Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w88 10/15 kur. 25-29
  • Mtaabiko wa Akilini—Wakati Unaposumbua Mkristo

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Mtaabiko wa Akilini—Wakati Unaposumbua Mkristo
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Sababu kwa Nini Wakristo Si Wasioweza Kugonjweka
  • Visababisbi vya Mtaabiko wa Akilini
  • Mambo Ambayo Wazee Wanaweza Kufanya
  • Wale ‘Wanaohitaji Tabibu’
  • Je! Ni Kusumbuliwa na Roho Wabaya?
  • Dawa za Magonjwa ya Akili
  • Matibabu ya Kimaongezi
  • “Maneno ya Kiroho” kwa Wenye Kutaabika Akilini
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
  • Maswali Kutoka kwa Wasomaji
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Afya ya Akili—Tatizo la Ulimwenguni Pote
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova (Toleo la Watu wote)—2023
  • Mambo Unayopaswa Kujua Kuhusu Magonjwa ya Akili
    Amkeni!—2014
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1988
w88 10/15 kur. 25-29

Mtaabiko wa Akilini​—Wakati Unaposumbua Mkristo

WASTADI wa afya ya akilini wanasema kwamba labda 1 kati ya watu 5 katika United States ana namna fulani ya kasoro inayoonekana ya kiakili. Tengenezo la Afya Ulimwenguni linaongezea kwamba huenda kukawa na visa visivyotibiwa vinavyofikia milioni 40 vya ugonjwa wa akilini katika mabara yanayositawi. Matatizo ya kiakili yamegunduliwa hata miongoni mwa wakaaji fulani wa visiwa vya Pasifiki vilivyo na hali za kiparadiso.

Kwa hiyo haipasi kutushangaza kwamba hesabu fulani ya Wakristo leo wanapatwa na magumu ya kiakili au kihisia-moyo kuanzia kuwa na hangaiko dogo tu na mshuko mdogo wa moyo kufikia magonjwa mazito kama vile mshuko wa moyo ulio mkubwa, kasoro-kasoro za bipolar (mshuko wa moyo ulio wa ukichaa), hofu zisizo za kiafya za kuogopa-ogopa vitu bila sababu, na kutenda-tenda mambo ya kiajabu-ajabu kwa mwenendo usio wa akili timamu (skizofrenia). Watu fulani walikuwa na matatizo hayo kabla ya kuwa Mashahidi, hali wengine wameanza kuwa na mtaabiko katika miaka yao ya umri mkubwa zaidi.

Sababu kwa Nini Wakristo Si Wasioweza Kugonjweka

Mwanamke mmoja Mkristo aliye na zaidi ya miaka 20 ya utumishi wa kujiweka wakfu anaripoti kuwa aliteswa-teswa na sauti zenye kani nyingi na zisizoacha kusumbua. “Hali nikiwa ninafikiria habari nyingine yoyote ile,” yeye anasema, “ndipo inapokuja ile sauti ikisema, ‘jiue.’ . . . Unasikia-sikia sauti hizo mpaka unakuwa huwezi kuvumilia tena.” Ni jinsi gani inavyowezekana kwa Mkristo mwaminifu kuteseka kwa njia hiyo? Je! kwani 2 Timotheo 1:7, NW, haisemi: “Mungu alitupa sisi si roho ya woga-woga, bali ile ya nguvu na ya upendo na ya utimamu wa akili”?

Ndiyo, lakini utimamu wa akili kwa ujumla unarejeza, si hasa sana kwenye hali njema yetu ya fikira za akilini bali zaidi sana kwenye uwezo wa Mkristo wa kujizoeza kufanya hukumu inayotegemea msingi wa Biblia. Tofauti na mtu wa ulimwengu aliye “katika giza kiakili,” au ‘aliyefisidiwa katika akili,’ Mkristo ‘amebadili akili yake’ kwa kujifunza Neno la Mungu. (Waefeso 4:17, 18; 2 Timotheo 3:8; Warumi 12:2, NW) Pasipo shaka hiyo inasaidia sana kuendeleza usawaziko wa Mkristo wa kihisia-moyo na kiakili, hata hivyo haimfanyi awe asiyeweza kugonjweka matatizo ya afya ya akilini. Watumishi fulani waaminifu wa Mungu katika nyakati za Biblia, kama vile Epafrodito, walikuwa na namna fulani za mtaabiko wa akilini.​—Wafilipi 2:25, 26; Luka 2:48.

“Katika Adamu wote wanakufa,” mtume Paulo anatukumbusha. (1 Wakorintho 15:22) Wengi wetu wana magonjwa ya kimwili yenye kuonekana wazi. Wengine wana ugonjwa wa kiakili au wa kihisia-moyo.

Visababisbi vya Mtaabiko wa Akilini

Visababishi vya kimwili vinaonekana kuwa kwenye shina la visa vingi vya mtaabiko wa akilini. Mathalani, Biblia inaeleza juu ya mtu ambaye macho yake ‘yanaona mambo ya kiajabu-ajabu.’ Ni nini kisababishi cha kuona mambo hayo ya kifumbo ya kuwaziwa-waziwa tu? Ni “kukaa muda mrefu pamoja na divai”! (Mithali 23:29-33, NW) Kwa uwazi, kileo kinaweza kusababisha ubongo uwazie-wazie mambo yasiyokuwako. Madaktari wanasema kwamba kwa njia inayofanana na hiyo, utendaji wenye kasoro wa kemikali za ubongo, visababishi vya chembe za urithi, na labda hata ulaji wa mtu unaweza kusababisha utendaji wenye kasoro wa ubongo. Magumu ya kiakili na kihisia-moyo yanaweza kutokea.a

Mifinyo mikali ya kifikira, kama vile mkaziko wa mawazo, huenda pia ukafyatusha matatizo ya kihisia-moyo. Na kule kujaribu kwenyewe kudumisha utakato wa kiadili na utu wa Kikristo katika hizi “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo” kunaweza kuwa chanzo cha mkaziko wa mawazo. (2 Timotheo 3:1-5, NW) Ala, Loti ‘alikuwa akitesa-tesa nafsi yake yenye uadilifu’ juu ya uovu uliomfichukia kila siku katika Sodoma! (2 Petro 2:8, NW) Zaidi ya hilo, Wakristo fulani wameathiriwa kiakili kwa sababu ya kunajisiwa, kutumiwa vibaya kingono, au kwa sababu ya vitendo vya wakati uliopita vya kuishi maisha ya ngono za ovyoovyo au ya utumizi mbaya wa dawa za kulevya. Mambo kama hayo yanaweza kuvuruga sana afya ya akilini ya mtu.

Mambo Ambayo Wazee Wanaweza Kufanya

Wazee wanahangaikia kuchunga kundi lote lililotiwa katika kabidhi ya utunzaji wao​—kutia na wale walio na mtaabiko wa kihisia-moyo. (1 Petro 5:2; Isaya 32:1, 2) Ni kweli, wao si madaktari, na hawawezi kuponya watu mmoja mmoja magonjwa yao kama vile pia mtume Paulo hakumponya Epafrodito ugonjwa wake wa kimwili au mshuko wa moyo uliofuata. (Wafilipi 2:25-29) Hata hivyo, kwa kuonyesha hangaikio halisi na hisia-mwenzi, mara nyingi wao wanaweza kufanya mengi kuwasaidia na kuwatia moyo watu hao.​—1 Petro 3:8.

Basi, namna gani ikiwa ndugu anaanza kufanya mambo kiajabu-ajabu au analalamika juu ya msukosuko wa kihisia-moyo? Wazee wanaweza kwanza kujaribu kuchota maoni ya ndani ya mwenye kusumbuka, wakijaribu kujua ni nini hasa kinachomsumbua. Je! afa fulani la kibinafsi au mastakimu yenye kumkaza mawazo isivyo kawaida​—labda upotevu wa kazi au kifo cha mpendwa​—limemwondolea usawaziko kwa muda? (Mhubiri 7:7) Je! mwenye usumbuko ameshuka moyo kidogo kwa sababu ya upweke na hivyo anahitaji mtu fulani wa ‘kunena naye kwa kumliwaza’? (1 Wathesalonike 5:14, NW) Au je! ingeweza kuwa kwamba ndugu huyo anafadhaika juu ya kosa fulani la kupungukiwa kibinafsi? Uhakikishio wa upendo na rehema ya Mungu​—pamoja na shauri linalofaa​—huenda ukasaidia kutuliza mahangaiko yake. (Zaburi 103:3, 8-14) Wema mwingi unaweza kutimizwa kwa kusali tu pamoja na ndugu yule mwenye kutaabika.​—Yakobo 5:14.

Wazee wanaweza pia kushiriki hekima yenye mafaa pamoja na mwenye kusumbuka. (Mithali 2:7) Mathalani, tuliona kwamba huenda mifadhaiko fulani ya kihisia-moyo ikawa inahusiana na ulaji wa mtu. Kwa hiyo huenda wazee wakadokeza kwamba ndugu yule ale milo iliyosawazika na kuepuka kupita kiasi katika ulaji wake. Au huenda wakatambua kwamba mwenye kutaabika amekuwa chini ya mfinyo mkubwa katika kazi yake na angenufaika kutokana na “konzi moja ya pumziko”​—kupata kwa ukawaida zaidi usingizi wa kutosha usiku.​—Mhubiri 4:6, NW.

Wale ‘Wanaohitaji Tabibu’

Ingawa hivyo, wakati mtaabiko mkali sana unaposonga mbele, ni vizuri kukumbuka maneno ya Yesu: “Wenye afya hawahitaji tabibu, bali walio hawawezi.” (Mathayo 9:12) Watu wengi wenye mtaabiko hawataki kuona tabibu. Hivyo huenda wazee na washiriki wa jamaa wakahitaji kutia ndugu moyo atafute matibabu, kama vile kuchunguzwa kabisa kabisa na daktari anayeitibariwa. Anasema hivi Profesa Maurice J. Martin: “Namna nyingi sana za magonjwa ya kimwili zinaonekana kama kwamba ni kasoro za akili.” Na hata mahali ambapo kwa kweli ugonjwa wa kiakili ndio unaohusika, mara nyingi kunakuwa kuna matibabu mazuri.

Mke wa mzee mmoja anaeleza jinsi ambavyo mume wake mwenye kufadhaika “akawa akiogopa kuwa karibu na akina ndugu na hakutaka kwenda kwenye mikutano. . . . Yeye alitaka sana kufa!” Lakini baada ya kupokea matibabu ya kitaalamu, mke wake aliweza kuripoti hivi: “Sasa yeye hashuki moyo tena kwa kina kirefu, wala hataki kukaa mbali na mikutano. Asubuhi hii yeye ndiye alitoa hotuba ya watu wote!”

Kwa kukiri wazi, si hali zote zinazotatuliwa kwa urahisi hivyo. Sayansi imeanza sasa tu kufumbua mafumbo ya matatizo ya kiakili. Kuchunguzwa ugonjwa kwa njia ifaayo na kutibiwa kunaweza kuwa utaratibu mrefu, wenye kutatanisha​—lakini mara nyingi kunakuwa na malipo.

Je! Ni Kusumbuliwa na Roho Wabaya?

Watu fulani wenye magumu ya kiakili wanahofu kwamba wako chini ya shambulio la roho wabaya, wakidai kwamba nyakati nyingine wanasikia “sauti.” Ni kweli, roho wabaya wamejulikana kufanya watu mmoja mmoja walio timamu akilini watende kwa njia ya kutofikiri vizuri. (Marko 5:2-6, 15) Hakuna uthibitisho wa kwamba roho wabaya wanahusika katika vingi vya visa vya mwenendo wa kigeni-kigeni, sawa tu na vile kusivyo na uthibitisho kwamba wao wanahusika katika visa vyote vya ububu, upofu, na kifafa. Hata hivyo, kule nyuma katika nyakati za Biblia, nyakati fulani roho wabaya walisababisha (au angalau walizidisha) magonjwa hayo hayo! (Mathayo 9:32, 33; 12:22; 17:15-18) Ingawa hivyo, Biblia inafanya upambanuzi wa wazi kati ya “wale waliokuwa wagonjwa na wale ambao walikuwa na roho wabaya.” (Marko 1:32-34; Mathayo 4:24; Matendo 5:16, NW) Basi, kwa uwazi vilivyo vingi sana vya visa vya upofu au kifafa leo vinasababishwa na mambo ya kimwili, si na roho wabaya. Hilo hilo linaweza kusemwa bila shaka juu ya visa vilivyo vingi vya mtaabiko wa akilini.

Hata hivyo, ni lazima ikumbukwe kwamba Shetani na roho wabaya wake ‘wanafanya vita’ pamoja na watu wa Mungu na wamejulikana kuwa wenye kusumbua-sumbua Wakristo waaminifu. (Ufunuo 12:17; Waefeso 6:12) Roho wabaya ni watesaji wakatili, na haitupasi kushangaa kwamba wao wanaona upendezo katika matendo ya kikatili sana kwa kutesa-tesa nafsi fulani zenye mtaabiko wa akilini​—wakiongezea magumu yao.

Kwa hiyo ikiwa wazee wana sababu nzuri ya kushuku kwamba uvutano wa kishetani unahusika, hakuna dhara katika kuulizia-ulizia jambo hilo. Mathalani, mtu huyo amepokea kwa njia ya moja kwa moja na kimakusudi vitu vyovyote vya kutiliwa shuku kutoka kwa watu mmoja mmoja wanaohusika katika namna fulani ya kuwasiliana na roho wabaya? Kuondolea mbali vyombo hivyo huenda kukaleta kitulizo. (Matendo 19:18-20) Kwa kuwa Wakristo wanaambiwa ‘wampinge Shetani,’ wazee wanaweza pia kumshauri mwenye kusumbuliwa akatae “sauti” zozote za kigeni ambazo zingeweza kuwa na awali ya roho wabaya. (Yakobo 4:7; Mathayo 4:10) Ikiwa mtu anahisi akiwa chini ya shambulio, inampasa asali kwa juhudi nyingi, akiita juu ya jina la Yehova kwa sauti kubwa.​—Waefeso 6:18; Mithali 18:10.

Hata hivyo, inaonekana kwamba roho wabaya wanahusika katika visa vichache sana​—si kwa kawaida. Dada mmoja anasimulia hivi: “Mimi nilifikiri nilipagawa na roho mbaya mpaka nilipotafuta msaada wa kitiba na kujulishwa kwamba nilikuwa na kutosawazika kwa kemikali. Nilipata kitulizo kikubwa sana kugundua kwamba ni ugonjwa fulani uliokuwa ukisababisha vitendo vyangu wala si roho mbaya mwenye utu aliyekuwa ndani yangu!”

Dawa za Magonjwa ya Akili

Namna mbalimbali za dawa zinatumiwa sasa na madaktari katika utibabu wa mifadhaiko ya akilini. Utumizi wenye kusimamiwa kitiba wa dawa fulani-fulani umewezesha Wakristo walio wagonjwa sana watende kikawaida. Ingawa hivyo, ndugu fulani wamevunja wagonjwa moyo kwa madhumuni mazuri wasitumie dawa walizoandikiwa, labda wakihofu kwamba huenda zikawa na madhara au zenye uzoelevu. Bila shaka, kuna hatari zinazohusiana na utibabu wa aina yoyote, na “mwenye busara huangalia sana aendavyo,” akifikiria matokeo ya muda mrefu wa baadaye.​—Mithali 14:15.

Hata hivyo, kwa kupendeza, dawa nyingi za utibabu wa akili si za kufanya mtu aone vituko vya kuwazia tu, si za kumtuliza mtu, au kumtia uzoelevu; hizo zinatumikia tu kuwa virekebishaji vya hali ya kutosawazika kwa kemikali katika ubongo. Mathalani, dawa za antisaikotiki huenda zikasaidia kusawazisha zile dalili za kigeni-kigeni ambazo mara nyingi mgonjwa wa skizofrenia anakuwa nazo. Lithiamu inaweza kusaidia kupunguza mshuko wa moyo na kudumisha mshuko-moyo ulio wa ukichaa katika kiwango kimoja ili usiwe ukibadilika-badilika kwa kuchacha-chacha na kupoa-poa.

Ni kweli, dawa za kulevya zilizo na nguvu nyingi zinatumiwa nyakati fulani kutuliza mgonjwa au kukandamiza maelekeo ya kutaka kujiua. Hata hivyo, ikiwa ndugu anatumia dawa alizoandikiwa si kwa kusudi la kuona raha bali ili aweze kutenda kikawaida, jambo hilo linapasa kuonwa kama lile la mgonjwa wa sukari kutumia insulini.

Inapasa kukumbukwa kwamba mara nyingi dawa za magonjwa ya akili zinafanya kazi polepole na huenda zikawa na athari zisizopendeza. Nyakati nyingine, pia, kwa kadiri fulani daktari anatumia dawa kwa kusudi la kutafuta ni ipi hasa iliyo na matokeo mazuri na/au ni kiasi gani kinachotokeza kadiri ndogo zaidi ya athari za kando. Mara nyingi wagonjwa huvunjika moyo. Kwa hiyo washiriki wa jamaa na wengine wanaweza kumtegemeza mtu yule anayepatiwa utibabu, wakimtia moyo awe na saburi na kuonyesha ushirikiano kwa wanatiba wanaostahili. Namna gani ikiwa yeye ana maswali kuhusu dawa fulani? Au namna gani ikiwa matatizo yanatokea au utibabu fulani unaonekana kuwa usiofanya kazi vizuri? Matatizo kama hayo yanapasa kuzungumziwa pamoja na tabibu wake.b Ikihitajiwa kabisa, kauli ya pili inaweza kutafutwa.

Matibabu ya Kimaongezi

Katika visa fulani, inaweza pia kufikiriwa kumwambia mgonjwa aongee na mtaalamu aliyesomea kazi yake kwa kumwambia mambo yake ya ndani. Labda daktari wa kijamaa mwenye kuitibariwa ambaye anafahamiana na mgonjwa yule anaweza kutumikia kwa njia hiyo. Ingawa hivyo, namna gani kukubali utibabu kutoka kwa daktari wa akili au msaikolojia? Huo ungekuwa uamuzi wa kibinafsi unaopasa kufanywa kwa tahadhari inayofaa. Watabibu wa kimazoezi wanatofautiana katika njia za utibabu. Mathalani, baadhi yao wangali wanazoea namna fulani za kuchanganua-changanua mno fikira za mtu kwa kutumia mtindo wa Freud, jambo ambalo uhalali walo unakinzwa na wengi katika uwanja wa afya ya akilini.

Jambo la kuhangaisha hata zaidi ni uhakika wa kwamba watabibu wenye madhumuni mazuri wametoa ushauri unaopingana kabisa na Biblia. Kwa kutoelewa kanuni za Kikristo​—hata kuwa na rai ya kwamba hizo ni “upumbavu”​—watabibu fulani wa kimazoezi hata wamekata shauri kwamba kufuata lile fungu la sheria zenye kufuatiliwa sana kuhusiana na maadili ndicho chanzo cha magumu ya mtu!​—1 Wakorintho 2:14.

Hata hivyo, watabibu fulani, kutia na wasaikolojia na madaktari wa akili, wanatolea watu namna fulani za utibabu wa kimaongezi ambao kwa kweli si kuchanganua-changanua mno fikira za mtu bali ni njia ya kusaidia mgonjwa aelewe ugonjwa wake, wakitilia kani uhitaji wa kutumia dawa, na kunyoosha matatizo yaliyo ya kihalisi. Huenda Mkristo akaona matibabu hayo ya kimazoezi kuwa yenye msaada, lakini anahitaji kujua kabisa mambo ya uhakika kabla ya kukubali utibabu: Utibabu wenyewe unahusisha nini hasa? Ni ushauri wa aina gani ambao utatolewa? Je! tabibu yule anaelewa na kustahi itikadi za Mashahidi wa Yehova?c Ukiafikiana na utibabu wa kimaongezi, ‘yajaribu [yatahini, NW] maneno’ ya daktari badala ya kukubali kila jambo tu bila kuuliza maswali.​—Ayubu 12:11, 12.

Basi, kwa sehemu iliyo kubwa zaidi, mtaabiko wa akilini unaweza kuonwa kuwa tatizo la kitiba​—si la kiroho. Kwa kuelewa uhakika huo, jamaa, wazee, na washiriki wa kundi wanaweza kwa njia nzuri zaidi kuwategemeza wenye kuteseka. Nyakati nyingine wenye kutaabika wanahitaji pia utegemezo wa kiroho. Itazungumziwa katika toleo fulani la wakati ujao ni jinsi gani kundi linaweza kuuandaa.

[Maelezo ya Chini]

a Ona matoleo ya Oktoba 8, 1988 (Kiswahili), na Septemba 8, 1986 (Kiingereza) ya gazeti letu andamani, Amkeni!

b Sosaiti haipendekezi wala kutoa hukumu juu ya dawa mbalimbali na matibabu yanayotumiwa na watabibu. Hata hivyo, huenda utafiti katika vichapo vya Sosaiti ukathibitika kuwa wenye msaada.

c Ikiwa mgonjwa ana ugumu wa kueleza tabibu au mtoaji matibabu ya kimazoezi juu ya msimamo wake wenye kutegemea msingi wa Biblia, labda Mkristo fulani aliyekomaa anaweza kumsaidia.

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kwa kuwa wasikilizaji na washauri wenye huruma, mara nyingi wazee wanaweza kusaidia watu walio na mtaabiko wa kihisia-moyo

[Picha katika ukurasa wa 29]

Nyakati fulani inashaurika mgonjwa wa akili atafute msaada wa kitiba

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki