajili ya hali njema yako ya milele na ile ya wasiri wako, jifunze yote yanayomaanishwa na “Jina la Mwana wa Mungu.” Weka matumaini yako yote katika tegemezo la Mungu kwa utawala wa kifalme wa Mwanawe, na ndipo nawe vile vile unapoweza ‘kujua ya kuwa una uzima wa milele, wewe unayeliamini Jina la Mwana wa Mungu.’—1 Yohana 5:13.