‘Kuonekana kwa Nje Kama Watu Wenye Kumcha Mungu’
KWA sababu ya kupungukiwa na watu wa kuyaunga mkono, makanisa yanajaribu sana kuwakusanya pamoja au kuwarudisha washiriki wayo. Lakini njia wanazotumia mara nyingi zinafanya mambo yaharibike zaidi. Wanatumia njia ya kufurahisha watu kwa anasa. Namna gani? Angalia mifano michache ya mambo ambayo makanisa yanafanya ili kuvuta wale wasioenda kanisani:
“Leo kuna vikundi 3,000 vya huduma ya kufanya mambo ya kuchekesha katika U.S. ambao wanavaa pua kubwa-kubwa na suti za rangi nyingi ili kumtumikia Mungu,” linaripoti gazeti Time. Waigizaji wenye kujiita ‘Wapumbavu kwa Ajili ya Kristo’ au ‘Wapumbavu Watakatifu’ wanacheza dansi, wanafanya viinimacho vya kuchekesha, wanaigiza michezo kwa ishara za mdomo bila kutoa sauti, wanaendesha baiskeli ndani ya kanisa na kupitishia watu mahindi ya kukaangwa na kutupia wahudhuriaji wa kanisa vikaratasi vya rangi mbalimbali na mipira iliyopulizwa pumzi ndani. Katika Saskatoon, Kanada, mkusanyiko wa Ushirika wa Kikanada wa Elimu ya Wachungaji ulitia ndani masomo ya kusomea “michezo ya Kikristo ya kuchekesha watu kwa upumbavu” ili iwe njia ya kuwavuta watu.
“‘Kuvuta Fikira Zao’—Mwevanjeli Afanya Hivyo kwa Kutumia Mchezo wa Kupigana Karate.” Hicho kilikuwa kichwa cha makala ya gazeti lenye kueleza habari za “mahubiri yenye maonyesho” yanayofanywa na mhubiri Mbaptisti mwenye kusafiri. “Watu hawataki kuja nje wasikie mhubiri akihubiri, na kuwaambia makosa wanayofanya,” akaeleza. “Lakini watakuja nje waone mwenye kuwaonyesha ustadi wa kupigana karate.” Mhubiri huyo alisema kwamba watu walio wengi wanabaki kusikiliza mahubiri yake baada ya kuona onyesho lake. “Ni mara chache tu mtu mmoja mmoja anapoondoka na kwenda zake,” akaongezea. “Lakini si mara nyingi mno.”
Chini ya kichwa chenye kusema “Makanisa Yanatumia Miujiza ya Kiinimacho Kuvuta Wanakanisa,” jarida linaloitwa The Wall Street Journal linataja maneno ya mchungaji mmoja wa Indiana kuwa akisema kwamba “wakati mwenye kufanya miujiza ya kiinimacho anapoenda kwenye mimbara ya kanisa, watu ambao hawajahudhuria muda wa miezi mingi wanakuja kwenye ibada.” Ule Ushirika wa Wafanya Miujiza ya Kiinimacho usio wa dini yo yote unakadiria kwamba kuna wahudumu-wafanya-miujiza zaidi ya elfu moja katika taifa lote, na ushirika huo unadhamini kila majira ya kiangazi seminari za kufundisha njia mpya za kufanyia viinimacho.
“Kuna Mtoa-Mavazi Katika Mimbara ya Kanisa.” Hivyo ndivyo gazeti moja la kutangaza habari lilivyoripoti juu ya tukio lililoendelea katika kanisa la Wapinga-Utatu huko Dallas. Kanisa hilo lilionyesha “mchezi dansi wa kushangaza sana” katika ibada yalo ya Jumapili, na “wakati mwanamke huyo alipomaliza mchezo wake kilichobaki ni kipande chembamba tu cha nguo chenye kufunika sehemu iliyo katikati ya miguu yake kwa kufungwa kiunoni, nao wahudhuriaji wa kanisa walibaki wakiwa wanafikiri-fikiri,” ndivyo ilivyosema ripoti hiyo. Watoto pamoja na washiriki 200 wa kanisa hilo walio watu wazima walihudhuria maonyesho hayo. “Mimi sijasikia lalamiko hata moja,” akasema mhudumu wa kanisa hilo. “Jambo hilo lilipatana vizuri sana na ibada yetu.”
Kwa vyo vyote hivyo si visa vinavyotokea mara chache tu katika madhehebu fulani za kiajabu-ajabu tu. Yale makanisa ambayo yamekuwako kwa muda mrefu, yanayosemwa kuwa yenye kuheshimika ati, yanaanza kutumia njia zile zile za kupumbaza watu. Zaidi ya kuwa na wachezaji wa michezo ya ucheshi wa upumbavu na kutumia miujiza ya kiinimacho, makanisa yanatumia pia maonyesho ya waimbaji wa nyimbo za vituko vya mashambani, wachezaji wa muziki wa roki, wacheza-dansi wa kutumia matumbo, maonyesho ya wanaanga, ya wachezaji wa sinema walio hodari na ya watu wengine wenye kusifiwa sana. Kusudi la jitihada hiyo ni kujiimarisha ili yaache kupungukiwa na washiriki.
Lakini hata ikiwa nyingine za “nafsi zilizopotea” zinavutwa kwa njia hiyo zije kanisani, je! kweli zinasaidiwa ziwe ‘zenye kumpenda Mungu’ ikiwa kinachowapendeza ni dansi ‘ya kiajabu-ajabu’ au onyesho la miujiza ya kiinimacho? Badala ya kuwa hivyo, je! kwa njia hiyo hawafanywi wawe ‘wapenda anasa’ zaidi sana, wakiwa na dhamiri iliyotulizwa kwa sababu sasa wanaweza kujitia katika anasa kwa kukubaliwa na kanisa lao? Kwa kweli, wao wamekuwa watu ambao ‘kwa nje wanaonekana kama watu wenye kumcha Mungu, lakini wanaikana nguvu yake.’—2 Timoteo 3:5, HNWW.
Unabii Unatimizwa
Yote hayo yalimsukuma padri William Rauscher kusema: “Leo makanisa mengi mno yamekuwa sehemu kuu za vitumbuizo vya Mzuka Mtakatifu ambavyo si vitakatifu hasa, bali kwa kadiri kubwa vinahusiana na mizimu. Kadiri kubwa ya ile inayosingizia kuwa dini ingemshtua Mtakatifu Paulo kama angekuwapo sasa.” Lakini, kusema kweli mtume Paulo hangeshtuka sana kama angekuwapo. Kwa sababu gani? Kwa sababu, kama vile tumeona, yeye aliongozwa na Mungu aandike kwamba katika siku za mwisho watu ‘wangeweka anasa katika mahali pa Mungu’!
Kwa kutumia maneno “wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu” (Union Version), mtume Paulo anavuta fikira kwenye hali ya watu hao yenye mpingano na isiyo na upatani, na kwa hiyo ni hali ya unafiki. Ingawa bado wao wanataka dini iwe katika maisha yao, wameweka anasa katika mahali pa Mungu ikiwa ndicho kipenzi chao wanachokifuatia kwa juhudi nyingi. Kwa kufanya hivyo, wamefanya anasa iwe mungu wao.
Kuongezeka kwa hali ya kufuatia mambo ya kimwili na kupungua kwa uungaji mkono wa watu kwa makanisa ni shuhuda nyingine za wazi za kuonyesha kwamba tunaishi katika siku za mwisho za mfumo wa mambo ya sasa. Lakini, zaidi ya hilo, mambo hayo yanaonyesha kwamba tunaishi kwenye ule mwisho wenyewe, sehemu ya kumalizia, ya siku za mwisho.