Timotheo Anapata Mashauri kwa Mwanamume Mzee
MIAKA kadha iliyopita wazee wa kundi fulani la kisasa la Mashahidi wa Yehova walipokea kutoka kwa Mkristo mwenzao barua ambayo, kwa sehemu, ilisema hivi: “Ninyi mmenisaidia sana nami nataka kuwajulisha nashukuru sana kwa yote ambayo mmefanya. Leo mimi ni mmoja wa watu walio na furaha zaidi ulimwenguni. Upendo wenu na usaidizi mlionipa umenisaidia niwe nilivyo. Asanteni sana.”
Ni wazi kabisa kwamba barua hiyo iliwafurahisha wazee hao. Sikuzote wazee waaminifu wamefurahia sana heshima wanayoonyeshwa na ndugu na dada zao Wakristo. Nao wazee wa zamani zaidi wamewapa mara nyingi wazee vijana na wasio na ujuzi mwingi kama wao mashauri mazuri juu ya namna wanavyoweza kujithibitisha wanastahili kuheshimiwa hivyo. Kwa mfano, mtume Paulo alifanya hivyo katika barua zake mbili alizomwandikia Timotheo mzee mwenzake aliyekuwa kijana akilinganishwa naye.
Uhusiano wenye upendo uliokuwa kati ya Paulo na Timotheo ulitokeaje? Sisi tunaweza kujifunza nini kutokana na mashauri ya Paulo?
Uhusiano wa Paulo Pamoja na Timotheo
Ni wazi kwamba Timotheo alikutana na Paulo karibu na miaka ya 47-48 W.K. wakati Paulo alipokuja Listra akiwa katika safari yake ya kwanza ya umisionari. Wakati huo huenda ikawa Timotheo alikuwa kijana-tineja tu. Wakati wa ziara hiyo Timotheo, mama yake Eunike na Loisi bibi (nyanya) yake wakawa Wakristo. Lakini, baba ya Timotheo alikuwa Mgiriki asiyeamini. Labda jambo hilo hasa ndilo lililomfanya Paulo akataka kuona Timotheo akiwa na hali njema. Vyo vyote iwavyo, Timotheo alifanya maendeleo mazuri na akasitawisha imani “isiyo na unafiki.” (1 Timotheo 1:5) Wakati Paulo aliporudi Listra akiwa katika safari yake ya pili ya umisionari, karibu miaka miwili baadaye, ndipo alipomchagua Timotheo awe mwenzi wake wa kusafiri naye.
Ndipo ikafuata miaka 15 ya kushirikiana na mtume Paulo. Ilikuwa ni wakati wa kutumikia akiwa katika cheo cha mzee huko Efeso kwamba Timotheo alipokea barua ya kwanza ya Paulo. Barua hiyo iliandikwa muda fulani baada ya Paulo kufunguliwa gerezani huko Roma mwaka wa 61 W.K. na kabla ya kufungwa kwake mara ya pili mwaka wa 64 W.K. Barua ya pili labda iliandikwa mwaka wa 65 W.K., muda mfupi kabla ya kifo cha Paulo.—2 Timotheo 4:6-8.
Shauku ya upendo ambayo Paulo alikuwa nayo kwa Timotheo inaonekana wazi, kwa maana anamwita “mwanangu hasa katika imani,” hata “mwanangu mpendwa.” Kwa hiyo shauri ambalo Paulo alimpa kama kwamba alikuwa baba yake kwa kumwambia ‘atumie mvinyo kidogo, kwa ajili ya tumbo lake, na magonjwa yaliyompata mara kwa mara’ halikutolewa kwa mtu ambaye hakufaa kuambiwa hivyo. Na wakati Paulo anapojua kwamba anakaribia sana kufa, inafaa sana aandike hivi: “Jitahidi kuja kwangu upesi”! Hasa kupendezwa kibinafsi kwa Paulo katika Timotheo kunaonyeshwa katika barua yake ya pili, ambamo vijina vya kibinafsi kama “wewe,” “-ako” na “wewe mwenyewe” vinapatikana kwa wingi karibu asilimia 25 zaidi ya hesabu ambazo vinapatikana katika barua yake ya kwanza. Ni wazi kwamba huyo mzee mwenye umri mkubwa zaidi alimpenda kwa shauku mwenzi wake kijana na alipendezwa na kuona akiwa na hali njema ya kibinafsi.—1 Timotheo 1:2; 5:23; 2 Timotheo 1:2; 4:9.
Zaidi ya hilo, tena kwa maana zaidi, Paulo alimtaka Timotheo atumikie vizuri faida za kundi la Kikristo. Kwa kujua upungufu mbalimbali wa Timotheo upande wa kimwili na kiakili, na pia kwa kujua kwamba ujana wake akilinganishwa na Paulo ulimfanya awe na maelekeo ya kuweza kuwa na “tamaa za ujanani,” Paulo alimshauri hivi: “Jitunze nafsi yako, na mafundisho yako. Dumu katika mambo hayo; maana kwa kufanya hivyo utajiokoa nafsi yako na wale wakusikiao pia.” (2 Timotheo 2:22; 1 Timotheo 4:16) Bila shaka Timotheo alishukuru sana kupokea mashauri ya kimungu kwa mzee mwenye umri mkubwa zaidi na ujuzi mwingi kuliko yeye! Leo pia wazee wenye umri mdogo zaidi wanathamini msaada na mwelekezo wa namna hiyo. Lakini mashauri ya Paulo kwa Timotheo yalikuwa na mambo gani ndani?
“Ukae Katika Mambo Yale Uliyofundishwa”
Ili mtu aendelee kufuata mwendo wa uaminifu akiwa Mkristo—akiwa mzee au akiwa vingine—kumtegemea Mungu kabisa kunatakwa. Mtu asitegemee kamwe nguvu au uwezo wa ujana kwa kadiri inayopita kiasi. Sala ina ubora mkubwa sana. Basi wazo hili la Paulo lilifaa: ‘Endelezeni sala, mkiinua mikono yenye ushikamanifu, bila ghadhabu na majadiliano.’ (1 Timotheo 2:8, NW) Ni jambo la maana sana kwamba wazee waombe uongozi wa kimungu wanapokutana pamoja kuzungumza mambo ya kundi! Wonyesho huo wa ushikamanifu kwa Yehova unazuia kusiwepo majadiliano (mabishano) yasiyofikia mwisho na labda mifoko ya hasira.
Ili Wakristo wavumilie, ni lazima wakae karibu na kundi na kutaka kuliona likiwa na hali njema. Kwa kusudi hilo, Paulo alitoa wazo la kwamba sala isemwe “kwa ajili ya wafalme na wote wenye mamlaka.” Bila shaka, Timotheo alijua kwamba hizo hazikupasa kuwa sala za kubariki wanasiasa kama zile zinazotolewa na viongozi wa kidini wa siku hizi. Bali, zilikuwa maombi aliyopelekewa Mungu ili awasukume wenye mamlaka ya serikali za ulimwengu waruhusu Wakristo waendelee ‘kuishi maisha ya utulivu na amani,’ wakiuhubiri ujumbe wa Ufalme “katika utauwa wote na ustahivu.”—1 Timotheo 2:1, 2.
Mtume Paulo alijua kwamba kuangalia mwendo wa uaminifu wa wengine kungesaidia Timotheo ‘akae katika mambo yale aliyofundishwa.’ Kwa hiyo Paulo aliandika hivi: “Wewe umeyafuata mafundisho yangu, na mwenendo wangu, na makusudi yangu, na imani, na uvumilivu, na upendo, na saburi; tena na adha zangu na mateso.” (2 Timotheo 3:14,10,11) Maelfu ya wazee wengine leo wanaweka mfano uo huo mwema kama wa Paulo. Hiyo inatia ndani njia wanazotumia kufundisha.—1 Wakorintho 4:17.
“Shika Kielelezo cha Maneno Yenye Uzima”
“Kila andiko limepewa kwa maongozi ya Mungu, na linafaa kwa mafundisho, na kwa kuonya watu juu ya makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa mafundisho katika haki.” Ujumbe safi wa kweli ya Kimaandiko ndio unaofanya Mkristo ‘awe mukamilifu, ametengenezwa kabisa kwa kila tendo jema.’—2 Timotheo 3:16, 17, ZSB.
Lakini, wengine wa Wakristo Waefeso hawakuwa tena wakitenda kupatana na kile ambacho Paulo alikiita “kielelezo cha maneno yenye uzima.” (2 Timotheo 1:13) Wao walikuwa na “wazimu wa kuwazia habari za maswali, na mashindano ya maneno.” Wengine waliingia katika magomvi yenye jeuri juu ya vijambo vidogo sana. (1 Timotheo 6:4, 5) Kwa hiyo shauri la Paulo lilikuwa ‘kuyakataa maswali ya upumbavu yasiyo na elimu, kwa kujua ya kuwa huzaa magomvi.’ (2 Timotheo 2:23) Vivyo hivyo leo, inawapasa wazee wakaze fikira zao nyakati zote juu ya mambo yaliyo ya maana kweli kweli, yale yatakayosaidia Wakristo ‘washike uzima ule wa milele.’ Mambo hayo ya maana ni mambo gani? Ni Ufalme wa Mungu uliosimamishwa, kazi ya kuhubiri na kufuata njia ya maisha ya Kikristo.—1 Timotheo 6:11, 12.
Katika siku za Timotheo Himenayo na Fileto, na labda wengine pia, walikuwa wakieneza mafundisho ya uongo, “kuipindua imani ya watu kadha wa kadha.” Kwa sababu ya kupotoka hivyo kwa kuiacha kweli, Paulo alisema, “Nimempa Shetani watu hao.” Inaonekana kuwa wazi kwamba walitengwa na ushirika wa kundi. (2 Timotheo 2:17, 18; 1 Timotheo 1:20) Haitupasi kutazamia kuona hali tofauti leo. Paulo alionya kwamba “nyakati za mwisho wengine watajitenga na imani, wakisikiliza roho zidanganyazo, na mafundisho ya mashetani.” (1 Timotheo 4:1) Mzee kijana asiye na ujuzi angeweza kuudhiwa isivyofaa na jambo hilo, lakini haimpasi kuudhika. Uasi-imani unaofanywa na watu wengine hauibadili kweli kwa njia yo yote. Jambo hilo linawaonyesha tu waasi-imani kuwa watu ambao ‘kwa kuzifuata nia zao wenyewe wanajiepusha wasisikie yaliyo kweli.’—2 Timotheo 4:3, 4.
Linalotiwa ndani ya ‘kushika kielelezo cha maneno yenye uzima,’ au kufuata “mafundisho yenye uzima,” ni kuishi maisha yaliyo na unyofu wa kiadili. (2 Timotheo 1:13; 4:3) Huenda wazee fulani walio vijana zaidi kwa umri wakawa na maoni ya kwamba inawapasa kuchukua msimamo unaopatana na maisha ya kisasa, kufuata maoni yenye kuwapa watu uhuru mwingi kuhusu “dhambi,” au kufuata yale yanayosemwa kuwa ni juu ya dhamiri ya mtu kuamua. Lakini ubishi wa kutegemea hekima ya kilimwengu katika kutetea makosa ni “semi tupu-tupu zinazotia unajisi kilicho kitakatifu.” Jiepushe na falsafa za kilimwengu, Paulo akahimiza, “na maneno ya kupinga ya kile kinachoitwa kwa uongo ‘maarifa.’ “—1 Timotheo 6:20, 21, NW.
Maarifa ya kweli yanapatikana kwa kujifunza kibinafsi mtu akiwa chini ya uongozi wa roho ya Mungu na tengenezo lake. Hilo ndilo jambo linalowezesha mzee, au Mkristo ye yote, kuwa ‘mtenda kazi asiye na sababu ya [kuona aibu], akitumia kwa halali neno la kweli.’ Yeye hatakuwa kama walimu wa uongo wa kidini ‘wanaojifunza sikuzote, ila wasiweze kabisa kuufikia ujuzi wa kweli.’—2 Timotheo 2:15; 3:7.
‘Kusimamia kwa Njia Nzuri’
Ili ‘kusimamia kwa njia nzuri’ mzee Mkristo anahitaji “kuwa mwanana kwa watu wote, awezaye kufundisha, . . . akiwaonya kwa upole.” (1 Timotheo 5:17, NW; 2 Timotheo 2:24, 25) Ni lazima washiriki wote wa kundi washughulikiwe wakiwa mmoja mmoja. Miaka ya Paulo aliyojionea mambo mwenyewe ilikuwa imemfundisha hekima ya kutendea wanaume wazee kama akina baba, “vijana kama ndugu; wanawake wazee kama mama; wanawake vijana kama ndugu wa kike; katika usafi wote.”—1 Timotheo 5:1, 2.
Wakati mtu anapoendelea kuongeza ujuzi wake anazidi kuwa macho aone matatizo ya wengine na mahitaji yao. Timotheo alipaswa kujua hali fulani ambazo huenda zingehitaji kushughulikiwa naye. Je! walikuwako wajane wa kike, kwa mfano, wasio na watu wa ukoo wa karibu, waliohitaji kutunzwa? Je! wo wote wa watumwa Wakristo na matajiri wa kazi Wakristo (kama vile Mkristo aliyeandikwa kazi na tajiri wake wa kazi leo aliye Mkristo) walikuwa na maoni mabaya juu ya uhusiano wao hata maoni hayo yahitaji kurekebishwa? Kwa kuwa waliishi huko Efeso, makao yaliyokuwa na utajiri wa kibiashara, je! wengine walihitaji kukumbushwa kwamba “hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi, na tamaa nyingi zisizo na maana, zenye kudhuru”? Je! Wakristo wenye utajiri walihitaji kushauriwa “wasijivune, wala wasiutumainie utajiri usio yakini, bali wamtumaini Mungu”?—1 Timotheo 5:3-16; 6:1, 2, 9, 17-19.
Je! wengine kundini walikuwa wamejua na hata wakaona matendo yenye dhambi ya wale wasiokuwa na nia ya kufuata sheria za Mungu? “Karipia mbele ya watazamaji wote [hao wenye kuona] watu wanaozoea dhambi,” Paulo akaonya kwa upole, “ili wale wengine wote [wale wanaojua habari za dhambi hiyo] waweze pia kuwa na woga.” Namna gani washiriki wa kike wa kundi? Je! wao walikuwa “wastahivu; si wasingiziaji; watu wa kiasi, waaminifu katika mambo yote”? Au wengine wao walikuwa wakipuza mpango wa Mungu ambao ‘haukumpa mwanamke ruhusa ya kufundisha, wala kumtawala mwanamume’ katika kundi?—1 Timotheo 5:20, NW; 3:11; 2:11, 12.
Je! wanaume waliowekwa watumikie wakiwa wazee na watumishi wa huduma walikuwa wakichaguliwa kwa uangalifu na kwa hadhari iliyohitajiwa? “Usimwekee mtu mikono kwa haraka,” Paulo akashauri. Kuwekwa kwa wazee na watumishi wa huduma hakupasi kutegemea maoni ya kibinafsi, bali kutegemee msaada wa matakwa ya kimungu. Wanapozungumza hatua za kuweka watu hivyo, ingewafaa wazee vijana wayapime kwa uangalifu maoni yanayotolewa na wazee walio na umri mkubwa zaidi na wenye ujuzi mwingi kuliko wao.—1 Timotheo 5:22; 3:1-10.
“Uwe Kielelezo kwa Waaminio”
Inaonekana kuwa Timotheo alikuwa mtu mwenye haya-haya, au mwoga. Huenda ikawa alikuwa akisita-sita kutumia mamlaka yake. Lakini hakupaswa kuwa hivyo. “Mtu awaye yote asiudharau ujana wako,” Paulo akamwambia. “Bali uwe kielelezo kwao waaminio.” Namna gani? “Katika usemi na mwenendo, na katika upendo na imani na usafi.”—1 Timotheo 4:12.
Leo mzee Mkristo angeweza pia kusita-sita na kuona haya kwa sababu ya ujana wake akilinganishwa na wengine. Angeweza kusita-sita kutoa maelezo kwenye mikutano ya wazee. Kwa upande mwingine, angeweza kuwa na maelekeo ya kufanya kimbelembele, kuonyesha ana ukosefu wa unyenyekevu. Ni jambo la maana sana kukumbuka kwamba pendeleo lo lote la Kikristo ambalo huenda tukapewa “si kwa kadiri ya matendo yetu sisi, bali kwa kadiri ya makusudi yake [Mungu] na neema yake”!—2 Timotheo 1:9.
Katika hali ya kimwili, huenda wazee wenye umri wa ujana zaidi wakaweza zaidi ya wengine kuongoza katika kufanya “kazi ya mhubiri wa Injili.” (2 Timotheo 4:5) Ikiwa ndivyo, basi inawapasa kuongoza. Hiyo ni kazi ambayo LAZIMA ifanywe, kwa sababu mapenzi ya Yehova ni kwamba “watu wote waokolewe, na kupata kujua yaliyo kweli.” Tafrija, mapendezi ya mtu ya nyakati za starehe, malikizo au michezo isiruhusiwe kuingia katika wakati uliowekwa vizuri kwa ajili ya huduma yetu ya Kikristo.—1 Timotheo 2:4; 4:8.
Kupatana na shauri la Paulo kwa Timotheo, wala haiwapasi wazee vijana zaidi kuruhusu hali ya kuogopa wanadamu iwazuie kuchukua hatua. Paulo alimkumbusha Timotheo kwamba “Mungu hakutupa roho ya woga, bali ya nguvu na upendo na ya moyo wa kiasi.” Mzee Mkristo, au Mkristo mwingine ye yote, hapaswi ‘kuuonea haya ushuhuda wa Bwana wetu.’ Kwa kweli, inawapasa Wakristo wote wawe na nia ya kushiriki ‘kuvumilia mabaya kwa ajili ya Injili.’—2 Timotheo 1:7, 8.
Kwa sababu ya kutetea kwa ujasiri ibada ya kweli, Timotheo yule mzee kijana zaidi na Paulo yule mzee mwenzake aliyekuwa na umri mkubwa zaidi walipata kupendwa na kuheshimiwa sana na ndugu zao wa Kikristo. Kwa kuiga mfano wa hao waangalizi wa karne ya kwanza, wazee katika karne hii ya 20 watafurahia pia kupendwa na kuheshimiwa sana na ndugu na dada zao wa Kikristo. Ndiyo, wawe ni vijana au wenye umri mkubwa, “wanaume wanaohudumu kwa njia nzuri wanajipatia wenyewe msimamo mwema.”—1 Timotheo 3:13, NW.
[Picha katika ukurasa wa 21]
Inawapasa wazee wawe na nia ya kujifunza kutokana na wale walio na umri mkubwa zaidi na wenye ujuzi mwingi kuliko wao