Anasa Imewekwa Mahali pa Mungu—Kwa Sababu Gani?
“SI WEWE peke yako,” linasema tangazo lenye herufi kubwa na nene. “Jumapili hii, Waamerika wengine milioni 61 walichagua pia kutokwenda kanisani.” Tangazo lenyewe ni jaribio la kuwafanya wengine kati ya mamilioni hayo, ambayo ni asilimia 41 ya Waamerika wote walio na umri wa miaka 18 au zaidi, waende kanisani.
Mahali kwingine, hasa katika Ulaya ya Magharibi, mambo yako namna ile ile, isipokuwa asilimia yenyewe ni ya kiasi cha juu zaidi. Kwa mfano, wakati wa Jumapili yo yote katika Uingereza, karibu asilimia 98 ya washiriki wale milioni 28 wa “Church of England” (Kanisa la Uingereza) hawaoni kwenda kanisani kuwa jambo la maana. Ingawa hapa na pale hesabu ya wenye kwenda imeongezeka-ongezeka, ulimwenguni pote maelekeo ya kushuka chini kwa hesabu ya wanaokwenda yanaonekana wazi.
Sababu Inayofanya Watu Waache
Ni nini kinachofanya umati mkubwa wa watu waache kwenda makanisani? Ni wazi kwamba hilo ni ulizo gumu sana. Hali ya kutokuamini Mungu yuko, utafutaji mwingi wa mali, kushindwa kwa makanisa kutosheleza watu na mambo mengine mengi yameshiriki kuwafanya watu waache kwenda. Lakini je! wote walioacha walifanya hivyo kwa sababu wameacha kumwamini Mungu na hivyo wanaiona dini kuwa kitu bure tu? Sivyo.
Katika kitabu chao kinachoitwa The Search for America’s Faith, George Gallup, Mwana, na David Poling walioshirikiana kukiandika walionyesha mshangao kwa kukuta kwamba “inastaajabisha sana kuona kwamba wengi wa wasioenda kanisani ni waamini sana; wala katika visa vingi si ukosefu wa imani ambao umefanya watu wawe hawaendi kanisani.” Basi, je! ni kitu gani kinachowafanya wakae bila kwenda?
Gallup na Poling waliandika mambo manne makuu yanayowavuta wale wasioenda kanisani:
“1. Michezo, tafrija, na mapendezi ambayo watu wanataka kufanya wasipokuwa katika kazi za kawaida
2. Kushirikiana utendaji mbalimbali pamoja na rafiki zao
3. Kuwa na orodha ya kazi inayofanya iwe vigumu kwenda kanisani
4. Tamaa ya kutaka ‘wakati mwingi zaidi kwa ajili yangu binafsi na kwa ajili ya jamaa.’”
Je! si kweli kwamba watu walio wengi sasa wanaifikiria na kuitazamia siku ya Jumapili kuwa wakati wa kustarehe na kujipumzisha? Kwa wale walio na pesa, kuendesha motokaa wakatembee sehemu za mashambani, kwenda kufanya pikniki (mandari) au kuzunguka sehemu za nje ni mambo yenye kuburudisha sana zaidi ya ibada za kanisani. Wanaona kwamba kunyosha maungo kwa kukimbia, kuogelea, kucheza mpira au mchezo mwingine wa namna hiyo ni jambo lenye kuchangamsha mtu zaidi ya kusikiliza mahubiri yasiyo na upendezi. Na, kwa kawaida, watu wanafanya utendaji huo mbalimbali wakiwa wamejitoa na kutia juhudi kweli kweli, hayo yakiwa na mambo ambayo yangeweza kuaibisha mwenda-kanisani wa wastani.
Matokeo ni nini? Ni wazi kwamba maoni hayo ya kupenda anasa yamepunguza vibaya sana hesabu ya wenye kwenda makanisani. Lakini jambo lililo zito zaidi kwa watu mmoja mmoja ni kwamba kufanya hivyo kumemaanisha kwamba kupenda anasa kumechukua nafasi ya kumpenda Mungu. Dini, au kiasi kilichobaki cha dini, imeachiwa nafasi ya vipindi vichache vya pekee katika maisha, kama vile arusi na maziko, na huku kuwa na hali ya kumcha Mungu kungali kunaonwa kuwa jambo la maana kabisa. Kufuatia mambo ya kimwili kumechukua nafasi inayopasa kuwa ya kufuatia mambo ya kiroho.
Wimbi hilo lenye kuongezeka la ufuatiaji wa mambo ya kimwili kati ya watu wanaosema wanamwamini Mungu linalingana na jambo ambalo mtume Paulo alikuwa akifikiria wakati aliposema watu wangekuwa “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu.” Naye alipokuwa akisema habari za watu hao, alikuwa akiwatumia kama onyo na kama jambo lenye kuonyesha kufika kwa “siku za mwisho” ambapo “kutakuwako nyakati za hatari.” (2 Timotheo 3:1, 2, 4) Uhakika wa kwamba watu wengi sana leo ‘wanaweka anasa katika mahali pa Mungu,’ kama Paulo alivyotabiri, ni mmoja wa shuhuda nyingi zinazoonyesha kwamba sisi tunaishi katika siku za mwisho.—The New English Bible.