Je! Ungeweza Kuonyesha Upendo kwa Njia Nzuri Zaidi?
KATI ya sifa zote tunazoweza kusitawisha ‘katika hizo iliyo kuu ni upendo.’ (1 Wakorintho 13:13) Namna ya upendo ambao mtume Paulo alikuwa akitaja hapa si éros, upendo unaotegemea uvutano wa hali za kiume na kike; wala hakuwa akitaja storgé, upendo unaotegemea uhusiano wa kijamaa; wala hakuwa akitaja philía, upendo unaotegemea ufanani wa mambo ambayo watu wawili wanapenda au wasiyoyapenda wote pamoja. Bali, neno la Kigiriki ambalo mtume alitumia hapa lilikuwa agápe, upendo wenye kuelekea mema unaotegemea kanuni na wenye kujitoa kweli kweli ili kusaidia wengine.
Kati ya njia ambazo tunaweza kuonyesha upendo ni kuwapa watu vitu vya kimwili. Tendo lenyewe la kufanya hivyo ni zuri, lakini je! kunaweza kuwa na njia nzuri zaidi? Mwanafunzi mmoja wa Biblia mwenye kupendwa sana wa miaka ya zamani anasemekana kuwa alitoa maoni haya: ‘Kama tunaweza kuchagua kati ya kutoa pesa nyingi zaidi zitumike kwa kazi ya Bwana au kutoa mwingi zaidi wa wakati wetu na nguvu zetu, mwendo wa hekima zaidi ungekuwa ni kuchagua kufanya jambo hilo la pili—kutoa mwingi zaidi wa wakati wetu na nguvu zetu.’ Kwa sababu gani? Kwa sababu kufanya hivyo kunaweza kufanya Mungu apate heshima na sifa nyingi zaidi na hata mtu mwenyewe ajipatie furaha zaidi.
Kwa wingi, mashahidi Wakristo wa Yehova wanaithamini kanuni hiyo. Miaka michache iliyopita, kichwa cha gazeti moja la Pittsburgh kilisema hivi: “Mashahidi wa Yehova Wachanga Nguvu Zao Kujenga Jumba la Makusanyiko Karibu na Uwanja wa Ndege.” Makala hiyo ilikuwa na picha kubwa ya kazi hiyo yenye kuendeshwa na ikaeleza kwamba maelfu walikuwa wamejitolea kusaidia na kwamba nyakati nyingine wengi kupita kiasi walikuja kusaidia. Aliposoma ripoti hiyo, afisa wa kidini wa kanisa la Kiprotestanti alilalamika juu ya itikio dogo sana alilokuwa akipata alipoita washiriki waje kumsaidia katika shughuli fulani aliyokuwa akisimamia: “Ebu ifikirie hesabu kubwa sana ya makanisa ya Kiprotestanti na vikundi vyote vyenye ushirika vinavyohusika katika shughuli hii . . . [na hali] ni shida kwangu kupata watu sita kwa safari moja wenye nia ya kutumia siku nzima wakifanya kazi bila malipo.” Ni wazi kwamba waenda-kanisani hao wengi waliona ni vyepesi kuchanga pesa zao kuliko kujitoa wao wenyewe, kutoa wakati na nguvu zao.
Walakini, tukitoboa mambo wazi kama walivyofanya waandikaji wa Biblia walioongozwa na Mungu, tutasema kwamba wale wanaojisema kuwa ni watumishi waliojiweka wakf kabisa kwa Yehova Mungu huenda nyakati nyingine hata wao wakapungukiwa katika jambo hilo. Kwa mfano, kwa habari ya ujenzi wa Jumba la Makusanyiko la Mashahidi wa Yehova lililojengwa majuzi, mwenye kusimamia ujenzi alisema kwamba akina ndugu walitoa michango ya pesa kama mwujiza; ingawa jumba lenyewe linagharimu karibu dola milioni moja, wakati liishapo litakuwa karibu kumaliza kulipiwa. Walakini, ulipokuwa ni wakati wa kusaidia ujenzi kwa kutoa wakati na jitihada zao wenyewe, hali ya kuthamini waliyoonyesha upande wa pesa ilikosekana.
Kwa sababu gani kulikuwa na tatizo? Ni wazi kwamba wengi walikuwa na maoni ya kwamba michango yao ya pesa walizotoa kwa ukarimu ilitosha. Ni kweli kwamba walifanya vizuri sana kutoa michango kwa ukarimu. Lakini kwa sababu tu walitoa pesa, hiyo haikuonyesha kwamba sasa walikuwa huru wasiweze kusaidia kwa kutoa wakati na nguvu zao kama wangeweza kufanya hivyo. Inaweza kusemwa kwamba Yesu Kristo alionyesha hivyo wakati alipomwambia mtawala fulani kijana mwenye utajiri amfuate, licha ya kuuza mali zake na kuwapa maskini pesa zilizotokana na mali hizo.—Luka 18:18-23.
Kanuni iyo hiyo inahusu pande zote za utumishi wa Kikristo. Kwa kweli, je! lisingekuwa jambo zuri zaidi mtu akitumia wakati wote na nguvu zake zote katika utumishi wa Mungu ikiwa anaweza kufanya hivyo? Huenda likawa jambo jepesi kutumbukiza pesa katika sanduku la michango kwenye Jumba la Ufalme kuliko kufika kwenye jumba lenyewe ili kulisafisha na kutunza wanja zinazolizunguka wakati unapopaswa kufanya hivyo. Lakini je! jambo hilo la pili silo linaloweza kuonyesha upendo zaidi? Huenda ikawa vyepesi kuchanga pesa za kuchapa Biblia na vitabu vya kusaidia watu waifahamu Biblia kuliko kutumia wakati kupelekea watu vitabu hivyo katika nyumba zao, kuzihubiri habari njema za ufalme wa Mungu na kujitahidi kufanya wanafunzi. Lakini tena, je! jambo hilo la pili silo njia nzuri zaidi ya kuonyesha upendo, na je! silo lililotabiriwa na Yesu katika unabii na akawaagiza wafuasi wake walifanye? Ndilo, kama inavyoweza kuonekana katika Mathayo 24:14 na Mathayo 28:19, 20.
Kanuni hiyo inahusika katika jamaa pia. Ni jambo la kusifika mume akitumia pesa kununulia mkewe vitu. Lakini je! kuonyesha upendo kwa kumpa mkewe wakati wake (kushinda pamoja), kumsikiliza na kupendezwa naye siyo mambo yanayoonyesha upendo mwingi zaidi? Kwa kweli, huenda yeye akawa mkarimu sana katika mambo ya pesa na asiwe anampenda mkewe kikweli. Kulingana na jambo hilo, wakati mmoja alikuwako mwanasheria aliyekuwa mashuhuri kisiasa ambaye alimpa mkewe vitu vingi kwa ukarimu. Lakini mke huyo akashangaa sana siku moja alipojua kwamba mume huyo alikuwa na mwanamke mwingine wa kando. Kwa hiyo huenda hata kutoa vitu vya kimwili kusiwe ni wonyesho wa upendo wa kweli. Ikitegemea hali, huenda waume wakaweza kutoa vitu vingi zaidi au vichache zaidi vya kimwili, lakini kwa habari ya ile “njia iliyo bora,” matajiri kwa maskini wana nafasi zinazolingana.—1 Wakorintho 12:31–13:13.
Hali inakuwa ivyo hivyo kwa habari ya wazazi kuonyesha watoto wao upendo. Kwa sababu wazazi fulani walipata vitu vichache vya ulimwengu huu walipokuwa watoto, wanaazimia kwamba watoto wao watapata wingi wa vitu vizuri-vizuri, mavazi mazuri, vitu vya kuchezea, pesa za kufanyia mambo mengine ya kuburudisha akili na kadhalika. Lakini wakiacha mambo yaishie hapo, wao wamekosa sana hekima. Jambo la maana zaidi ni kwamba wajitoe wao wenyewe, watoe wakati wao, mapendezi na nguvu zao, na kuelekeza hayo yote kwa watoto wao. Ni kweli kufanya hivyo kunaweza kuwagharimu zaidi upande wa kujinyima, lakini mwendo wa namna hiyo ni wenye thawabu nyingi zaidi pia. Ndiyo kusema, usiache televisheni au yaya akae badala yako kukulelea watoto, isipokuwa katika hali zisizokuwa zimetazamiwa au nyakati nyingine chache; hapana, msifanye hivyo ninyi wazazi ndipo mpate nafasi ya kwenda-kwenda kwenye vilabu vya usiku ati!
Kwa hiyo na tukumbuke daima kwamba njia iliyo nzuri zaidi ya kuonyesha upendo ni kujitoa sisi wenyewe, kutoa wakati wetu, nguvu zetu, mapendezi yetu, usikivu wetu, mapenzi yetu yenye shauku. Kutoa vitu vya kimwili kusaidia kazi ya Mungu au wale tunaowapenda ni jambo zuri, kwa maana vitu hivyo vinahitajiwa kabisa; lakini haitupasi kamwe kutosheka na utoaji wa namna hiyo ikiwa tunaweza kuvitoa pia vitu vilivyo na thamani zaidi. Kisha ikiwapo nafasi ya kuchagua moja kati ya mambo hayo mawili, acheni tuuonyeshe upendo ulio mzuri zaidi na vilevile hekima iliyo kubwa zaidi kwa kujitoa sisi wenyewe, kuwapa watu hata “nafsi zetu wenyewe.” Hivyo ndivyo alivyofanya mtume Paulo, na lo! Mungu alimbarikije!—1 Wathesalonike 1:6-10; 2:8, NW.