Je! Mungu Anawajali Wenye Ugonjwa wa Akili?
FLORENCE alikuwa kijana mwanamke mwenye kuvutia. Alikuwa ameanza tu kazi yenye kusisimua ya kujipamba kwa mavazi ili kutangaza mitindo ya mavazi alipopatwa na ugonjwa wa akili. Akahuzunika sana na kujifungia katika nyumba ya wazazi wake. Akiwa amepoteza shauku ya kuishi, akapuuza kabisa sura yake ilivyoonekana. Mwishowe, akapanga kujiua.
Florence hayuko peke yake. Misiba kama hiyo inawapata watu ulimwenguni pote. Kwa kweli, kasoro ya akili ni mojawapo maradhi yaliyo ya kawaida zaidi leo. Mungu ana maoni gani juu ya wenye ugonjwa wa akili? Je! kweli kweli anawajali?
Wengine wanaelekea kusadiki kwamba Mungu anashughulika tu na watu wanaofikiriwa kuwa wana akili ya kawaida. Wengine hata wanafikiri kwamba maradhi ya akili ni namna fulani ya adhabu ya moja kwa moja kutoka kwa Mungu. Lakini je, Mungu ndiye mwenye lawama? Kwa kweli ni nini sababu ya maradhi ya akili?
Sababu ya Msingi
Wakati uliopita kwa kawaida watu walisadiki kwamba karibu kasoro zote za akili zilikuwa na vyanzo visivyo vya kibinadamu, na wengine wanafikiri hayo ndiyo maoni ya Biblia ya kasoro za akili au kukosa akili timamu. Ni kweli kwamba Biblia inaeleza juu ya visa ambavyo watu walipagawa na roho wabaya, lakini hiyo maana yake si kwamba inasema kasoro za namna zote za akili ni kupagawa na mashetani.
Bila shaka, yapasa ikumbukwe kwamba Biblia si kitabu cha utibabu chenye kueleza sababu ya maradhi mbalimbali. Hata hivyo inaeleza sababu kuu ya maradhi yote ya kibinadamu, ya akili na ya mwili. Inaonyesha kwamba sisi tumepatwa na kutokamilika kunakotokeza kifo kilichopokezwa jamii ya kibinadamu na babu yetu mwenye dhambi Adamu. Ni kama mtume Paulo anavyoeleza: “Kwa mtu mmoja dhambi iliingia ulimwenguni, na kwa dhambi hiyo mauti; na hivyo mauti ikawafikia watu wote kwa sababu wote wamefanya dhambi.” (Warumi 5:12) Hiyo maana yake ni kwamba kila mzao wa Adamu si mkamilifu na kwa hiyo kwa njia fulani ana kasoro katika akili na mwili. Kwa hiyo, kasoro za akili ni namna kali tu za udhaifu tuliorithi ambao sote tunao.a
Maandalizi ya Mungu kwa Ajili ya Wenye Ugonjwa wa Akili
Maandalizi ambayo ametayarisha Mungu yanaonyesha kwamba yeye anawajali wenye ugonjwa wa akili. Kwanza, anaweka daraka la kuwatunza juu ya Washiriki wao wa karibu zaidi. Katika 1 Timotheo 5:8 tunasoma hivi: “Lakini mtu ye yote asiyewatunza walio wake, yaani, wale wa nyumbani mwake hasa, ameikana Imani, tena ni mbaya kuliko mtu asiyeamini.” washiriki wa nyumba walio wagonjwa wanatiwa ndani.
Hiyo maana nyake ni kwamba wenzi wana madaraka hayo kwa mmoja na mwenzake. Mke mmoja Mkristo aliyeamua mara moja kumtunza mumeye nyumbani alipopatwa na ugonjwa mkali wa akili alieleza hivi: “Unafunga ndoa hata mambo yawe mazuri au mabaya, sivyo?” Kwa upendo alimtunza kwa miaka mingi mpaka alipokufa mume.
Vivyo hivyo, Mungu amewapa wazazi daraka la kutunza watoto wao wagonjwa. Huenda wazazi wakawa waliwapokeza kasoro ya chembe zinazonakili tabia. Mume na mke mmoja Waswedi ambao mvulana wao wa miaka mitatu alizaliwa akiwa na kasoro ya chembeuzi isiyoweza kuponywa ikamfanya awe akili-punguani sana walisema: “Yeye ni mtoto wetu. Tulimleta ulimwenguni. Hatuwezi kufikiria kumwacha kwa mtu mwingine. Tunampenda sana. Tunataka kumsaidia afaidike kabisa na maisha yake. Ni kazi kubwa, lakini anafanya maendeleo kweli kweli, na hilo linatufurahisha.”
Ni hali moja na hiyo wazazi wa mtu wanapohitaji uangalizi. Neno la Mungu linaoonyesha kwamba watoto waliokua pia wana daraka la kutunza wazazi wao waliozeeka ambao hawajiwezi, kutia wale ambao sasa hawana akili timamu.—1 Timotheo 5:4.
Bila shaka, kwaweza kuwa hali fulani ambazo zinafanya lisiwe jambo la busara kumtunzia mgonjwa wa akili nyumbani. Huenda akawa anajihatirisha mwenyewe au kuhatirisha wengine, huenda akahitaji utibabu wa pekee au kutunzwa daima na wataalamu, au huenda akawa hataki kabisa kukaa nyumbani. Kumtunza pia huenda kukawa mzigo mkubwa sana kwa washiriki wengine wa jamaa, kuwe kunaharibu sana afya yao na hali njema yao. Lakini ikiwa hali hizo hazipo, mahali bora pa kumtunzia paweza kuwa ni nyumbani, mahali ambapo mpango wa jamaa ulioanzishwa kwa upendo na Mungu waweza kufanya mtu huyo afanye maendeleo ya kupata nafuu.
Jinsi Neno la Mungu Linavyosaidia
Uandalizi wa Mungu unaoweza kutumiwa wakati wa kutunza watu waliovurugika akili ni kuwasaidia watwae maarifa ya Biblia. Mifano inaonyesha kwamba watu waliovurugika akili wameondolewa wasi-wasi mwingi na huzuni nyingi, na nyakati nyingine hata wamepona, kwa mawazo yao kurekebishwa kupitia maarifa katika Neno la Mungu. Kwa sababu gani? Kwanza kwa sababu Biblia ni kitabu kinachotoa uongozi wa kiroho na kutia tumaini katika mtu. (Warumi 15:4, 13) Hasa tumaini ni la maana sana kwa wenye huzuni kubwa. Na roho ya Mungu, pamoja na tumaini lenye nguvu, yaweza kumsaidia mtu aliyevurugika arekebishe mawazo yake na kuanza tena kufuata mambo yenye kujenga.
Kwa hiyo, funzo la Biblia la kawaida wakati mwingi limefaidi. Akili inayoenda mbali na njia ya kawaida ya kufikiri inahitaji rekebisho, sawa na saa ambayo wakati wote inaenda polepole sana au haraka sana. Huenda saa hiyo ikawa yenye manufaa ikiwa inarekebishwa kwa kulingana na saa iliyo sahihi. Kupitia Biblia Yehova Mungu amewapa wanadamu “saa sahihi,” kiwango cha mawazo yanayofaa. Ikiwa mtu aliyevurugika akili anasaidiwa kwa ukawaida atumie uandalizi huo mzuri, unaleta faraja, imani na tumaini kwa akili ya mtu huyo mwenye kutaabika.
Ndivyo ilivyokuwa kwa Florence, yule kijana mwanamke aliyesimuliwa mwanzoni mwa makala hii. Mwanamke mmoja kutoka kundi la Mashahidi wa Yehova la mahali hapo alitembelea wazazi wake akapanga awe akifanya funzo la Biblia la kila juma pamoja na Florence. Shahidi huyo anasema: “Hapo mwanzoni alikuwa mwenye kuona haya sana na mwenye kujiona hafai akawa akikimbia kutoka kwenye chumba hicho na kulia. Lakini polepole, kwa kadiri alivyopokea maarifa ya Biblia, akawa mwenye usawaziko zaidi. Kisha, nikamjulisha kwa watu wengine niliowaalika waje kwenye funzo, na hatimaye, kwa mara ya kwanza baada ya miaka kadha, aliweza kutoka nyumbani aandamane nami kwenye mkutano. Sasa Florence anaishi maisha ya kawaida. Ameolewa, ana watoto wawili wadogo na yeye mwenyewe anaongoza mafunzo ya Biblia pamoja na wengine. Maneno yake mwenyewe yalikuwa haya: ‘Singaliweza kamwe kusimama tena bila ukweli na tumaini kutoka Biblia.’”
Uwezo wa Sala
Kutoa sala kwa ukawaida pamoja na mtu aliyevurugika akili kwaweza pia kusaidia kuleta utaratibu bora zaidi kwa akili iliyovurugika. Uandalizi huo unaotoka kwa Mungu waweza kuwa mlango wa kutoa mawazo yenye kuhuzunisha sana. Mtume Petro alikamatanisha kuwa “timamu katika akili” na “kukesha kwa habari ya sala.” (1 Petro 4:7, NW) Kupitia sala Mungu anaweza kufikiwa wakati wo wote, mchana au usiku. Na yeye anatualika tumwombe “katika kila neno,” hiyo ikiwa ni kutia matatizo ya akili pia.—Wafilipi 4:6.
Faida ya sala yaweza kuonekana kwa mfano ufuatao: Mwanamume mmoja aliyeoa katika Ubelgiji alikuwa amepatwa na kasoro kubwa sana za akili tangu utoto. Alikubali funzo la Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova na anaandika hivi:
“Mara tu nilipoelewa kwamba Yehova ndiye Mungu wa kweli mmoja, nilisali, nikamuuliza anisaidie nibadilike kwa sababu nilitambua kwamba tabia yangu haikuwa ya kawaida. Kufikia wakati huo hakuna utibabu wa wataalamu wa matatizo ya akili uliokuwa umeleta faida, nijapofungiwa katika hospitali ya akili mara tatu na kufanyiwa uchunguzi wa namna zote. Nikafikiria kukataa madawa, kwa kujua hayakufaa kitu, lakini ni nini kingechukua mahali payo?
“Mara tu nilipoacha kutumia dawa za kutuliza akili, mkazo wa akili ukawa mkubwa kiasi cha kushindwa kutafuna chakula changu. Nilimsihi Yehova nyakati nyingi kila siku na kila wakati nikajisikia mwenye amani. Mawazo ya Biblia yaliyokuja akilini mwangu yalinisaidia sana pia. Kwanza, hilo lilikuwa jambo la muda mfupi, lakini niliendelea. Nilitambua kwamba roho ya Mungu ilikuwa ikinisaidia kweli kweli nifaulu. Kidogo kidogo, kwa kadiri majuma, miezi na miaka ilipopita, mashambulio hayo yakapungua kwa wingi na ukali. Nikashinda vita! Naweza kuhakikisha kwamba wakati huu ninaishi maisha ya kawaida, nikiwa na uwezo wa kuchukua madaraka yangu na kusitawisha utu wa Kikristo. Jambo bora ninaloweza kufanya ni kutia moyo wote walio na matatizo kama hayo wamgeukie Mungu wetu, Yehova, wapate msaada.”
Kutunzwa Kupitia Kundi la Kikristo
Kungali njia nyingine ambayo kwayo Yehova Mungu anaonyesha kutunza kwake walio wagonjwa akili, na njia hiyo ni kupitia kundi la Kikristo. Humo Mungu amepanga kwa upendo wazee waongoze. Wanajaribu sana kufuata shauri: “Mseme kwa kuzifariji nafsi zilizoshuka moyo, mwasaidie waliolegea, mwe wastahimilivu kwa watu wote.” (1 Wathesalonike 5:14, NW) Miaka mingi ya kujifunza Neno la Mungu na mambo waliyojionea katika kushughulika na matatizo, yamewafanya wazee Wakristo wawe wenye kustahili kusaidia watu wa aina zote wanaowajia. Wanapendezwa kikweli, kwa subira wakisikiliza maneno yote anayotaka kusema mwenye shida. Wazee Wakristo wanatambua umaana wa kujaribu kuelewa badala ya kufanya haraka kutoa uamuzi juu ya jinsi mtu alivyo au kuonyesha maoni yake hayana maana sana. Yajapokuwa makosa na vizuizi vyao, wazee wanajaribu kwa moyo mweupe kufariji na kusaidia. Mwanamume huyo Mbelgiji aliyepata nafuu alisema: “Lazima nikazie upendo walioonyesha wazee ambao, ingawa sikuzote hawakuwa wenye kuelewa hali, walikuwapo wapate kunitegemeza mimi pamoja na jamaa yangu.”
Pia wazee wanataka kuwasaidia wenye shida wahudhurie mikutano ya kundi la Kikristo. Mikutano hiyo inayofanywa kwa roho yenye amani na ya utimamu inatoa ushirika wenye kujenga na mazingira yenye kutuliza kwa wote wenye nia ya kupata faida kutoka hiyo.
Namna Gani Visa vya Ugonjwa Usioponyeka?
Kwa wazi, si kila kisa cha ugonjwa wa akili kinachoweza kuponeshwa kupitia maandalizi yaliyotajwa humu. Hata hivyo, mambo yaliyotokea yameonyesha kwamba watu wengi wanaotaabishwa na akili au mawazo ya ndani wamepata nafuu au angalau wakapata kadiri fulani ya faraja kutoka taabu hizo. Bila shaka, kuna visa vya ugonjwa huo kuwa mkubwa sana hata kwamba mgonjwa hawezi kushika maarifa ya Biblia na kuelewa mambo ya kiroho. Lakini hata katika visa hivyo, faraja fulani imepatikana kwa kumruhusu mtu akae katika mazingira ya upendo na usalama.
Huenda hali nyingine zikaonekana kuwa zisizo na tumaini na ngumu kuvumilia. Hiyo haimaanishi kwamba Mungu hajali. Kuhusu utawala wa Mfalme wa Kimasihi wa Mungu, ilisemwa hivi kwa njia ya unabii: “Atamwokoa mhitaji aliapo, na mtu aliyeonewa iwapo hana msaidizi. Atamhurumia aliye dhaifu na maskini, na nafsi za wahitaji ataziokoa.”—Zaburi 72:1, 12, 13.
Faraja ya kudumu ikiwa mbele, Mungu ameruhusu hali hiyo ya kutokamilika ya kibinadamu iwepo kipindi fulani kifupi. Lakini si milele! Maandiko yanatuhakikishia kwamba hali zote zisizopendeza za maisha ya kibinadamu zitakwisha wakati serikali ya Ufalme ya kimbingu ya Mungu itakapochukua mahali pa utawala wa Kishetani kuwe utawala wa Mungu juu ya dunia.—Danieli 2:34, 44; Ufunuo 21:4.
Ndiyo, karibuni Yehova Mungu ataondoa sababu za kasoro zote za kibinadamu, za mwili na za akili. Yeye anajali kweli kweli.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa mazungumzo ya ukamili zaidi, tafadhali ona Amkeni! (Kiingereza) ya Aprili 22, 1975.