Ongezeko la Kutokutii Sheria—Ni Ishara ya Mwisho wa Ulimwengu?
“NI NINI itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?”
Katika kujibu Yesu Kristo alifunua wazi kwamba kipindi fulani cha historia kingekuwa na vita vya kimataifa, upungufu wa vyakula na matetemeko ya ardhi, kisha akaongezea hivi: “Kwa sababu ya kuongezeka kwa kutokutii sheria upendo wa wengi zaidi utapoa. Lakini yeye ambaye amevumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.”—Mathayo 24:3, 7-13, NW.
Kuongezeka kwa kutokutii sheria—hakika hilo ni tukio lenye kutisha kweli kweli kwa kuwa neno la kwanza lililotumiwa katika Kigiriki linatoa wazo la kudharau sheria za Mungu zinazojulikana. Mkazo wa neno hilo unaonyeshwa na jambo la kwamba mtu anayafanya maisha yake yamtegemee yeye binafsi, wala si Mungu. Yesu hakusema kungekuwa na ‘mwanzo’ wa kutokutii sheria, bali “kuongezeka” na kuenea kwa kutokutii sheria. Jambo hilo lingetukia kwa njia kubwa sana mpaka wingi wa watu, walio “wengi zaidi,” kati ya wenye kujiita Wakristo wapatwe na matokeo ya hali hiyo. Upendo wao kwa Mungu, sheria zake na jirani zao ungekuwa baridi, sawa na vile kinywaji chenye moto kinavyotiwa baridi na upepo wenye barafu!
Kuna ushuhuda wenye nguvu unaoonyesha kamba, hasa kuanzia Vita ya Ulimwengu ya kwanza, karne yetu ya 20 ilileta ongezeko la kutokutii sheria kwa kipimo kikubwa zaidi ya kinginecho chote tangu Yesu alipotamka maneno hayo. Ikiwa ndivyo, hiyo inamaanisha tunaishi katika “siku za mwisho”—katika sehemu ya mwisho ya “umalizio wa mfumo wa mambo.” (2 Timotheo 3:1; UV; Mathayo 24:3, NW) Je! wewe hutaki sana kuuona mwisho wa mfumo huu usiotii sheria ambao umejaza dunia yetu jeuri, ufisadi na udhalimu, na kuona mahali pake pakichukuliwa na jamii ya watu wenye upendo, “dunia mpya” ambamo uadilifu utakaa?—2 Petro 3:13, NW.
‘Lakini ngoja kidogo,’ wanasema wanafunzi wengine wanaochunguza historia. ‘Kwani karne ya 20 siyo yenye ustaarabu mwingi zaidi ya karne zote katika historia? Je! jeuri na ufisadi uliokuwako katika karne zilizopita haukuwa mbaya zaidi kwa sababu hakukuwa na maendeleo mengi?’
Nyakati Zilizopita Zilikuwa Mbaya Kadiri Gani?
“Hakuna mtu angeweza kujisikia akiwa na usalama wa kukosa hatari kwake binafsi au kwa mali zake kama alitembea barabarani usiku, wala hakuna mwanadamu ye yote angeweza kujihakikishia usalama akiwa amelala kitandani pake,” ndivyo alivyoomboleza mkuu wa London wa wanasheria wa mahakama ndogo-ndogo katika mwaka wa 1785. Wengine wakati huo walionyesha woga mwingi juu ya uhalifu.
Lakini kwa kweli uhalifu ulikuwa wa kiasi gani nyakati zilizopita? Hakuna anayeweza kueleza kwa uhakika, hasa kwa sababu maandishi ya mahakamani hayakuwekwa kwa usahihi sana. Na kwa sababu ya ukosefu wa maandishi yenye kutegemeka au ya waziwazi juu ya idadi ya watu nyakati zilizopita, hakuna njia yenye kutegemeka ya kulinganishia hesabu ya matendo ya uhalifu na idadi ya watu katika siku zetu. Viishara fulani vinaonyesha kwamba, kwa kulinganisha, karne za mapema zaidi ndizo zilizokuwa zenye amani. “Hakuna wakati mwingine katika historia ya Massachusetts ambapo uhai, uhuru na mali zimekuwa katika hali ya usalama kuliko sasa,” akaeleza mkuu wa sheria wa serikali mwaka wa 1859.
Lakini wakati wa miaka 150 iliyoutangulia mwaka wa 1914 mfululizo wa matukio—yasiyo na kifani katika historia yote—ilitayarisha njia ya kutokea kwa hali ya kutokutii sheria katika karne ya 20 ambayo haikutangulia kuwa na mfano wake.
Kipindi cha Viwanda Vingi
“Hicho ndicho kipindi cha mabadiliko makubwa zaidi katika historia yote ya kibinadamu.” Hayo ndiyo maelezo yaliyotolewa na maprofesa wa historia M. Klein na H. A. Kantor katika kitabu chao Prisoners of Progress wakati wanapoeleza matokeo yaliyoipata United States ya Amerika kutokana na Kipindi cha Viwanda Vingi kati ya mwaka wa 1850 na wa 1920. Matumizi makubwa ya mashine mpya-mpya zilizotengenezwa viwandani, kama gari-moshi la mwanzo-mwanzo, na utengenezaji wa bidhaa nyingi kwa wakati mmoja yalianza huko Uingereza. Yakaingia katika sehemu zote za Ulaya kama wimbi la bahari, mpaka yakafikia United States na kuharibu mtindo wa maisha uliofuatwa na watu kabla ya hapo.
Wakifikiria kipindi kilichokuwa kabla ya kile cha Viwanda Vingi, Klein na Kantor waliendelea kusema hivi: “Kwa kulinganishwa na kizazi chetu wenyewe, maisha yaliendelea kuwa yenye utaratibu na utulivu mwingi zaidi. Wakati huo wanadamu bado waliona dini kuwa ya maana sana na walipanga mapendezi yao na mitindo yao ya maisha kwa kutegemea imani yao ya kidini.”
Wakati huo watu walio wengi walikuwa wakijifanyia kazi zao wenyewe zisizo za kuandikwa na walijivunia kazi yao—lengo lao la kufanya biashara halikuwa kuchuma pesa tu Ingawa walikuwako wevi na wauaji, na imani za kidini zilichanganywa na uchawi na ushirikina, kwa ujumla mtu wa kawaida katika yaliyoitwa mataifa ya Kikristo aliheshimu sheria za Mungu.
Kati ya mwaka wa 1880 na wa 1913 bidhaa zilizotengenezwa ulimwenguni ziliongezeka haraka kwa kiasi cha mara tatu kuliko idadi ya watu wa ulimwengu—hicho kikiwa ni kiasi ambacho hakijawa na ulinganifu kabla ya hapo wala baada ya hapo. Basi, wafanya kazi zaidi walikuwa na kiasi kikubwa zaidi cha pesa za kutumia wanunue bidhaa hizo zilizotengenezwa karibuni. Lakini watu wengi waliposikiliza maelezo yenye kuwasifu kwamba walikuwa wameiacha hali ya umaskini mwingi wakafikia utajiri mkubwa waliabudu mafanikio yao yakawa mungu wao mdogo wa kike.
Biblia inaonya kwamba “hao watakao kuwa na mali huanguka katika majaribu na tanzi . . . kupenda fedha; ambayo wengine hali wakiitamani hiyo wamefarakana na Imani.” (1 Timotheo 6:9, 10) Jambo hilo lilipata umati mkubwa wa watu. Watu walifanya maisha yao yakategemea kazi kabisa. Maisha ya jamaa yakapata hasara kwa maana yalilazimika kutegemea orodha ya kufanya kazi karibu saa 60 kwa juma. Wakati wanawake wengi walipojiunga katika kufanya kazi, mara nyingi watoto waliachwa bila uongozi nao wakawa wasio wazazi. Kwa sababu ya watu kujibidiisha sana kujipatia riziki, wengi walisukuma dini nyama.
Nietzsche mwanafalsafa Mjeremani aliye mashuhuri alihimiza ya kwamba, “Uwe namna-ulivyo!” Choyo na pupa zikaleta mizozo yenye hasira kati ya wafanya kazi—visa 2,093 vya migomo ya wafanya kazi na vya matajiri kuwasimamisha kazi waajiriwa kwa muda katika United States katika muda wa miezi sita tu ya kwanza ya mwaka wa 1916! Biashara za kumalizia wengine mali zao bila huruma zilizoewa na watu wengi. Wengi walifuata mfano wa mfanya-biashara aliyesemwa katika kitabu cha hadithi cha mwaka wa 1905: “Yeye ndiye mbwa mkubwa kupita wote, na biashara yetu imekuwa ya kuumizana mtu na mwenzake kama mbwa mwenye kutafuna mbwa mwenzake.” Kweli kweli, upendo kwa jirani ulianza kupoa kila mahali.
Miji Yenye Kuongezeka Watu kwa Haraka
Watu walimiminika mijini kwa wingi wakitafuta elimu, sifa, kujiingiza katika matendo ya kishujaa, lakini hasa wakitafuta pesa. Katika mwaka wa 1815 ni asilimia inayopungua 2 kati ya watu wote wa Ulaya iliyoishi katika miji yenye watu zaidi ya 100,000; kufikia mwaka wa 1910 hesabu ya wenye kuishi huko ikawa asilimia 15—hao wakiwa ni watu wengi mara saba kuliko wale waliotangulia, nayo idadi ya watu iliongezeka ikawa maradufu tu. Katika United States hesabu ya watu wenye kuishi katika miji yenye watu 8,000 au zaidi iliruka kutoka 131,000 mwaka wa 1790 ikawa zaidi ya milioni 18 mwaka wa 1890—kutoka asilimia 3 kufika asilimia 29 ya idadi ya watu wote!
Miji ya sehemu zote za ulimwengu zenye viwanda ilipanuka kwa mwendo wenye kustaajabisha sana. “Kwa kweli, kupanuka kwa miji kumesonga mbele kwa haraka zaidi na kukaongezeka zaidi sana katika wakati wa karne moja na nusu iliyopita kuliko katika wakati mwingineo wote uliotangulia katika historia ya ulimwengu,” akaandika Kingsley Davis, mwandikaji juu ya mpanuko wa miji.—Mwa-ndiko wa italiki ni wetu.
Hesabu kubwa ya wale waliokuja mjini kutoka mashambani walikuwa vijana na hawakuwa wameoa au kuolewa. Kwa kuwa katika mji wangeweza kufichika wasionekane wanatenda nini, wao hawakuzuiwa tena kutenda waliyotaka na ule uhusiano wa kijamii uliokuwa katika vijiji kwa maana mjini kulikuwa na roho ya uhuru mwingi wa kujifanyia lo lote. “Ingekuwa vigumu kupata kijana mwanamume au kijana mwanamke, anayezidi umri wa miaka kumi na saba, ambaye ni bikira,” akaandika mtazamaji mwenye makini juu ya wenye kufanya kazi katika mji mmoja. Mwanamume huyo, aliyeishi wakati wa pambazuko la karne ya 20, aliongezea hivi: “Ngono, ambayo sana-sana imetokea kwa sababu ya hayo majumba ya dansi, imeongezeka kwa wingi sana kati ya vijana wa leo. Inachukuliwa kuwa jambo la asili na la kikawaida tu.”
Ndiyo, watu wengi walionyesha madharau juu ya sheria za Mungu juu ya adili. Biblia inaamuru hivi: “Mjiepushe kabisa na maisha ya zinaa. . . . Anayedharau... hamdharau mtu, bali amdharau Mungu.” (1 Wathesalonike 4:3, 8, HNWW) Lakini, vijana fulani wa kiume katika Ulaya walijisifu wakisema wamelala na malaya ili kuonyesha wao ni wanaume—hata wakajivuna ikiwa walijipatia ugonjwa wa kisonono au kaswende kutokana na malaya hao! Kulingana na uchunguzi mmoja uliofanywa katika nchi moja ya Ulaya na ukachapishwa mwaka wa 1914, karibu mmoja kati ya kila wanaume watano wa huko alikuwa na ugonjwa wa kaswende.
“Bila shaka miji ni mahali penye ukosefu wa adili,” akaandika mwanahistoria Adna Weber mwaka wa 1899. Alionyesha kwamba, kwa wastani hesabu ya watoto wa haramu katika miji ya sehemu nyingi za Ulaya ilikuwa mara mbili zaidi ya hesabu ya watoto haramu wa mashambani. Katika Uingereza wakati huo miji ilikuwa na kiasi cha uhalifu kilichozidi kile cha mashambani kwa mara mbili au hata mara nne.
Lakini si Kipindi cha Viwanda Vingi tu na miji yenye kuongezeka watu iliyotayarisha njia ya ongezeko la karne yetu ya 20 la kutokutii sheria; tukio jingine—la siku zetu pia ambalo halilingani na lo lote pia—lingekuwa na matokeo yenye kutazamisha.
Ile Vita Kuu
Vita hiyo ilitokea kwa ghafula mwaka wa 1914, nayo ikaitwa “pigano lililo la umwagaji wa damu nyingi zaidi na lenye kuleta hasara kubwa zaidi katika historia ya wanadamu” kupita mapigano mengine yote yaliyoutangulia wakati huo. Yaliyoshiriki zaidi katika tendo hilo la kinyama la kutokutii sheria ni mataifa yanayoitwa “ya Kikristo” ati! Barua iliyoandikwa katika gazeti moja la kutangaza habari la mwaka wa 1914 iliteta kwa kufanya mzaha huu: “Mataifa na yapigane kama Wakristo, au angalau kama waungwana.”
Kwa sababu ya vita hiyo, kutumia nguvu na jeuri kukaanza kuonwa kuwa jambo linalokubalika. “Wakati kanuni za jamii ya watu wastaarabu zinapoachwa kwa muda, wakati mauaji yanapokuwa biashara na ishara ya kuonyesha nguvu na ushujaa,” akaandika kiongozi wa kidini Charles Parsons katika mwaka wa 1917, “basi linaelekea kuwa jambo la bure kuzungumza juu ya uhalifu katika maana ya kawaida.” Basi si ajabu kwamba wachunguzi D. Archer na R. Gartner walikuta kwamba mengi ya mataifa waliyochunguza yaliyohusika katika Vita ya Ulimwengu ya Kwanza yalikuwa na “maongezeko makubwa baada ya vita” katika hesabu ya mauaji—Italia ilikuwa na ongezeko la asilimia 52 na Ujeremani ongezeko la asilimia 98 kupita ongezeko lililoitangulia vita hiyo! Lakini vita hiyo ilileta namna tofauti ya kutokutii sheria.
Yehova Mungu, ambaye ‘anachukia talaka analihesabu tendo la kuondosha mwenzi wa ndoa kwa njia isiyopatana na Maandiko kisha kuoa au kuolewa na mwingine kuwa dhambi nzito. (Malaki 2:16, NW) Baada ya Vita ya Ulimwengu ya Kwanza hesabu ya talaka ilitokea kwa wingi kuliko katika wakati uliotangulia. Kwa mfano, katika Uingereza na Wales wakati wa miaka ile 50 iliyokuwa kabla ya mwaka wa 1911, hesabu ya talaka ilikuwa na wastani ya 516 kila mwaka. Katika mwaka wa 1919, ambao ndio mwaka wa kwanza baada ya ile vita, kulikuwa na talaka 5,184—zaidi ya mara 10 kupita wastani ya kipindi kilichotangulia cha miaka 50!
Vita hiyo ilikusanya wanaume 65,000,000 ikawapeleka wakapigane, na hivyo ikatenganisha wengi na jamaa zao kwa muda wa miaka mingi. Kulingana na wanahistoria G. Rowntree na N. H. Carrier, ‘si kwamba tu ile mikazo isiyofaa na mitenganisho iliyofanywa kwa kutumia nguvu muda wa Vita ya 1914-18 iliongeza hesabu ya talaka, bali pia ilitumia ujanja ikafanya watu wawe na maoni ya kisasa ya kutokuchukizwa. . . . Maoni hayo ya kutokujali sana ambayo yalianzishwa baada ya vita, yanaelekea kuwa yameendelea kwa muda mrefu zaidi.’ Maoni hayo ya kutazama mambo kwa akili zisizochukizwa upesi yalianza wakati huo na yameendelea kuwako mpaka leo!
Kwa hiyo kwa sababu ya yale yanayoitwa mataifa “ya Kikristo” kufanya haraka kupeleka watu katika miji yenye viwanda, na pia kwa sababu ya masomo ambayo watu walifunzwa na Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, njia ikawa tayari ya kuingia kwa ongezeko kubwa la kutokutii sheria lisilopata kuonekana kabla ya hapo. Matokeo yamekuwa nini tangu mwaka wa 1914? Je! upendo wa hesabu iliyo kubwa zaidi ya wenye kujiita Wakristo umepoa kweli kweli?
Ongezeko la Sasa la Kutokutii Sheria
Huko nyuma katika mwaka wa 1945 watu wengi katika United States walishangaa kwa sababu jumla ya matendo ya uhalifu yaliyoripotiwa kwa polisi yalipanda yakafika 1,566-000. Lakini miaka 35 baadaye jumla ilifika 3,295,000—na bado inapanda! Hilo ni ongezeko la asilimia 750, na hali idadi ya watu iliongezeka kwa karibu asilimia 60! Matendo ya kuingilia wanawake kwa nguvu yaliongezeka kwa asilimia zaidi ya 600! Matendo ya uhalifu wa kutumia jeuri yaliongezeka kwa karibu asilimia 900 kwa ujumla! Ebu wazia, katika mwaka wa 1981 moja kati ya kila jamaa tatu ilifikiwa na namna fulani ya uhalifu! Na elekeo hilo halimo United States peke yake. “Lile jambo moja unaloona unapotazama hali ya uhalifu ulimwenguni pote,” akaandika mchunguzi mashuhuri wa matendo ya uhalifu, Sir Leon Radzinowicz, katika kitabu chake The Growth of Crime, “ni ongezeko linaloenea na kuendelea kila mahali. Sehemu ambazo hazina ongezeko hilo ni chache, na huenda karibuni zikakumbwa na wimbi hilo lenye kuongezeka.”
Je! maongezeko hayo yote yametokea kwa sababu tu njia bora zimepatikana za kuripoti kwa polisi matendo ya uhalifu? Ili kutoa jibu, kikundi cha watu chenye kuongozwa na Dakt. Herbert Jacob wa Kituo cha Uchunguzi wa Mambo ya Mijini kwenye Chuo Kikuu cha Kaskazini-magharibi kilichunguza takwimu za matendo ya uhalifu, gharama walizopata polisi na njia walizotumia kupambana na uhalifu, hesabu ya waliokamatwa, na habari nyingine nyingi za miji 396 katika United States wakati wa kipindi cha kati ya mwaka wa 1948 na wa 1978. Katika mahoji yaliyofanywa pamoja na mwakilishi wa gazeti hili, Dakt. Jacob alisema hivi: “Hesabu ya matendo ya uhalifu yanayoripotiwa imeongezeka kila mahali katika U.S. Sababu moja bila shaka ni kwamba kumekuwa na njia bora za polisi na raia kuripoti matendo ya uhalifu. Lakini njia hizo tu sizo zinazofanya kuwe na ongezeko lote hilo.”
“Jambo la kushangaza,” akaendelea kusema Dakt. Jacob, “ni kwamba katika kila namna ya mji—kaskazini au kusini, wenye kuendelea kupungua watu au kuongezeka watu, wenye idadi kubwa ya watu au watu wachache—uhalifu ulipanda kwa karibu kiasi kile kile. Lilikuwa elekeo la taifa zima.” Je! polisi wanaweza kukomesha elekeo hilo lenye dalili mbaya? “Jeshi la polisi kwa ujumla limeshindwa kwa sababu ya mavutano fulani ya kijamii wasiyoweza kuyazuia,” akajibu Dakt. Jacob.
Bila shaka, uhalifu sicho kiishara cha pekee chenye kuonyesha ongezeko la kutokutii sheria. Wewe tazama tu namna watu kwa ujumla wanavyokosa kujali sheria za Mungu. Uzazi wa watoto wa haramu katika United States wa 7.1 kwa kila wanawake 1,000 wasioolewa katika mwaka wa 1940 unakuwa wa hesabu ndogo unapolinganishwa na hesabu ya 27.8 katika mwaka wa 1979. Zile talaka 83,000 zilizotokea katika mwaka wa 1910 zimeongezeka zikawa 1,182,000 katika mwaka wa 1980, hilo likiwa ni ongezeko la asilimia 1,300! Sasa, badala ya kuwako talaka moja kwa kila ndoa 11 zinazofanywa wakati wa mwaka, kama ilivyokuwa katika mwaka wa 1910, nchi ya United States inakuwa na talaka moja kwa kila ndoa 2! Maelekeo yanayofanana na hilo yanaripotiwa duniani pote.
Fikiria pia yale matendo ya kinyama yaliyofanywa katika karne yetu ya 20. Ni wakati gani mwingine katika historia yote ya kibinadamu ambapo kumetokea mpango uliofanywa kwa makini wa kuua Wayahudi milioni 6 katika kambi za mateso za Nazi wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili? au jumla ya hesabu ya vifo vilivyosababishwa na vita hiyo—watu 55,000,000? Hivi majuzi, ebu fikiria ripoti za mwaka wa 1979 zilizoonyesha uwezekano wa kuuawa kwa Wakambodia zaidi ya milioni 2. Ni kizazi gani kingine kilipata kutengeneza na kutumia silaha ambayo kwa mlipuko mmoja tu ilipata mwishowe kuua watu wanaoweza kuwa ni 140,000, kama lile kombora la atomi lililoangushwa juu ya Hiroshima, Japani?
Hatuna nafasi ya kutosha ituwezeshe kueleza mambo mengine juu ya vile sheria za Mungu zimedharauliwa, lakini habari ambazo zimetajwa zinaonyesha wazi kwamba tangu mwaka wa 1914 kuna ongezeko la kutokutii sheria la kiasi kisichopata kulinganishwa katika kipindi cho chote cha historia! Ndiyo upendo kwa Mungu na jirani umepoa kati ya hesabu iliyo kubwa zaidi ya wenye kujiita wafuasi wa Yesu, sawasawa na vile Yesu alivyotabiri.
Lakini, wewe usiache hali hiyo inayoongezeka ya kutokutii sheria igeuze moyo wako. Endelea kumpenda Mungu na sheria zake kwa uchangamfu, na huenda ukawa na furaha ya kuokolewa uingie katika “dunia mpya” iliyoahidiwa, ambamo hamtakuwa kamwe tena na pigo la kutokutii sheria.—2 Petro 3:13; Mathayo 24:12,13, NW.
[Grafu katika ukurasa wa 6]
(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)
Jumla ya hesabu ya matendo mabaya sana ya uhalifu yaliyotendwa katika United States iliongezeka kwa zaidi ya asilimia 1,000 kutoka mwaka wa 1935 mpaka 1980, na hali idadi ya watu iliongezeka kwa karibu asilimia 78 wakati wa kipindi icho hicho!
1935 1,138,000
1950 2,220,000
1965 2,780,000
1980 13,295,000
[Hisani]
Chanzo cha habari: Ripoti za Uhalifu Zenye Upatano Zilizotolewa na Idara ya Serikali ya Uchunguzi zikionyesha mauaji, matendo ya kuingilia wanawake kwa nguvu, ya unyang’anyi, mashambulizi yenye kufanyiwa uchochezi, kuvunja nyumba za watu na kuiba, matendo ya wivi wa kuchukua vitu vya watu kwa ujanja na wivi wa magari ulioripotiwa kwa polisi. Kwa sababu ripoti hazikuwa kamili, hesabu za mwaka wa 1935 na wa 1950 zimerekebishwa ziwakilishe jumla ya idadi ya watu
[Picha katika ukurasa wa 5]
KIPINDI CHA VIWANDA VINGI
VITA YA ULIMWENGU YA KWANZA
MIJI YENYE KUONGEZEKA WATU KWA HARAKA
Matukio haya, ambayo ni ya namna yake kwa kizazi chetu cha kisasa, yameshiriki kuleta ongezeko la kutokutii sheria lililo kubwa zaidi katika historia yote