Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 12/15 kur. 5-9
  • Kuna Njia ya Kuondoa Ukosefu wa Furaha

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kuna Njia ya Kuondoa Ukosefu wa Furaha
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Kujitazama Wenyewe
  • Kuongoza Mawazo Yetu
  • Kufurahia Kile Ambacho Mungu Anatupa Sisi
  • Sisi Hatuko Peke Yetu
  • “Ee Mungu, Unichunguze”
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1993
  • Yehova, ‘Ngome Yetu Wakati wa Taabu’
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
  • Mtumikie Yehova kwa Moyo Wenye Kujaa Furaha
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Je, Wewe Hukubali Msaada wa Yehova?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2004
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 12/15 kur. 5-9

Kuna Njia ya Kuondoa Ukosefu wa Furaha

WATU wanaweza kujihuzunisha sana wenyewe! Jambo hilo linaweza kutukia kwa ghafula, kwa sababu tu ya maneno yaliyosemwa au mambo yaliyotendwa na mtu fulani au kwa sababu ya kupatwa na jambo la kuchukiza. Nyakati kama hizo hatufikirii jambo lo lote jingine ila kujisikitikia. Na inakuwa kwamba, tusipoona njia ya kuondoka katika ugumu wetu, uhusiano wetu na Mungu unaweza kuharibika. Huenda tukafikiria kujiacha tushindwe katika lile pigano la imani. (Yuda 3) Furaha yetu inafifia kisha tunaingia sana katika roho ya kukata tamaa. (Mithali 18:14) Sisi tunataka kwa moyo mweupe tubaki katika “njia ya uzima,” lakini inaonekana kama mwendo unatuwia mgumu mno.​—Zaburi 16:11.

Ni jambo gani linaloweza kufanywa wakati hali zetu zinapokuwa zenye taabu kali? Je! ni lazima tuendelee kujikokota tu tukiwa na huzuni-huzuni? Au kuna njia fulani ya kuondoa ukosefu wa furaha?

Kujitazama Wenyewe

Watu wanatofautiana sana katika hali yao ya kutenda wakati wanapopatwa na matatizo. Kwa hiyo wakati tunapoelekeana na magumu, ni vizuri kujitazama wenyewe kwa unyofu. Huenda kukawa na jambo fulani ndani yetu linalotaka kurekebishwa.​—Zaburi 139:23, 24.

Watu fulani wanaweza kutaabika sana wakiwa wamenyamaza, na wengine wanaelekea kushinda magumu yao upesi kuliko wengine. Sababu inaweza kuwa ni malezi yao, utu wao au hali ya afya. Kwa mfano, ikiwa mtu hakuonyeshwa upendo wala hakupewa malezi mazuri katika ujana wake, huenda akatatizwa sana na mambo katika maisha ya baadaye.

Wale walionyimwa upendo wakiwa katika umri mdogo maishani wanakuwa na kawaida ya kufanya haraka mno kufikiri kwamba watu hawawapendi na kwa sababu hiyo wametendea watu mambo yasiyofaa. Kwa upande mwingine, wale walioharibiwa kwa kuhurumiwa mno wanakuwa na kawaida ya kutazamia kila jambo la maisha liwahusu wao, na kwa sababu hiyo huenda urafiki wanaofanya na watu usiendelee kwa muda mrefu, Kwa wale wenye matatizo ya afya, kutendwa udhalimu na kuaibishwa kunaweza kuwatia katika jaribu kali. Mara nyingi wao wanakuwa na maoni ya kwamba hawawezi kuvumilia kupatwa na ubaya unaozidi hapo. Kwa hiyo ikiwa sisi tuna maelekeo ya kukasirika upesi, ni vizuri kufikiria mambo hayo, hasa wakati tunapojisikia kuwa tumeangukia mfululizo wa magumu yasiyoshindika.

Wakati tunapohangaika kwa sababu ya jambo fulani, je! tunaelekea kujitenga pia na watu wale wengine? Hilo ni tendo linalojitokeza lenyewe katika hali hiyo, lakini halipasi kuachwa liendelee kuwapo kwa muda mrefu sana. Ama sivyo, kuna hatari ya kwamba, tukifikiria sana matatizo yetu tutaanza kumhesabu kila mtu aliye karibu nasi kuwa anatufanyia matata. Huenda tukajitenga wenyewe kwa njia isiyo ya hekima. Kisha, kwa usemi wa mfano, huenda ikawa ni kama tumejiwekea ndani ya nyumba vioo vingi vya kujitazama-tazama ili tujikumbushe nyakati zote kwamba tuna taabu kubwa.​—Mithali 18:1.

Kadiri ambavyo uchangamfu wetu unavyozidi kupungua ndivyo tunavyozidi kuelekea kuwalaumu wale walio karibu nasi kwa sababu ya huzuni yetu. Tukifanya pia lile kosa la kuwahesabia watu makusudi mabaya wanapofanya mambo, jambo hilo linaweza kuleta mkazo mwingi. Ni afadhali zaidi kutokuwashuku watu isivyofaa!—Linganisha 1 Timotheo 6:4.

Je! inaweza kuwa tunaudhika-udhika upesi mno juu ya vikosa vya wale tunaoshirikiana nao? Maisha yangekuwa ya kupendezea zaidi tukionyesha subira na ufahamu. Kumbuka kwamba Yesu Kristo alisema hivi: “Mkiwasamehe watu makosa yao, na Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi.” Badala ya kujishika shavu kwa huzuni tukifikiria-fikiria sana vile watu wametutendea, inatupasa tupelekee Yehova sala, kumwomba asaidie wale ambao wametutendea kwa njia isiyo ya fadhili. Ingawaje, si wao ndio wanaojiumiza wenyewe kuliko sisi? Ndiyo, “kwa kuwa cho chote apandacho mtu, ndicho atakachovuna.”​—Mathayo 6:14; Wagalatia 6:7.

Tunapokazwa sana, labda tunampelekea Yehova sala kwa njia ya kiutoto hivi, kumwomba atufanye turudiwe na furaha. Bila shaka, tunaweza kufanya hivyo tukitaka. Lakini je! tunaweza kutazamia kwamba yeye ataondoa hapo kwa hapo kila wazo na kumbukumbu lenye kututaabisha akilini? Mambo fulani yametukia, lakini ni wapi hasa penye kisababishi kikubwa zaidi cha ukosefu wa furaha? Je! kisababishi chenyewe ni jambo ambalo limetukia au ni njia mbaya tunayotumia kulichukua jambo lenyewe? Je! kisababishi chenyewe si kuudhika kwetu, hasira yetu na kujisikitikia kwetu? Mambo hayo ndiyo sana-sana yanayotuondolea furaha na usawaziko wa kiroho?

Basi, tungekuwa wenye hekima tukigandamiza maoni hayo yenye kusumbua moyo mara tu yanapoanza kujitokeza. Ama sivyo, huenda tukachochea maoni yetu ya moyoni kwa kiasi cha kwamba tutaingia katika hali itakayoelekea kutokuwa na tumaini lo lote. Hapo tukimwomba Yehova atusaidie, yeye atatupa msaada. Lakini haitupasi kutazamia miujiza, kwa maana huenda tukalazimika kurudisha fikira nyuma tukaone ni wapi hasa tulipoanza kuingia katika kipito kisichofaa. Kwa hiyo sawazisha mambo bila kukawia, ikiwa lazima. Kutembea-tembea mtu akiwa na dhamiri mbaya na roho ya kukosa furaha kunamletea taabu kali, na hali kukubali makosa yake kusingemletea taabu kubwa. Acheni “tuchunguze njia zetu” kisha tuazimie kwa nishati zilizofanywa upya kwamba tutajitahidi kwa nguvu za Mungu tufanye maendeleo.​—Maombolezo 3:40-42.

Kuongoza Mawazo Yetu

Kwa kweli, jambo la kama sisi tuna furaha kikweli au hatuna linatutegemea sana sisi. Hiyo ndiyo sababu tunahitaji kuongoza mawazo yetu yasiruke mpaka. Ama sivyo, kumbukumbu za mambo ya kuchukiza, viwazo vya kishenzi au hata misukumo ya kutaka kufanya maovu itatushinda nguvu. Tukijikuta katika hali ya kukosa furaha, ingefaa tujiulize hivi: Mimi nilikuwa nikifikiria nini muda mfupi tu kabla sijashuka sana moyo kwa ghafula? Ni wazi kwamba tunaweza kufunga televisheni tusitazame kipindi kibaya, lakini mawazo mabaya yanapotokea, si jambo jepesi kuyaondoa. Lakini, ni baraka kama nini kwamba tunaweza kusali Mungu atupe msaada! Kupitia roho takatifu yake, au kani (nguvu) ya utendaji, Yehova atafurahi kutusaidia tuongoze mawazo yetu yasiruke mpaka. Wakati mmoja mtunga zaburi Daudi alisema hivi: “Wakati mawazo yangu yenye kuvuruga utulivu yalipokuwa mengi ndani yangu, faraja zako mwenyewe [Yehova] zilianza kuipiga pambaja nafsi yangu.”​—Zaburi 94:19, NW.

Tukimsihi sana Yehova atusaidie, kwa sababu yo yote, ni lazima tumsikilize yeye wakati anaposema nasi. Hekima na upendo wake usio na mipaka vinaonyeshwa katika Maandiko, na mashauri juu ya kila hali ambayo inaelekea kuwa itatupata yameonyeshwa wazi katika Biblia. Kwa hiyo, furaha yetu inaweza kurudishwa au kuhakikishwa tukitumia mashauri ya Yehova maishani. Yesu alisema: “Heri walisikiao neno la Mungu na kulishika.”​—Luka 11:28.

Tunaweza kutolea mawazo yetu mwelekezo wenye mafaa kwa kuweka andiko fulani la Biblia akilini kwa saa kadha au hata kwa siku nzima. Wakati wo wote tunapokuta maneno ya kufariji sana au ya kututia nguvu tunapojifunza Biblia, tunaweza kuyakaza akilini. Halafu mara kwa mara, tunapoona uhitaji, tunaweza kuvirudia visehemu hivyo vya Neno la Yehova. Kwa njia hiyo “Mungu wa faraja yote” atatusaidia, na “amani ya Mungu” ‘itahifadhi mioyo yetu na nia zetu.’ Halafu tutaweza kuvumilia katika utumishi wake tukiwa na furaha tujapokuwa na matatizo. Ndiyo, zaidi ya kupaswa kujua maoni ya Mungu juu ya mambo inatupasa pia tufanye yale anayotuambia,—2 Wakorintho 1:3, 4; Wafilipi 4:6, 7.

Kufurahia Kile Ambacho Mungu Anatupa Sisi

Hakika inatupasa tusikilize Mungu, kwa maana anatuonyesha upendo na kutupa “kila zawadi njema.” (Yakobo 1:17, NW) Nyakati za kupatwa na mkazo mkali na kuvunjika moyo, huenda tukasahau kwamba kungali kuna mambo mengi ya kufurahika. Tena, Baba yetu wa kimbingu anataka tujipatie kwa wingi vitu vyote vizuri anavyotutolea. Naye anatutaka tuwe wenye furaha, sawasawa na vile mkusanyaji alivyoonyesha aliposema hivi: “Mimi niliyoyaona kuwa ndiyo mema na ya kufaa, ni mtu kula na kunywa, na kujiburudisha kwa mema katika kazi yake yote . . . Kwa kuwa mtu hatazikumbuka mno siku za maisha yake; kwa sababu Mungu humtakabali katika furaha ya moyo wake.” (Mhubiri 5:18-20; 9:7-10) Sisi sote tunapatwa na mambo fulani ya kutuhuzunisha, lakini tukifungua macho yetu, bado tutaona kwamba kuna mengine ya kupendeza, hata yanapokuwa yamezungukwa na yale ya kusikitisha.

Kati ya vipawa vizuri zaidi tulivyopewa na Mungu wako rafiki zetu wa Kikristo. Tunatamani sana waje kutusaidia tunapokuwa na magumu. Wakati huo ndipo tunapohitaji mtu aliye na nia ya kutusikiliza kwa ufahamu. Mara nyingi sisi tunajua tunalopaswa kufanya, lakini tunashindwa kulifanya kwa sababu ya mioyo yetu kuwa imeumia. Haifai tuone aibu kumwomba mshiriki fulani tunayemthamini sana katika kundi la Kikristo atusaidie kwa upendo. Wazee wenye ujuzi katika makundi ya Mashahidi wa Yehova watafurahi kutusaidia kwa njia zenye mafaa na hasa kwa kututolea msaada unaolitegemea Neno la Mungu.​—Yakobo 5:13-16.

Hata tuwe tunaishi wapi katika dunia hii, sisi tuna ‘rafiki wadogo-wadogo’ kila mahali. Ili rafiki hao watuonyeshe sisi urafiki, tunalohitajiwa kufanya ni kuwafanya watuamini sisi. Rafiki hao ni wanyama na ndege ambao pasipo shaka watatujia tukiwapa chakula kidogo. Linakuwa jambo la kufurahika kama nini wanapoacha kutuogopa kisha wanaanza kula chakula tulichoweka mkononi mwetu!

Namna gani watoto katika ujirani? Wao watafurahi kututembelea tukiwa wafadhili au wakarimu au tukiwaacha watusaidie kikazi fulani. Sisi hatutakuwa wapweke wala hatutakosa furaha tukifikiria baraka zetu na kufurahia kila kitu ambacho Yehova anatupa.

Tunastareheka na kusaidika tuingize ndani ya akili zetu mawazo yenye kujenga tukienda kupunga hewa. Watu ambao ubongo wao haupati oksijeni ya kutosha hawatakuwa na roho ya kuchangamka. Watu wengi wamerudiwa na usawaziko wao wa kiroho baada ya kutembea mwendo mrefu. Na wakati tunapotembea na kupita bustani mbalimbali au tunapotembea katika mwitu wenye miti mingi, inatupasa tujaribu kufikiria na kufahamu vitu tunavyoona. Mara nyingi sana tunatembea au kuketi katika mahali peupe na kuangalia-angalia hivi hivi tu kisha tunaingiliwa na namna zote za mawazo ya kuhuzunisha. Lakini kila mti, kila mmea, kila mnyama na hata anga lenyewe linaweza kutueleza jambo fulani juu ya Muumba ikiwa tu tutaruhusu uzuri wa maumbo hayo, fahari ya rangi za vitu hivyo na kila jambo tunalogundua liwe na matokeo fulani juu yetu. Tunapozitazama mbingu zenye nyota nyakati za jioni zisizo na mawingu, maneno kama haya ya mtunga zaburi yanaweza kutuchangamsha: “Mbingu zauhubiri utukufu wa Mungu, na anga laitangaza kazi ya mikono yake.” (Zaburi 19:1) Nyakati kama hizo mahangaiko yote ya kibinadamu yanafifia, nasi tunahisi tukiwa na maoni ya kiasi fulani cha fahari ya Mungu. Hapo hatutakuwa na ugumu wa kusukuma nyuma mambo yanayotuhangaisha na kumpelekea Muumba Mkuu wetu maneno ya shukrani na sifa.

Usingizi wetu ni kingine cha vipawa tulivyopewa na Mungu. Mwishoni mwa siku yenye shughuli nyingi tunaweza kupumzika, tukiutumaini kabisa ulinzi wa Mungu. Jambo hilo linatusaidia tuianze siku inayofuata tukiwa na nishati zilizofanywa upya. Lakini tukilala vibaya, tunaweza kufanya nini? Tunaweza kumpelekea sala Baba yetu wa kimbingu, vilevile tuwakumbuke waamini wenzetu katika maombi hayo. Tunaweza kufikiria Neno lake na ahadi zake za ajabu. (Zaburi 77:6; Waefeso 6:17-20) Ni vizuri zaidi kufanya hivyo badala ya kufikiria matatizo yetu tu! Tunahitaji kujaza akili yetu mema mengi ya kiroho. Na hapo ndipo tutakapoweza kujiambia, ‘Lala salama.’

Sisi Hatuko Peke Yetu

Bila shaka, sisi sio watu wa pekee walio na matatizo. Kama tungewaomba wengine watueleze magumu yao, labda tungepatwa na fikira ya kusema: Ni afadhali sisi tukae kimya. Kwa kweli, huenda tukapendelea kuwa na matatizo tuliyo nayo badala ya kupatwa na yale yanayowapiga watu wengine wengi.

Sisi Wakristo tuliojiweka wakf hatuwezi kuwa huru tusipatwe na magumu ya namna zote wakati huu, kwa maana Yesu alisema wafuasi wake wangepatwa na mateso. (Yohana 15:20) Sisi hatuko peke yetu katika kupatwa na mambo tunayoweza kuletewa na adui yetu aliye mkubwa wa wote, Shetani Ibilisi, kwa maana “mambo ayo hayo kwa namna ya mateso yanatimizwa katika ushirika mzima wa ndugu [zetu] ulimwenguni.” Lakini jambo la maana zaidi ni kwamba sisi na Wakristo wenzetu wanaoteswa tuna msaada wa kimungu. Kwa hiyo acheni tumtumaini “Mungu wa fadhili zote zisizostahilika,” ambaye yupo pamoja nasi. Halafu na tuitazamie kwa uhakika siku ile inayokaribia sana ambapo dhiki zetu hazitakuwapo tena.​—1 Petro 5:6-11, NW; 2 Wathesalonike 1:6-10.

Wakati wenye magumu unaowapata sasa Wakristo wote waaminifu uko karibu kwisha, kwa maana tunakaribia mbiombio kipindi kipya chenye kuleta furaha. Sisi tupo ukingoni pa “mbingu mpya na nchi mpya.” (Ufunuo 21:1-4) Hakika hiyo ni sababu kubwa ya kuwa na furaha!

Yesu Kristo alifundisha wafuasi wake kumwomba Mungu hivi kwa sala: “Ufalme wako uje.” (Mathayo 6:9) Kwa hiyo acheni tutumainie kweli kweli Ufalme huo na kuutazamia wakati ujao tukiwa na furaha. Yesu aliweza kuvumilia aibu kubwa na maumivu makali sana ya mti wa mateso kwa sababu, katika mateso yake yote, yeye aliikumbuka “furaha iliyowekwa mbele yake.” (Waebrania 12:1-3) Baada ya muda mfupi angemwona tena Baba yake wa kimbingu uso kwa uso na kuzungukwa na washirika wenzake wote wa kimbingu wenye furaha.

Katika muda wa karne nyingi, wafuasi wa Kristo wamevumilia majaribu mengi, hata wakaelekeana na wanyama-mwitu katika uwanja wa maonyesho ya Kiroma na matendo ya unyama mkubwa katika kambi za mateso. Wameweza kuyavumilia yote hayo kwa sababu wamejaribu kupendeza Yehova na wakakaza macho yao juu ya ile zawadi ya uzima wa milele. Yehova Mungu hatawasahau wao. Wala hatatusahau sisi tukiwa waabudu wake waaminifu na kubaki katika ile “njia ya uzima.” Kwa hiyo, kwa kuwa tuna tumaini zuri ajabu mbele yetu, tunaweza kutokeza mlio wa furaha nyingi na kusema: “[Wewe Mungu wetu, Yehova] waufumbua mkono wako, wakishibisha kila kilicho hai matakwa yake.”​—Zaburi 145:16.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki