Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • si kur. 234-237
  • Kitabu cha Biblia Namba 54—1 Timotheo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kitabu cha Biblia Namba 54—1 Timotheo
  • “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YALIYOMO KATIKA TIMOTHEO WA KWANZA
  • KWA NINI NI CHENYE MAFAA
  • Timotheo Anapata Mashauri kwa Mwanamume Mzee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Shika Imani na Dhamiri Njema
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1991
  • Timotheo—“Mtoto Halisi Katika Imani”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
  • Kitabu cha Biblia Namba 55—2 Timotheo
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
Pata Habari Zaidi
“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
si kur. 234-237

Kitabu cha Biblia Namba 54—1 Timotheo

Mwandikaji: Paulo

Mahali Kilipoandikiwa: Makedonia

Uandikaji Ulikamilishwa: c. (karibu) 61-64 W.K.

1, 2. (a) Maelezo juu ya kutiwa gerezani kwa Paulo yana tofauti gani katika Matendo na katika Timotheo wa Pili? (b) Yaelekea Timotheo wa Kwanza iliandikwa wakati gani, na kwa nini?

SIMULIZI la Luka juu ya maisha ya Paulo katika kitabu cha Matendo laisha huku Paulo akiwa katika Rumi akingojea tokeo la ombi lake la rufani kwa Kaisari. Paulo aonyeshwa kuwa akikaa katika nyumba yake mwenyewe ya kukodi, akihubiri Ufalme wa Mungu kwa wote waliomjia, na kufanya hivyo “kwa ujasiri [uhuru wa uneni, NW] mwingi, asikatazwe na mtu.” (Mdo. 28:30, 31) Lakini katika barua yake ya pili kwa Timotheo, Paulo aandika hivi: “Mimi nateswa na uovu kufikia hatua ya vifungo vya gereza kama mtenda maovu,” na anena kwamba kifo chake chakaribia. (2 Tim. 2:9, NW; 4:6-8) Lo! ni badiliko lililoje! Mara ya kwanza, alitendewa kama mfungwa mwenye kuheshimika, mara ya pili kama mhalifu mkubwa. Ni jambo gani lililokuwa limetukia kati ya wakati wa kueleza kwa Luka juu ya hali ya Paulo 61 W.K., mwishoni mwa miaka miwili akiwa katika Rumi, na kuandika kwa Paulo mwenyewe juu ya hali yake akimweleza Timotheo, ambako kwaonekana kuliandikwa muda mfupi kabla ya kifo chake?

2 Ule ugumu wa kuwapo muda wa kutosha ili kuandikwa kwa barua za Paulo kwa Timotheo na Tito kuweze kuwa kulifanyika katika kipindi kinachohusishwa na kitabu cha Matendo umeongoza waelezaji fulani wa Biblia wakate shauri kwamba Paulo alifanikiwa katika ombi lake la rufani kwa Kaisari na aliachiliwa karibu 61 W.K. Chasema hivi The New Westminster Dictionary of the Bible: “Mstari wa umalizio wa Matendo wapatana vizuri zaidi na wazo hilo [kwamba Paulo aliachiliwa baada ya miaka miwili ya kuzuiwa] kuliko ile dhana ya kwamba ufungwa gerezani uliokwisha elezwa ulifikia mwisho kwa hukumu ya mtume huyo na kifo. Luka akazia uhakika wa kwamba hakuna yeyote aliyezuia kazi yake, hivyo bila shaka akitoa wazo la kwamba mwisho wa utendaji wake haukuwa karibu.”a Basi, kuandikwa kwa Timotheo wa Kwanza kulifanyika katika kipindi cha kati ya kuachiliwa kwake kutoka kifungo chake cha kwanza gerezani katika Rumi, na kufungwa gerezani kwake kwa mwisho huko, au karibu 61-64 W.K.

3, 4. (a) Alipofunguliwa kutoka gerezani, ni wazi Paulo alifanya nini? (b) Yeye aliandikia wapi Timotheo wa Kwanza?

3 Alipofunguliwa kutoka gerezani, kwa wazi Paulo alianza tena utendaji wake wa umisionari kwa kushirikiana na Timotheo na Tito. Kama Paulo alipata kufika Hispania, au la, kama wanavyodhania wengine, si hakika. Clement wa Rumi aliandika (karibu 95 W.K.) kwamba Paulo alifika “kwenye ukingo wa mwisho kabisa wa M[agharibi],” ambao ungeweza kuwa ulitia ndani Hispania.b

4 Paulo aliandikia wapi barua yake ya kwanza kwa Timotheo? Timotheo wa Kwanza 1:3 yaonyesha kwamba Paulo alipangia Timotheo akaangalie mambo fulani ya kundi katika Efeso huku yeye mwenyewe akishika njia kwenda Makedonia. Yaonekana kwamba akiwa huko, aliandika barua hiyo iende kwa Timotheo huko nyuma katika Efeso.

5. Kuna ushuhuda gani juu ya uasilia wa zile barua kwa Timotheo?

5 Zile barua mbili kwa Timotheo zimekubaliwa kuanzia nyakati za mapema kabisa kuwa ziliandikwa na Paulo na ya kuwa ni sehemu ya Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu. Waandikaji wa mapema wa Kikristo, kutia na Polycarp, Ignatio, na Clement wa Rumi, wote huafikiana juu ya jambo hilo, na barua hizo zimetiwa katika orodha za karne chache za kwanza kuwa ni miandiko ya Paulo. Mjuzi mmoja aandika hivi: “Kuna miandiko michache ya A[gano] J[ipya] iliyo na ushuhuda wa kuithibitisha kwa kadiri hiyo . . . Kwa hiyo ni lazima makatao ya uasilia yaonwe kuwa yametungwa siku hizi kinyume cha uthibitisho imara wa kanisa la mapema.”c

6. (a) Paulo aliandika Timotheo wa Kwanza kwa sababu gani mbalimbali? (b) Malezi ya Timotheo yalikuwaje, na nini kinachoonyesha kwamba yeye alikuwa mfanya kazi mkomavu?

6 Paulo aliandika barua hii ya kwanza kwa Timotheo ili apangilie wazi taratibu fulani za kitengenezo katika kundi. Pia kulikuwako uhitaji wa yeye kumwonya Timotheo awe macho kwa habari ya mafundisho bandia na kuwaimarisha akina ndugu wajiepushe na hayo ‘maarifa bandia.’ (1 Tim. 6:20, NW) Jiji la kibiashara la Efeso lingetoa pia vishawishi vya ufuatiaji vitu vya kimwili na “kupenda pesa,” na kwa hiyo ungekuwa wakati ufaao kutoa ushauri fulani juu ya jambo hilo pia. (6:10, NW) Kwa hakika Timotheo alikuwa na malezi mazuri ya ujuzi na mazoezi mazuri hivi kwamba angeweza kutumiwa kwa kazi hii. Yeye alizaliwa kwa baba Mgiriki na mama Myahudi mwenye kumhofu Mungu. Haijulikani barabara wakati Timotheo alipogusana mara ya kwanza na Ukristo. Paulo alipotembelea Listra kwenye safari yake ya pili ya umisionari, yaelekea mwisho-mwisho wa 49 W.K. au mapema 50 W.K., Timotheo, (labda akiwa katika miaka yake ya mwisho-mwisho ya utineja au ya mapema 20) tayari alikuwa ‘ameripotiwa vema na akina ndugu katika Listra na Ikonio.’ Kwa hiyo Paulo akapanga ili Timotheo asafiri pamoja na Sila na yeye mwenyewe. (Mdo. 16:1-3, NW) Timotheo hutajwa kwa jina katika 11 kati ya barua 14 za Paulo na pia katika kitabu cha Matendo. Sikuzote Paulo alipendezwa naye kama baba na katika pindi kadhaa akampa mgawo atembelee na kutumikia makundi tofauti—uthibitisho wa kwamba Timotheo alikuwa amefanya kazi njema katika shamba la umisionari na alistahili kushughulikia madaraka mazito.—1 Tim. 1:2; 5:23; 1 The. 3:2; Flp. 2:19.

YALIYOMO KATIKA TIMOTHEO WA KWANZA

7. Kwa nini Paulo amtia moyo Timotheo akae katika Efeso?

7 Mahimizo ya kuwa na imani yenye dhamiri njema (1:1-20). Baada ya kumsalimu Timotheo kama “mwanangu hasa katika imani,” Paulo amtia moyo abaki katika Efeso. Apaswa kusahihisha wale wanaofundisha “fundisho tofauti,” linaloongoza kwenye maswali yasiyo na maana badala ya kutoa imani. Paulo asema kwamba shabaha ya amri hii ni “upendo kutokana na moyo safi na kutokana na dhamiri njema na kutokana na imani isiyo na unafiki.” Yeye aongezea hivi: “Kwa kukengeuka kutoka kwenye mambo haya watu fulani wamegeuziwa kando kuingia katika maongeo ya upuuzi.”—1:2, 3, 5, 6, NW.

8. Kuonyeshwa rehema kwa Paulo kulikazia nini, naye amtia moyo Timotheo apige vita gani vizuri?

8 Ingawa hapo kwanza Paulo alikuwa mkufuru na mnyanyasi, hata hivyo, neema ya Bwana “ilizidi sana, pamoja na imani na pendo lililo katika Kristo Yesu,” hivi kwamba alionyeshwa rehema. Alikuwa amekuwa wa mbele kabisa kati ya watenda dhambi, na kwa hiyo akawa wonyesho wa ustahimilivu wa Kristo Yesu, ambaye “alikuja ulimwenguni awaokoe wenye dhambi.” Lo! Mfalme wa umilele astahili kama nini kupokea heshima na utukufu milele! Paulo amwagiza Timotheo apige vita vizuri, “akiwa mwenye imani na dhamiri njema.” Ni lazima asiwe kama wale ambao ‘wameangamia kwa habari ya imani yao,’ kama vile Himenayo na Aleksanda (Iskanda), ambao Paulo amewatia nidhamu (adabu) kwa sababu ya kukufuru.—1:14, 15, 19.

9. (a) Ni sala gani ambazo zapasa kutolewa, na kwa nini? (b) Ni nini lasemwa kuhusu wanawake katika kundi?

9 Maagizo kuhusu ibada na tengenezo katika kundi (2:1–6:2). Sala zitolewe kuhusu watu wa namna zote, kutia na wale walio katika daraja la juu, kwa kusudi la kwamba Wakristo wapate kuishi kwa amani katika ujitoaji kimungu. Ni mapenzi ya Mungu, yule Mwokozi, kwamba “namna zote za watu waokolewe na waje kwenye maarifa sahihi ya ukweli. Kwa maana kuna Mungu mmoja, na mpatanishi mmoja kati ya Mungu na wanadamu, binadamu, Kristo Yesu, ambaye alijitoa kuwa ukombozi unaolingana kwa ajili ya wote.” (2:4-6, NW) Paulo aliwekwa awe mtume na mwalimu wa mambo haya. Kwa hiyo awatolea wito wanaume wasali kwa uaminifu-mshikamanifu na wanawake wavalie kwa kiasi na kiakili, kama iwafaavyo wale ambao humcha Mungu. Ni lazima mwanamke ajifunze kuwa mnyamavu na asijizoeze mamlaka juu ya mwanamume, “kwa maana Adamu ndiye aliyeumbwa kwanza, na Hawa baadaye.”—2:13.

10. Ni nini sifa za waangalizi na watumishi wa huduma, na kwa nini Paulo aandika mambo haya?

10 Mwanamume ambaye hujitahidi kufikia kuwa mwangalizi atamani kazi njema. Ndipo Paulo aorodhesha sifa kwa waangalizi na watumishi wa huduma. Ni lazima mwangalizi “awe bila lawama, mume wa mke mmoja, mwenye kiasi katika mazoea, timamu katika akili, mwenye utaratibu, mkaribishaji wa wageni, mwenye kustahili kufundisha, si mpiga kelele ya ulevi, si mpigaji, bali mwepesi kukubali maoni ya wengine, si mtaka vita, si mpenda fedha, mwanamume mwenye kusimamia nyumba yake mwenyewe kwa njia nzuri, mwenye kutiisha watoto kwa uzito wote . . . , si mwanamume aliyeongoka hivi karibuni . . . Imempasa awe na ushuhuda mzuri kutoka kwa watu walio nje pia.” (3:2-7, NW) Kuna matakwa yenye kufanana na hayo kwa watumishi wa huduma, na yawapasa wapitie mtihani juu ya kufaa kwao kabla ya kutumikia. Paulo aandika mambo haya ili Timotheo apate kujua jinsi yeye apaswa kujiendesha mwenyewe katika kundi la Mungu aliye hai, ambalo ni “nguzo na msingi wa kweli.”—3:15.

11. (a) Ni matatizo gani yatakayotokea baadaye? (b) Timotheo apaswa kutoa uangalifu kwenye nini, na kwa nini?

11 Katika nyakati za baadaye watu fulani wataacha imani kupitia mafundisho ya roho waovu. Watu wanafiki wanaonena uwongo watakataza ndoa na kuamuru kushika mwiko wa vyakula ambavyo Mungu aliviumba ili viliwe kwa shukrani. Akiwa mhudumu mzuri, ni lazima Timotheo akatae hadithi bandia na “hadithi za kizee.” Kwa upande mwingine, yampasa awe akijizoeza mwenyewe ujitoaji kimungu ikiwa ndiyo shabaha yake. “Kwa maana twajitaabisha na kujitahidi kwa kusudi hili,” asema Paulo, “kwa sababu tunamtumaini Mungu aliye hai, aliye Mwokozi wa watu wote, hasa wa waaminio.” Kwa hiyo ni lazima Timotheo aaendelee kutoa amri hizi na kuzifundisha. Hapaswi kuacha mtu yeyote adharau ujana wake bali, kwa kinyume, awe kielelezo katika mwenendo na utumishi wa kumcha Mungu. Apaswa kufuata sana mambo haya na kujiangalia daima na fundisho lake, kwa maana kwa kukaa katika mambo haya, ‘atajiokoa nafsi yake na wale wamsikiao.’—4:7, 10, 16.

12. Ni shauri gani ambalo latolewa juu ya kushughulika na wajane na wengine katika kundi?

12 Paulo amshauri Timotheo juu ya jinsi ya kushughulika na watu mmoja mmoja: wanaume wazee kama akina baba, wanaume wachanga zaidi kama akina ndugu, wanawake wazee kama akina mama, wanawake wachanga zaidi kama akina dada. Mpango ufaao wapasa kufanywa kwa ajili ya wale walio wajane kweli kweli. Hata hivyo, familia ya mjane yapaswa kumtunza ikiwa yawezekana. Kushindwa kufanya hivyo kungekuwa ni kukana imani. Akiwa angalau na miaka 60, mjane aweza kutiwa katika orodha ikiwa “ameshuhudiwa kwa matendo mema.” (5:10) Kwa upande mwingine, wajane wachanga zaidi, ambao huacha misisimuko yao ya kingono iwatawale, wapaswa kukataliwa hilo. Badala ya wao kutanga-tanga na kupiga porojo, acha wafunge ndoa na kuzaa watoto, ili wasimpe mpinzani sababu ya kulaumu.

13. Ni ufikirio gani ambao wapasa kuonyeshwa kwa wanaume wazee, ni jinsi gani watu wenye kuzoea dhambi wapasa kushughulikiwa, na ni daraka gani laanguka juu ya watumwa?

13 Wanaume wazee ambao husimamia kwa njia nzuri wapaswa kuhesabiwa wastahili heshima maradufu, “hasa wao wajitaabishao kwa kuhutubu na kufundisha.” (5:17) Shtaka halipasi kukubaliwa kuhusu mwanamume mzee isipokuwa kwa ushuhuda wa mashahidi wawili au watatu. Watu ambao huzoea dhambi wapaswa kukaripiwa mbele ya watazamaji wote, lakini hakupasi kuwe kutangulia kuhukumu bila kusikiliza kwanza au upendeleo katika mambo haya. Watumwa wapaswa wastahi wenyeji wao, wakitoa utumishi mwema, hasa kwa akina ndugu, ambao ni ‘waamini na wapendwa.’—6:2.

14. Paulo ana nini la kusema juu ya kiburi na kupenda pesa kuhusiana na “ujitoaji kimungu na kuridhika”?

14 Shauri juu ya “ujitoaji kimungu pamoja na kuridhika” (6:3-21). Mtu asiyekubali kufuata maneno yenye afya amejivimbisha kwa kiburi na ni mgonjwa kiakili kuhusu maswali, yenye kuongoza kwenye ugomvi wenye jeuri juu ya mambo madogo-madogo. Kwa upande mwingine, “ujitoaji kimungu pamoja na kuridhika” ni njia ya pato kubwa. Mtu apaswa kuridhika na chakula na nguo. Kuazimia kuwa tajiri ni mtego wenye kuongoza kwenye uharibifu, na kupenda pesa ni “mzizi wa namna zote za mambo yenye kuumiza.” Paulo asihi Timotheo, akiwa mtu wa Mungu, ayakimbie mambo haya, afuatie mema ya Kikristo, apige lile pigano zuri la imani, na ‘ashike imara ule uhai wa milele.’ (6:6, 10, 12, NW) Ni lazima aishike amri “kwa njia isiyo na doa wala yenye kulaumika” mpaka ule udhihirisho wa Bwana Yesu Kristo. Wale walio matajiri wapaswa ‘kuweka tumaini lao, si juu ya mali zisizo na uhakika, bali juu ya Mungu,’ ili washike imara uhai ulio kweli kweli. Katika kumalizia, Paulo amtia moyo Timotheo alinde amana yake ya kimafundisho na kugeukia mbali kutoka kwenye uneni wenye kuchafua na kutoka kwenye “mapinganisho ya yale yaitwayo ‘maarifa’ kwa ubandia.”—6:14, 17, 20, NW.

KWA NINI NI CHENYE MAFAA

15. Ni onyo gani latolewa juu ya dhana-dhana na mabishano?

15 Barua hii yatoa onyo kali kwa wale wanaojiingiza katika dhana-dhana za ubatili na mabishano ya kifalsafa. “Mashindano ya maneno” yahusiana na kiburi na yapasa kuepukwa, kwa maana Paulo atuambia kwamba huzuia ukuzi wa Kikristo, yakitokeza tu “maswali wala si madaraka ya Mungu yaliyo katika imani.” (6:3-6; 1:4) Pamoja na matendo ya mwili, mabishano hayo hayapatani na “mafundisho yenye uzima; kama vile ilivyonenwa katika Habari Njema ya utukufu wa Mungu ahimidiwaye.”—1:10, 11.

16. Ni shauri gani alilotoa Paulo juu ya kupenda mali?

16 Wakristo katika Efeso lenye pupa ya pesa kwa wazi walihitaji shauri juu ya kupigana na kupenda mali na vikengeushaji vyake. Paulo alitoa shauri hilo. Ulimwengu umemnukuu sana kwa kusema, ‘Kupenda pesa ni shina la mabaya ya kila namna,’ lakini jinsi walivyo wachache wanaotii maneno yake! Kinyume cha hilo, Wakristo wa kweli wahitaji kutii ushauri huo wakati wote. Wamaanisha uhai kwao. Wao wahitaji kukimbia kutoka kwa mtego wenye kuumiza wa kupenda mali, wategemeze tumaini lao, si kwenye “utajiri usio yakini, bali wamtumaini Mungu atupaye vitu vyote kwa wingi ili tuvitumie kwa furaha.”—6:6-12, 17-19.

17. Ni ushauri gani kwa Timotheo ulio wa wakati unaofaa kwa wahudumu wote wachanga wenye bidii leo?

17 Barua ya Paulo yaonyesha kwamba Timotheo mwenyewe alikuwa kielelezo kizuri cha anavyopasa kuwa Mkristo mchanga. Ingawa kwa kulinganishwa alikuwa mchanga katika miaka, yeye alikuwa mkomavu katika ukuzi wa kiroho. Yeye alikuwa amejitahidi astahili kuwa mwangalizi na alibarikiwa sana katika mapendeleo aliyoonea shangwe. Lakini kama wahudumu wote wachanga wenye bidii leo, yeye alihitaji kuendelea kutafakari mambo hayo na kuyafuata sana ili aendelee kufanya maendeleo. Ushauri wa Paulo ni wa wakati unaofaa kwa wote wanaotafuta shangwe yenye kuendelea katika kufanya maendeleo ya Kikristo: “Jipe mwenyewe uangalifu wa kudumu na kwa kufundisha kwako. Kaa kando ya mambo hayo, kwa maana kwa kufanya hivyo wewe utajiokoa mwenyewe na wale wanaokusikiliza wewe.”—4:15, 16, NW.

18. Ni mipango gani ya utaratibu katika kundi inayoelezwa waziwazi, na ni jinsi gani Paulo atumia Maandiko ya Kiebrania kuwa mamlaka?

18 Barua hii iliyopuliziwa na Mungu yatia uthamini kwa ajili ya mipango yenye utaratibu ya Mungu. Yaonyesha jinsi wanaume na wanawake waweza kufanya sehemu zao katika kudumisha upatano wa kitheokrasi katika kundi. (2:8-15) Kisha yaendelea kuzungumza juu ya sifa za waangalizi na watumishi wa huduma. Hivyo roho takatifu huonyesha matakwa ya kutimizwa na wale wanaotumikia katika nyadhifa (vyeo) maalumu. Barua hii pia yatia moyo wahudumu wote walio wakfu watimize viwango hivyo, kwa kusema: “Ikiwa mwanamume yeyote anajitahidi kufikia cheo cha mwangalizi, yeye atamani kazi nzuri.” (3:1-13, NW) Mtazamo unaofaa wa mwangalizi kuelekea vikundi vya umri mbalimbali na jinsia tofauti-tofauti katika kundi wazungumzwa kwa kufaa kama vile katika kushughulikia mashtaka mbele ya mashahidi. Katika kukazia kwamba wanaume wazee wanaofanya kazi kwa bidii katika kunena na kufundisha wastahili heshima maradufu, Paulo ataja Maandiko ya Kiebrania mara mbili kuwa mamlaka: “Kwa maana andiko lasema, Usimfunge kinywa ng’ombe apurapo nafaka. Na tena, Mtenda kazi astahili ujira wake.”—1 Tim. 5:1-3, 9, 10, 19-21, 17, 18; Kum. 25:4; Law. 19:13.

19. Tumaini la Ufalme latangulizwaje, na ni mahimizo gani yanayotolewa kwa msingi huo?

19 Baada ya kutoa shauri hilo lote zuri, Paulo aongeza kwamba amri hiyo yapasa kufuatwa kwa njia isiyo na waa na isiyolaumika ‘hata kufunuliwa kwake Bwana Yesu Kristo kuwa Mfalme wa wafalme, Bwana wa mabwana.’ Kwa msingi wa tumaini hili la Kikristo, barua hiyo yamalizia kwa mahimizo yenye nguvu kwa ajili ya Wakristo “watende mema, wawe matajiri kwa kutenda mema, wawe tayari kutoa mali zao, washirikiane na wengine kwa moyo; huku wakijiwekea akiba iwe msingi mzuri kwa wakati ujao, ili wapate uzima ulio kweli kweli.” (1 Tim. 6:14, 15, 18, 19) Maagizo yote mazuri ya Timotheo wa Kwanza ni yenye mafaa kweli kweli!

[Maelezo ya Chini]

a 1970, kilichohaririwa na H. S. Gehman, ukurasa 721.

b The Ante-Nicene Fathers, Buku 1, ukurasa 6, “The First Epistle of Clement to the Corinthians,” sura 5.

c New Bible Dictionary, hariri ya pili, 1986, kilichohaririwa na J. D. Douglas, ukurasa 1203.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki