Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w77 4/15 kur. 183-185
  • Sala Zako Zina Ubora Gani?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Sala Zako Zina Ubora Gani?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • IMANI NA MAARIFA NI YA LAZIMA
  • MFANO WA KRISTO WA KUSALI
  • MAMBO YAFAAYO YA KUSALI
  • MIFANO MYEMA YA SALA
  • Uwe Imara Katika Sala
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
  • Jinsi ya Kusali na Kusikiwa na Mungu
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Mkaribie Mungu Katika Sala
    Biblia Inafundisha Nini Hasa?
  • Kumjia Msikiaji wa Sala
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1976
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1977
w77 4/15 kur. 183-185

Sala Zako Zina Ubora Gani?

WEWE husali mara ngapi? Je! unajisikia kwamba sala zako zinasikiwa? Je! unajisikia ukikosa kujua mambo ya kusema katika sala?

Sala ni mpango bora zaidi wa Muumba, zawadi halisi inayopaswa kuthaminiwa sana. Kwa hiyo yampasa mtu aangalie sana kwamba anatumia zawadi hii na kutoa sala zitakazojibiwa na Mungu.

Takwa la kwanza ili sala zimpendeze Mungu hata asikilize ni jepesi sana​—⁠ni kuwa na moyo mnyofu. Mtume Paulo aandika hivi: “Na tukaribie wenye moyo wa kweli, kwa utimilifu wa imani.” (Ebr. 10:22) Huenda mtu akatumia usemi bora au usio bora katika mtungo, akaueleza wazi au vibaya. Lakini Yehova haangalii mambo hayo ya juujuu bali huutazama moyo. “Ndiye azijuaye siri za moyo.”​—Zab. 44:21; 1 Sam. 16:7.

Kwa kweli, huenda sala ikawa si ya sauti kubwa, huenda ikawa ni kumsihi sana Yehova kwa moyo, kama alivyofanya Hana mwaminifu. “Alikuwa akinena moyoni mwake; midomo yake tu ilionekana kama anena, sauti yake isisikiwe.” Lakini Yehova alimjibu sala yake.​—1 Sam. 1:13, 20.

IMANI NA MAARIFA NI YA LAZIMA

Yako mambo mengine ya maana yanayotakiwa pamoja na moyo mnyofu. Lazima mwenye kusali amwamini Mungu. Imani hiyo si kuamini Mungu yuko tu, kwamba ndiye Muumba na Mwenye Nguvu Zote. Katika Neno lake aliloliongoza Mungu asema hivi: “Mtu amwendeaye Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko, na kwamba huwapa thawabu wale wamtafutao” kwa bidii.​—Ebr. 11:6.

Ili mtu huyo awe na imani, lazima amjue Mungu​—⁠ajue sifa zake, matendo yake, makusudi yake. Mtume aandika hivi: “Wamwiteje yeye wasiyemwamini? . . . Tena wamsikieje pasipo mhubiri?” Ikiwa mtu hajajifunza Neno la Mungu, basi yampasa kuomba msaada kwa wenye kulifahamu, ili wamfundishe amjue Mungu.​—Rum. 10:14.

Tukipata maarifa kidogo juu ya kusudi la Mungu, yatupasa tusali kupatana na kusudi hilo. Hatuwezi kumtazamia Mungu ajibu sala yenye kuomba mambo yaliyo kinyume cha mapenzi yake. Kutoa sala ya namna hiyo kungekuwa kumwomba Mungu ajipinge mwenyewe. Tena, lo lote lililo kinyume cha mapenzi ya Mungu lisingetufaidi. Ni kama vile Yesu alivyowaambia watu: “Ikiwa ninyi, mlio waovu, mnajua kuwapa watoto wenu vipawa vyema, je! si zaidi sana Baba yenu aliye mbinguni atawapa mema wao wamwombao?”​—Mt. 7:9-11.

Tunaposali lazima tujue kwamba Yehova ni mtu. Yehova ana mawazo ya moyoni, yenye nguvu kuliko yetu, ya shauku ya upendo, ya huruma, rehema na nia ya kutusikiliza na kutusaidia. Yeye hututhamini sana tunapokuwa na nia ifaayo. Kwa hiyo yatupasa tuseme naye kweli kweli​—kwa heshima lakini kwa kummiminia yote yaliyomo mioyoni mwetu.

MFANO WA KRISTO WA KUSALI

Yesu Kristo alisali kwa kawaida. Alitoa kielelezo cha sala, kilichoandikwa katika Mathayo 6:9-13, chenye kuonyesha mambo makuu ya kuomba, nayo sala aliyotoa muda mfupi baada ya kuanza Chakula cha Bwana cha Jioni yatusaidia kujua mambo aliyosali. (Yohana sura ya 17) Kabla hajaweka mitume wake kumi na wawili alisali usiku kucha. (Luka 6:12, 13) Mwanadamu mkamilifu kama yeye, asiye na maelekeo yenye dhambi wala kasoro, aliwezaje kuwa na mambo mengi hivyo ya kusali?

Yesu alijua kwamba mitume wangekuwa mawe ya msingi ya kundi la Kikristo, ambalo yangekuwa “nguzo na msingi wa kweli” duniani. (1 Tim. 3:15) Walipaswa kuwa wanaume bora sana. Ilifaa Yesu azungumze na Baba yake wa mbinguni juu ya wanaume walioshirikiana naye​—⁠sifa za kila mmoja, udhaifu wake, mahitaji yake, kama alistahili kuwa katika kimojawapo cha vyeo hivyo kumi na viwili. Bila shaka Yesu alimwomba Yehova ampe hekima, kwa maana alijua Mungu ndiye aliyekuwa na daraka la kuwachagua. (1 Kor. 12:18) Vilevile, pengine alizungumza naye jinsi wale ambao wangechaguliwa wangezoezwa zaidi.

Tena, bila shaka Yesu alisali juu ya kazi iliyokuwa mbele yake. Pengine alizungumza habari za mpanuko ambao ungetokea baadaye katika kazi ya Injili, juu ya kuwekwa kwa wale 70, mahali ambapo Yesu mwenyewe angetembelea na mwishowe juu ya jaribu na kifo cha dhabihu kilichokuwa mbele yake.​—Luka 10:1; linganisha Luka 9:31.

MAMBO YAFAAYO YA KUSALI

Ni mambo gani tunayoweza kuzungumza na Yehova katika sala zetu za kipekee, za faraghani? Zaidi ya yale mambo makubwa, yaani, kutakaswa kwa jina la Yehova, kuja kwa ufalme wake wa Kimasihi na kuharibiwa kwa uovu, tunahitaji sana kusaidiwa kipekee. Twaweza kuzungumza juu ya matatizo yaliyotupata mchana. Twaweza kukubali makosa yetu​—kueleza hasa jinsi tulivyokosa.

Labda tumekatishwa tamaa na jinsi tulivyofanya kazi fulani. Pengine jambo lenyewe lilihusu kuongoza funzo la Biblia, kutoa hotuba, kumpa mtu fulani shauri au kufanya mpango wa kundi. Labda lilihusu kutumia ukichwa juu ya jamaa, au kuuheshimu. Lo lote liwalo, tutasikiwa tukikubali waziwazi kosa letu na kuomba tusaidiwe kufanya maendeleo wakati ule mwingine.​—⁠Ebr. 4:15, 16.

Halafu, kwa habari ya sala, twaweza kujiuliza maulizo kama haya: Ni matunda gani ya roho yanayokosekana katika maisha zetu? Je! tunaonyesha upendo na huruma halisi kwa wengine? Je! tunasali wengine wawe na hali njema, wafanikiwe? Je! tunafurahia kumtumikia Mungu? Tunaonyesha kujiweza, au tuna maelekeo ya kupasuka kwa hasira, na kujiumiza wenyewe na wengine?​—Mit. 25:28; 29:11; Gal. 5:22, 23, NW; 2 The. 1:11; Luka 6:27, 28.

Namna gani mahitaji ya kimwili? Mungu hupendezwa tunapomtambua kuwa Mpaji wa vitu vyote vizuri. Halafu, je! inafaa kuomba tupone ugonjwa yakiwa mapenzi ya Mungu? Naam. Mtume Paulo alimpa Mungu sifa ya kupona kwa rafiki yake Epafrodito mwaminifu. Aliandika hivi: “Kwa maana [Epafrodito] alikuwa hawezi kweli kweli, karibu na kufa; lakini Mungu alimhurumia.” (Flp. 2:27) Sisi pia twaweza kuomba kwamba, Mungu akiona yafaa, tuweze kuwa hai na kuendelea kumtumikia. Asipotuponya, hiyo haionyeshi amekataa sala yetu. Bali, twajua kwamba faida zake na zetu zinatimizwa vizuri zaidi kwa njia hiyo. Tunapokuwa wagonjwa twaweza kusali, tukiwa na tumaini hakika, kwamba tupewe nguvu za kuendelea kuwa na kiasi cha Kikristo, kwa maana tunapokuwa dhaifu kimwili huenda tukawa na maelekeo ya kukata tamaa na kukosa imani. Vivyo hivyo mtu aweza kusali kwa ajili ya Wakristo wenzake walio wagonjwa sana kimwili au kiroho.​—1 Yohana 5:16.

Wakati wa majaribu, au ndugu zetu wanapokuwa na magumu, twahitaji hekima ya pekee juu ya mwendo wa kufuata, au jinsi ya kushauri wengine na kuwasaidia. Yakobo, ndugu mzazi mmoja na Yesu aliandika hivi: “Ndugu zangu, hesabuni ya kuwa ni furaha tupu, mkiangukia katika majaribu mbalimbali; . . . mtu wa kwenu akipungukiwa na hekima, na aombe dua kwa Mungu, awapaye wote kwa ukarimu, wala hakemei; naye atapewa.”​—Yak. 1:2-5.

Huenda tukajisikia kwamba ombi letu litaonwa na Mungu kuwa lisilofaa kitu, kwa kuwa yeye ni mkuu sana, ni mwenye hekima yote, nasi huwa watu dhaifu kwa kawaida. Bila shaka wewe umepata kuomba mtu fulani akufanyie jambo, akakataa, au akaitikia kwa njia iliyokufanya ujisikie u mdogo sana na usiyefaa kitu, au mpumbavu. Lakini Mungu hatatulaumu kwa sababu ya “ujinga” au udhaifu. Yeye hutoa kwa ukarimu, kwa moyo wote, kwa njia inayofanya tufurahi kwa vile tulivyomwomba.

Pengine sisi wenyewe tumetenda dhambi nzito. Basi twahitaji sana sala. Ikiwa tumetubu na twataka kurudishiwa upendeleo wa Mungu, yatupasa tusali bila kukawia, kuungama dhambi yetu, kuonyesha hasa dhambi yetu imekuwa nini, na vilevile kufanya yote tuwezayo turekebishe mambo. (Mit. 28:13) Tukijisikia kwamba sala yetu imezuiwa, yatupasa tuombe wazee wa kundi watusaidie bila kukawia, kama inavyoelezwa katika Yakobo 5:13-15. Sala yao ina matokeo mema.​—Yak. 5:16.

MIFANO MYEMA YA SALA

Inafaa kusoma baadhi ya sala zilizomo katika Zaburi ili sala zetu ziwe bora zaidi. Utaona kwamba mara nyingi (katika New World Translation of the Holy Scriptures) kuna maandishi yaliyowekwa juu ya sura yenye kutaja kipindi chenyewe, na pia kwamba sala inayotolewa inalingana na wakati huo.

Kwa mfano, angalia sala ya Daudi iliyotoka moyoni, baada ya kukaripiwa na Mungu kwa sababu ya dhambi yake na Bath-sheba. (Zaburi 51) Alitegemea kabisa rehema ya Yehova. Alihangaikia hasa lawama ambalo lingekuwa juu ya jina la Yehova. (Mist. 1-4) Aliomba asamehewe kwa sababu alikuwa amerithi dhambi. (Mst. 5) Aliomba atakaswe, apewe roho mpya na thabiti. (Mist. 7-10) Aliogopa Mungu asije akamwondolea roho takatifu Yake. (Mst. 11) Aliungama hatia yake ya kumwaga damu. (Mst. 14) Aliahidi kuendelea kumtumikia Yehova. (Mist. 14, 15) Mwishowe, alionyesha alipendezwa sana na Sayuni na hasa ibada safi iliyoendeshwa huko.​—Mst. 18, 19.

Katika sala nyingine za Biblia twaona sifa au shukrani zikitolewa, maandiko yakitajwa katika sala hizo pamoja na sifa na kanuni njema za Mungu kama msingi wa kutazamia Yehova ajibu vizuri. Mambo hayo yaonekana katika Zaburi 86.

Kwa hiyo, ikiwa wewe umevunjika moyo ukafadhaika, ikiwa huna tumaini halisi, unaweza kufanya nini? Mtafute Yehova Mungu. Jifunze habari zake kwa wale wanaomtumikia. Jinyenyekeze umwombe kupitia kwa Yesu Kristo. Atakuonyesha tumaini halisi la uzima chini ya utawala wa Ufalme wa Kristo, wakati “dunia itajawa na kumjua [Yehova], kama vile maji yanavyoifunika bahari.”​—Isa. 11:9.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki