Neno la Mungu Li Hai
Hakuna Uchawi Unaoweza Kukuumiza Wewe
JE! WEWE? ni kama mtu huyu? Yeye anaogopa kwamba mtu fulani atamwumiza kwa kumloga. je! unapaswa kuogopa uchawi au uganga?
Hapana, hupaswi kuogopa. Ingawa wengine wameumizwa na mambo hayo, Yehova anatoa uhakikisho wa kuwalinda wale wanaomtii yeye. “Jina la [Yehova] ni ngome imara,” Biblia inasema. “Mwenye haki huikimbilia, akawa salama.”—Mithali 18:10.
Mungu anachukia mazoea yote ya kichawi. Biblia inasema: “Asionekane kwako mtu . . .atazamaye bao, wala mtu atazamaye nyakati mbaya, wala mwenye kubashiri, wala msihiri, wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo, wala mchawi, wala mtu awaombaye wafu.”—Kumbukumbu la Torati 18:10, 11.
Biblia inaeleza juu ya mwanamume mmoja aliyezoea namna moja ya uchawi iitwayo uaguzi. Hilo ni zoea la kujaribu kuujua wakati ujao, au kujua jambo lisilojulikana, kwa msaada wa roho zisizoonekana. Mwanamume huyo alikuwa Balaamu, anayeonekana hapa akimpiga punda wake. Alikuwa akienda kuwalaani watu wa Mungu wakati malaika mmoja aliposimama barabarani, na jambo hilo likamfanya punda huyo alale chini.—Hesabu 22:7, 20-35.
Yehova alifanya uaguzi wa Balaamu uwe kazi bure. Aliibadili laana hiyo ikawa baraka, Balaamu alilazimika kukubali hivi: “Hapana uchawi juu ya Yakobo, wala hapana uganga juu ya Israeli.”—Hesabu 23:23.
Yehova anaendelea kuwashinda wale wanaozoea uaguzi, hata wasiweze kuwaumiza wale wanaobaki wakiwa waaminifu kwake. Je! unaona uganga wa mchawi huyu ukishindwa kuwaumiza Mashahidi wa Yehova? Yeye alitumia uchawi kuwaumiza watu, lakini wakati huu alishindwa. Mashahidi wa Yehova walisema: “Wewe utaona kwamba Yehova, Mungu wetu, ni mwenye nguvu zaidi!” Walisimama imara, na mchawi huyu akaanguka chini.
Ndiyo, “malaika wa [Yehova] hufanya kituo, akiwazunguka wamchao na kuwaokoa.” (Zaburi 34:7) Tukimtumaini Mungu kabisa na kuvaa silaha za kiroho anazotoa, Yehova atamshinda ye yote anayejaribu kutuumiza kwa uchawi.—Waefeso 6:10-18.