Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 9/15 kur. 7-13
  • Iko Wapi Ile Kweli Inayoweza Kutuweka Huru?

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Iko Wapi Ile Kweli Inayoweza Kutuweka Huru?
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Matumaini Yasiyotegemea Kweli
  • Kuijaribu “Kweli” ya Kidini
  • Kumtumaini Yule Mungu wa Kweli
  • Watu Huru Lakini Wanaotakwa Watoe Hesabu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Je! “Utaratibu wa Ulimwengu Mpya” wa Mwanadamu U Karibu?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Usikose Kusudi la Uhuru wa Kupewa na Mungu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Acha Yehova Akuongoze Kupata Uhuru wa Kweli
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2012
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 9/15 kur. 7-13

Iko Wapi Ile Kweli Inayoweza Kutuweka Huru?

“Yesu akawaambia . . . Mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.”​—YOHANA 8:31, 32.

1. Ni mauhuru gani yaliyo kati ya yale ambayo watu katika ulimwengu huu wanatamani kuwa nayo?

UHURU! Neno hilo limesisimua akili na mioyo ya watu muda wa karne nyingi! Vita vimepigwa kutafuta uhuru. Mamilioni ya watu wamekufa wakipigania uhuru. Wengi wana maoni kama ya mwanataifa Mwamerika Patrick Henry aliyetangaza hivi miaka zaidi ya 200 iliyopita: “Kama hutaki kunipa uhuru basi nipe kifo.” Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, Rais Franklin D. Roosevelt alidai kuwe na “mauhuru manne”: uhuru wa kusema, uhuru wa kuabudu, uhuru wa kutokuwa na ukosefu wa vifaa, na uhuru wa kutokuwa na woga.

2, 3. Ni lazima kitu gani kiwe katika uhuru wa kweli?

2 Hata hivyo uhuru wa kweli, katika maana ya ndani zaidi, ni lazima utie ndani mambo zaidi ya hayo. Kwa mfano, je! wo wote wa mauhuru hayo unaweza kutuletea uhuru wa kutokamilika kwa kibinadamu? Je! yanaweza kutuletea uhuru wa kutokuwa na magonjwa? Tena, hata mtu awe ana afya ya kiasi gani, bado anaelekeana na tatizo la kwamba, baada ya muda fulani, watu wanazeeka na kufa. Je! kuna lo lote la kufurahia huko kaburini? Biblia inajibu hivi: “Wafu hawajui neno lo lote.” Ndiyo sababu inasema hivi pia: “Ni afadhali mbwa aliye hai kuliko simba aliyekufa.”​—Mhubiri 9:4, 5.

3 Ili tuwe na uhuru kamili kabisa, ni lazima utumwa wa kutokamilika, magonjwa na kifo uondolewe kabisa kati yetu. Na tena, tunahitaji kuondolewa umaskini, uonezi, uhalifu, chuki na vita, yale mambo mabaya sana ambayo yamekuwako kwa wingi sana nyakati zilizopita. Lakini ni nani anayeweza kutupa sisi uhuru wa namna hiyo? Je! wewe unamjua daktari ye yote anayeweza kutoa uhakikisho thabiti kwamba atakuponya ugonjwa wa kansa, ugonjwa wa moyo, na magonjwa yale mengine yote? Je! kuna mwanasayansi ye yote anayeweza kukuzuia usizeeke na kufa, au akurudishe kwenye uzima ukiisha kufa? Je! wewe unamjua kiongozi ye yote wa siasa anayeweza kutoa uhakikisho thabiti kwamba dunia itakuwa na amani, iwe na uhuru wa kutokuwa na vita hata milele? Je! kuna meya ye yote au mkuu wa polisi katika mji wo wote wa ulimwengu anayeweza kukupa uhakikisho thabiti kwamba kutakuwako uhuru wa kukosa uhalifu? Ni mfumo gani wa mambo ya kiuchumi unaoweza kutokeza uhuru wa kutokuwa na umaskini, hali ya kukosa kazi au infuleshoni, kisha umpe kila mtu ufanisi wa kweli​—daima dawamu?

4. Ni lazima uhuru wa kweli utegemee nini?

4 Ikiwa kuna tumaini lo lote kwamba hali nyingi zilizo mbaya ambazo sasa zimewazunguka sana wanadamu zinaweza kuondolewa kabisa, ni lazima njia ya kuziondoa iwe inaitegemea ile kweli. Uhuru wa kweli hauwezi kutegemea madanganyo wala uongo. Hivyo, mtu ye yote, awe ni kiongozi wa ulimwengu, mwanasayansi, mwanauchumi au kiongozi wa dini, akitoa maoneleo yake juu ya kitu kitakachoyaleta mauhuru ambayo yametamaniwa kwa muda mrefu, ni lazima ulizo hili liulizwe: Je! yeye anasema ile kweli? Nao wanadamu wamekuwa na muda mrefu sana wa kuona kama maoneleo, ahadi na jitihada za wanadamu zimepatana na ile kweli.

Matumaini Yasiyotegemea Kweli

5. Ni kwa kadiri gani tumaini la kupata uhuru wa kutokuwa na magonjwa limetimizwa?

5 Kwa mfano, miongo fulani ya miaka iliyopita watu wengi walidhani kwamba kwa sababu ya elimu ya tiba kuongezeka wanadamu wangewekwa huru na magonjwa. Ingawa kumekuwako maendeleo fulani katika mambo ya dawa, je! yameleta uhuru wa kutokuwa na magonjwa? Hapana, kwa maana mapigo makubwa kama ugonjwa wa kansa na moyo yameua watu wengi sana, sana. Pia, wakati fulani ilidhaniwa kwamba magonjwa ya kisonono na kaswende yangemalizwa nguvu na dawa mpya ‘zenye kufanya maajabu.’ Lakini kichapisho cha Kiingereza kinachoheshimiwa, kinachohusiana na tiba, yaani The Lancet, kinataarifu hivi: “Tengenezo la Afya Ulimwenguni limekata kauli kwamba kuna visa vipya vipatavyo milioni 250 vya kisonono na visa vipya milioni 50 vya kaswende kila mwaka. Magonjwa mengine yanayopokezanwa kupitia ngono yanaweza kuwa yakitukia kwa wingi hata zaidi.”​—Linganisha Mithali 7:10, 21-23.

6. Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba sayansi na ufundi wa viwandani vimekatisha watu tumaini?

6 Namna gani, pia, juu ya yale matumaini makuu yaliyotolewa na wanasayansi na wanaviwanda ili kusisimua watu karne moja au mbili zilizopita? Kwa mfano, motakaa ilishangiliwa kuwa uvumbuzi mkubwa, na kweli kwa njia fulani ulikuwa uvumbuzi mkubwa. Lakini imesaidia kula sana miji mikubwa msongamano wa magari, kelele na uchafu wa hewa. Ulimwenguni kote watu zaidi ya 200,000 wanauawa na aksidenti za magari, na mamilioni wanaumizwa kila mwaka! Masikitisho yenye kuletwa na ufundi wa tekinolojia yalitajwa na Orville Wright, mmoja wa wavumbuzi wa ndege. Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili alimwandikia Henry Ford maneno yafuatayo: “Wilbur na mimi tulidhani ndege ingeharakisha kuleta amani ya ulimwengu. Kufikia sasa inaonekana imefanya kinyume. Mimi nafikiri wakati wewe ulipotafuta njia ya kuzidisha magari​—na huo ulikuwa mmoja wa mavumbuzi makuu ya vizazi vingi​—hukufikiri sana kwamba uvumbuzi huo ungetumiwa . . . kutengeneza vifaru vya kuharibu ulimwengu. Inaonekana kwamba hakuna kitu chenye faida kinachoweza kuanzishwa na kikose kutafutiwa matumizi mabaya sana na mtu fulani.”

7. Je! wo wote wa mifumo ya kibiashara ya ulimwengu huu unaweza kuletea watu wote ufanisi?

7 Je! baada ya karne zote za kufanya majaribio ya mifumo mbalimbali ya uchumi, kumepatikana angaa namna moja ya uchumi iliyo imara na yenye kuletea watu wote ufanisi wa daima? Hapana, kwa sababu ukosefu wa uthabiti katika uchumi umeenea sana leo. Ni kama vile Jack Weldon, profesa wa hali za uchumi wa Chuo Kikuu cha McGill huko Montreal, alivyotamka: “Mwanauchumi ye yote aliye hodari na mnyofu wa kusema kweli atakubali kwamba kwa uhakika hatujui kuyatatua matatizo makubwa yanayokabili sasa mengi ya mataifa makubwa yaliyo na viwanda vingi.” Hali ni mbaya zaidi katika mataifa yasiyo na maendeleo mengi. Katika nchi moja ya namna hiyo, gazeti Time linataarifu kwamba ‘wanaishi watoto zaidi ya milioni 2 ambao wametorokwa na wazazi wasio na riziki ya kuwapa na kuna milioni 14 wengine wanaoishi katika umaskini mwingi sana kiasi cha kwamba wazazi wanaona ni afadhali zaidi kuwatoroka. Katika sehemu nyingine ya ulimwengu gazeti Philippine Daily Express lilisema: “Karibu nusu bilioni [milioni 500] ya Waasia wanakadiriwa kuwa miongoni mwa watu ‘walio maskini kabisa kabisa’ na hesabu yao itaelekea kuongezeka zaidi.”

8. Ni kwa kadiri gani demokrasi imeletea raia za nchi usalama wa kibinafsi?

8 Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilisemwa kwamba vita hiyo ilikuwa ikipigwa ili ‘kuufanya ulimwengu uwe salama kwa ajili ya demokrasi.’ Leo, ni nchi chache zenye demokrasi. Hata mahali ambako demokrasi inasemwa inatawala, raia wa huko wako salama kadiri gani? Katika United States, moja kati ya kila jamaa tatu inapatwa na namna fulani ya uhalifu. Hakimu Mkuu wa Mahakama Kuu Zaidi, Warren Burger, alitamka hivi: “Tunakaribia hali ya kuwa jamii ya watu walio hoi kabisa​—jamii yenye uwezo mchache sana wa kudumisha usalama wa kiasi kidogo tu barabarani, shuleni, na katika nyumba za watu wetu.” Akaongezea: “Kwa muda wa miaka 10 iliyopita, wengi wa viongozi wetu wa kitaifa na wale wa nchi zile nyingine wamekuwa wakisema juu ya uharamia wa kimataifa. Lakini kawaida ya maisha yetu, uharamia wa kila siku katika karibu mji wo wote mkubwa wa United States unazidi hesabu ya misiba yote inayoripotiwa kutendwa na ‘maharamia wa mataifa yote’ katika muda wa mwaka wo wote.”​—Linganisha Mhubiri 8:11.

9. Katika karne hii, kulitukia nini kwa yale matabiri ya kwamba vita vingekoma?

9 Vita ya Ulimwengu ya Kwanza ilielezwa huko nyuma kuwa “ile vita ya kukomesha vita vyote.” Kitabu Encyclopedia Americana kinasema: “Wakati wa vita wanasiasa na wanamagazeti walisema siku zijazo zingekuwa za mambo mazuri sana, kwamba kusingekuwa tena na vita, silaha, mizozo kati ya mataifa.” Lakini mambo yakawa kinyume kabisa. Kichapisho cha Afrika Kusini, The Natal Mercury, kilisema majuzi hivi: “Rais Woodrow Wilson aliieleza Vita ya Ulimwengu ya Kwanza kuwa ‘ile vita ya kuvikomesha vita vyote.’ Utabiri wake ungalikuwa sahihi sana kama [ingalikuwa imeitwa] ‘vita ya kukomesha amani.’ “Makala hiyo iliongezea hivi: “Tangu mwaka wa 1914 ulimwengu labda umepatwa na jeuri nyingi na msukosuko mwingi zaidi ya wakati mwingineo tangu historia ilipoanza kuandikwa.” Gharama zinazotokana na utayarishaji wa vifaa vya vita ulimwenguni pote zilipanda zikawa dola zaidi ya bilioni 500 sasa, kila mwaka. Leo mataifa yana silaha za nyukilia zinazotosha kufagilia mbali miji mikubwa zaidi ya milioni moja, na hesabu ya miji iliyoko haifikii idadi hiyo.

10. Kweli ni nini kuhusu maendeleo yo yote yaliyofanywa katika pande mbalimbali za jitihada za kibinadamu?

10 Hapana, ukweli ni kwamba maendeleo yo yote ambayo yamefanywa katika pande mbalimbali za utaalamu hayakuweka wanadamu huru kutokana na mambo yanayowafanya watumiwe vibaya kwa faida ya wengine, wataabike, wawe maskini, watendwe uhalifu, kuwe na vita, woga, magonjwa na kifo. Hivyo, madai, ahadi na maoneleo ya viongozi wa ulimwengu hayakuitegemea kweli, kama ushuhuda wa karne nyingi unavyoonyesha wazi. Kweli iko sawa na vile Biblia inavyosema kwenye Petro wa Pili 2:19: “Wakiwaahidia uhuru, nao wenyewe ni watumwa wa uharibifu.”

Kuijaribu “Kweli” ya Kidini

11. Ili ionekane kama madai ya kidini ni ya kweli, ni jaribu gani linaloweza kufanywa?

11 Zaidi ya sisi kuhitaji uhuru tutoke katika hali zenye kutaabisha sana leo, tunahitaji pia kuwekwa huru kutoka utu-mwa wa akilini unaoletwa na mafundisho ya uongo ya kidini. Hata hivyo dini za Jumuiya ya Wakristo na za sehemu ile nyingine yote ya ulimwengu zinashindania kwamba imani zao ndizo kweli. Ni rahisi kudai hivyo, lakini mambo ya hakika yanaonyesha nini? Kumbuka Neno la Mungu linasema: “Imani pasipo matendo imekufa.” (Yakobo 2:26) Pia, Yesu Kristo alitamka hivi: “Jihadharini na manabii wa uongo, watu wanaowajia wamevaa mavazi ya kondoo, walakini kwa ndani mbwa-mwitu wakali. Mtawatambua kwa matunda yao.” Ndiyo, mifumo ya dini inaweza kutambuliwa kuwa ya kweli au ya uongo kutokana na mazao, wala si kutokana na madai inayoyatamka tu. Juu ya ile ya uongo, Yesu alionya hivi: “Kila mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni.”​—Mathayo 7:15-20.

12. Hali ya dini za ulimwengu huu zinafunua nini?

12 Ikiwa dini inaiwakilisha ile kweli, tunda lililo dogo zaidi inalopaswa kuzaa ni kuwa dini yenye kani (nguvu) ya kuunganisha wale wanaoifuata. Yesu alisema wale walio na ile kweli “wote wawe na umoja.” (Yohana 17:21) Neno la Mungu linasema hivi pia: “Nyote mnene mamoja.” “Pasiwe kwenu faraka.” “Mhitimu katika nia moja na shauri moja.” (1 Wakorintho 1:10) Hivyo ndivyo wanavyopaswa kuwa wale wanaomwakilisha Mungu kweli kweli, kwa maana “Mungu si Mungu wa machafuko, bali wa amani.” (1 Wakorintho 14:33) Hata hivyo dini za ulimwengu huu zimegawanyika katika maelfu ya madhehebu mbalimbali, na kuna mafundisho na mazoea yenye kupingana ambayo mara nyingi yanaendeshwa katika dini ile ile moja, si katika dini zilizo tofauti-tofauti tu. Mchafuko na makosa hayo haungeweza kuwa umetokana na Mungu. Gazeti la kikanisa katika Australia, Leader’s Vision, lilikubali wazi hivi: ‘Kuishi katika hali ya kukosa umoja ni kuwako katika hali ya dhambi ya kibiblia. Tunaonyesha wazi kwamba tunaikana kazi ya Roho Mtakatifu.’

13. (a) Ukosefu wa umoja katika dini ya uongo umekuwa na matokeo gani? (b) Basi, hiyo dini ya uongo imetoka wapi?

13 Uthibitisho zaidi wa kwamba dini hizo haziwezi kuiwakilisha kweli, na kwamba haziwezi kuwa zimetoka kwa Mungu, unatokana na matokeo ya kukosa umoja. Ikiwa dini inafundisha kweli, jambo la kwanza ni kwamba angalau washiriki wake hawapaswi kuuana. Wakiuana wao kwa wao, hiyo ingekuwa ni kweli ya aina gani, udugu wa aina gani? Hata hivyo, historia inaonyesha kwamba watu wa dini ile ile moja kati ya dini mbalimbali za ulimwengu wameuana kwa ukawaida wakati wa vita. Wameuana kwa mamilioni kwa sababu tu walikuwa wakiishi katika nchi mbalimbali. Nyakati nyingine, watu wa dini ile ile moja hata wanauana ndani ya nchi ile ile moja, katika fujo za kiraia au mapinduzi. Kwenye 1 Yohana 3:10-12, Biblia inasema kwamba “watoto wa Ibilisi” ndio huua ‘ndugu’ zao. (Linganisha Mwanzo 4:8.) Watoto wa Mungu hawauani, bali wanakuwa na upendo usiovunjika kwa mmoja na mwenzake. Yesu alisema hivi waziwazi: “Hivyo watu wote watatambua ya kuwa ninyi mmekuwa wanafunzi wangu, mkiwa na upendo ninyi kwa ninyi.”​—Yohana 13:35.

14. Kwa kuitumia kanuni ya Yesu inayosema “kwa matunda yao,” kweli ni nini juu ya dini ya kilimwengu?

14 Hivyo, kwa matunda yao mabaya, ukosefu wa umoja, kupigana kwao na pia ufisadi wenye kuenea sana na unafiki unaoonekana sana katika dini za ulimwengu huu, inaonekana wazi kuwa sizo zinazowakilisha ile kweli​—hazimwakilishi Mungu. Hizo ni miti mibaya, yenye kuzaa mavuno yaliyooza. Ziko tayari ‘kukatwa zitupwe motoni.’

Kumtumaini Yule Mungu wa Kweli

15. Inatupasa tuweke tumainio letu kamili katika nani, na kwa sababu gani?

15 Kushindwa kwa wanadamu kuleta uhuru wa kweli katika mambo yaliyo ya maana maishani kunakazia yanayosemwa katika Biblia kwenye Yeremia 10:23: “Njia ya mwanadamu haimo katika nafsi yake; kuelekeza hatua zake si katika uwezo wa mwanadamu.” Hapana, Mungu hakuumba mwanadamu akiwa na uwezo au haki ya kutokutegemea mwelekezo wa Mungu na bado apate mafanikio. Hiyo ni sababu moja iliyofanya Mungu aruhusu mwanadamu ajitawale kwa maelfu mengi sana ya miaka, ili kuonyesha mara moja tu kwa wakati wote kwamba utawala wa kibinadamu hauwezi kuleta uhuru na furaha ya kweli. Ndiyo sababu Zaburi 146:3 inashauri kwa hekima hivi: “Msiwatumainie wakuu, wala binadamu ambaye hakuna wokovu kwake.” Basi tunaweza kutumaini nani? Biblia inajibu hivi: “Mtumaini [Yehova] kwa moyo wako wote, wala usizitegemee akili zako mwenyewe; katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyosha mapito yako.”​—Mithali 3:5, 6.

16. Tunaweza kuwa na uhakika gani katika Yehova?

16 Kwa sababu gani tunaweza kuweka matumaini kamili hayo katika Yehova? Kwa sababu, kama Zaburi 31:5 (NW) inavyosema, ‘Yehova ndiye Mungu wa ukweli.’ Ikiwa kweli tunataka kusikia ile kweli juu ya masuala yote ya maana maishani, na majibu kwa maulizo yanayofadhaisha hata viongozi wa ulimwengu, basi Mungu ndiye mwenye majibu hayo. Kwa kuwa “Mungu hawezi kusema uongo,” asemavyo ndivyo itakavyokuwa. “[Yehova] wa majeshi ameapa, akisema, Hakika yangu kama vile nilivyoazimia, ndivyo itakavyokuwa; na kama nilivyokusudia, ndivyo itakavyotokea.”​—Waebrania 6:18; Isaya 14:24.

17. Yehova amewatoleaje chanzo cha kweli wale wanaotafuta kweli kwa moyo mweupe?

17 Hakika Mungu anaweza kuwajulisha kweli zake wale wanaoitafuta kweli kwa moyo mweupe, kwa maana kwenye Yohana 8:23 Yesu alisema: “Tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru.” Pia alimwambia Mungu hivi katika sala: “Neno lako ndiyo kweli.” (Yohana 17:17) Ni wapi ambapo “neno” la Mungu, kweli yake, limeonyeshwa? Mtume Paulo anajibu: “Kila andiko limepewa kwa maongozi ya Mungu.” (2 Timotheo 3:16, ZSB) Muumba mweza yote wa ulimwengu mzima anadai kwa njia hiyo kwamba ndiye aliyeitunga Biblia. Kupitia kani ya utendaji wake yenye nguvu nyingi, au roho takatifu, yeye aliongoza wanaume waaminifu waandike mawazo yake. Kwa hiyo wakati tunapoyasoma Maandiko, ni kama kwamba Mungu anasema nasi.​—1 Wathesalonike 2:13; 2 Petro 1:20, 21.

18. Kwa sababu gani ni jambo lisilo la akili kufikiri kwamba si Mungu aliyeitunga Biblia?

18 Wengine wanasema Mungu siye aliyeitunga Biblia. Lakini wanadamu wanaweza kutunga vitabu na Mungu ndiye aliyewaumba wanadamu. Je! Muumba mkuu zaidi wa wanadamu ashindwe kufanya jambo linaloweza kufanywa na wanadamu duni? Kwa kutumia vifaa vya umeme, wanasayansi wanapeleka maagizo ili kuyapa masetilaiti (vyombo vyenye kuchunguza anga za juu) maagizo juu ya mambo yatakayofanya, na kuyaelekeza katika mwendo yatakayoufuata. Mtangazaji katika radio husema katika kikuza-sauti, kisha ujumbe wake unasikiwa maelfu ya maili huko mbali. Hata kutoka huko mwezini, picha za mambo yaliyotukia zinasafirishwa mpaka ndani ya nyumba zetu zionekane katika televisheni. Lakini Yehova ndiye aliyetengeneza sikio, jicho, umeme, sauti. Je! yeye hangeweza kutumia ‘nishati zake zenye nguvu nyingi’ apelekee watumishi wake duniani mawazo yake? Kwa uhakika, Muumba wa huu ulimwengu mzima wenye fahari ya ajabu angeweza kuumba kitabu!—Isaya 40:26, NW.

19. Kwa sababu gani Mungu alipoitunga Biblia alifanya sehemu fulani iwe ngumu kueleweka?

19 ‘Lakini,’ wengine wanasema, ‘Biblia ni ngumu kueleweka.’ Ndiyo, sehemu fulani ya Biblia ni ngumu. (2 Petro 3:16) kwa sababu gani Mungu aliitunga ikiwa hivyo? Ni kwa sababu yeye ndiye anayeamua ni nani ataipata ile kweli. Mtume Paulo alisema hivi juu ya kweli za Mungu: “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji; bali mwenye kukuza ni Mungu.” (1 Wakorintho 3:6) Paulo alitaja pia hekima ya Mungu na siri takatifu: “Ni kwetu sisi Mungu ameyafunua kupitia roho yake.” (1 Wakorintho 2:10, NW) Kwa njia hiyo Mungu anajiwekea mwenyewe haki ya kuwafunulia kweli zake wale tu wanaozitaka na ambao wana nia ya kuishi kulingana nazo na kumtumikia kwa uaminifu: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hatafanya hata jambo moja asipokuwa amefunua jambo lake la siri kwa watumishi wake.”​—Amosi 3:7, NW; Danieli 2:28, 47.

20. Iko wapi kweli inayoweza kutuweka huru?

20 Ndiyo, yuko Mungu wa ukweli. Kweli zake zinapatikana katika Neno aliloliongoza kwa roho yake, yaani, Biblia Takatifu. Yeye anawafunulia watumishi wake wanyenyekevu, waliounganishwa kwa umoja, ufahamu wa Maandiko matakatifu. Basi, je! ni kweli gani za maana kabisa zilizo katika Neno lake ambazo Mungu anawafunulia watafutaji wa ukweli hasa katika wakati wetu? Makala inayofuata itachunguza nyingine za kweli hizo.

Je! wewe unakumbuka mambo haya?

□ Ni uhuru gani ambao wanadamu wanahitaji kweli kweli?

□ Ni kwa njia gani matumaini ya ulimwengu huu yamekuwa ya kukatisha tumaini? Kwa sababu gani?

□ Tunaweza kutofautishaje dini ya kweli na ya uongo?

□ Kuna sababu gani za kutumaini Yehova kikamili?

□ Yehova anafunulia nani kweli zake?

[Picha katika ukurasa wa 8]

Wanadamu wana uhitaji mkubwa sana wa kuwekwa huru watoke katika hali nyingi zenye kuwataabisha sana

[Picha katika ukurasa wa 11]

Yesu alionya hivi juu ya dini ya uongo: “Kila mti usiozaa tunda zuri hukatwa ukatupwa motoni”

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki