Kataa Uasi wa Imani, Ambatana na Ile Kweli!
“Kila apitaye cheo, wala asidumu katika mafundisho ya Kristo, yeye hana Mungu. Yeye adumuye katika mafundisho hayo, huyo ana Baba na Mwana pia.”—2 YOHANA 9.
1, 2. (a) Nyakati nyingine Shetani amejaribuje kuizima nuru ya kweli kati ya watu wa Yehova? (b) Kwa sababu gani inahitajiwa kabisa kwamba Mashahidi wa Yehova waukatae uasi wa imani?
YEHOVA MUNGU ndiye Chanzo cha kweli ya kiroho. Basi, kwa kufaa mtunga zaburi alimpelekea sala hii: “Peleka nuru yako na kweli yako.” (Zaburi 43:3, NW) Kulingana na hilo, kweli ni alama yenye kuwatambulisha wenye kumwabudu Yehova.—Yohana 8:31, 32; 17:17.
2 Akiwa katika jitihada ya kuizima nuru ya kweli iliyo kati ya watu wa Yehova, nyakati nyingine Shetani Ibilisi amejaribu kulichafua kundi la Kikristo kwa kutumia mafundisho ya uasi wa imani. (2 Wakorintho 4:1-6; Yuda 3, 4) Lakini majaribio yake hayo yameshindwa kupata matokeo kwa sababu mashahidi waaminifu wa Yehova wanakataa uasi wa imani na kuambatana na kweli ya kiroho. Kwa kweli, kufanya hivyo kunahitajiwa kabisa ikiwa tutadumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova Mungu na Yesu Kristo, kwa maana mtume Mkristo Yohana aliongozwa na Mungu kuandika hivi: “Kila apitaye cheo, wala asidumu katika mafundisho ya Kristo, yeye hana Mungu. Yeye adumuye katika mafundisho hayo, huyo ana Baba na Mwana pia.”—2 Yohana 9.
3. Ni maulizo gani yatakayojibiwa tunapozungumza Yohana wa Pili na wa Tatu?
3 Lakini inawapasa Mashahidi wa Yehova wafanye nini ili kupinga sana uasi wa imani? Na wanaweza kuendelezaje faida za Kikristo wakiwa “wenzi-wafanya-kazi katika ile kweli”? (3 Yohana 8, NW) Ili tupate majibu, tutazizungumza barua za pili na tatu za Yohana zilizoongozwa na Mungu, zikaandikwa huko Efeso au karibu na huko, katika Asia Ndogo, wapata mwaka wa 98 W.K.
Kweli na Upendo Ni Mambo Yanayohitajiwa Kabisa
4, 5. (a) Kwa sababu gani mtume Yohana angeweza kwa kufaa kujitaja kuwa “mzee”? (b) “Mama mteule” na “watoto” wake walikuwa nani?
4 Yohana alifungua barua yake ya pili kwa maneno haya:
“Mzee, kwa mama mteule na watoto wake niwapendao katika kweli; wala si mimi peke yangu, bali na wote waijuao ile kweli; kwa ajili ya hiyo kweli ikaayo ndani yetu, nayo itakuwa pamoja nasi hata milele.”—2 Yohana 1, 2.
5 Kufikia mwisho wa karne ya kwanza W.K. mtume Yohana alikuwa “mzee” kweli kweli, maana alikuwa na umri wapata miaka 100 na pia alikuwa mzee mwenye ukuzi au umri mpevu sana wa kiroho. (Linganisha Wagalatia 2:9.) Kwa kumwambia maneno hayo yule “mama mteule,” labda alikuwa akimaanisha kundi fulani lililokuwa mahali fulani pasipofichuliwa wazi, na labda alitumia maneno hayo kuvuruga akili za watesi ili wasijue mahali hapo. Kama ni hivyo, “watoto” wa mama huyo walikuwa ni watoto wa kiroho, washiriki wa kundi hilo na Wakristo waliozaliwa kwa roho na wakawa ‘wameteuliwa’ na Mungu kwa ajili ya mwito wa kimbingu. (Warumi 8:16, 17; Wafilipi 3:12-14) Kwa upande ule mwingine, neno Kyria (neno la Kigiriki la kusema “Bibi,” Mama) huenda likawa lilikuwa ni jina la mwanamke fulani mmoja Mkristo.
6. (a) “Ile kweli” aliyoitaja Yohana ni nini? (b) “Ile kweli” inakaaje katika Wakristo wa kweli na kubaki “milele” pamoja nao?
6 Vyo vyote iwavyo, huyo “mama mteule na watoto wake” walipendwa na Yehova kweli kweli, pia na mashahidi wale wengine wote wa Yehova waliokuwa wamepata kuijua “ile kweli.” “Kweli” hiyo ilikuwa ndio ujumla mzima wa mafundisho ambayo msingi wayo ulikuwa Yesu Kristo. Kuambatana sana nayo kulihitajiwa kabisa ili kupata wokovu. (Yohana 4:24; Waefeso 1:13,14; 1 Yohana 3:23) Sababu moja ya msingi inayoonyesha kwa nini mashahidi wa zamani na wa sasa wa Yehova wanapendana wao kwa wao ni kwamba wana upendo wa ujumla kwa “ile kweli.” ‘Inakaa ndani’ yao katika maana ya kwamba inaendelea kukaa katika mioyo yao. Kweli hiyo itakaa pamoja na Wakristo wa kweli wa namna hiyo “milele,” ikiwa mwenzi wao wa daima. Hiyo hakika ni mali yenye kuthaminiwa sana ya Mashahidi wa Yehova leo, nao wanamshukuru Baba yao wa kimbingu kwa sababu ya kweli hiyo.
7. Fadhili zisizostahilika, rehema na amani, yote hayo yanatokanaje na Mungu na Kristo pia?
7 Wale wanaoshikilia “ile kweli” kwa uaminifu wanahakikishiwa kupata baraka za kimungu. Akionyesha hilo wazi, mtume aliongeza hivi:
“Pamoja nasi kutakuwako fadhili, zisizostahilika, rehema na upendo kutoka kwa Mungu huyo Baba na kutoka kwa Yesu Kristo Mwana wa Baba huyo, pamoja na kweli na upendo.” (2 Yohana 3, NW)
Fadhili zisizostahilika zinatokana na wote wawili, Yehova na Yesu, katika maana ya kwamba wanadamu wenye dhambi “wanaendelea sasa kutangazwa kuwa wenye haki kwa fadhili zisizostahilika [za Mungu] kupitia kuwekwa huru kwa ukombozi uliolipwa na Kristo Yesu.” (Warumi 3:23, 24, NW) Vivyo hivyo, Baba wa kimbingu ndiye Chanzo cha rehema, lakini rehema hiyo inafikia wanadamu wasio wakamilifu kupitia Kristo. (Waebrania 4:14-16; Yuda 20, 21) Tena, ili wawe na amani pamoja na Yehova, watenda dhambi wanahitaji kulipiwa malipo kwa makosa yao, na jambo hilo limewezeshwa kupitia kufa kwa Yesu akiwa dhabihu ya ukombozi.—Wakolosai 1:18-20.
8. Kwenye 2 Yohana 3, ni nini kinachoweza kuwa kilimaanishwa na maneno “pamoja na kweli na upendo”?
8 Yohana aliongeza maneno “pamoja na [au, “katika”] kweli na upendo.” (Kingdom Interlinear Translation) Hivyo huenda akawa alikuwa akisema kwamba Wakristo wa kweli wanafurahia fadhili zisizostahilika, rehema na amani “pamoja na kweli na upendo.” Au inaweza kuwa Yohana alimaanisha kwamba watumishi wa Yehova wangepata baraka hizo wakibaki katika ile kweli na kuendelea kuonyesha upendo.
‘Kuenenda Katika Kweli na Upendo’
9, 10. (a) Kwa sababu gani Yohana alikuwa na sababu ya ‘kufurahi mno’? (b) Kwa habari ya ile kweli, “baadhi ya’’ watu fulani walikuwa wakifanya nini?
9 Mtume alitaja sababu ya kuwa na furaha ya kibinafsi na pia akatoa onyo la upole lenye kufaa alipoongeza hivi:
“Nalifurahi mno kwa kuwa nimewaona baadhi ya watoto wako wanaenenda katika kweli, kama vile tulivyopokea amri kwa Baba. Na sasa, mama, nakuomba, si kwamba nakuandikia amri mpya, bali ile tuliyokuwa nayo tangu mwanzo, kwamba tupendane.”—2 Yohana 4, 5.
10 Yohana alikuwa na sababu ya kuwa na furaha kubwa kwa sababu “baadhi ya” watu fulani walikuwa “wanaenenda katika kweli.” Walikuwa na imani katika jina la Yesu Kristo, wakawa wanapendana na kujitahidi sana kujipatanisha na kiolezo kilichowekwa na Mwana wa Mungu. (Waebrania 12:1-3; 1 Yohana 3:23) Ikiwa Yohana alikuwa anamwandikia mwanamke mwenye kuitwa Kyria (Kiria), basi wengine wa watoto wake wa uzazi wa asili walikuwa katika ile kweli. Lakini ikiwa alikuwa akitumia maneno “watoto” na “mama mteule” kwa usemi wa mfano, angeweza kufurahi sana kwamba washiriki wengine wa kundi la mahali hapo pasipofichuliwa walikuwa wameupinga sana uasi wa imani na walikuwa wakiambatana ile kweli na kufuatia maisha ya uaminifu kwa Yehova. Kwa kweli, mashahidi Wakristo wa Yehova walio washikamanifu wamechukua sikuzote kushikilia ile kweli, au ‘kuenenda katika’ hiyo, kuwa wajibu wanaopaswa kutimiza. Kwao, hiyo ni amri ya Baba yao wa kimbingu, nao hawaoni ni mzigo kuishika.—Linganisha 1 Yohana 5:3.
11. (a) Kuishika amri ya ‘kupendana’ kulihitaji nini’ (b) Kwa sababu gani Yohana angeweza kusema kwamba hiyo ‘haikuwa amri mpya’?
11 Mtume alimwomba yule “mama” ashike ile amri ya “kwamba tupendane.” (Linganisha 1 Yohana 3:11.) Akieleza mapenzi ya Yehova kwa watu wenye kumcha Mungu, Yesu alikuwa amewaamuru wanafunzi wake ‘wapendane kama alivyokuwa amewapenda.’ Amri hiyo haikutaka wawe na upendo wa jirani tu bali pia upendo wa kujinyima, kufikia hatua ya kutoa uhai kwa ajili ya mtu na mwenzake. (Mambo ya Walawi 19:18; Mathayo 22:39; Yohana 10:14, 15; 13:34; 15:13) Amri hiyo ilikuwa imekuwa yenye kupasa kufuatwa na wafuasi wa Kristo “tangu mwanzo” wa uhusiano wao pamoja na Mungu wa kujiweka wakf—ndiyo, tangu Yesu alipoitoa mara ya kwanza na bila shaka tangu mwanzo wa kundi la Kikristo kwenye Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K. Basi, katika maana hiyo ‘haikuwa amri mpya,’ kama Yohana alivyosema.
12. Yohana alimaanisha nini alipokuwa akisema: “Hii ndiyo ile amri . . . mwenende [mwendelee kutembea, NW] katika hiyo”?
12 Akielekeza kwenye upendo, Yohana aliongeza hivi:
“Na huu ndio upendo: tuenende kwa kuzifuata amri zake. Hii ndiyo ile amri, kama mlivyosikia tangu mwanzo kwamba mwenende [mwendelee kutembea,NW ] katika hiyo.” (2 Yohana 6)
Waabudu wa kweli wanamtii Yehova kwa furaha kwa sababu wanampenda kwa moyo wao wote, nafsi yote, nguvu zote na akili yote. (Luka 10:27) “Tangu mwanzo,” yaani, tangu wakati wa huduma ya Yesu au tangu walipojiweka wakf kwa Mungu, “watu” ambao Yohana aliandikia walikuwa wamekuwa na ile amri inayohusu upendo. Lakini mtume alimaanisha nini aliposema, “Hii ndiyo ile amri . . . mwenende [mwendelee kutembea, NW] katika hiyo”? Ingawa neno “hiyo” lingeweza kumaanisha ile “amri” inayohusu upendo (The New English Bible), inawezekana kuwa kinachomaanishwa na neno hilo ni “upendo” wenyewe. Hata neno hilo likichukuliwa kwa yo yote ya njia hizo mbili, ‘kuendelea kutembea katika hiyo’ kulimaanisha kuendelea kuonyeshana upendo.—1 Yohana 3:18; linganisha Warumi 13:8-10.
Jihadhari na Waasi wa Imani
13. (a) Ni kati ya akina nani “wadanganyifu” walikuwa wakijaribu kujipatia waongofu? (b) Ni fundisho gani la uongo lililokuwa likienezwa na “wadanganyifu” nao?
13 Jitihada ingetakwa ili kuendelea kutembea katika upendo na kweli. Akieleza sababu, Yohana aliandika hivi:
“Kwa maana wadanganyifu wengi wametokea duniani, wasiokiri ya kuwa Yesu Kristo yuaja katika mwili. Huyo ndiye yule mdanganyifu na mpinga Kristo.” (2 Yohana 7)
Kwa wazi, walimu fulani wa uongo walikuwa wamekuwa wakitanga-tanga kujaribu kujipatia waongofu kati ya Wakristo wa kweli. (Linganisha Matendo 20:30.) Ingawa wao wenyewe walidai kuwa ni Wakristo, “wadanganyifu” hao wenye kupoteza watu hawangekiri (kukubali) kwamba Yesu Kristo alikuwa amekwisha kuja akiwa na mwili kama binadamu. Mafundisho kama hayo ya uongo yangepunguza cheo cha Yesu cha kuwa Masihi na mkombozi, kutia ndani cheo chake cha kimbingu cha kuwa katika hali ya utukuzo.—Marko 1:9-11; Yohana 1:1, 14; Wafilipi 2:5-11.
14. Kwa sababu gani Yohana aliwaita hao waasi wa imani “yule mdanganyifu na mpinga Kristo”?
14 Yohana aliwaita waasi hao wa imani “yule mdanganyifu na mpinga Kristo” kwa sababu mafundisho yao yalikuwa ya udanganyifu na wao wenyewe walikuwa wakimpinga Kristo. Mtajo wa mtume wa “wapinga Kristo wengi” unaonyesha kwamba walikuwako maadui wengi mmoja mmoja wa Kristo, ingawa kwa ujumla wote wangeweza kuwa kama mtu mmoja mwenye kuitwa “mpinga Kristo.” (1 Yohana 2:18) Kukana kwamba Yesu siye Kristo wala Mwana wa Mungu kunatia ndani kukana fundisho lo lote au mafundisho yote ya Maandiko yanayomhusu. Mashahidi waaminifu wa Yehova wanayakataa kabisa kabisa maoni ya walimu waongo wa namna hiyo.
15. (a) Kwa ‘kujiangalia’ nafsi zao, ni “thawabu timilifu” gani ambayo Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho wangepata? (b) Kwa sababu gani inampasa kila shahidi wa Yehova ajihadhari na mafundisho ya kuasi imani?
15 Kwa kuwa kulikuwa na hatari ya kugeuziwa kando na kuiacha kweli ili kuingilia uasi wa imani, Yohana alihimiza hivi:
“Jiangalieni nafsi zenu msiyapoteze [yale ambayo tumefanyia kazi kuyazaa, NW] bali mpokee thawabu timilifu. Kila apitaye cheo, wala asidumu katika mafundisho ya Kristo, yeye hana Mungu. Yeye adumuye katika mafundisho hayo, huyo ana Baba na Mwana pia.” (2 Yohana 8, 9)
Kupitia kazi ngumu kama vile kuhubiri “habari njema,” Yohana na wengine walikuwa ‘wameyazaa’ matunda yaliyofanya wapokeaji wa kwanza kabisa wa barua hii waongolewe. Lakini ni kwa ‘kujiangalilia wenyewe nafsi zao’ tu wangeweza kuepuka ‘kupoteza’ fadhili zisizostahilika, rehema na amani kutoka kwa Yehova na Mwanaye, na pia uenzi wenye kudumu pamoja na wale wanaofunganishwa pamoja katika kweli na upendo. Kama wangekuwa waaminifu, waamini wenzi wa Yohana waliotiwa mafuta kwa roho wangeendelea kufurahia kumtolea Yehova utumishi wenye kuthawabisha. Kwa kunena habari za “thawabu timilifu,” ni wazi kwamba Yohana alitaka kutia ndani “taji” ya kimbingu inayopokewa na Wakristo washikamanifu waliotiwa mafuta. (Ufunuo 2:10; 1 Wakorintho 9:24-27; 2 Timotheo 4:7, 8; Yakobo 1:12) Bila shaka, inampasa kila shahidi wa Yehova akatae mafundisho ya kuasi imani kwa sababu yanaweza kumnyang’anya uzima wa milele ama katika mbingu ama katika dunia.
16. (a) Wale waasi wa imani walikuwaje ‘wakipita cheo’? (b) Ni kwa njia gani mashahidi waaminifu wa Yehova wana “Baba na Mwana pia”?
16 “Wadanganyifu” hao wenye kuasi imani ‘walikuwa wakipita cheo’ wala ‘hawakudumu katika mafundisho ya Kristo’ kwa sababu hawakukwama kwenye ile kweli iliyofunzwa na Yesu na mitume wake waaminifu. Kwa hiyo, hao wapinganisha-imani ‘hawakuwa na Mungu,’ kwa maana hawakuwa katika mwungano pamoja na Yehova wala hawakuwa na uhusiano pamoja naye. (1 Yohana 1:5, 6; 2:22-25) Lakini, mashahidi waaminifu wa Yehova ‘wanakiri ya kuwa Kristo alikuja katika mwili,’ kwa maana wanajizoeza imani katika dhabihu ya ukombozi wake na wanakwama kwenye mambo yaliyofunzwa na yeye na mitume wake washikamanifu. (Mathayo 20:28; 1 Timotheo 2:5, 6; 2 Yohana 7) Wakristo hao wa kweli wanaambatana na ile kweli na basi wao ‘wana Baba na Mwana pia’ kwa sababu ya kuwajua, kuzithamini sifa zao na kuendelea kufurahia uhusiano wa kindani pamoja nao.
Nia ya Kuwa Nayo Kuelekea Waasi wa Imani
17. Kulingana na 2 Yohana 10, 11, Wakristo washikamanifu wangewatendeaje “wadanganyifu” hao?
17 Wakristo wanapaswa kuwa wakaribishaji, lakini si kuelekea waasi wenye kuiacha imani ya kweli. (1 Petro 4:9) Yohana alifahamiza wazi jambo hilo kwa kusema:
“Mtu akija kwenu, naye haleti mafundisho hayo, msimkaribishe nyumbani mwenu, wala msimpe salamu. Maana yeye ampaye salamu azishiriki kazi zake mbovu.” (2 Yohana 10, 11)
“Wadanganyifu” hao walikuwa wakitanga-tanga na kueneza mafundisho ya uongo kwa bidii. Bila shaka, lingalikuwa kosa kwa Mkristo ye yote aliye wakf kunyosha mkono wa ushirika kwa kuwaruhusu walimu wa uongo hao waingie nyumbani mwake. Isingalifaa pia kuwapa waasi wa imani salamu yo yote, iwe ilikuwa ni ya kuwakaribisha wafikapo au ya kusema “Kwa heri ya kuonana, Mungu akujalie” wakati wa kuondoka kwao (Authorized Version) Hakuna Mkristo mshikamanifu angemtakia mafanikio ya kazi mtu anayeendeleza mafundisho ya uongo kwa makusudi. Basi, kwa uhakika hakuna shahidi mwaminifu wa Yehova ambaye angeshirikiana kirafiki na mtu wa namna hiyo.—1 Wakorintho 5:11-13.
18. Kwa sababu gani haingempasa shahidi ye yote wa Yehova aliye mshikamanifu kusalimu mwasi wa imani?
18 Zaidi ya hilo, mtumishi wa Yehova aliye wakf akimkaribisha mwalimu mdanganyifu wa namna hiyo nyumbani mwake, angekuwa ni “msaidizi” katika “matendo maovu” ya mtu huyo. (The New English Bible) Basi, hakuna shahidi wa kisasa wa Yehova ambaye angesalimu mwasi-imani aliyetengwa na ushirika au aliyejitenga mwenyewe wala kumruhusu atumie nyumba yake ya Kikristo kama mahali ambapo ni makao yake ya kuenezea makosa ya mafundisho. Kwa hakika, mwamini angekuwa na wajibu wa kumtolea Mungu jibu kubwa kama angempa ukaribishaji mtu mwenye kuasi imani na kama tendo hilo lingeleta kifo cha kiroho cha mwabudu mwenzake wa Yehova.—Linganisha Warumi 16:17, 18; 2 Timotheo 3:6, 7.
19. Mashahidi washikamanifu wa Yehova wanachukua msimamo gani kuhusu waasi wa imani wa kisasa?
19 Watu fulani ambao wakati mmoja walitumikia wakiwa Mashahidi wa Yehova wamekataa maoni mbalimbali ya Kimaandiko ambayo msingi wayo ni mafundisho ya Yesu Kristo na mitume wake. Kwa mfano, wanasisitiza ya kwamba hatuishi katika “siku za mwisho,” ijapokuwa kuna ushuhuda mwingi ajabu wa kuonyesha tunaishi katika siku hizo. (2 Timotheo 3:1-5) Waasi hao wa imani ‘wametoka kwetu kwa sababu hawakuwa wa kwetu.’ (1 Yohana 2:18, 19) Kwa hiyo, hawana tena ushirika pamoja na mashahidi washikamanifu wa Yehova waliotiwa mafuta wala pamoja na wenzi wa hao, na basi wapinganisha-imani hao wenye kujitafutia faida zao wenyewe hawana “ushirika” pamoja na Baba na Mwana, hata kama watajisifu majisifu makubwa namna gani wakisema wana uhusiano wa kindani pamoja na Mungu na Kristo. Badala ya hivyo, wao wamo katika giza la kiroho. (1 Yohana 1:3, 6) Ni lazima wapendao nuru na kweli wachukue msimamo imara kupinga watu hawa wenye kuendeleza mafundisho ya uongo. Kwa vyo vyote mashahidi washikamanifu wa Yehova hawataki kuwa wasaidizi katika “matendo maovu” ya watu hao wasio waaminifu kwa kuunga mkono maneno na matendo yao ya kutomcha Mungu. Bali, acheni ‘tupigane kwa ajili ya imani ambayo Mungu amewajalia watu wake [watakatifu, NW] mara moja tu kwa wakati wote.’—Yuda 3, 4, 19, HNWW.
Ambatana na Ile Kweli
20. Badala ya kuendelea kuandika, Yohana alitumainia kufanya nini?
20 Alipokwisha kuwahimiza waamini wenzake wakatae uasi wa imani na kuambatana na ile kweli, Yohana alimalizia barua yake ya pili iliyoongozwa na Mungu kwa kusema maneno haya:
“Kwa kuwa ninayo mambo mengi, sitaki kuyaandika kwa karatasi na wino; lakini nataraji kuja kwenu, na kusema nanyi mdomo kwa mdomo, ili furaha yetu iwe imetimizwa. Watoto wa ndugu [dada, NW] yako aliye mteule, wakusalimu.” (2 Yohana 12, 13)
Mtume aliona ni afadhali asikiandike kile ambacho bado alikuwa nacho moyoni. Kwa hiyo aliiweka kando karatasi yake ya mafunjo, kalamu ya matete na wino yake (inaelekea kuwa ilikuwa mchanganyiko mweusi wa gundi, masizi na maji). Ijapokuwa alikuwa mzee sana, yeye alitumainia kuwatembelea na kuongea nao “ana kwa ana” (NW), au, kwa uhalisi, “mdomo kwa mdomo,” na hivyo wafurahie upashanaji-habari wa kindani. (Linganisha Hesabu 12:6-8.) Ziara ya huyo mtume mzee kwa uhakika ingetokeza ubadilishanaji wenye kuthawabisha kiroho wa kitia-moyo, pamoja na upendezi tele.—Linganisha Warumi 1:11, 12.
21. Ni nini kilichoonekana wazi katika maneno ya kumalizia ya Yohana wa Pili?
21 Upendo wa Kikristo unaofunganisha waabudu wa Yehova pamoja ulionekana wazi katika salamu ambazo Yohana alipeleka. Ikiwa alikuwa akiandikia mtu mmoja mwenye kuitwa Kiria, inaonekana kwamba mama huyo alikuwa na dada wa kimwili ambaye watoto wake wa uzawa wa asili walimpelekea salamu zao za kumtakia mafanikio. Lakini ikiwa mtume alikuwa akilitaja kundi jingine bila kusema wazi (labda lile la huko Efeso), basi “ndugu” (dada) aliyemtaja ni kundi hilo kwa ujumla na “watoto” ni washiriki mmoja mmoja wa kundi hilo.
22. (a) Barua ya pili ya Yohana iliyoongozwa na Mungu inasaidia Mashahidi wa Yehova kufanya nini? (b) Ni jambo gani ambalo bado linahitaji mazungumzo?
22 Katika barua yake ya pili yenye kuongozwa na Mungu, Yohana alikuwa ametoboa mambo waziwazi kwa kutoa mashauri ya upendo ambayo yangesaidia waamini wenzake wakatae uasi wa imani na kuambatana na ile kweli. Kwa msaada wa Mungu, Mashahidi wa Yehova wa leo wamejipiga moyo konde (wamejikaza) wafanye lilo hilo. Lakini ni lazima pia tuendeleze faida za Kikristo tukiwa “watenda kazi pamoja” wenye ushirikiano. (3 Yohana 8) Jambo hilo linawezekanaje?
Wewe Unaweza Kujibu?
□ Maana yake nini ‘kuenenda katika ile kweli’?
◻ “Wadanganyifu” walikuwa wakieneza fundisho gani la uongo?
◻ Kulingana na 2 Yohana 10, 11, Mashahidi wa Yehova wanapaswa kuwa na maoni gani juu ya waasi wa imani
[Picha katika ukurasa wa 11]
Sikuzote mashahidi washikamanifu wa Yehova wameukataa uasi wa imani