Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • si kur. 237-239
  • Kitabu cha Biblia Namba 55—2 Timotheo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kitabu cha Biblia Namba 55—2 Timotheo
  • “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • YALIYOMO KATIKA TIMOTHEO WA PILI
  • KWA NINI NI CHENYE MAFAA
  • Ni Nini Kinachoweza Kutusaidia Kutumia Neno la Kweli Sawasawa?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Timotheo Anapata Mashauri kwa Mwanamume Mzee
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1984
  • Kitabu cha Biblia Namba 54—1 Timotheo
    “Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
  • Timotheo—“Mtoto Halisi Katika Imani”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1999
Pata Habari Zaidi
“Kila Andiko, Lenye Pumzi ya Mungu, Lafaa”
si kur. 237-239

Kitabu cha Biblia Namba 55—2 Timotheo

Mwandikaji: Paulo

Mahali Kilipoandikiwa: Rumi

Uandikaji Ulikamilishwa: c. (karibu) 65 W.K.

1. Ni mnyanyaso gani uliowaka katika Rumi karibu 64 W.K., na yaonekana ilikuwa hivyo kwa sababu gani?

KWA mara nyingine tena Paulo alikuwa mfungwa katika Rumi. Hata hivyo, hali za hiki kifungo cha gerezani zilikuwa kali zaidi ya zile za kwanza. Kwa kukadiria ilikuwa kama 65 W.K. Moto mkubwa ulikuwa umekumba Rumi katika Julai 64 W.K., ukisababisha hasara ya mweneo mkubwa katika 10 kati ya mikoa 14 ya jiji hilo. Kulingana na Tacitus mwanahistoria Mrumi, Maliki Nero hakuweza ‘kuondolea mbali ile imani mbaya ya kwamba moto huo ulitokea kwa agizo fulani. Hivyo, ili kuondolea mbali ripoti hiyo, Nero aliweka kisingizio na akaleta mateso makali kabisa juu ya jamii moja iliyochukiwa kwa sababu ya machukivu yao, ambayo iliitwa Wakristo na halaiki ya watu. . . . Umati mkubwa sana ulishtakiwa, hasa si juu ya uhalifu wa kuliwasha jiji moto, bali juu ya kuchukia ainabinadamu. Dhihaka za kila namna ziliongezewa kwenye vifo vyao. Kwa kufunikwa ngozi za wanyama, wao waliraruliwa na mbwa wakaangamia, au wakatundikwa kwenye misalaba, au wakaangamizwa kwa miali ya moto na kuteketezwa, ili wawe kimuliko wakati wa usiku, wakati ambapo mchana ulikuwa umekwisha. Nero alitoa bustani zake zitumiwe kwa tamasha hiyo . . . kukatokea hisia ya huruma; kwa maana wao hawakuwa wakiangamizwa kwa faida ya umma kama ilivyoonekana, bali ili kutosheleza ukatili wa binadamu mmoja.”a

2. Ni chini ya hali gani Paulo aliandika Timotheo wa Pili, na kwa nini yeye anena kwa kumthamini Onesiforo?

2 Yawezekana ilikuwa karibu na wakati wa wimbi hilo la mnyanyaso wenye jeuri kwamba Paulo akajipata tena akiwa mfungwa katika Rumi. Wakati huu alikuwa katika minyororo. Hakutarajia kuachiliwa bali alingojea hukumu ya mwisho na kuuawa tu. Wageni wenye kuzuru walikuwa wachache. Kwa kweli, kujitambulisha kwa mtu yeyote waziwazi kuwa Mkristo kulikuwa ni kujiingiza katika hatari ya kukamatwa na kuuawa kwa kuteswa-teswa. Kwa hiyo Paulo angeweza kuandika kwa uthamini kuhusu mgeni mwenye kumzuru kutoka Efeso: “Bwana awape rehema walio wa nyumba ya Onesiforo; kwa sababu mara nyingi aliniburudisha, wala hakuona haya kwa sababu ya munyororo wangu; lakini, wakati alipokuwa katika Rumi, alinitafuta kwa bidii, na kunipata.” (2 Tim. 1:16, 17, ZSB) Akiandika chini ya uvuli wa kifo, Paulo ajieleza kuwa “mtume wa Kristo Yesu, kwa mapenzi ya Mungu; kwa ajili ya ahadi ya uzima ulio katika Kristo Yesu.” (1:1) Paulo alijua kwamba uhai katika muungano na Kristo ulimngoja. Alikuwa amehubiri katika mengi ya majiji yale makubwa-makubwa ya ulimwengu uliojulikana, kuanzia Yerusalemu mpaka Rumi, na labda hata kufika mbali kule Hispania. (Rum. 15:24, 28) Alikuwa amepiga mbio katika mwendo kwa uaminifu mpaka mwisho.—2 Tim. 4:6-8.

3. Timotheo wa Pili iliandikwa lini, nayo imefaaje Wakristo katika vipindi vile vyote?

3 Labda barua hiyo iliandikwa karibu 65 W.K., mara tu kabla ya Paulo kuuawa kwa ajili ya imani yake. Labda Timotheo alikuwa angali Efeso, kwa maana Paulo alikuwa amemtia moyo akae huko. (1 Tim. 1:3) Sasa, mara mbili Paulo amsihi Timotheo aje kwake upesi, naye amwomba aambatane na Marko, na pia lile joho na hati-kunjo ambazo Paulo aliacha Troa. (2 Tim. 4:9, 11, 13, 21) Ikiwa imeandikwa wakati wa hatari hivyo, barua hii ilikuwa na kitia-moyo chenye nguvu kwa Timotheo, nayo imeendelea kutoa kitia-moyo chenye mafaa kwa Wakristo wa kweli katika vipindi vyote vya tangu hapo.

4. Ni nini yathibitisha Timotheo wa Pili ni asilia na yenye kukubalika?

4 Kitabu cha Timotheo wa Pili ni asilia na ni chenye kukubalika kwa sababu zile zilizozungumzwa tayari chini ya Timotheo wa Kwanza. Kilitambuliwa na kutumiwa na waandikaji na waelezaji wa mapema, kutia na Polycarp katika karne ya pili W.K.

YALIYOMO KATIKA TIMOTHEO WA PILI

5. Ni imani ya aina gani ambayo yakaa katika Timotheo, na bado yeye apaswa kuendelea kufanya nini?

5 “Kushika kigezo cha maneno yenye afya,” NW (1:1–3:17). Paulo amwambia Timotheo kwamba hamsahau yeye kamwe katika sala zake, na kwamba atamani sana kumwona. Akumbuka ‘imani isiyo na unafiki’ iliyo katika Timotheo na ambayo ilikaa kwanza katika Loisi nyanya yake na Eunike mama yake. Timotheo apaswa kukichochea kama moto kipawa kilicho ndani yake, ‘kwa maana Mungu hakupatia roho ya woga, bali ile ya nguvu na ya upendo na ya utimamu wa akili.’ Kwa hiyo acha yeye asione haya kutoa ushahidi na kupatwa na uovu kwa ajili ya habari njema kwa sababu fadhili zisizostahilika za Mungu zimeonyeshwa wazi kupitia udhihirisho wa Mwokozi, Kristo Yesu. Timotheo apaswa ‘kufuliza kushika kigezo cha maneno yenye afya’ aliyosikia kutoka kwa Paulo, akikilinda kama amana nzuri.—1:5, 7, 13, NW.

6. Paulo atoa shauri gani juu ya kufundisha, na Timotheo awezaje kuwa mfanya kazi mwenye kukubaliwa na chombo chenye kuheshimika?

6 Timotheo apaswa kukabidhi mambo aliyojifunza kutoka kwa Paulo kwa “wanaume waaminifu, ambao, nao, watakuwa wastahili vya kutosha kufundisha wengine.” Timotheo apaswa kujithibitisha kuwa askari mzuri wa Kristo Yesu. Askari huepuka kujitatanisha katika mambo ya biashara. Zaidi ya hilo, mwenye kuvikwa taji michezoni hushindana kulingana na sheria. Ili kupata ufahamu, Timotheo apaswa kufikiria daima maneno ya Paulo. Jambo la maana kukumbuka na kukumbusha wengine ni kwamba “Yesu Kristo aliinuliwa kutoka kwa wafu na alikuwa wa mbegu ya Daudi” na kwamba wokovu na utukufu wa milele katika muungano pamoja na Kristo, kutawala wakiwa wafalme pamoja naye, ni thawabu za wachaguliwa ambao watavumilia. Timotheo apaswa kufanya yote yote awezayo ili kujitokeza kwa Mungu akiwa mfanya kazi mwenye kukubaliwa, akiepuka kabisa maneno matupu ambayo huchafua kilicho kitakatifu, ambayo huenea kama donda-ndugu. Kama vile katika nyumba kubwa chombo chenye kuheshimika huwekwa kando na kisicho na heshima, hivyo Paulo ashauri Timotheo akimbie “kutoka kwenye tamaa ambazo hutukia ujanani, lakini ufuatie uadilifu, imani, upendo, amani, pamoja na wale ambao huitia Bwana kutokana na moyo safi.” Mtumwa wa Bwana ahitaji kuwa mwanana kwa watu wote, mwenye kustahili kufundisha, akiagiza kwa upole.—2:2, 8, 22, NW.

7. Kwa nini Maandiko yaliyopuliziwa na Mungu yapasa kuwa yenye mafaa hasa katika “siku za mwisho”?

7 “Katika siku za mwisho,” kutakuwako nyakati zilizo ngumu kushughulika nazo na watu wanaothibitika kuwa bandia kwa onyesho lao la ujitoaji kimungu, “sikuzote wakijifunza na bado wasiweze kamwe kufikia maarifa sahihi ya ukweli.” Lakini Timotheo amefuata kwa ukaribu fundisho la Paulo, mwendo wake wa maisha, na minyanyaso yake, ambayo Bwana alimkomboa kutoka kwayo. “Kwa uhakika,” yeye aongezea, “wote wale wanaotamani kuishi kwa ujitoaji kimungu katika ushirika pamoja na Kristo Yesu watanyanyaswa pia.” (NW) Hata hivyo, Timotheo apaswa aendelee katika mambo aliyojifunza kuanzia utoto mchanga, ambayo yaweza kumhekimisha kwa ajili ya wokovu, kwa maana “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa.”—3:1, 7, 12, 16.

8. Paulo ahimiza Timotheo afanye nini, na katika habari hii Paulo ashangiliaje?

8 Kuitimiza huduma kikamili (4:1-22). Paulo amwagiza Timotheo ‘alihubiri’ neno kwa uharaka. (4:2) Wakati utakuja ambapo watu hawatachukuliana na fundisho lenye afya na watageukia walimu bandia, lakini acha Timotheo aweke fahamu zake, ‘afanye kazi ya mweneza-evanjeli, akitimiza huduma yake kikamili.’ Akitambua kifo chake ki karibu, Paulo ashangilia kwamba yeye amepiga lile pigano zuri, kwamba ameukimbia mwendo mpaka mwisho na akaishika imani. Sasa atazama mbele kwa uhakika kwenye ile thawabu, “taji la uadilifu.”—4:5, 8, NW.

9. Paulo aeleza ana uhakika gani katika nguvu ya Bwana?

9 Paulo amsihi Timotheo amjie haraka na atoa maagizo kuhusu safari hiyo. Paulo alipofanya utetezi wake wa kwanza kila mtu alimwacha, lakini Bwana alimwingiza nguvu ili kuhubiri kuweze kutimizwa kikamili miongoni mwa mataifa. Ndiyo, yeye ana uhakika kwamba Bwana atamkomboa kutoka kila kazi mbovu na kumwokoa kwa ajili ya Ufalme Wake wa kimbingu.

KWA NINI NI CHENYE MAFAA

10. (a) Ni mafaa gani hasa ya “kila andiko” inayokaziwa katika Timotheo wa Pili, nao Wakristo wapaswa kujitahidi kuwa nini? (b) Ni uvutano gani upaswao kuepukwa, nalo hilo laweza kufanywaje? (c) Kwaendelea kuwa uhitaji wenye uharaka kwa ajili ya nini?

10 “Kila andiko, lenye pumzi ya Mungu, lafaa.” Lina mafaa kwa ajili ya nini? Paulo atuambia hivi katika barua yake ya pili kwa Timotheo: “Kwa mafundisho, na kwa kuwaonya watu makosa yao, na kwa kuwaongoza, na kwa kuwaadibisha katika haki; ili mtu wa Mungu awe kamili, amekamilishwa apate kutenda kila tendo jema.” (3:16, 17) Kwa hiyo mafaa ya “mafundisho” yakaziwa katika barua hii. Wapenda uadilifu wote leo watataka kufuata shauri lenye hekima la barua hiyo kwa kujitahidi kuwa walimu wa Neno na katika kufanya yote yote ili kuwa wafanya kazi wa Mungu waliokubaliwa, ‘wakitumia kwa halali neno la kweli.’ Kama katika Efeso ya siku za Timotheo, ndivyo katika kizazi cha ki-siku-hizi, kuna wale wanaojishughulisha katika “maswali ya upumbavu yasiyo na elimu,” ambao “wakijifunza sikuzote, ila wasiweze kabisa kuufikia ujuzi wa kweli,” na wanaokataa “mafundisho yenye uzima” kwa kupendelea walimu wanaotekenya masikio yao jinsi wanavyotaka kwa ubinafsi. (2:15, 23; 3:7; 4:3, 4) Ili kuepuka uvutano huo wa kilimwengu wenye kuchafua, ni lazima kuendelea ‘kushika kielelezo cha maneno yenye uzima’ katika imani na upendo. Zaidi ya hayo, kuna uhitaji wenye uharaka wa watu zaidi na zaidi ‘kufaa kufundisha wengine’ ndani na nje ya kundi pia, kama vile Timotheo, “mtumwa wa Bwana.” Wenye furaha ni wote wanaobeba daraka hilo, kuwa ‘wanaofaa kufundisha kwa uanana,’ na wanaohubiri neno “kwa uvumilivu wote na mafundisho”!—1:13; 2:2, 24, 25; 4:2.

11. Ni ushauri gani unaotolewa kwa habari ya vijana?

11 Kama alivyoeleza Paulo, Timotheo alikuwa ameyajua maandishi matakatifu “tangu utoto” kwa sababu ya maagizo yenye upendo ya Loisi na Eunike. “Tangu utoto” pia yaonyesha wakati wa kuanza maagizo ya Biblia kwa ajili ya watoto leo. Lakini vipi ikiwa, katika miaka ya baadaye, vichocheo vya mapema vya bidii vyaanza kufifia? Ushauri wa Paulo ni kuamsha kichocheo hicho tena katika roho ya “nguvu na ya upendo na ya moyo wa kiasi,” kwa kutunza imani isiyo na unafiki. “Siku za mwisho,” yeye alisema, kutakuwako nyakati za hatari, kukiwa na matatizo ya kutokutii na mafundisho bandia. Ndiyo sababu ni jambo la lazima sana hasa kwa vijana, na wengine wote, ‘kuwa na kiasi katika mambo yote, na kutimiliza huduma yao.’—3:15; 1:5-7; 3:1-5; 4:5.

12. (a) Paulo alielekezaje uangalifu kwenye Mbegu ya Ufalme, naye alieleza tumaini gani? (b) Watumishi wa Mungu leo wawezaje kuwa na mtazamo ule ule wa akili kama Paulo?

12 Thawabu yastahili kushindaniwa. (2:3-7) Kwa habari hii, Paulo aelekeza uangalifu kwenye Mbegu ya Ufalme, akisema: “Mkumbuke Yesu Kristo, aliyefufuka katika wafu, wa uzao [mbegu, NW] wa Daudi kama inenavyo injili.” Tumaini la Paulo lilikuwa ni abaki katika muungamano na Mbegu hiyo. Mbele zaidi anena juu ya kuuawa kwake kulikokuwa kwakaribia kwa maneno ya shangwe ya ushindi: “Baada ya hayo nimewekewa taji ya haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa siku ile; wala si mimi tu, bali na watu wote pia waliopenda kufunuliwa kwake.” (2:8; 4:8) Jinsi walivyo na furaha wale wote wanaoweza kutazama nyuma kwenye miaka mingi ya utumishi wa uaminifu na kusema vivyo hivyo! Hata hivyo, hilo lataka kutumikia sasa katika ukamilifu, na upendo kwa ajili ya udhihirisho wa Yesu Kristo, na kuonyesha uhakika ule ule kama Paulo alipoandika hivi: “Bwana ataniokoa na kila neno baya, na kunihifadhi hata nifike ufalme wake wa mbinguni. Utukufu una Yeye milele na milele. Amina.”—4:18.

[Maelezo ya Chini]

a The Complete Works of Tacitus, 1942, kilichohaririwa na Moses Hadas, kurasa 380-1.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki