Kumhubiri Kristo—Kwa Wivu au Nia Njema?
SIKUZOTE watumishi wa Mungu wamepingwa vikali kwa kujitahidi kusaidia watu. Wapinzani wa Yesu Kristo walitumia dhihaka na malawama ya namna zote, wakamfanyia mashtaka ya uongo juu ya kila kajambo kadogo walikoweza kupata.
Walimshtaki Yesu kwamba alikuwa mlafi na mlevi kwa sababu alikula na kunywa. (Mt. 11:19) Walisema alikuwa akichangamana na watenda dhambi kwa sababu ya kwenda nyumbani kwa watenda dhambi, walipomkaribisha akawaeleze habari njema. (Marko 2:15, 16) Alipoponya watu magonjwa yao mabaya sana, walitaka kumzuia wakisema alivunja sheria zao wenyewe kuhusu siku ya Sabato.—Mt. 12:9-14.
Wanadini hao walipendelea kuona watu wakitaabika kwa kujaribu kumwondolea Yesu mbali, kwa sababu kuhubiri kwake na matendo yake yalionyesha wao walikuwa waalimu wasiofaa kitu. (Mt. 15:14) Walitaka kuheshimiwa na wanadamu badala ya wao kumheshimu Mungu au kuheshimiwa naye.—Mt. 23:5-7.
Mitume pia walipingwa. Wakati wapinzani wa kidini walipochochea fitina Paulo akatiwa gerezani Rumi kwa sababu ya kueneza nuru ya habari njema zenye kuwapa watu uhuru, wapinzani hao walijitahidi sana kuharibu matokeo mazuri ya kuhubiri kwake. Paulo alisema: “Wengine wanahubiri habari za Kristo kwa sababu ya husuda na fitina; na wengine kwa nia njema. . . . [wale wa kwanza] wanamhubiri Kristo kwa fitina, wala si kwa moyo mweupe, wakidhani kuongeza dhiki za kufungwa kwangu.”—Flp. 1:15-17. ‘
Wale waliokuwa “wakidhani kuongeza dhiki” ya Paulo walikuwa Wayahudi hasa waliojidai kuwa Wakristo, lakini walikuwa wameacha kufundisha mafundisho safi ya mitume. Waliogopa kushutumiwa na kuteswa kama Kristo. (Gal. 6:12, 13) Hawakuwa na makusudi mema, bali walitaka kutia mashaka katika wengine, magomvi, migawanyiko—kwa ufupi, walitaka kubomoa kazi ya mtume na hali ya kiroho ya wale aliokuwa amejitahidi sana awajenge. Walitaka kumvunja mtume roho kwa kumwongezea mzigo huo juu ya vifungo vyake gerezani.
Alipokuwa akiandikia kundi la Korintho juu ya wapinzani hao, Paulo alieleza habari za magumu ambayo yeye na wenzake walipatwa nayo, “kwa utukufu na aibu; kwa kunenwa vibaya na kunenwa vema; kama wadanganyao, bali tu watu wa kweli.” (2 Kor. 6:8) Naam, wapinzani hao wa Paulo hata walifikia hatua ya kusema alikuwa mdanganyifu, kwamba alikuwa akipotoa wanafunzi. Kusudi lao lilikuwa kuona kundi likivunjika—ili Wakristo wa kweli waondoke katika makundi. Wao hawakujitahidi sana kujipatia wanafunzi wapya wao wenyewe huko nje katika ulimwengu. Walitaka kulishambulia kundi la Kikristo, “wawavute hao wanafunzi” wa Kristo, na kuzuia wengine wasiusikilize ujumbe ambao wanafunzi hao wa kweli waliutangaza.—Matendo 20:30.
Kwa hiyo, ni wazi kwamba wapinzani hao wa Wakristo wa kwanza hawakuwa wakijaribu kujenga wengine, ingawa wao wenyewe walijidai kuwa Wakristo. Wao wenyewe hawakuwa wakifanya kazi ya kufanya watu wawe wanafunzi wa Kristo, bali walijaribu kubomoa wale waliotaka kusikiliza habari njema.
MAHUBIRI YA KWELI YAJENGA
Namna gani leo juu ya hali ya kuzihubiri habari njema za ufalme wa Kristo na utawala wake unaokuja utawale dunia? Mashahidi wa Yehova, ambao ni Wakristo wa kisasa, wanajitahidi kumhubiri kila mtu habari njema hizi. Wao hawasemi kwamba hawana makosa. Wala wao si manabii wenye kuongozwa na Mungu. Lakini wanajaribu kuishi maisha safi na kusaidia watu kwa kuwafundisha habari njema. Mamilioni ya watu wanaitikia.
Je! kazi hiyo inajenga? Apaswalo kufanya mtu ni kutazama matokeo tu. Tuchunguzapo utendaji huu, je! hatuwezi kuona mfano bora ajabu wa umoja wa mafundisho, mwenendo na upendo ulimwenguni pote? Twaona watu mamia ya maelfu kila mwaka wakibadili nyutu zao ili wawe raia wenye kutii sheria, wenye kudumisha adili za Maandiko, kukuza jamaa ziwe zenye furaha, kufanya wengine wawe na kanuni izo hizo bora. Ni mahali gani pengine tunapoona watu wakitumia wakati wao wenyewe na mali zao kuonyesha upendo kwa wanadamu wenzao kwa kuwatembelea nyumbani kwao na kufundisha wanaopendezwa kweli za Neno la Mungu? Ni mahali gani pengine tunapoona mpango kama huo ukiendeshwa katika mataifa yote kuondoa ukabila kati ya wanaofundishwa, tena ni wapi pengine ‘wanapofua panga zao ziwe majembe, wasijifunze vita tena’? (Isa. 2:4) Ni mahali gani pengine tunapoona jamii ya watu wanaopendezwa na kuunga mkono na kutetea kweli ya Biblia isichafuliwe hata kutokee nini?—1 Tim. 3:15.
KUBOMOA BILA KUJENGA UPYA
Hata hivyo, kama vile Wakristo wa kwanza walivyokuwa na wapinzani, ndivyo ilivyo kwa Mashahidi wa Yehova leo. Wengine wanatoka kati yao wenyewe, kama ilivyokuwa kwa Wakristo wa kwanza. (Matendo 20:30) Lakini kusudi la watu hao ni nini? Ni kubomoa. Mambo wanayosema na kutangaza kwa ujumla hushambulia Mashahidi wa Yehova. Je! tunawaona wakijenga mtu ye yote? Je! wanashiriki kukusanya sana Wakristo wenye maisha safi, wenye kuuhubiri Ufalme? Wakimvuta mtu fulani anayeshirikiana na Mashahidi wa Yehova, mtu huyo atakwenda wapi? Atajengwa wapi kiroho?
Maulizo ayo hayo yalitokea Yesu alipokuwa duniani. Wengine walianza kunung’unika na kumwacha Yesu kwa sababu alisema jambo walilokataa kulikubali. Ndipo Yesu alipouliza wanafunzi wake: “Je! ninyi nanyi mwataka kuondoka?” Simoni Petro akajibu: “Bwana! Twende kwa nani? Wewe unayo maneno ya uzima wa milele.” (Yohana 6:67, 68) Wangeweza kujengewa wapi kiroho? Wangeweza kuwaendea watu hao wenye kunung’unika wasaidiwe nao? Walijua wasingeweza. Kama wangalifanya hivyo wangaliacha mambo waliyokuwa wameamini na kubaki mikono mitupu, au warudie dini ya Wayahudi, ambako Kristo alikuwa amewafungua.—Gal. 4:8-11.
Je! wapinzani wa kisasa wa Mashahidi wa Yehova wana mpango wa kujenga watu katika maarifa ya Mungu? Je! wanawatolea watu elimu ya kiroho yenye kuendelea? Sivyo. Kwa kawaida wao hujiunga na taratibu za kidini za Jumuiya ya Wakristo, na kupendekeza watu wajiunge na madhehebu wanayowachagulia. Nyakati nyingine viongozi wa dini wanaruhusu watu hao wenye manung’uniko wasimame katika jukwaa zao, si kuzihubiri Injili, bali kujaribu kubomoa Mashahidi wa Yehova. Tena, watu hao wanarudia mambo ambayo wao wenyewe walikuwa wameyaacha wakayatangaza hadharani kuwa uongo, yaani, fundisho la Utatu (‘Mungu katika nafsi tatu’), kutokufa kwa nafsi ya kibinadamu, moto wa mateso ya waovu, na mafundisho mengine yasiyopatana na Maandiko. Wanasema Mashahidi waliwadanganya, wengine wao kwa miaka mingi—na hilo hilo ndilo shtaka alilofanyiwa Paulo na “mitume wa uongo.” Lakini sasa wanasema wameona nuru kwa ghafula—kwamba mafundisho yale waliyokuwa wameyakataa kwanza yalikuwa ya kweli muda wote huo. Wanatubu kwamba walitilia mashaka mafundisho hayo na kuyapinga walipokuwa wakishirikiana na Mashahidi.
Je! kuyumba-yumba huko kwa wapinzani hao hakutokezi mashaka juu ya unyofu wao? Wengi wao hapo kwanza walikuwa wanakanisa waliotangaza baadaye kwamba mafundisho hayo yalikuwa ya uongo, yenye kutokana na dini zisizo za Kikristo. Walipokuwa wakishirikiana na Mashahidi wa Yehova walitolea watu wengine uhakikisho wa imani yao walipowahubiri. Je! watu hawa wanapogeuka na kupinga Mashahidi wa Yehova, wanafuata mfano wa mtume Paulo? Yeye hapo kwanza alikuwa mwamini wa dini ya Wayahudi, akiamini kwamba angeweza kupata haki kwa matendo ya sheria ya Musa. Lakini aliyatupa mambo hayo baada ya kuwa Mkristo. Wapinzani wake walisema kwamba Wakristo wanapaswa kuanza tena kutii mambo ya Torati, na kutumainia matendo hayo ili kupata wokovu. Paulo alijibu hivi: “Nikiyajenga tena yale niliyoyabomoa, naonyesha ya kuwa mimi mwenyewe ni mkosaji.”—Gal. 2:18.
Ni jambo baya sana kuwakilisha Mungu na Kristo kwa njia moja, kisha tufahamu kwamba tulikuwa tumeelewa vibaya mafundisho makuu ya Maandiko, kisha turudie mafundisho yale yale ya kwanza ambayo baada ya kujifunza miaka mingi, tulikuwa tumeamua kabisa kwamba ni makosa. Wakristo hawawezi kuyumbayumba juu ya mafundisho hayo ya msingi. Mtu awezaje kuamini kwamba watu hao ni wanyofu na wana uamuzi mzuri?
Tena, Yesu alisema juu ya wanafunzi wake hivi: “Wao si wa ulimwengu.” (Yohana 17:16) Lakini ni nani awezaye kukana kwamba makanisa ya Jumuiya ya Wakristo ni washiriki wakubwa wa ulimwengu? Wale wanaorudi kujiunga na makanisa hayo wanapuza uhakika wa kwamba viongozi wa dini wamevibariki vita vya mataifa, washiriki wa madhehebu ile ile wakasali upande huu na ule wakiomba jeshi lao wenyewe lishinde na kuharibu upande ule mwingine. Watu wanaorudi kuunga mkono madhehebu hizo wanajiletea tena hatia ya damu waliyokuwa wameondolewa zamani.—Linganisha Hesabu 35:33; Ufunuo 18:24.
Ikiwa mtu ameacha mafundisho yanayomdharau Mungu—Utatu, mateso ya kishetani ya nafsi katika moto wa milele, kuharibiwa kwa Dunia yetu, kuunga mkono vita vya mataifa vya umwagaji wa damu na imani za namna hiyo zinazochafua Mkristo na kumfanya sehemu ya ulimwengu—kisha anayarudia tena mafundisho hayo, yeye anafanya kama watu walioelezwa na mtume Petro siku zake. Petro aliandika hivi: “Kwa maana wale waliokwisha kuyakimbia machafu ya dunia kwa kumjua Bwana na Mwokozi Yesu Kristo, kama wakinaswa tena na kushindwa, hali yao ya mwisho imekuwa mbaya kuliko ile ya kwanza. Maana ingekuwa heri kwao kama wasingaliijua njia ya haki, kuliko kuijua, kisha kuiacha ile amri takatifu waliyopewa. Lakini imetukia kwao sawa-sawa na ile mithali ya kweli, Mbwa ameyarudia matapiko yake mwenyewe, na nguruwe aliyeoshwa amerudi kugaagaa matopeni.”—2 Pet. 2:20-22.
KUHAKIKISHA HAU YAKO
Basi, je! mtu awezaje kuhakikisha kwamba hali yake inafaa ikiwa amezidi kumwamini Yehova Mungu na ufalme Wake kwa kujifunza na Mashahidi wa Yehova? Juu ya jambo hili mtume Paulo alimwonya Timotheo kwa upole, aliyekutana na watu waliotaka kutikisa imani yake. Paulo alimwambia hivi: “Bali wewe ukae katika mambo yale uliyofundishwa na kuhakikishwa, kwa maana unajua ni akina nani ambao ulijifunza kwao; na ya kuwa tangu utoto umeyajua maandiko matakatifu, ambayo yaweza kukuhekimisha hata upate wokovu kwa imani iliyo katika Kristo Yesu.”—2 Tim. 3:14, 15.
Shauri hilo lilimfaaje Timotheo? Timotheo alikuwa amelelewa na mama Myahudi na bibi watawa. Alijua yaliyosemwa na Maandiko ya Kiebrania. Alisihiwa ayaamini, na kuwa na imani “isiyo na unafiki.” (2 Tim. 1:5) Halafu, aliposikia mafundisho ya mtume Paulo, alisihiwa zaidi (si kwa ujanja, bali kwa kuhakikisha mafundisho ya Paulo kwa kutumia Maandiko) aukubali Ukristo. Sasa Paulo amwambia Timotheo akumbuke watu waliomfunza: je! walikuwa wakimfunza wajipatie faida—wapate pesa au wamfanye mtumwa wao, au walifanya hivyo kwa sababu walimpenda kweli kweli? Je! alifanywa mwanafunzi wa mwanadamu, Paulo, au wa Bwana Yesu Kristo? Akijua mambo hayo, ataweza kufahamu kwamba mtu atakayejaribu kumpotoa atakuwa ana kusudi baya.
Vivyo hivyo, Mashahidi wa Yehova leo, na wale wanaofunzwa nao, wanaweza kufikiria haya: Ni uwezo gani wenye kusihi ulionisadikisha mambo ambayo nimeamini? Ulikuwa ujanja wa wanadamu? Je! nililazimishwa? Namna gani wale walinifunza? Je! walikuwa wakijipatia pesa? Je! waliniomba niwalipe pesa za wakati na gharama walizotumia kuja kwangu kwa kawaida? Je! walinifanya nikawa mwanafunzi wao wenyewe, na je! walipokuwa wakinifundisha, waliniagiza mambo ya kufanya kwa ‘hekima’ yao wenyewe, au walitumia uongozi wa Maandiko? Je! wenye kunitembelea walipendezwa nami? Je! matengenezo mengine ya kidini yalikuwa yamependezwa hivyo nami? Paulo alisema yafuatayo juu yake mwenyewe na wenzake walipokuwa Thesalonike, “Tulikuwa wapole katikati yenu, kama vile mlezi awatunzavyo watoto wake mwenyewe. Vivyo hivyo nasi tukiwatumaini kwa upendo mwingi, tuliona furaha kuwapa, si Injili ya Mungu tu, bali na [nafsi] zetu pia, kwa sababu mmekuwa wapendwa wetu.” (1 The. 2:7, 8) Je! ulipendwa pia na wale waliokujia, na je! walijitoa mara nyingi wakutumikie, kama kwamba ‘wakikutolea nafsi zao wenyewe’?
Basi, Wakristo hao wangeona tofauti kubwa sana wakifikiria jinsi wapinzani walivyo! Ni kama vile Paulo alivyoandikia kundi katika Rumi: “Ndugu zangu, nawasihi, waangalieni wale wafanyao fitina na mambo ya kukwaza kinyume cha mafundisho mliyojifunza; mkajiepushe nao. Kwa sababu walio hivyo hawamtumikii Bwana wetu Kristo, bali matumbo yao wenyewe; na kwa maneno laini na ya kujipendekeza waidanganya mioyo ya watu wanyofu.”—Rum. 16:17, 18.
MATOKEO KWA WALE WANAOSHAMBULIA WATUMISHI WA MUNGU
Tuseme nini basi juu ya jitihada za watu wachache wenye manung’uniko wanaojaribu kubomoa kazi na matokeo ya mahubiri ya Mashahidi wa Yehova? Wako kama wale ambao mtume aliandika habari zao waliohubiri wambomoe: “Yadhuru nini? lakini kwa njia zote, ikiwa ni kwa hila, au ikiwa ni kwa kweli, Kristo anahubiriwa, na kwa hiyo nafurahi.” (Flp. 1:18)Watu hao bila kujua hufanya wengine watake kujua habari zaidi juu ya mambo yanayosemwa na Mashahidi wa Yehova, wanaposhindana nao. Paulo ataja wachawi Wamisri siku za Musa kuwa mfano wa mambo yatakayopata wapinzani hao. Asema: “Kama vile Yane na Yambre walivyopingana na Musa, vivyo hivyo na hawa wanapingana na ile kweli; ni watu walioharibika akili zao, wamekataliwa kwa mambo ya imani. Lakini hawataendelea sana; maana upumbavu wao utakuwa dhahiri kwa watu wote, kama vile na upumbavu wa hao ulivyokuwa dhahiri.”—2 Tim. 3:8, 9.
Katika Waebrania 6:4-8 mtume anaeleza hali yenye hatari hata zaidi ya wanaoanguka na kuiacha kweli. Kisha anasema habari ya wale ambao wamemtumikia Mungu kwa uaminifu na unyofu, akisema hivi: “Lakini, wapenzi, ijapokuwa twanena hayo, katika habari zenu tumesadiki mambo yaliyo mazuri zaidi, na yaliyo na wokovu. Maana Mungu si dhalimu hata aisahau kazi yenu, na pendo lile mlilolidhihirisha kwa jina lake, kwa kuwa mmewahudumia watakatifu, na hata hivi sasa mngali mkiwahudumia. Nasi twataka sana kila mmoja wenu aidhihirishe bidii ile ile kwa utimilifu wa matumaini hata mwisho; ili msiwe wavivu, bali mkawe wafuasi wa hao wazirithio ahadi kwa imani na uvumilivu.”—Ebr. 6:9-12.
Kwa kufuata mashauri mema ya Maandiko, kila mtu aliyeanza kulichukua jina la Kristo na la Yehova Baba yake na aendelee kujenga ndugu zake Wakristo kwa imani na saburi ili arithi ahadi nzuri ajabu ya uzima wa milele na kusaidia wengine pia waupate.—1 Tim. 4:15, 16.