Je! Wewe Utaushikilia Sana Ukweli?
IKIWA wewe umeanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, ulizo kuu ambalo ni lazima ujibu kwa njia ya kuridhisha mwenyewe ni kwamba, je! huo ndio ukweli? Ikiwa wewe umepata kwamba huo ndio ukweli, je! utaushikilia sana? Maulizo kama hayo yalikabili watu katika siku za Yesu Kristo na mitume wake.
Wakati mitume walipohubiri juu ya Yesu, watu waliitikiaje? Basi, habari kuhusu Ufalme wa Kristo, miujiza yake, dhabihu ya ukombozi yake, ufufuo wake, na uzima wa milele zilisikika kuwa njema, na watu wengi walikubali waliyosikia kuwa ukweli. Lakini walio wengi hawakukubali. Kwa kweli, tengenezo la Kikristo la wakati huo ‘lilinenwa vibaya’ kila mahali. (Matendo 28:22) Kwa hiyo kuzikubali kweli ambazo wanafunzi wa Yesu walihubiri kulimaanisha kutenda kinyume cha maoni yaliyopendwa na wengi na kukamaanisha kukabiliana na upinzani. Watu wenye kupendezwa walilazimika kujithibitishia kwa njia yenye kujiridhisha kwamba mafundisho ya Kikristo yalikuwa ndiyo ukweli. Ni hapo tu wangeweza kuchukua msimamo imara.
Wakati Paulo na Barnaba walipotembelea Antiokia katika Esia Ndogo, watu wengi walisikiliza ujumbe wao kwa kupendezwa sana. Maandishi ya Biblia yanasema: “Na walipokuwa wakitoka, wakawasihi waambiwe maneno haya sababo ya pili. Hata sababo ya pili, watu wengi, karibu mji wote, wakakusanyika walisikie neno la [Yehova].” (Matendo 13:42, 44) Lakini kupendezwa huko kwa kwanza kulififia katika hesabu kubwa ya watu wakati waliposikia wapinzani wenye kutoa-toa maoni makali wakinena dhidi ya mitume.
Mstari 45 wa Matendo sura 13 unasema: “Bali Wayahudi, walipowaona makutano, wakajaa wivu, wakayakanusha maneno yaliyonenwa na Paulo, wakibisha na kutukana.” Ndipo mstari 50 unaendelea kusema: “Lakini Wayahudi wakawafitinisha wanawake watauwa wenye cheo na wakuu wa mji, wakawataharakisha watu wawaudhi Paulo na Barnaba; wakawatoa katika mipaka yao.” Watu wenye kupendezwa walilazimika kuamua kama wangeendelea kusikiliza wafuasi wa Yesu ujapokuwako upinzani. Ilikuwa lazima ama wakubali waliyosikia kuwa ukweli ama wafunge masikio yao yasiyasikie.
Upinzani Leo
Hata kama vile Wakristo walivyopingwa katika karne ya kwanza W.K., ndivyo pia walivyo wapinzani wa kisasa wanaojaribu kufunga masikio ya watu wenye kupendezwa wasisikie kweli za Kimaandiko ambazo Mashahidi wa Yehova wanafundisha. Marafiki, watu wa ukoo, na viongozi wa kidini wanajaribu mara nyingi kwa njia zote wawavunje moyo watu wenye kupendezwa wasijifunze Biblia pamoja na Mashahidi. Bila kutumia uthibitisho wa Kimaandiko, wapinzani wanapinganisha mambo yanayofundishwa na kutoa mashtaka ya uwongo.
Inawapasa watu wanaopendezwa wafanye nini? Je! waruhusu maneno ya wapinzani yafunge akili na masikio yao kama wengine walivyofanya katika Antiokia? Au inawapasa wajithibitishie wenyewe kutokana na Biblia kama mambo wanayojifunza ndiyo ukweli au siyo?
Watu wenye kuitikia katika mji wa Beroya walisifiwa kwa sababu waliyachunguza Maandiko waone kama mambo ambayo Paulo aliwaambia yalikuwa ndiyo ukweli. Walipoona kwamba Paulo alinena ukweli, wao walichukua msimamo imara kwa ajili ya ukweli huo. Tunaambiwa hivi: “Watu hawa [Waberoya] walikuwa waungwana kuliko wale wa Thesalonike, kwa kuwa walilipokea lile neno kwa uelekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku, waone kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo.”—Matendo 17:10, 11.
Watu wa Beroya hawakuruhusu maneno ya wapinzani yafunge akili zao zisipokee habari njema. Bali, wao waliyachunguza Maandiko kila siku kuhakikisha kwamba mambo waliyosikia yalikuwa ya ukweli. Wao walikuwa wamepata hazina yenye thamani kubwa nao hawangeruhusu wapinzani wawaondoe kwenye hazina hiyo. Je! huo sio ungekuwa mwendo wa kiakili kuchukua kuhusu habari njema zile zile ambazo Mashahidi wa Yehova wanatangaza leo?
Sababu Inayofanya Wengine Wapinge
Nyakati nyingine wapinzani wanakuwa ni watu wa ukoo wenye makusudi mema ambao wewe unawapenda na kuwaheshimu, nawe una kila sababu ya kuamini kwamba wanapendezwa kwa moyo mweupe na masilahi njema yako. Lakini unahitaji kufikiria sababu inayowafanya wapinge kujifunza kwako kwa Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Je! wao wana uthibitisho imara wa Kimaandiko kwamba mambo unayojifunza siyo ukweli? Au upinzani wao unasababishwa na mambo ambayo wengine wamewaambia? Je! wao wana ukosefu wa maarifa sahihi juu ya mambo yanayofundishwa na Mashahidi? Wengi waliopinga Yesu walifanya hivyo kwa kutokujua mambo aliyofundisha na kwa sababu wao waliamini mashtaka ya uwongo ya wapinzani.
Wakati Yesu alipokuwa akining’inia juu ya mti wa mateso, watu wenye kupita karibu “wakamtukana, wakitikisa-tikisa vichwa, wakisema, Ahaa! wewe mwenye kulivunja hekalu na kulijenga katika siku tatu, jiponye nafsi yako, ushuke [kwenye mti wa mateso]. Kadhalika na wakuu wa makuhani wakamdhihaki wao kwa wao, pamoja na waandishi, wakisema, Aliponya wengine; hawezi kujiponya mwenyewe. Kristo, mfalme wa Israeli, na ashuke sasa [kwenye mti wa mateso] tupate kuona na kuamini.” (Marko 15:29-32) Sababu ya mwelekeo huo mbaya ilikuwa nini?
Watu walikuwa wameruhusu wapewe maoni hayo juu ya Yesu na viongozi wa kidini waliomchukia kwa sababu yeye alikuwa amewafunua wazi kuwa walimu wa uwongo ambao vitendo vyao havikupatana na madai yao ya kuwa wawakilishi wa yule Mungu wa kweli. Kwa kusema mambo wazi, Yesu alikuwa amewaambia: “Mbona ninyi nanyi huihalifu amri ya Mungu kwa ajili ya mapokeo yenu? Enyi wanafiki, ni vema alivyotabiri Isaya kwa habari zenu, akisema, Watu hawa huniheshimu kwa midomo; ila mioyo yao iko mbali nami. Nao waniabudu bure, wakifundisha mafundisho yaliyo maagizo ya wanadamu.”—Mathayo 15:3, 7-9.
Viongozi wa kidini walimchukia Yesu kwa kadiri kubwa sana na kweli alizofundisha hata wakatunga hila ya kumwua na wakafanya kila jitihada kugeuza watu wawe dhidi yake. Leo, viongozi wengi wa kidini wanapinga Mashahidi wa Yehova kwa kadiri kubwa jinsi ile ile. Na kama ilivyokuwa kwa Wakristo wa kwanza kwanza, Mashahidi ‘wananenwa vibaya’ kila mahali. Lakini je! ni jambo la hekima kuruhusu upinzani unaofanywa na wengi ukufanye uwe na fikira hizo?
Kweli zile zile za Kimaandiko juu ya Ufalme wa Mungu ambazo Yesu na mitume wake walihubiri zinatangazwa leo na Mashahidi wa Yehova. Mamia ya maelfu ya watu katika sehemu zote za ulimwengu wanazikubali habari njema bila kujali upinzani mkali sana unaofanywa na marafiki, watu wa ukoo, na viongozi wa kidini. Wale wanaokubali ujumbe wa Ufalme wamethibitisha kwa njia yenye kuwaridhisha kwamba huo ndio ukweli, nao wanapiga moyo konde waushikilie sana.
Kwa hiyo mbona uwe kama wale watu wa karne ya kwanza walioruhusu wengine wawageuze kutoka kwenye kweli zinazotoa uzima za Kimaandiko zilizowajia kupitia wafuasi wa Yesu Kristo wasiopendwa sana na wengi? Badala ya hivyo, endelea kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi, ukitumia Neno la Mungu lililoandikwa kujithibitishia kwa njia yenye kukuridhisha kwamba mambo unayojifunza ndiyo ukweli kwa uhakika. (Yohana 8:32) Na kwa msaada wa Mungu shikilia sana ukweli huo.