Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w80 2/1 kur. 17-19
  • Ufalme wa Mungu—Tumaini Peke Yake

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Ufalme wa Mungu—Tumaini Peke Yake
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • KWELI YA BIBLIA YENYE MAANA SANA
  • VIONGOZI WA KIDINI NDIO WENYE LAWAMA
  • MAONI YA MAKANISA
  • MAONI YENYE MAKOSA
  • MAONI NA MSIMAMO WA MKRISTO
  • YATAKAYOLETWA NA UFALME WA MUNGU
  • Manabii Wawongo Leo
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1992
  • Ufalme wa Mungu Ni Nini?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1985
  • Serikali ya Mungu—Tumaini Pekee La Wanadamu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
  • Ufalme Wa Mungu
    Amkeni!—2013
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1980
w80 2/1 kur. 17-19

Ufalme wa Mungu​—Tumaini Peke Yake

WANADAMU wanataabishwa na kila namna ya taabu. Lakini kuna ufumbuzi. Kinachohitajiwa ni serikali ya ulimwengu yenye haki ambayo itasimamia mambo ya dunia katika njia ya upendo, na yenye kufikiria na kufaidi watu wote. Je! wewe ungefikiria ufumbuzi huo kuwa kichwa cha mahubiri ya Yesu?

Ndio uliokuwa kichwa. “Ufalme ndio uliokuwa kichwa kikubwa cha mahubiri yake,” lasema gazeti Christianity and Crisis, na kuongeza: “Hakuna habari nyingine iliyokuwa akilini mwake sana au iliyokuwa kuu sana katika ujumbe wake. Inatajwa zaidi ya mara mia katika masimulizi ya Injili.” Ndiyo, Yesu alisema hivi: “Imenipasa kuihubiri habari njema ya ufalme wa Mungu katika miji mingine pia: maana kwa sababu hiyo nalitumwa.” (Luka 4:43) Yeye aliwafundisha wafuasi wake kuombea ufalme wa Mungu uje.​—Mt. 6 :9, 10.

Basi, bila shaka, ni jambo la maana kwetu kujua majibu ya maulizo kama vile: ‘Ufalme wa Mungu ni nini? Utakujaje kumaliza taabu za ulimwengu?’

KWELI YA BIBLIA YENYE MAANA SANA

Watu wengi wanajua kwamba mfalme ni mtawala, na ya kwamba ufalme wa mfalme unatia ndani milki au nchi anayotawala juu yake. Kwa hiyo, halipaswi liwe jambo gumu kufahamu kwamba ufalme wa Mungu utakuwa utawala au serikali juu ya dunia yote, ikisimamiwa na Mwana wake mwenyewe, Yesu Kristo. Ufalme huu wa Mungu utachukua mahali pa serikali zote za dunia.

Kwa muda wa miaka 100 moja kweli hii ya Biblia juu ya Ufalme imekaziwa katika Mnara wa Mlinzi. Kwa kweli, tangu 1939 jina rasmi la gazeti hili limekuwa “Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova.” Toleo la Desemba 1881 lilisema hivi: “Kusimamishwa kwa ufalme huu, bila shaka, kutahusu kupinduliwa kwa falme zote za dunia, kwa kuwa zote—hata zile zilizo bora zaidi—msingi wake ni ukosefu wa haki na haki zisizolingana na kuonewa kwa wengi na kupendelewa kwa wachache—kama tusomavyo: ‘Utavunja falme hizi zote vipande vipande na kuziharibu, nao utasimama milele na milele.’”​—Dan. 2:44.

Walakini, kwa watu wengi, hata wale wanaodai kuwa Wakristo, kweli hii ya Biblia haijulikani. Ebu chunguza. Unapokuwa na wakati, uliza watu: ‘Ufalme wa Mungu ni nini, nao utakujaje?’ Utashangaa kuona kwamba kuna mvurugo mwingi sana juu ya habari hiyo, na inafahamika kidogo sana. Sababu gani iko hivyo?

VIONGOZI WA KIDINI NDIO WENYE LAWAMA

Ni kwa sababu viongozi wa kidini wenyewe wanavurugika juu ya Ufalme. Habari ya mhariri katika The Church Quarterly Review ilikubali hivi :

“Tumekuwa katika hatari kwa muda ya kuangamizwa na mawimbi yanayoinuka ya makisio na makisio yenye kushindana kuhusu ni wazo gani la Ufalme lililo la maana kweli kweli.”

Sana sana kwa sababu ya mvurugo wa kidini, makanisa yamesema machache sana juu ya habari hiyo. Francis P. Miller, Mpresbyteri anayejulikana sana, alilalamika hivi:

“Unyamavu wa Wakristo wengi juu ya Ufalme wa Mungu ni mojawapo ya misiba iliyo mikubwa sana ya wakati wetu.” Kwa hiyo kwa kumalizia aliandika: “Kama mtu wa kawaida mimi nawasihi wataalam wetu wa elimu ya dini na viongozi wetu wa kidini: Tuambieni habari za Ufalme wa Mungu; tuelezeni ni nini na namna utahusianishwa na ulimwengu wa wakati wetu . . . Uhitaji ni mkubwa. Wataalam wetu wa elimu ya dini na viongozi wa kidini lazima waseme katika maneno yanayoweza kufahamika kwa watu wa kawaida juu ya Ufalme wa Mungu ambao umekaribia.”​—Christianity and Crisis, June 13, 1960.

Je! wamefanya hivyo? Kutofahamu na mvurugo wa watu wengi juu ya ufalme wa Mungu unafunua kwamba hawakufanya hivyo. Ebu fikiria kwa muda mfupi juu ya mawazo ambayo umesikia watu wakisema juu ya Ufalme. Je! yanaonyesha maoni haya ambayo makanisa yamefundisha.

MAONI YA MAKANISA

Kwa muda mrefu sana imefundishwa kwamba Kanisa Katoliki la Kirumi lilikuwa, kana kwamba, ndilo ufalme wa Mungu duniani. Lakini mapema katika karne hii, The Catholic Encyclopedia (1910) kilisema hivi chini ya “Ufalme wa Mungu”:

“‘Ufalme’ haumaanishi sana mradi wa kufikiliwa au mahali . . . Badala yake ni hali ya akili (Luka, xviii, 20-21), unamaanisha maongozi ambayo lazima yaenee katika akili za watu ikiwa watakuwa na umoja Naye na kufikia mawazo Yake.”

Je! maoni hayo yanasikika kuwa yanajulikana sana? Yamejulikana sana na watu wengi nayo yamesemwa sana na viongozi wa kidini. Kwa mfano, Kusanyiko la Wabaptisti wa Kusini (mwa United States) la 1925 lilisema juu yake hivi:

“Ufalme wa Mungu ni utawala wa Mungu katika mioyo na maisha ya mtu mmoja mmoja katika kila uhusiano wa wanadamu, na katika kila namna na matengenezo ya jamii iliyoungana. . . . Ufalme wa Mungu utakamilika wakati kila wazo na nia ya mwanadamu itakapotekwa na kutiishwa chini ya nia ya Kristo.”

Walakini, kuna maoni mengine yanayojulikana sana na watu wengi. Vilevile makanisa yameuhusianisha ufalme wa Mungu na jitihada za kisiasa za kibinadamu za kumaliza matatizo ya ulimwengu. Martin K. Hopkins padre Mkatoliki, akizungumza juu ya sala aliyofundisha Yesu, anaandika hivi: “Mapenzi yako yatimizwe hapa duniani kama huko mbinguni. Hii inaeleza namna mwishowe ufalme wa Mungu utakuja. Inatutaka tuangalie mbele kupita siku za sasa na kufanyia kazi kurudishwa kwa matengenezo yote ya kibinadamu katika Kristo.”

Namna gani juu ya maoni haya yanayotofautiana? Je! Ufalme unategemea katika njia yo yote jitihada za kibinadamu za kufanya matengenezo na jamaa zote za watu kuwa za Kikristo? Je! Ufalme ni “utawala wa Mungu katika mioyo na maisha ya mtu mmoja mmoja”?

MAONI YENYE MAKOSA

Maoni hayo yaliyo hapo juu kuhusu ufalme wa Mungu, ambayo ni maoni ya watu wengi, ni yenye makosa. Hayapatani na Biblia. Na hilo limekubaliwa katika nyakati za karibuni na viongozi wa makanisa wenyewe. The Dictionary of the Apostolic Church, iliyotengenezwa na James Hastings, inasema hivi:

“Hakuna wazo lo lote katika nyaraka za kale kwamba Kanisa duniani lilikuwa ndilo Ufalme wa Mungu. Nalo wazo la waandikaji wengine wa kisasa wa elimu ya dini, kwamba ulimwengu huu kama tuujuavyo sisi utasitawi chini ya maongozi ya Kikristo mpaka uwe ndio Ufalme, halipatani hata kidogo ni wazo lao.”

Ijapokuwa viongozi wa makanisa walikuwa na kawaida ya kuutaja Ufalme kama ‘hali ya akili,’ au ‘utawala katika moyo wa mtu,’ kwa kawaida maoni haya sasa yanakataliwa, kama lisemavyo The Church Quarterly Review:

“Wengine wetu tunaweza kukumbuka siku ambazo ulizo hili halikuhusu ugumu wo wote. Ufalme ulikuwa kwa vyepsi utawala wa Mungu katika moyo na maisha ya mtu mmoja mmoja . . . Leo wepesi huo ni kama utoaji wa habari usiotumika tena au wa siasa za jukwaani.”

Walakini, tofauti na maoni ya makanisa yenye makosa, ujumbe wa Ufalme unaotangazwa katika kurasa za Mnara wa Mlinzi umejionyesha kuwa unapatana na Biblia. Ndiyo, Maandiko yanaonyesha waziwazi kwamba ufalme wa Mungu ni utawala wa Mungu kupitia kwa Mwanawe, Yesu Kristo. Utawala huu ulitabiriwa katika Biblia katika maneno haya: “Maana kwa ajili yetu mtoto amezaliwa, tumepewa mtoto mwanamume; na uwezo wa kifalme utakuwa begani mwake . . . Maongeo ya [serikali] yake na amani hayatakuwa na mwisho kamwe.” (Isa. 9:6, 7) Katika wakati wake, serikali hii ya kifalme itazipindua na kuchukua mahali pa serikali zote za kibinadamu.​—Dan. 2:44.

MAONI NA MSIMAMO WA MKRISTO

Je! Wakristo wa kwanza walifahamu mambo katika njia hii? Je! wao waliuona ufalme wa Mungu kuwa utawala wa Mungu ambao ungechukua mahali pa taratibu hizi zilizopo? Ebu fikiria yale yaliyosemwa na The Dictionary of the Apostolic Church:

“Ikiwa ye yote wa waandikaji hawa [wa Biblia] angeulizwa kama Ufalme upo sasa, angejibu, Hapana. Kristo alikuwa Mfalme, lakini Ufalme Wake ungeonyeshwa tu wakati Yeye angekuja. Ikiwa angeulizwa zaidi Ufalme ungekuwa nini, au ungekuwa na uhusiano gani na ulimwengu uliopo, labda angejibu kwamba karibu kila kitu kinachoufanyiza ulimwengu huu uliopo kitatoweka—kutokamilika, dhambi, kifo.”

Kwa hiyo, msimamo unaofaa wa Mkristo kuhusiana na taratibu hii, ambayo ufalme wa Mungu utachukua mahali pake ni msimamo gani? Biblia inaeleza kwamba taratibu iliyopo iko chini ya utawala wa Shetani. (Mt. 4:9; Yohana 12:31; 14:30; 2 Kor. 4:4, NW) Zamani sana likivuta fikira kwenye kweli hii, toleo la Desemba la gazeti la Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) lilieleza hivi:

“Ikiwa tunaona waziwazi kwamba serikali zilizopo ni zile za ‘Mkuu wa ulimwengu huu’ na lazima zote ziponda-pondwe na kuuondokea Ufalme wa Mungu ambao tunaombea, ‘ufalme wako uje,’ basi sisi hatutakuwa na tamaa tena ya kuchangamana nazo katika njia yo yote.”

Tofauti na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo, kwa miaka 100 iliyopita Mnara wa Mlinzi umeonyesha wasomaji wake msimamo wa Kikristo unaofaa, kama alivyosema Yesu: “Ninyi si sehemu ya ulimwengu.” Mara nyingi umekazia fundisho la Yesu: “Ufalme wangu si wa ulimwengu huu.” (Yohana 15:19, NW; 18:36) Kwa hiyo, badala ya kujiingiza katika mambo ya kisiasa ya ulimwengu huu, Wakristo wa kweli wamekuwa wakiunga mkono serikali ya ufalme wa Mungu kwa moyo wote.​—Yohana 6:15.

YATAKAYOLETWA NA UFALME WA MUNGU

Wewe ungetazamia nini kutoka kwa serikali ya Mungu? Kwanza kabisa, bila shaka ungetazamia mtawala wake awe mwenye haki ya hukumu, mwenye fadhili na mwenye huruma. Naye Yesu Kristo amejionyesha mwenyewe kuwa mtu wa namna hiyo. (Mt. 11:28-30) Chini ya uongozi wa Mungu, Kristo amechagua watu walio na sifa zile zile watawale pamoja naye mbinguni. (Luka 22:28-30; Ufu. 5:9, 10; 20:6) Mmoja wa wanaume hawa alimwandikia mwingine aliyeshiriki tumaini hili hivi: “Tukiendelea kuvumilia, tutatawala pia pamoja naye.”​—2 Tim. 2:12, HHWW.

Bila shaka tungetazamia utawala wa wafalme hawa uwe wa haki na amani, ukiwaletea wanadamu wote—raia zake duniani furaha na afya. Kristo alionyesha uwezo wake aliopewa na Mungu wa kuponya kila namna ya magonjwa alipokuwa duniani; hata aliwafufua wafu! Chini ya utawala wa Ufalme yeye atatumia tena uwezo huu wa kimwujiza kwa baraka na faida ya kila mtu duniani! Na katika wakati wake dunia yote itageuzwa kuwa paradiso nzuri ajabu ifurahiwe na wote.​—Luka 23:43, NW; Ufu. 21:4.

Bila shaka ufalme wa Mungu ndio tumaini peke yake la kupatia baraka tunazotamani sana sisi sote!

[Sanduku/Picture katika ukurasa wa 17]

MAONI YA BIBLIA

“Ufalme wangu sio wa ulimwengu huu.”​—Yesu, Yohana 18:36.

“Na uweza wa kifalme [au, serikali, AV] utakuwa begani mwake. . . . Maongeo ya enzi yake na amani hayatakuwa na mwisho.”​—Isa. 9:6, 7.

MAONI YA MAKANISA

“Ufalme wa Mungu utakuja kwa . . . kufanyia kazi kurudishwa kwa matengenezo yote ya kibinadamu katika Kristo.”​—Padre Mkatoliki

“Ufalme wa Mungu ni utawala wa Mungu katika mioyo na maisha ya mtu mmoja mmoja.”​—Kusanyiko la Wabaptisti wa Kusini (U.S.A.)

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki