Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 11/1 kur. 5-10
  • Iweke Ndoa Yako Katika Hali ya Kuheshimika

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Iweke Ndoa Yako Katika Hali ya Kuheshimika
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Ukosefu wa Kupashana Habari Kibinafsi
  • Kusitawisha Njia ya Kupashana Habari Kibinafsi
  • Zungumzeni Matatizo Yale Yenye Kuamsha Hasira kwa Urahisi
  • Sheria ya Fadhili za Upendo Juu ya Ulimi
  • Mchukuliane Tofauti za Kutokuelewana na za Kutokamilika
  • Imarisha Ndoa Yako Kupitia Mawasiliano Mazuri
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2013
  • Baada ya Siku ya Harusi
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Ndoa​—Zawadi Kutoka kwa Mungu
    Jinsi ya Kudumu Katika Upendo wa Mungu
  • Mambo Yanayoweza Kukusaidia Kuwasiliana na Mwenzi Wako
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2006
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 11/1 kur. 5-10

Iweke Ndoa Yako Katika Hali ya Kuheshimika

“Ndoa na iheshimiwe na watu wote.”​—WAEBRANIA 13:4.

1. Mwandikaji mmoja wa habari za gazeti aliuliza ulizo gani, na mume mmoja alijibuje?

“KAMA ingekupasa kuchagua tena, je! wewe ungeoa au kuolewa na mtu yule mnayekaa pamoja sasa?” Ulizo hilo liliulizwa na mwandikaji wa habari za gazeti anayejulikana na watu wengi. Zaidi ya nusu ya watu 50,000 waliokubali kufanyiwa uchunguzi huo walijibu wakasema “Ndivyo.” Wewe ungalijibu namna gani? Mwanamume mmoja Mkristo, ambaye amekuwa mtu aliyeoa kwa muda wa miaka 33, aliulizwa ulizo hilo na mke wake. Akiwa na uso wenye kung’aa akasema, “Hakika ningekuoa wewe! Ninapotazama siku za huko nyuma, najua kuna nyakati ambazo mambo yalikuwa magumu​—tulikuwa na matatizo. Lakini ndoa yetu imekuwa nzuri, na kwa hiyo jitihada tulizofanya kuifanya iwe hivyo zilistahili. Tuna ndoa yenye thamani kubwa sana!”

2. Kwenye Waebrania 13:4, neno “iheshimiwe” lina maana gani?

2 Kwa kuwa Mungu ndiye Mwanzilishi wa ndoa, ndoa inaweza kuwapa watu uradhi na furaha ya kweli. Hata hivyo ndoa nyingine​—hata nyingine-nyingine kati ya Wakristo waliojiweka wakf​—zina matatizo chungu zima. Basi mtume Paulo alihimiza hivi, “Ndoa na iheshimiwe [“ichukuliwe kuwa ya bei kubwa, yenye thamani sana . . . ya bei ghali sana”a] na watu wote.” (Waebrania 13:4) Kwa sababu ndoa inaleta “dhiki katika mwili,” unaelekeana na mwito wa ushindani, wa kuiweka ndoa yako katika hali ya kuheshimika. (1 Wakorintho 7:28) Lakini unaweza kufanya hivyo namna gani? Kwanza, ni lazima ujue moja la matatizo yaliyo makubwa zaidi.

Ukosefu wa Kupashana Habari Kibinafsi

3, 4. (a) Ni nini moja la matatizo yaliyo makubwa zaidi katika ndoa? (b) Ni jambo gani linalohusika katika kuwa kwa watu wawili waliooana “mwili mmoja”?

3 Mume na mke mmoja Wakristo walikuwa wameoana kwa muda upatao miaka 20. Kwa ghafula, ndoa yao ilivunjwa-vunjwa na uzinzi. Jambo hilo lingeweza kutokeaje? “Mimi niliporudia kuchunguza-chunguza yaliyokuwa yametukia miaka yote hiyo,” akasema mke, “niliona kwamba tulikuwa tukizungumza mambo ya kinyumbani, hata utumishi wetu kwa Mungu. Lakini lile jambo la kupashana habari kwa njia ya kibinafsi​—hilo hatukuwa tukilifanya.” Ukosefu huo wa kuwa na ukaribiano wa kirafiki, wa kuelezana mawazo ya moyoni, ulizidi pole kwa pole kulegeza ule wajibu wa kufunganika pamoja. Ulimfanya pia mume wa mwanamke huyo afanye uzinzi. Kuharibika hivyo kwa njia za kupashana habari zenye mafaa makubwa kumetajwa na uchunguzi mbalimbali wa matukio kuwa moja ya sababu kubwa zaidi zinazoleta ama talaka ama “ndoa zisizo na upendo.”

4 Hata hivyo Yehova alisema: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye ataambatana na mkewe, nao watakuwa mwili mmoja.” (Mwanzo 2:24) Basi ndoa inapasa kuwa ndio uhusiano wenye ukaribiano wa kirafiki kupita uhusiano mwingineo wote wa kibinadamu. Inaunganisha watu wenye nyutu mbili zinazotofautiana, na hiyo si kazi rahisi hata kidogo! Ili mwungano huo ulete matokeo mazuri, ni lazima kila mmoja amweleze mwenzake mambo kwa unyofu na kumfunulia wazi maoni yake ya moyoni.

5. (a) Ni nini kinachozuia kupashana habari kwa njia ya kibinafsi? (b) Wengine wanaweza kuheshimuje ndoa?

5 Ni nini kinachozuia njia hiyo ya kupashana habari kibinafsi? Nyakati nyingine, desturi ya nchi ni kwamba mtu awe mbali na mwenzi wa ndoa. Wengine ni watu wa kunyamaza-nyamaza, watu wenye haya-haya wasiotoa maoni yao. Na bado wengine wamefanywa mateka na ulimwengu wetu wenye kufuatia mambo ya kimwili na wenye kufikiria sana mambo ya tafrija. Wao wanakuwa wenye kupendezwa zaidi na vitu kuliko vile wanavyopendezwa na ndoa yao. Kuacha ndoa yako iingiliwe na watu wengi mno, au kushikamana mno na wazazi kunaweza pia kuzuia ukaribiano wenu. Bila shaka watu wale wengine wanapaswa kuheshimu jambo la kwamba watu waliooana wana uhitaji wa kuachiwa nafasi ya kuwa peke yao wala si kutumia muda wao isivyofaa wala kutaka wakaziwe fikira ambazo mwenzi wa ndoa ndiye anayezistahili.​—Mithali 25:17.

6. (a) Mwenzi wa ndoa anaweza kuwaje kama “mji wa nguvu” na “mashindano” yawe kama “mapingo” ya ngome? (b) Ni maulizo gani yaliyo katika sanduku lililo hapa yanayofunua ubora wa njia yenu ya kupashana habari?

6 Lakini labda sababu kubwa zaidi inayoleta ukosefu wa kupashana habari kibinafsi ni ile inayoelekea kutajwa kwenye Mithali 18:19: “Ndugu aliyechukizwa ni mgumu kuliko mji wa nguvu; na mashindano ni kama mapingo ya ngome.” Kwa mfano, huenda mke akamweleza mwenzi wake yaliyomo moyoni mwake. Lakini itakuwaje ikiwa maoni yake yanapuzwa au kudharauliwa, labda hata kutumiwa kama njia ya kumfanyia uchokozi safari nyingine? Huenda mke akachukua hatua ya kujenga ukuta wenye nguvu wa kuzuia mwelezano wa maoni ili aepuke kuumizwa tena moyoni, na hivyo awe kama “mji wa nguvu” uliojengewa ngome. Huenda vita ya kutendana mambo kwa kiburi ikafuata, kila mmoja akikataa kujishusha ili mambo yawe sawa. Mashindano ya bure namna hiyo yanaweza kufunga njia ya kupashana habari kibinafsi na kuzuia upatano kama kwamba watu hao wawili waliooana wametenganishwa na mapingo ya chuma ya ngome! Lakini wewe unaweza kufanya nini uletee maendeleo njia ya kupashana habari?

Kusitawisha Njia ya Kupashana Habari Kibinafsi

7. Andiko la Wafilipi 2:4 linaonyesha ni nini kinachohitajiwa ili kusitawisha njia ya kupashana habari kibinafsi?

7 Ni lazima wewe uendelee ‘kupendezwa kibinafsi’ katika mahangaikio ya mwenzi wako. (Wafilipi 2:4, NW) Jambo hili linataka wakati utumiwe kuzungumza pamoja mambo ya kibinafsi. Kwa mfano, mume na mke mmoja Wakristo wanaweka kando wakati fulani mara tu mume akifika nyumbani kutoka kazini ili wanywe kikombe cha chai na kuzungumza pamoja. Kwa muda usiopungua dakika 15 wanajulishana mawazo na maono ya kila mmoja wao kabla hawajaanza kazi ndogo-ndogo za jioni. Wao wamekuwa wakifanya hivyo kwa ukawaida muda wa miaka 27!

8. Kwa sababu gani kusikiliza kwa makini kunahitajiwa sana?

8 Lakini mengi zaidi yanahitajiwa, si kuzungumza tu. Alipoulizwa ni jambo gani alilopenda zaidi ya yote juu ya mume wake, mke Mkristo alijibu hivi: “Yeye ananisikiliza. Yeye ndiye rafiki yangu mkubwa kupita wote.” Kusikiliza kwa makini, badala ya kusikia maneno bila kujali sana, kunamwambia mwenzi wako hivi: ‘Wewe ni mtu wa maana kwangu. Mimi nataka kujua mawazo na maono yako ya moyoni, kushiriki pamoja nawe mambo yaliyokupata​—hata yale yasiyopendeza.’ Kuwa msikilizaji mzuri ni ufundi wa moyoni. Kunataka mtu awe na kile ambacho Petro alikiita “hali ya kujisikia kama vile wengine wanavyojisikia” (kwa uhalisi, “kutaabika pamoja na”) na awe pia na ‘huruma yenye upole mwororo’ na ‘unyenyekevu.’ (1 Petro 3:8, NW) Kwa hiyo ambianeni mambo yaliyo ndani ya mioyo yenu. Elezaneni hata vile vijambo vidogo-vidogo tu. Badala ya kukaa na maono ya moyoni bila kuyatoa nje, ongeeni.

9, 10. Watu waliooana wanaweza kuigaje njia ya Isaka, ya mke wa Manoa na ya Elkana ya kuwatendea mambo wenzi wao?

9 Ebu wazia ukaribiano mwingi ulio kuwa kati ya Isaka na Rebeka. Aliposumbuliwa sana na maoni ya moyoni, yeye aliweza kummwagia mume wake yaliyokuwa moyoni mwake. Wakati mmoja aliomboleza akisema, “Rohoni mwangu sina raha.” Je! Isaka alimtia aibu kwa sababu ya maoni yake? Hapana, yeye alisikiliza kwa huruma akachukua hatua za kupunguza hofu zake. (Mwanzo 27:46–28:5) Mke wa Manoa alimwona mume wake huyo akiwa na hangaiko, akampa maneno ya kumfariji.​—Waamuzi 13:22, 23.

10 Elkana alikuwa mwepesi wa kushughulikia maoni ya mke wake. Alipomwona mke wake akiwa ameshuka moyo alijitahidi ‘kuchota’ makusudi ya moyo wake kwa maulizo ya upole, akisema: “Hana, unalilia nini? kwani huli chakula? Kwa nini moyo wako una huzuni?” (1 Samweli 1:8) Namna gani wewe? Je! unakuwa mwepesi kuchungua kindani sababu ya maoni ya mwenzi wako? Je! unamfanya mume au mke wako ajione huru kujielezea mwenyewe maoni yake bila kumfanya ajisikie atalaumiwa kwa kufanya hivyo? Nyakati nyingine kinachohitajiwa ni kusikiliza mtu kwa huruma badala ya kumtolea mashauri mengi.​—Mithali 20:5; 21:13.

Zungumzeni Matatizo Yale Yenye Kuamsha Hasira kwa Urahisi

11-13. (a) Sana-sana ni wakati gani njia ya kupashana habari kibinafsi inapokuwa ngumu? (b) Kwa sababu gani Sara aliudhika sana? (c) Yeye angaliweza kufanya nini, hata hivyo alifanya nini?

11 Namna gani mwenzi wako akifanya au akiruhusu jambo fulani litukie ambalo linakuumiza na ambalo lingeweza hata kuleta uharibifu fulani katika ndoa yenu? Unaweza kumpashaje habari nyakati kama hizo? Mfululizo wa matukio yaliyotukia katika maisha ya Abrahamu na Sara unatoa ufahamu wenye msaada.

12 Katika siku ambayo Isaka mwanaye aliachishwa kunyonya, Sara alimwona Ishmaeli, mwana ambaye Abrahamu alijipatia kupitia Hajiri yule mtumwa, ‘akifanya dhihaka’ juu ya Isaka.b Bila shaka, Ishmaeli huyo aliyekuwa amefika umri wa miaka 13 alimcheka-cheka kwa madharau mdogo wake wa miaka mitano na nusu, ambaye sasa alikusudiwa achukue nafasi ya Ishmaeli akiwa ndiye mrithi wa Abrahamu aliyewekwa na Mungu. Sara aliudhiwa sana sana na usemi huo wa kutisha-tisha. Ingekuwaje kama mume wake angekufa kwa ghafula? Je! labda Hajiri angeweza kusadikisha watu wale wengine kwamba mwanaye, wala si Isaka, ndiye anapaswa kuwa mrithi wa ile ahadi?​—Mwanzo 17:19; 21:8, 9.

13 Sara angaliweza kuogopa kwamba Abrahamu angechukizwa na kwa hiyo akose kumwambia maoni yake ya moyoni, kwa maana alijua kwamba alimpenda sana Ishmaeli. Huenda ikawa Sara hakuwa ametokeza mambo mengine kama hili lenye kutatiza, kwa kuruhusu upendo wake uyafunike. Yeye alijulikana kuwa mke ‘aliyemtii Abrahamu, akamwita Bwana.’ (1 Petro 3:6) Lakini hiyo ilikuwa hali yenye hatari. Bila shaka, Sara angaliweza kumnyamazia Abrahamu na kuwa akimtendea mambo kwa kununa, akitumaini kwamba Abrahamu angekuja kujua kilichokuwa kikimsumbua. Lakini sivyo. Sara alimpasha habari! “Fukuza kijakazi huyu na mwana wake,” akasema, “kwa maana mwana wa kijakazi huyu hatariti pamoja na mwana wangu, hata na Isaka”!​—Mwanzo 21:10, ZSB.

14. Abrahamu alichukua hatua gani, na kwa sababu gani?

14 Abrahamu alichukizwa sana na dai hilo; aliruhusu shauku ya upendo aliyomwonea Ishmaeli imzuie kufikiria mambo vizuri, hata kama ni kwa muda mfupi tu. Lakini je! Abrahamu alifoka akisema hivi kwa ukali: ‘Unasema na nani kwa njia hiyo! Thubutu! Unafikiri nani kichwa cha jamaa hii?’ Hapana. Kwa kweli, Mungu alimwambia hivi: “Usiache lo lote ambalo Sara anaendelea kukuambia liwe lenye kukuchukiza juu ya yule kivulana na juu ya msichana aliye mtumwa wako. Sikiliza Sauti yake.” Hivyo ndivyo Abrahamu alivyofanya asubuhi yake Hatua hiyo ikahifadhi amani na kusudi la Mungu likatimizwa​—ingawa Abrahamu aliona maumivu makali sana.​—Mwanzo 21:11-14, NW.

15, 16. (a) Taja matatizo fulani yanayoweza kuleta mgogoro katika ndoa za watu. (b) Watu waliooana wanaweza kuwaigaje Abrahamu na Sara, na matokeo yatakuwa nini? Toa mfano.

15 Leo matatizo mengi yanaweza kuleta mgogoro katika ndoa yako. Kwa mfano, huenda ukawa na maoni ya kwamba mwenzi wako anamfikiria mtu mwingine kwa njia isiyofaa. Uchunguzi pamoja na matukio ya kweli yasiyohesabika unaonyesha kwamba ikiwa mume au mke anatumia wakati mwingi mno kuongea na rafiki wa kibinafsi, sana-sana ikiwa huyo ana umbo lililo tofauti na lake (la kike au kiume), jambo hilo linaleta mgogoro kweli kweli katika ndoa. Au inaweza kuwa kwamba mwenzi wako anatumia sana muda mwingi kutunza kazi yake, kufanya jambo fulani la kujifurahisha tu au namna ya tafrija inayoharibu ndoa yenu. Huenda ikawa mwenzi wako amekuwa baridi kwa maoni yako ya moyoni. Je! wewe unafuata mfano wa Sara na kuzungumza mambo hayo yenye kuudhi na labda uzuie kusiwe na madhara zaidi? Na ikiwa mwenzi wako atatokeza jambo litakalokuumiza moyoni, je! utatenda kama Abrahamu, ufikirie kwa uzito mwelekezo wa Mungu? Je! kutenda hivyo kusingemtia moyo ili njia ifunguke ya kupashana habari waziwazi?​—Mithali 27:5.

16 Bila shaka, “mapendo yanafunika zambi nyingi.” (1 Petro 4:8, ZSB) Kwa hiyo usitokeze matata katika hali zote za kutokuelewana na katika vikosa vya kibinadamu. Lakini wengine wamesitasita sababu ya woga, wakakosa kuzungumza matatizo mazito; au kama waliyazungumza, mwenzi wa ndoa aliwaonyesha madharau. Ni jambo la kusikitisha kwamba kwa njia hiyo inaimarishwa mienendo isiyogeuka ambayo mara nyingi inaleta msiba wa ndoa. Mke mmoja Mkristo aliudhika sana kwa muda fulani kwa sababu mume wake hakuwa akifikiria maumbile yake ya kimoyoni wakati wa kufanya ngono. Alijisikia kwamba alikuwa ‘akitumiwa’ kwa kusudi la kutosheleza tamaa za mume wake. Akafikiria kumwacha mume wake. Hakuwa hata amezungumza jambo hilo na mume wake, akiogopa kwamba hangeelewa mambo. Aliposhauriwa na Mkristo aliyekomaa, mke huyo mwishowe alifunulia mume wake maoni yake ya kuudhika. Kumbe mume hakuwa amejua namna matendo yake yalivyokuwa yakimwumiza mke wake! Alifanya mabadiliko yaliyohitajiwa na sasa tatizo hilo haliharibu furaha yao. Endeleza hali ya kuheshimika ya ndoa yako kwa kusitawisha upashanaji-habari wa kibinafsi.

Sheria ya Fadhili za Upendo Juu ya Ulimi

17. Ni “sheria” gani inayopasa kuwa juu ya ulimi wa watu waliooana? Toa mfano.

17 Lakini je! uhitaji wa kupashana habari kibinafsi unampa mtu kibali ya kuropoka maneno bila kufikiri? “Kuna anenaye bila kufikiri, kama kuchoma kwa upanga; bali ulimi wa mwenye haki ni afya.” (Mithali 12:18) Ndiyo, hata kama wewe ndiwe uliye upande wa haki na makusudi yako ni mazuri kabisa wakati kunapokuwa na tatizo, bado maneno yanayosemwa bila kufikiri ‘yanachoma.’ Basi kuna sababu nzuri ya kumtaja mke hodari kuwa ni mwenye “sheria ya fadhili za upendo” juu ya ulimi wake. (Mithali 31:26, NW) Anakuwa na kawaida ya kunena kwa fadhili bila ugeugeu mpaka usemi wake unaitwa sheria. Wakati mwanamume anaposhindwa kutimiza jambo fulani analojitahidia, anathamini sana ikiwa ulimi wa mke wake una sheria hiyo! Mume mmoja Mkristo alipondeka moyo kwa sababu ya kupata hasara katika kazi yake. “Hata hivyo umejaribu,” akasema mke wake mwenye fikira za huruma. “Safari ile nyingine mambo yatakuwa mazuri zaidi.” Mume wake alijisikia vizuri weee!

18. Mke mmoja aliifuataje “sheria” hiyo kwa ukamili zaidi?

18 Sana-sana maneno ya fadhili yanahitajiwa wakati wa mabishano. Maneno ya dharau kali ya mke mwenye kuleta magombano yanaweza kufukuzia mbali mume wake na kumfanya apendelee kukaa katika jangwa lisilozaa kitu. (Mithali 19:13; 21:19) Mke Mkristo aliamua kuifuata kwa ukamili zaidi sheria hiyo kwa sababu ya magombano yaliyokuwa katika ndoa yake. Kwa njia gani? “Siku hizi ninaposumbuliwa na jambo fulani sipayuki ovyo kama zamani,” akaeleza. “Naungoja wakati unaofaa kabisa wakati tunapokuwa peke yetu. Hata nazuia hali za uso wangu zisionyeshe nimeudhika wala simshushii mume wangu heshima mbele ya watoto. Hakika kufanya hivyo kumeleta maendeleo!” Bila shaka, ni lazima wote wawili, mume na mke, wafikirie namna maneno yao yanavyoweza kuleta mafaa makubwa au madhara makubwa katika hali yao ya kuheshimiana.​—Mithali 25:11; Wagalatia 5:15.

19, 20. (a) Kuwa na “busara” kunatia nini ndani? (b) Busara ilizuiaje mume mmoja asikasirike, na matokeo yakawa nini? (c) Ni nini mengine ya maulizo yenye kuonyesha wazi namna mtu alivyo?

19 Ni nini kinachohitajiwa wakati maono ya moyoni yanapowaka? Ni busara! “Moyo wa mwenye hekima unafanya kinywa chake kionyeshe busara, nao unaongezea midomo yake usadikishi.” (Mithali 16:23, NW) Busara inatia ndani kufikiria matokeo ya baadaye, si kufikiria mambo ya wakati huo tu. Kwenye Nehemia 8:8 neno la Kiebrania limetafsiriwa kuwa “maana.” Busara inakomeshaje ubishi? Mume mmoja aliingia ndani ya nyumba akakuta mke wake akitupa kwa hasira vijiko, visu na nyuma katika chumba alimokuwa. “Wewe hunijali!” akampayukia mume wake huku akitokwa na machozi. “Kazi yako ni kuja nyumbani na kutumia wakati wako katika bustani. Mimi nahitaji msaada!” Lakini kuvurugika kimwili na katika maoni ya moyoni ndiko kulikuwa kukimsumbua-sumbua mke huyo. Juzi tu alikuwa amezaa mtoto na sasa alikuwa akitazamia kuzaa mwingine. Alijisikia kuwa mfungwa wa nyumbani. Mume wake alikuwa na busara. Yeye hakukasirishwa na mropoko wa maneno ya mke wake yasiyo ya Kikristo. Alifahamu ni nini kilichokuwa kikimvuruga mke wake. Basi alijibuje? “Pole, mpenzi. Ingalinipasa kuwa ndani nikikusaidia.” Baada ya muda mfupi mke akapoa. “Nilianza kumpa heshima kubwa zaidi,” ndivyo mke alivyofunua baadaye.

20 Yanasema kweli kabisa maneno ya Mithali 19:11: “Busara ya mtu huiahirisha hasira yake; nayo ni fahari yake kusamehe makosa”! Je! wewe unaonyesha busara hiyo? Je! badala ya kukasirishwa na maneno ya mwenzako, unafikiria kwanza sababu gani yamesemwa? Je! wewe unaweza kusamehe mwenzako kwa kosa alilokutenda? Busara inaweza kuongezea pia usadikishi wa ombi unalomtolea yule mwingine. Ndiyo, mwenzi aliye na akili, mwenye busara, ni kipawa kutoka kwa Yehova naye anasaidia kufanya ndoa iwe ya thamani kubwa.​—Mithali 19:14.

Mchukuliane Tofauti za Kutokuelewana na za Kutokamilika

21. Kuchukuliana tofauti za kutokuelewana kunaweza kuiwekaje ndoa yenu iwe yenye thamani kubwa?

21 Hakuna watu wawili waliooana watakaokubaliana katika kila jambo, hata wafanye jitihada nzuri namna gani. Kutakuwako tofauti za kutokuelewana. Mwangalizi Mkristo anayesafiri, ambaye amekuwa mtu aliyeoa kwa muda wa miaka inayozidi 25, alitoa maoni haya: “Watu fulani waliooana wanasema, ‘Sisi ni watu wenye kutofautiana sana katika utu wetu!’ Halafu saa zote wanaweka fikira zao juu ya tofauti zao na baada ya muda mfupi wanaona hawawezi kuishi tena pamoja. Ni kweli kwamba mke wangu nami tunatofautiana katika mapendezi fulani, lakini tunapatana pia katika mapendezi mengine mengi. Kwa kukaza fikira juu ya mambo tunayoyapenda sisi wote, ndoa yetu inazidi kuwa yenye thamani kubwa kila siku.” Je! wewe pia una nia iyo hiyo ya kuchukuliana tofauti za kutokuelewana katika ndoa yenu?

22. (a) Ni nini kinachoweza kusaidia wenzi wa ndoa wapate uradhi katika ndoa? (b) Ni nini kichocheo kilicho na nguvu zaidi cha kuiweka ndoa yenu katika hali ya kuheshimika?

22 Mwenzi mkamilifu hawezi kupatikana mahali po pote. Uradhi unaweza kupatwa kwa kujifunza kuvumilia tofauti za kutokuelewana na kuvumiliana katika udhaifu mdogo-mdogo. (Wakolosai 3:13) Uhakika ni kwamba kichocheo kilicho na nguvu zaidi cha kuiweka ndoa yetu ikiwa katika hali ya kuheshimika ni uhusiano wetu pamoja na Mungu, kumtaka abaki akiwa Rafiki yetu. Mwendo wa Wakristo ambao wamejitahidi kufanikisha ndoa yao kwa sababu ya kuheshimu uhusiano wao na Yehova unastahili sifa kweli kweli.

23. Tunaweza kuiwekaje ndoa yetu katika hali ya kuwa yenye thamani kubwa?

23 Ndoa yo yote inayoachiliwa bila kutunzwa itaharibika. Lakini unaweza kuirudishia matumaini mazuri kwa kufanya jitihada ya kweli ya (1) kusitawisha njia ya kupashana habari kibinafsi, (2) kushika sheria ya fadhili za upendo juu ya ulimi wako na (3) kuchukuliana tofauti za kutokuelewana na za kutokamilika. Mambo hayo, pamoja na baraka ya Mungu, yataiweka ndoa yenu ikiwa yenye thamani kubwa, si kwenu tu, bali pia kwa Mwanzilishi Mkuu wa ndoa.

[Maelezo ya Chini]

a Kamusi inayoitwa A Greek-English Lexicon of the New Testament, ya J. H. Thayer. Neno ilo hilo linatumiwa kueleza “damu yenye thamani kubwa” ya Kristo,—1 Petro 1:19, NW.

b Biblia inafunua kwamba lililohusika halikuwa mchezo wa kitoto tu, bali ni zaidi ya hilo. Yalikuwa ‘mateso.’​—Wagalatia 4:29, 30, NW.

Wewe Unaweza Kukumbuka?

□ Kwa sababu gani kupashana habari kibinafsi kunahitajiwa sana?

□ Kufuata mfano wa Abrahamu na Sara kutaletaje maendeleo ya kupashana habari?

□ Mtu anaonyeshaje kwamba “sheria ya fadhili za upendo” iko juu ya ulimi wake (awe ni mume au mke)?

□ Busara inafanyaje ndoa izidi kuwa yenye kuheshimika?

[Sanduku katika ukurasa wa 6]

Njia ya Kupashana Habari Ikoje Kati Yenu??

(1) Ni muda wa kiasi gani mnaotumia mkiwa pamoja kuongea tu?

(2) Ni mangapi kati ya mazungumzo yenu yanayokuwa ya kutaja mambo ya kikazi tu (mambo ya kinyumbani, watoto, mali, na hivyo hivyo) badala ya kuelezana mawazo na maoni ya moyoni mliyo nayo?

(3) Je! Kuna matatizo fulani au maoni ya moyoni uliyo nayo, lakini hujioni ukiwa huru kuyazungumza na mwenzi wako?

(4) Ni muda gani umepita tangu mmoja wenu alipompa mwenzake zawadi, kwa kusudi la kuonyesha shauku ya upendo tu?

(5) Ni mara ngapi mnaposhikana mikono au kugusana, bila kuhesabu zile nyakati za kufanya ngono?

[Picha katika ukurasa wa 8]

Mke aliye na “sheria ya fadhili za upendo” juu ya ulimi wake anathaminiwa sana sana, hasa nyakati za mkazo

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki