Neno la Mungu Li Hai
Ufalme wa Mungu Utafanya Nini?
KATIKA Mahubiri juu ya Mlima yanayojulikana sana ambayo Yesu Kristo aliyatoa, yeye alifundisha wafuasi wake sala ile inayoitwa na wengi kuwa Sala ya Baba Yetu au Sala ya Bwana, Labda wewe umerudia kuisema mara nyingi. Mamilioni mengi ya watu wamefanya hivyo. Wamesali hivi kwa Mungu: “Ufalme wako uje.” (Mathayo 6:9) Wakati wewe unapotoa ombi hilo, je! unajua ni kitu gani unachoomba?
Labda wewe umeyasema maneno hayo bila kufikiria sana maana ya maneno yenyewe, kama watu walio wengi wanavyofanya. Lakini kwa kuwa Ufalme wa Mungu ni serikali halisi, ni jambo gani litakalopata serikali za kisasa za ulimwengu wakati Ufalme wa Mungu utakapokuja? Je! wewe umepata kufikiria jambo hilo?
Biblia haituachi katika shaka lo lote la kutokujua jibu. Katika unabii unaoelekeza kwenye siku zetu, Biblia inasema hivi: “Katika siku za wafalme hao Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme [huo ni Ufalme wa Mungu, ambao Wakristo wanaomba] ambao hautaangamizwa milele. . . . Utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu [serikali za sasa za ulimwengu], nao utasimama milele na milele.”—Danieli 2:44.
Fikiria jambo hilo! Ufalme wa Mungu utaharibu serikali zote za kisasa za ulimwengu. Na wakati wewe unaposali, “Ufalme wako uje,” unakuwa ukisali jambo hilo lifanyike. Hata hivyo, kwa uhakika badiliko hilo linahitajiwa. Hakuna wakati wo wote katika historia ambapo serikali yo yote ya kibinadamu imekuwa yenye kuridhisha kabisa. Kwa hiyo jambo linalofaa zaidi ya yote ni kuwa na serikali kamilifu yenye kuongozwa na Mungu ili ichukue nafasi ya serikali zote za kibinadamu!
Kwa sababu Yehova Mungu ni mwenye nguvu zote, Ufalme wake utatosheleza tamaa za watu wenye maelekeo ya kupenda uadilifu. “Uufalme wako ni uufalme kwa nyakati zote,” Biblia inaeleza hivyo. “Unaufumbua mkono wako na kutosheleza tamaa ya kila kilicho hai.” (Zaburi 145:13, 16, NW) Wewe ungependa kuona tamaa gani zikitoshelezwa? Je! ni kumalizwa kwa vita, njaa, udhalimu, makao ya kimaskini, uhalifu, magonjwa na hata kifo? Matatizo yote hayo na mengine yataondolewa kabisa na Ufalme wa Mungu. Biblia inaahidi “wingi wa amani hata mwezi utakapokoma.”
Inasema, “bali waovu watatengwa na nchi.” Ndiyo, wakati huo watu “watajenga nyumba, na kukaa ndani yake.” “Naye Mungu mwenyewe atakuwa pamoja nao. Naye atafuta kila chozi katika macho yao, wala mauti haitakuwapo tena.”—Zaburi 72:7, 8; Mithali 2:22; Isaya 65:21-23; Ufunuo 21:3,4.
Lo, zitakuwa baraka kama nini kwa jamaa ya kibinadamu! Je! wewe ungependa kuwa raia wa Ufalme wa Mungu? Basi jifunze namna unavyoweza kuwa. Jifunze Neno la Mungu kisha ufuate mambo utakayojifunza.—Yohana 17:3.
[Picha katika ukurasa wa 7, 8]
utaondoa kabisa mfumo huu
ulete mfumo mpya