Maoni Yetu Ni Nini Kuelekea Wanaoipinga Kweli?
‘‘Katika ninyi wenyewe watainuka watu, wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao.”—Matendo 20:30.
1, 2. (a) Matukio ya zamani katika historia ya Biblia yana faida gani leo? (b) Ni matukio gani hasa katika historia ya Israeli na kundi la kwanza la Kikristo yanayotuhusu sisi sasa, na kwa sababu gani?
WAKATI mtume Paulo alipokuwa akiandikia kundi katika Korintho aliwaambia waamini wenzake kwamba mambo yaliyoandikwa zamani zilizopita yalipasa kuwa mfano wa kuwaonya. Kanuni hiyo ina matokeo yenye kufika mbali, mpaka leo hii. Matukio mengi ya kale katika historia ya Biblia yanaweza kuwa na vifanani vya kisasa, na yanavyo hata sasa. Vifanani hivyo vinatusaidia na kutupa mwelekezo unaofaa katika maisha zetu.—1 Wakorintho 10:11; Warumi 15:4.
2 Basi, litakuwa jambo la faida tufikirie baadhi ya hayo matukio ya zamani katika historia ya Israeli na pia ya kundi la Kikristo la kwanza. Sana-sana tunapendezwa na matukio yanayohusiana na wale watu waliopinga kazi ya Mungu na namna matendo hayo yalivyowahusu watumishi waaminifu wa Yehova huko nyuma. Matukio hayo yanasaidia kutuamsha sisi watu wa Yehova, tuyalinganishe na matukio ya kisasa na kutuonyesha madaraka tuliyo nayo upande huo.—2 Timotheo 3:16, 17.
3. Yeremia alionywaje na alifarijiwaje pia?
3 Yapata miaka 40 kabla ya anguko la Yerusalemu mwaka wa 607 K.W.K., Yehova aliagiza Yeremia mtumishi wake mwaminifu atangazie watu wote dhuluma zilizokuwa zikitendwa katika Yuda. Hatimaye dhuluma hizo zingefanya watu wa huko wapoteze upendeleo wa Mungu na kupelekwa mateka katika Babeli. Yehova akamwonya Yeremia kwamba wengine wangempinga. Alisema: “Nao [wapinzani] watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, asema [Yehova], ili nikuokoe.” (Yeremia 1:19) Hiyo ilikuwa faraja kubwa sana kwa Yeremia, ikamtia nguvu atimize mapenzi kamili ambayo Mungu alitaka ayatimize!
4. (a) Ni nini mmoja wa upinzani ambao Yeremia alilazimika kuvumilia? (b) Maandishi kwenye Waebrania 11:32-38 yanatuambia nini juu ya wapinzani wa watumishi wa Mungu?
4 Mmoja wa wapinzani wa Yeremia alikuwa mwanamume mwenye kuitwa Pashuri. Alikuwa mwana wa kuhani mmoja katika Yuda, na pia alikuwa kamishna mkubwa katika nyumba ya Yehova. Masimulizi yanaonyesha vile Pashuri alivyomchapa Yeremia na kuamuru atiwe katika mikatale. Yehova alimkomboa Yeremia katika vizuizi hivyo, lakini upinzani ukaendelea. Hanania, nabii mmoja wa kutoka Gibeoni, alitamka waziwazi maneno ya kumpinga Yeremia, akamlaumu kuwa nabii wa maangamizi. Kwa kweli, Hanania alisema nira ya Babeli ingevunjwa, kisha Yuda irudie hali yake. (Yeremia, sura ya 28) Hata mmoja wa wafalme wa Yuda, jina lake Yehoyakimu, aliyapinga Sana maneno ya Yeremia hata akafikia kuvitupa motoni vitabu vya kukunjwa vyenye unabii wa Yeremia! (Yeremia, sura ya 36) Wengine walitia fitina Yeremia auawe, wakafanya atupwe ndani ya kisima chenye matope ili afe. (Yeremia, sura ya 38) Haya ni masimulizi ya mmoja tu wa manabii waaminifu Waebrania walionena kwa jina la Yehova, wakasingiziwa vibaya na kushambuliwa na wapinzani wa ujumbe wa hukumu uliotoka kwa Mungu.—Angalia Waebrania 11:32-38.
“Waacheni”
5. (a) Ni kwa kadiri gani Yesu alipatwa na upinzani? (b) Ni nini vingine vya vijambo vidogo tu vilivyotokezwa na wapinzani wa Yesu?
5 Upinzani kwa ile kweli ulikuwa mwingi sana katika karne ya kwanza pia ya Wakati wa Kawaida wetu, Bwana wetu Yesu Kristo alipokuwa duniani. Wapinzani waliokuwa kati watu wake mwenyewe walijaribu kuyazuia mema yaliyofanywa na Yesu. Lakini kama vile Yehova alivyokuwa amekuwa na Yeremia ndivyo alivyokuwa na Yesu, akamkomboa kwa maadui wake. (Luka 4:14-30; 11:53, 54; Yohana 7:1) Mara nyingi wenye kudhihaki Yesu walifanya vijambo vidogo vionekane kuwa matatizo makubwa. Walimshtaki Yesu juu ya kuwa mlafi, mnywaji wa kupindukia na mtu wa kushirikiana na watoza kodi na watenda dhambi. (Mathayo 11:16-19) Waliita wanafunzi wake wavunjaji wa Sabato kwa sababu ya kuchuma masuke ya nafaka ili wayale siku ya Sabato. (Marko 2:23-28) Walifanya mzaha juu ya wanafunzi wa Yesu kwa sababu ‘hawakunawa mikono walipokula chakula.’—Mathayo 15:1, 2.
6. Upinzani kwa Yesu ukawa na uzito kadiri gani?
6 Lakini wapinzani hao walikosea vijambo vidogo mpaka wakaja kukana kwamba si uwezo wa roho takatifu ya Mungu uliohusika katika miujiza ya Yesu. Yesu alipoponya mtu mwenye mashetani, aliye kuwa kipofu na bubu, wapinzani wake walisema: “Huyu hatoi pepo, ila kwa Beelzebuli mkuu wa pepo.” (Mathayo 12:22-28) Hata walimshtaki Yesu juu ya kutaka kumpindua Kaisari. (Luka 23:1, 2) Mwishowe wakadai auawe.—Luka 23:13-25.
7. Yesu alitendaje kuelekea wapinzani wa ile kweli?
7 Naye Yesu alitendaje kwa sababu ya wale waliompinga?Akiwaambia mitume wake, alisema: “Waacheni; hao ni viongozi vipofu wa vipofu. Na kipofu akimwongoza kipofu mwenzake, watatumbukia shimoni wote wawili,” (Mathayo 15:14) Shauri la hekima alilotoa Yesu ni kwamba, “Waacheni.” Baada ya muda fulani ingeonekana wazi namna walivyokuwa.
Upinzani Tokea Ndani
8, 9. (a) Ni kiolezo gani cha upinzani unaofanana na ule uliowapata Yeremia na Yesu kilichotabiriwa kulipata kundi la Kikristo? (b) Eleza namna jambo hilo lilivyotukia kuhusu lile shauri la tohara.
8 Baada ya Yesu kufa, wafuasi wake waaminifu walipatwa pia na upinzani mwingi. Lakini tafadhali angalia ya kwamba: Sawa na vile wapinzani wa Yeremia na Yesu walivyotokea ndani ya taifa la Kiyahudi, ndivyo ingekuwa kwamba kundi la Kikristo likiisha kuanzishwa upinzani ungekuja tokea ndani ya kundi hilo. (Matendo 20:29, 30) Na ingawa upinzani huo ulikuwa umetabiriwa, bado ungekuwa jaribu kubwa kwa wenye kutembea katika uaminifu. Hata hivyo, Yehova angekuwa pamoja na watu wake awakomboe, sawa na alivyokomboa Yeremia na Yesu.—Angalia 1 Petro 5:8-11.
9 Upinzani huo wa kindani uliotokea karne ya kwanza ulikuwa na mianzo yake midogo. Labda wapinzani fulani walijisikia wakiwa na kusudi zuri la kupinga, lakini tamaa yao ya kujipatia cheo cha kwanza, kufanya maoni yao yawe ndiyo ya kufuatwa, iliwaingiza katika hali ya kuwa wapiganaji dhidi ya ile kweli na juu ya wale wanaoshirikiana na kweli hiyo, wakati maoni yao yalipokataliwa kuwa si sahihi. (1 Timotheo 1:19, 20) Jambo la kustahili kuangaliwa ni kwamba, wakati shauri la tohara lilipokuwa fundisho lenye kushindaniwa sana kisha baraza la pekee likakutana Yerusalemu kulizungumza, moja la mambo yaliyotajwa katika ujumbe uliopelekewa kundi ni hili: “Tumesikia ya kwamba watu waliotoka kwetu wamewasumbua kwa maneno yao, wakipotosha roho zenu, ambao sisi hatukuwaagiza.” (Matendo 15:24) Watu hao waliokuwa ndani ya kundi la Kikristo walifanya matata yatokee, wakayapinga mafundisho ya baraza la wazee waliopewa kabidhi ya kuwa na madaraka mazito ya kuieneza ng’ambo nuru ya kweli.
10. (a) Ni nini mengine ya mafundisho ya kulegeza imani yaliyofunzwa katika karne ya kwanza na wapinzani wa ile kweli? (b) Paulo alimpa Timotheo onyo gani kuhusu wapinzani wa kweli?
10 Kwa mfano, wengine kundini walikuwa wakisema siku ya Yehova ilikuwa imekwisha kuanza. (2 Wathesalonike 2:1, 2) Wengine wakashindania kauli yao ya kwamba hakuna ufufuo. (1 Wakorintho 15:12-14) Na bado wengine wakasema ufufuo ulikuwa tayari umetokea. (2 Timotheo 2:16-18) Mtume Paulo alimwonya Timotheo juu ya uhitaji wa kuwa macho ajihadhari na wale waliotaka kuleta mgawanyiko na kupotosha watu waache ujumla wa kweli ya Kikristo iliyopatikana kwenye makundi. Sikia maneno ya mtume: “Uwakataze wengine wasifundishe elimu nyingine; wala wasiangalie hadithi na nasaba zisizo na ukomo, ziletazo maswali wala si madaraka ya Mungu yaliyo katika imani; basi ufanye hivyo. Walakini mwisho wa agizo hilo ni upendo utokao katika moyo safi na dhamiri njema, na imani isiyo na unafiki. Wengine wakiyakosa hayo wamegeukia maneno ya ubatili; wapenda kuwa waalimu wa sheria, ingawa hawayafahamu wasemayo wala mambo yale wayanenayo kwa uthabiti.”—1 Timotheo 1:3-7.
11. Je! tunaweza kujifunza lo lote kutokana na mawazo yenye kuleta mgawanyiko yaliyokuwa sana katika kundi la karne ya kwanza, na kwa sababu gani kuna uhitaji wa haraka kufanya hivyo leo?
11 Hapo tunaambiwa nini? Kwamba: kulikuwako matatizo ya njia ya kuwaza yenye kuleta mgawanyiko katika kundi la Kikristo la karne ya kwanza. Kulikuwa na upinzani tokea ndani, uliotokana na watu waliodai kuwa sehemu ya kundi la Mungu. Sababu ya upinzani huo ilikuwa nini? Paulo alisema hivi kwenye Wafilipi 1:15: “Wengine wanahubiri habari za Kristo kwa sababu ya husuda na fitina; na wengine kwa nia njema.” Tafsiri Today’s English Version ya Biblia inataja kwamba watu hao walikuwa na kusudi lisilofaa, wakiwa “wenye wivu na wenye kutafuta-tafuta ugomvi.” Ndiyo, mambo yaliyoandikwa zamani ni mfano wa kutuonya sisi, na hasa sasa maana tunaishi katika umalizio wa mfumo mbovu wa mambo unaoelekezwa na Ibilisi.—2 Timotheo 3:1-7.
Kusudi la Wapinzani
12, 13. (a) Je! leo sisi tunaona ulinganifu wo wote na upinzani wa karne ya kwanza kuielekea kweli? (b) Kusudi lenye kuwachochea wapinzani wa kisasa ni nini?
12 Tukigeuza fikira kwenye nyakati za kisasa, je! tunaona ulinganifu wa matukio ambayo tumezungumza kufikia hapo? Ndiyo, kumekuwako wengine kati yetu waliojaribu kuibomoa kazi nzuri inayofanywa na watu wa Yehova ulimwenguni pote. Wengine wamekuwa wenye wivu, watu wa matata-matata, wenye kujitakia sana makuu, mara nyingi wakitaka kujifanyia jina. Huenda wakawa ‘wanung’unikaji, walalamikaji juu ya fungu lao katika maisha, wakisonga mbele kulingana na tamaa zao wenyewe, wakivutiwa na nyutu za watu kwa ajili ya kutaka faida wenyewe.’ (Yuda 16, NW) Yote hayo yanaweza kutokeza mashaka, ugomvi migawanyiko kati ya watu wa Mungu. Katika kutafuta-tafuta makosa, watu wa namna hiyo wanaacha kuiona kazi ambayo Wakristo wamepewa na Mungu, ambayo ndiyo kazi ya maana kupita zote, yaani zaidi ya kuwa ‘wasikiaji tu’ wawe ‘watendaji wa lile neno’ pia, wakitimiza yale ambayo Yehova amewaamuru wafuasi waaminifu wa Mwanaye, Kristo Yesu.—Yakobo 1:22-25; Mathayo 28:18-20.
13 Katika kulishambulia kundi la Kikristo, kusudi la wapinzani hao ni kubomoa imani ya watu wa Yehova, kuvuta wengine waambatane nao wakiwa wanafunzi wao. Paulo alionya wanaume wazee wa Efeso juu ya jaribio bovu hilo wakati aliposema: “Tena katika ninyi wenyewe watainuka watu, wakisema mapotovu, wawavute hao wanafunzi wawaandamie wao.” (Matendo 20:30) Yuda alitoa onyo la namna hiyo, akasema: “Kwa maana kuna watu waliojiingiza kwa siri, watu [waliowekwa na Maandiko zamani za kale kwenye] hukumu hii, makafiri, wabadilio neema ya Mungu wetu kuwa ufisadi, nao humkana yeye aliye peke yake Mola, na Bwana wetu Yesu Kristo.” (Yuda 4) Hali za namna hiyo zimetokea katika hii karne ya 20 ndani ya kundi la watu wa Yehova!
14, 15. (a) Ni njia gani yenye hila (ujanja) inayotumiwa na wapinzani fulani leo? (b) Wapinzani hao? wanakosa kukumbuka nini?
14 Wapinzani hao hawafurahii kuishiriki kazi ile kuu ya kufanya watu wanafunzi. Bali, wanatumia ujanja kuendea wengine wa wale ambao tayari ni Mashahidi, kisha wanasema mambo ya kulegeza azimio la waaminifu hao la kutimiza kabisa wakf wao kwa Yehova. Wanawapa wazo la kwamba kwa kuwa Yehova ni Mungu mwenye upendo sana, hakika yeye hangetaka wale wanaotaka kumpendeza wafanye kazi ngumu sana kama ile ya kuhubiri nyumba kwa nyumba, na kulazimika kuvumilia mateso yanayotokana na wapinzani wa ile kweli. Huenda wakatoa hoja ya kusema Mungu anatutaka tuwe watu wema, tu, tuwatunze wengine kimwili, tupende jirani zetu, na basi.
15 Njia hiyo ya kufikia watu kwa ujanja inaweza kutatiza wengine. Ni kweli kwamba Yehova ni mwenye upendo na anataka tuwe watu wema. Kwa uhakika anataka Wakristo waonyeshe jirani zao upendo kwa kuwafadhili na kuwapa mahitaji ya kimwili inapokuwa lazima. (Luka 6:35, 36) Lakini hiyo haitoshi! Wale wanaopinga wanasahau mara nyingi kwamba Baba yetu Yehova amesema pia—sana-sana kupitia Mwanaye, Yesu Kristo—kwamba inatupasa tuwe wafanya-wanafunzi, tufundishe watu, tuzihubiri “habari njema za ufalme” katika ulimwengu wote kwa ushuhuda.—Mathayo 24:14, NW; Yohana 15:17-27.
16. Ni kwa kutumia “mapotovu” gani mengine wapinzani wanajaribu kupoteza watu wa Yehova leo?
16 Angalia mengine ya “mapotovu” yanayotumiwa kudanganya watu wa Mungu leo. Nyakati nyingine wapinzani wanatokeza mashaka juu ya mafundisho mbali-mbali yanayofuatwa kwa ujumla na watu wa Yehova. Mara nyingi unakuwa ni ubishi unaohusu maneno, kama katika karne ya kwanza. (1 Timotheo 6:3, 4) Huenda pia wakafanya ubishi wakisema hakuna uhitaji wa tengenezo la kuelekeza watu wa Mungu. Maoni yao ni kwamba, roho ya Mungu inaweza kuelekeza watu mmoja mmoja bila ya kuwa na baraza fulani kuu lililopangwa kitengenezo, la wanaume wenye kutoa mwelekezo. Wanatangaza kwamba jambo moja tu ambalo linahitajiwa kwa mtu ni kwamba asome Biblia, na basi. Lakini Jumuiya ya Wakristo imekuwa ikisoma Biblia muda wa karne nyingi. Na ebu ona vile tarumbeta ya Jumuiya ya Wakristo leo imekuwa ikitokeza mlio usiosikika vizuri! Tena ona mvurugo na hali iliyopo ya kutokuelewa vizuri ujumbe ulio wa kweli katika Neno la Mungu! Hakika hiyo inatofautiana sana na amani na umoja ulio kati ya Wakristo wa kweli ambao zaidi ya kuisoma Biblia wanaichunguza kabisa na kuyafuata kwa juhudi mafundisho yayo!—Waefeso 4:3-6.
Wapinzani Hawawezi Kuwa na Matokeo Mazuri
17. Basi, ni nini maoni yetu kuelekea wanaoipinga kweli?
17 Basi, je! maoni yetu ni nini kuelekea wale wanaoipinga na kujaribu kuibomoa imani ambayo tumeipokea kupitia Mashahidi wa Yehova na tengenezo la Kikristo analolitumia Yehova? Shauri la Yesu juu ya wapinzani ni hili: “Waacheni wawe hivyo. Hao ni viongozi vipofu.” (Mathayo 15:14, NW) Kufanya ugomvi na watu wa namna hiyo, kujadiliana na kubishana-bishana, ni kazi bure na hakika huo sio mwendo wa Kikristo. Hakuna mtu anayelazimishwa kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Hilo ni pendeleo na daraka ambalo sisi tumejichagulia kwa kupenda kwetu wenyewe. (Zaburi 110:3) Ikiwa watu fulani hawataki kuwa sehemu ya mpango unaokubaliwa na Yehova, mpango ambao yeye ameubariki, ni juu ya watu hao kujiamulia wenyewe.
18. Shauri la Paulo kwenye Warumi 16:17, 18 linatuhusuje leo?
18 Lengo letu linapasa kuwa kushughulika na wapinzani wa ile kweli kwa njia ya Kikristo. Walakini, kuna mambo fulani tunayopaswa kukumbuka. Paulo aliwaandikia wale wa kundi la Rumi akawashauri hivi: “Ndugu zangu, nawasihi, waangalieni wale wafanyao fitina na mambo ya kukwaza kinyume cha mafundisho mliyojifunza; mkajiepushe nao. Kwa sababu walio hivyo hawamtumikii Bwana wetu Kristo, bali matumbo yao wenyewe; na kwa maneno laini na ya kujipendekeza waidanganya mioyo ya watu wanyofu.” (Warumi 16:17, 18) Mtu akifanya ubishi na wale wenye kuleta migawanyiko wakiwa katika hadhara ya watu, angeonyesha hana uamuzi mzuri. Mwenendo wao hauwezi kuiharibu ile kweli, wala hauwezi kumkomesha Yehova asitimize yale ambayo Neno lake linasema atayafanya.
19. Kwenye Waebrania 6:4-8, Paulo anatoa maelezo gani juu ya wale wenye kuanguka na kuiacha kweli?
19 Basi, maneno ya nabii Isaya yanafariji sana: “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa, na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa.” (Isaya 54:17) Mtume Paulo alimweleza Timotheo habari za Yane na Yambre waliompinga sana Musa, akasema uwazimu wao ulionekana wazi na watu wote. (2 Timotheo 3:8, 9) Basi, wale wanaoleta mgawanyiko na kujaribu kufanyia watu wa Yehova msukosuko wana msimamo wenye hatari mbele za Yehova. Watu wo wote wa namna hiyo wasisahau kamwe maneno yenye onyo ya Paulo, yaliyo kwenye Waebrania 6:4-8 ambapo imeonyeshwa kwamba wanaoitenda dhambi roho takatifu ya Mungu kwa makusudi hawawezi ‘kufanywa upya watubu.’
20. (a) Kwa sababu gani hatuhitaji kamwe kushtuliwa na mambo ambayo huenda wapinzani wakajaribu kufanya? (b) Ni kwa kufanya nini tunaweza kuhakikishiwa ‘hatutatenganishwa kamwe na upendo wa Mungu’?
20 Basi, sisi tumeonyeshwa wazi, tena wazi sana, katika Neno la Mungu juu ya maoni tunayopaswa kuwa nayo kuelekea wapinzani. Sikuzote kumbuka kwamba sisi hatuko peke yetu; tuna utegemezo wa Yehova, Kristo Yesu na malaika watakatifu wote. (Mathayo 13:41, 42) Pia tuna uhakikisho wa Yesu mwenyewe unaosema angekuwa pamoja na wafuasi wake “siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” (Mathayo 28:20, NW) Kwa hiyo, hatupaswi kubabaika-babaika bure wakati wapinzani wanapojitokeza na kupigana na ile kweli. Hiyo ni sehemu moja ya jitihada ya Shetani ya kuukomesha mwenezo wa zile habari njema za Ufalme. Lakini kwa kubaki washikamanifu na kuweka mfano mwema wa utawa kwa mwenendo na maneno yetu, tutahakikishiwa ‘kushinda katika mambo yote kupitia yeye aliyetupenda.’ Basi na tuendelee kuwa wathibitifu (imara), “kujua hakika ya kwamba, wala mauti, wala uzima, wala malaika, wala wenye mamlaka, wala yaliyopo, wala yatakayokuwapo, wala wenye uwezo, wala yaliyo juu, wala yaliyo chini, wala kiumbe kinginecho chote hakitaweza kututenga na upendo wa Mungu ulio katika Kristo Yesu Bwana wetu.”—Warumi 8:37-39.—Kutoka The Watchtower, March 1,1983.
Maandiko yanayofuata yanatuambia nini juu ya wanaoipinga kweli?
◻ Mathayo 15:14; Warumi 16:17, 18
[Picha katika ukurasa wa 15]
“Waacheni; hao ni viongozi vipofu wa vipofu’’
[Picha katika ukurasa wa 17]
Usilegee kamwe katika azimio lako la kuitolea kweli ushuhuda