Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w88 5/15 uku. 27
  • Kujua Yaliyo Katika Habari

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kujua Yaliyo Katika Habari
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Habari Zinazolingana
  • Ni Nani Ataeneza Evanjeli Katika Uingereza?
    Amkeni!—1995
  • Kanisa La Kweli na Msingi Wake
    Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele
  • Uanastampu—Hobi Inyweayo Wakati Iliyo Biashara Kubwa
    Amkeni!—1995
  • Kanisa—Mabadiliko na Mvurugo
    Amkeni!—1993
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
w88 5/15 uku. 27

Kujua Yaliyo Katika Habari

Wacheshi wa Mambo ya Kipumbavu kwa Ajili ya Kristo?

“Wacheshi-Wapumbavu Barabarani” kilikuwa ndicho kichwa kikuu kilichotokea katika Church Times. karatasi-habari ya Kanisa la Uingereza. Kilikuwa kikitangaza ziara ya kila mwaka ya kikundi chenye kufanya Wonyesho wa Barabarani wa jeshi la Kanisa, ya kwenda kwenye sehemu teule za mapumzikio kando-kando ya bahari, katika Uingereza na Wales. Jeshi la Kanisa lilianzishwa kidogo tu zaidi ya miaka mia moja iliyopita likiwa tawi la Kanisa la Uingereza, nalo lilikusudiwa kueneza evanjeli “miongoni mwa watu waliotangazwa kuwa haramu katika jamii, na wahalifu wa mitaa ya kimaskini ya Westminster.”

Leo, viongozi wa Jeshi la Kanisa wangali wakihangaikia jambo la kwamba “uenezaji evanjeli unapasa kuwekwa mahali ambapo unafaa kuwa.” Lengo lao la kufanya Wonyesho wa Barabarani ni kutokeza ile gospeli “kwa njia ya kuwachekesha watu ambao hapo kwanza wamekuwa hawana ujuzi mwingi juu ya Mungu, na ambao hawangewazia kuja kwenye sherehe inayofanywa ndani ya kanisa au jumba la kikanisa.” Wale “Wacheshi wa Mambo ya Kipumbavu” waliovalia mavazi ya kimchezo katika ule wonyesho wa barabarani wanatumainia kwamba “utani-utani wao wa kipumbavu utafanya wapita-njiani wasimame na kusikiliza kwa kitambo kidogo,” inasema Church Times.

Hata hivyo, ingawa ni wazi kwamba nguo zao za kipumbavu-pumbavu, ucheshi wao wa kijinga-jinga, na vibofu vya kuchezea wanavyotoa bure vilivutia watoto wengi, watu wazima walibaki na mshangao wa kujiuliza njia hii inahusianaje na uenezaji evanjeli ulioanzishwa na Yesu Kristo.

Ni kweli kwamba mtume Paulo aliandika hivi: “Tumekuwa tamasha kwa dunia . . . Sisi tu wapumbavu kwa ajili ya Kristo.” (1 Wakorintho 4:9, 10) Lakini yeye alikuwa na fikira gani akilini? Je! ilikuwa ‘kufanya utani-utani wa kipumbavu’ ili kuvutia wapita-njiani? Hapana. Paulo alikuwa akitoa kielezi juu ya jinsi ulimwengu unavyowaona Wakristo kuwa wapumbavu, “waliofunuliwa wazi wafanyiwe dhihaka na kuaibishwa na watu wote,” kama vile The New International Dictlonary of New Testament Theology inavyoeleza jambo hilo, kwa ajili ya imani na mafundisho yao.

Tofauti na hao “Wacheshi wa Mambo ya Kipumbavu” wa Jeshi la Kanisa, Yesu aliwafundisha makutano “kama mtu mwenye mamlaka.” Huduma yake ilikuwa ya moja kwa moja na bila mbinu za ujanja. Kama yeye alivyoeleza, “Mimi nanena mambo haya sawa na vile Baba alinifundisha.” Tokeo lilikuwa nini? “Wengi walitia imani katika yeye.”​—⁠Mathayo 7:29; Yohana 8:28, 30, NW.

“Mzigo wa Dhamiri”

Eugene Stockwell, mkurugenzi wa Tume Inayohusiana na Mgawo wa Kazi ya Ulimwenguni Pote na Uenezaji Evanjeli wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, alikiri hivi majuzi kuhusu fungu la kazi ambalo limetimizwa na viongozi wa kidini na makanisa ya Jumuiya ya Wakristo wakati wa vita vyote viwili vya ulimwengu. “Ni mzigo mzito wa dhamiri kwa Wakristo kwamba vile vita viwili vikubwa vya karne hii vilifyatushwa miongoni mwa mataifa ambayo yamekuwa na mapokeo ya muda mrefu ya kuwa na Ukristo katikati yayo, na ambayo mashambulizi yayo ya kijeshi yalibarikiwa mara nyingi na viongozi wa makanisa ya Kikristo,” yeye akaambia kusanyiko la wawakilishi wa dini za ulimwengu katika Warsaw, Polandi.

Stockwell aliongezea hivi: “Mungu alitangazwa kwa harara kuwa upande huu au ule wa pambano hilo. . . . Inakuwa rahisi sana sisi Wakristo kuacha imani yetu iongozwe na jeuri yetu.” Yeye alisema kwamba Vita ya Ulimwengu ya Pili ilikuwa “ithibati kubwa sana ya kushindwa kwetu tukiwa ‘mataifa ya Kikristo’ kuishi kwa matendo yanayopatana na imani yetu, imani ambayo mara nyingi sana inaonyeshwa kwa maneno na kudhihirika sana ikikanwa kwa vitendo.”

Lakini je! huu “mzigo mzito wa dhamiri” umesaidia wale ambao eti wanaitwa Wakristo, na viongozi wao wa kidini, wajifunze somo? Kulingana na Uchapishaji wa Habari za Dini Ulimwenguni, Mkurugenzi Stockwell alikiri hivi: “Sisi tunaongea juu ya kupenda adui zetu, nasi tunawaua. Sisi tunaongea juu ya kugeuza shavu lile jingine, nasi tunajirundikia silaha kweli kweli. Sisi tunaongea juu ya amani inayopita uelewevu, nasi tunajitia katika vita inayozidi uelewevu wo wote. Sisi tunaongea juu ya imani katika Mungu nasi tunaweka imani yetu ya kweli katika silaha za uharibifu.”

Kwa uwazi viongozi wa kidini wa Jumuiya ya Wakristo wenye kuunga vita mkono, na wafuasi wao, wanafanana na “waongeaji wa mambo yasiyo na faida” katika siku za mtume Paulo. Kwa habari yao, yeye alisema hivi: “Wao wanatangaza peupe wanajua Mungu, lakini kwa kazi zao wao wanakana yeye si mwenye wao.”​—⁠Tito 1:10, 16, NW.

Stampu “Yenye Kuudhi”

Siku ya Novemba 19, 1987, Idara ya Usimamizi wa Posta Afrika Kusini ilipanga kutoa stampu nne za kumbukumbu kuhusiana na Biblia. Moja ya stampu hizo ilikuwa na semi hizi, katika Kigiriki “Neno la Mungu” na “Neno la Yehova” katika Kiebrania. Kulikuwa na uchapaji wa jumla ya nakala 1,750,000 za stampu hii.

Hata hivyo, muda mfupi kabla ya tarehe ya kutolewa kwa stampu hiyo, afisi za posta zilipokea simu-barua ikiziagiza kurudisha gawio lazo la stampu hii. Sababu? “Kwa sababu ilionwa na jumuiya ya Wayahudi wa kiorthodoksi kuwa yenye kuudhi,” ikaripoti The Star, karatasi-habari moja ya Johannesburg. Karatasi-habari hiyo iliongezea hivi: “Rabi David Hazdan wa Johannesburg alisema kwamba kwa kawaida jina la Mungu likiwa kama vile lilivyopigwa chapa katika stampu ile huwekwa akibani kwa ajili ya pindi za kidini zilizo za pekee tu.”

Inafaa kuangaliwa kwamba, pokeo la Kiyahudi lililo la hali moja na hiyo ndilo limesababisha watafsiri wengi wa ki-siku-hizi wa Biblia waepuke kutumia jina Yehova na kuweka mahali palo mitajo ya cheo tu, kama vile “Bwana” au “Mungu.” Si ajabu kwamba Yesu aliwaambia hivi viongozi wa kidini wa siku yake: “Ninyi mmefanya neno la Mungu liwe si halali kwa sababu ya pokeo lenu”!​—⁠ Mathayo 15:6, NW.

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki