Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • w83 12/15 kur. 9-14
  • Kutembea Pamoja na Mungu Katika Ulimwengu Wenye Jeuri

Hakuna video yoyote kwa sasa.

Samahani, haikuwezekana kupakia video.

  • Kutembea Pamoja na Mungu Katika Ulimwengu Wenye Jeuri
  • Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
  • Vichwa vidogo
  • Habari Zinazolingana
  • Maoni ya Mungu juu ya Jeuri
  • Ongezeko Kubwa la Jeuri
  • Maoni ya Kikristo juu ya Jeuri
  • Tutatembea Katika Jina la Yehova Mungu Wetu
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2005
  • Huu Ndio Wakati Tunaopaswa Kuwa Wenye Kulinda Zaidi
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—2003
  • Mwisho Wenye Kudumu wa Jeuri—Utakujaje?
    Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1996
  • Maoni ya Mungu Ni Nini Kuhusu Jeuri?
    Amkeni!—2002
Pata Habari Zaidi
Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova—1983
w83 12/15 kur. 9-14

Kutembea Pamoja na Mungu Katika Ulimwengu Wenye Jeuri

“Usisahau jambo hili: kutakuwako nyakati mbaya kabisa katika siku za mwisho.”​—2 TIMOTHEO 3:1, The New American Bible (ya Katoliki).

1. Ni nini kinachoonyesha kwamba kweli hizi ndizo “siku za mwisho”?

WEWE hukubali kwamba hizi ni nyakati mbaya kabisa? Maneno ‘mbaya kabisa’ yaliyo katika andiko la Biblia lililotajwa sasa hivi yametokana na neno la Kigiriki khalepos. Neno hilo limetafsiriwa pia kuwa “zilizo ngumu kushughulika nazo,” “zenye kuleta kihoro,” “ngumu,” na “ngumu sana.”a Kwenye Mathayo 8:28 neno ilo hilo linatumiwa kueleza habari ya wanaume wawili wenye mashetani na kuwataja kuwa “wakali mno” au “wenye jeuri.”b Ni kweli kabisa kwamba sasa sisi tunaishi katika nyakati mbaya kabisa na zenye jeuri. Nyakati hizi zinatimiza unabii ulioandikwa juu wa mtume Paulo, kuonyesha kwamba pasipo shaka hizi ndizo “siku za mwisho”!

2. (a) Wanadamu wasiomcha Mungu wameziletaje hizi nyakati mbaya kabisa? (b) Ni maandiko gani yanayojulisha chanzo kikuu cha ole wa leo, na ole huo umekuwa mwingi ukaenea kwa kadiri gani?

2 Ni kitu gani kimezitokeza hizi nyakati mbaya kabisa, “siku za mwisho”? Je! hazikutokezwa na hali ile aliyoitabiri Paulo, akisema: ‘Watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna’? Na watu hao wasiomcha Mungu wanatiwa moyo wa kufura na yule ambaye Biblia inamweleza kuwa ndiye “mungu wa huu mfumo wa mambo,” “yule anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayepoteza dunia nzima inayokaliwa na watu.” Matokeo ya tendo hilo ni hali mbaya sana tunayoiona kila mahali leo​—katika serikali, katika ulimwengu wa kibiashara, katika dini, katika jamii ya kibinadamu kwa ujumla.​—2 Timotheo 3:2-5, 13; 2 Wakorintho 4:4, NW; Ufunuo 12:9, 12, NW.

3. Kwa sababu gani inaweza kusemwa kwamba jeuri imefikia kipimo kinachopita kiasi?

3 Tunapozidi kusonga katika miaka ya 1980 ulimwengu unazidi kupatwa na jeuri ya kupita kiasi. Katika mwaka wa 1980 tu, United States (Amerika) iliripoti visa milioni 1.3 vya uhalifu wenye jeuri, hilo likiwa ni ongezeko la asilimia (%) 13 juu ya mwaka uliotangulia, na kuua binadamu kumekuwa kimoja cha visababishi vikubwa zaidi vya vifo vya wanaume wa miaka kati ya 25 na 44. Katika kumi la miaka iliyomalizika katika mwaka uo huo, Uingereza iliripoti ongezeko la asilimia 50 la mauaji ya kukusudia, ongezeko la asilimia 300 la mashambulizi ya kuotea na ongezeko la asilimia 200 la kuharibu-haribu mali za watu na mazingira kwa kusudi la kujifurahisha tu. Katika Ufaransa, jumla ya visa vya uhalifu imeongezeka kwa asilimia zaidi ya 260 tangu mwaka wa 1963. Ripoti zinazofanana na hizo zinatajwa kutoka sehemu zote za ulimwengu.

4. Hali ya kibinadamu imebadilikaje tangu mwaka wa 1914, na hali hiyo imetokeza maulizo gani?

4 Mwanahistoria Walter Laqueur aliripoti hivi: “Kwa ujumla, kipindi cha kufikia Vita ya Ulimwengu ya kwanza kilikuwa chenye huruma nyingi zaidi ya kibinadamu. Mimi nasikitika kusema kwamba katika wakati wetu uhai wa kibinadamu umezidi kuchukuliwa kuwa ovyo tu-moja ya sababu za hali hiyo ikiwa ni mauaji makubwa sana ambayo watu waliona yakitendeka wakati wa Vita vya Ulimwengu vya kwanza na pili. Vilevile, wakati wa sasa tuna watu wenye kufundisha wenzao mambo ya jeuri ambao hawakuwako katika karne ya 19. Watu hao wanafanya ubishi wakisema kwamba jeuri si mbaya bali ni nzuri sana, kwamba ukifanya jeuri utajisikia vizuri zaidi akilini, na kwamba tunahitaji sana kutenda jeuri.” Tangu vita ya ulimwengu ya kwanza ilipofyatuka mwaka wa 1914, jeuri imeenea sana ulimwenguni pote. Mungu ana maoni gani juu ya jeuri hiyo? Wakristo wanapaswa kuwa na maoni gani juu ya jeuri?

Maoni ya Mungu juu ya Jeuri

5. (a) Jeuri ilikuwa na mwanzo gani wa mapema? (b) Yesu alimtaja mwanzishi wa jeuri kuwa yuko namna gani?

5 Biblia inaeleza muda wa mapema zaidi katika historia, ambapo ‘dunia ilijaa dhuluma.’ Huo ulikuwa wakati wa miaka zaidi ya 4,300 iliyopita, baada ya ulimwengu wa wakati huo kupata mwanzo mbaya kutokana na kutokutii kwa Adamu na Hawa kisha kufukuzwa kwao watoke katika Paradiso ya Edeni. Baada ya muda fulani Kaini, mwana wao wa kwanza, alimwua Habili ndugu yake. Kumbukumbu la kimungu linatuambia hivi: ‘Kaini alikuwa wa yule mwovu, akamwua ndugu yake. Naye alimwua kwa sababu gani? Kwa sababu matendo yake yalikuwa mabaya, na ya ndugu yake yalikuwa ya haki.’ (Mwanzo 6:11; 1 Yohana 3:12) Yesu anamtambulisha “mwovu” huyo kuwa Ibilisi, akisema: “Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo.” (Yohana 8:44) Kuanzia Edeni, kwa uhakika Shetani amejijengea kumbukumbu la kustaajabisha la kuchochea wanadamu watende jeuri.

6. (a) Ni mabaya gani makubwa yaliyotukia siku za Henoko, nayo yalimfanya Yehova achukue hatua gani? (b) Kwa sababu gani Mungu “alimtwaa” Henoko? (Mwanzo 5:24)

6 Habili alipokwisha kuuawa na Kaini, ulimwengu huo wa kwanza ulizidi kuwa mbaya. Lameki mzao wa Kaini anatajwa pia kuwa mwuaji asiyekuwa ametazamia kuua. (Mwanzo 4:23, 24) Karibu na wakati huo “Henoko, mtu wa saba [wa ukoo wa Sethi] baada ya Adamu, alitoa maneno ya unabii juu ya [waovu], akisema, Angalia, Bwana alikuja na watakatifu wake, maelfu maelfu, ili afanye hukumu juu ya watu wote, na kuwaadhibisha wote wasiomcha Mungu, kwa ajili ya kazi zao zote za upotevu walizozitenda bila kumcha Mungu, na kwa ajili ya maneno magumu yote ambayo hao wenye dhambi wasiomcha Mungu wameyanena juu yake.” (Yuda 14, 15) Mungu alimhamisha Henoko kutoka ulimwengu huo, basi akawa halazimiki tena kuchukuliana na jeuri na matukano ya waovu hao. Kufufuliwa kwake ndani ya “nchi mpya” itakayoumbwa na Yehova kutakuwa thawabu kubwa kama nini!—2 Petro 3:13; Waebrania 11:5.

7. Ulimwengu ule wa kale ulikujaje kujawa na jeuri?

7 Katika wakati wa Noa aliyekuwa kitukuu cha Henoko, Shetani, yule mwovu, alipata malaika wa kujiunga naye kumtia nguvu. Hao walikuwa ni wana wa Mungu wa kiroho walioacha kumtii kwa kuja chini duniani waoe binti za wanadamu, wakawatumia hao kutokeza wazao wa mbegu-mchanganyiko​—wale Wanefili. Jina hilo linamaanisha “Waangushaji,” nao kweli walitimiza maana ya jina hilo kwa kufuata njia ya mauaji kati ya wanadamu. “Wao walikuwa watu hodari wa zamani, watu wenye sifa. . . . Mungu akamwambia Noa: Mwisho wa miili yote umekuja mbele yangu; kwa maana dunia inajaa na jeuri kwa sababu yao; na tazama, nitawaharibu pamoja na dunia.”​—Mwanzo 6:1-13, ZSB.

8. (a) Hali ya sasa ya ulimwengu ina ulinganifu gani na ile ya wakati wa Noa? (b) Noa alituachia sisi mfano gani, nasi tunaweza kufaidikaje kwa kuufuata?

8 Mtume Petro anatuambia hivi: “Ulimwengu wa wakati huo ulipatwa na uharibifu wakati ulipogharikishwa kwa maji. Lakini kwa neno lile lile [la Mungu] zile mbingu na dunia zilizopo sasa zimewekwa akiba kwa ajili ya moto nazo zimewekewa ile siku ya hukumu na ya kuharibiwa watu wasiomwogopa Mungu.” Utimizo wa unabii wa Biblia unaonyesha kwamba sasa ulimwengu uliopo umeikaribia sana siku hiyo ya hukumu. Ni jambo gani ambalo lazima tufanye ili tuokoke? Haya basi, Noa alifanya nini, pamoja na jamaa yake? Biblia inatupasha habari: “Noa alitembea pamoja na Mungu wa kweli. . . . Na Noa akafanya kulingana na yote ambayo Mungu alikuwa amemwamuru.” (2 Petro 3:6, 7, NW; Mwanzo 6:9, 22, NW; 7:5) Matembezi hayo yalitia ndani kuwa “mhubiri wa uadilifu.” Kupitia imani yake “akauhukumu makosa ulimwengu.” (2 Petro 2:5, NW; Waebrania 11:7) Je! haitupasi kuwa tunafuata kwa ukaribu mfano mzuri sana wa Noa na watu wa nyumba yake, tunapotafuta wokovu wa kuondolewa katika ulimwengu huu wa kisasa ambao kwa kweli “uko katika uwezo wa yule mwovu”?1 Yohana 5:19, NW.

Ongezeko Kubwa la Jeuri

9. (a) Ongezeko kubwa la jeuri siku za Noa lilitokeza nini? (b) Ni tukio gani linalolingana na hilo lililokuja kutukia baada ya Gharika, na liliongoza kwenye upeo gani?

9 Kulikuwako na ongezeko kubwa la jeuri katika ulimwengu ulioitangulia ile Gharika Kuu​—mpaka Mungu mwenyewe akaleta hukumu kwa kuharibu wale waliokuwa wakiharibu dunia. (Mwanzo 6:13, 17) Tangu wakati wa aliyekuwa kitukuu cha Noa, yaani, Nimrodi yule “mwindaji mwenye nguvu katika kupingana na Yehova,” kumetokea tena ongezeko kubwa la jeuri muda wa vizazi vyote vilivyopita. Labda jeuri hiyo iliongezeka polepole kwanza, lakini ikazidi moja kwa moja kuongeza mwendo. (Mwanzo 10:1, 6, 8, 9, NW) Baada ya muda fulani kukaja kutokea upanga, uta (upinde) na mshale, mkuki pia; na katika nyakati za kisasa kukatokea bunduki ya kizamani yenye mdomo mkubwa, halafu bunduki yenye kushikamana na kigari chayo kisha silaha nyingine za kutupa risasi. Lakini Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, iliyoanza mwaka wa 1914, ilitokeza silaha mpya za jeuri zenye kustaajabisha sana​—ndege, kifaru, na pia hewa yenye sumu. Katika vita hiyo, matumizi ya nyambizi (sabmarini) yaliwatia watu woga mwingi kisha bunduki-mimina-risasi zikafagia mamilioni ya watu.

10. (a) Unabii wa Yesu juu ya matukio ya “siku ya Bwana” umetimiaje? (b) Kwa sababu gani tumtazamie Yehova kuleta hukumu karibuni?

10 Bwana Yesu Kristo alikuwa ametabiri tukio la namna hiyo akisema lingetukia katika “siku ya Bwana.” Tumekuwa katika siku hiyo tangu mwaka wa 1914. (Ufunuo 1:10) Alieleza namna yeye angeendesha farasi mweupe akiwa Mfalme aliyetawazwa karibuni, huku akifuatwa na mwendeshaji wa farasi mwenye rangi ya moto. Huyo “alipewa kuiondoa amani katika nchi, ili watu wauane, naye akapewa upanga mkubwa”​—upanga wa Vita ya Kutumia Silaha za Namna Zote. Upanga huo wa mfano sasa unatia ndani vyombo vyenye maangamizi mabaya na jeuri kubwa kupita zote ambavyo mwanadamu amepata kutengeneza kwa wingi. Hiyo ni kutia ndani makombora ya nyukilia ambayo yakijumlishwa pamoja yanaweza kuipasua-pasua jamaa nzima ya kibinadamu imalizike duniani hata yabaki mengine ya kuweza kurudia tendo hilo mara nyingi! Ikiwa kuwapo kwa Wanefili majitu, pamoja na ubaya mwingi sana wa mwanadamu katika siku za Noa, kulitokeza sababu ya kumfanya Yehova ‘awaharibu wanadamu kwa maana dunia ilijaa jeuri kwa sababu yao,’ hakika kuna sababu kubwa zaidi ya kumtazamia uyo huyo Bwana Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote ‘awaharibu wale waiharibuo dunia’ leo! (Mwanzo 6:4, 7, 13, ZSB; Ufunuo 6:1-4, NW; 11:18) Akitaja habari za watu wasiomcha Mungu wa kizazi chetu, Bwana Yesu mwenyewe alisema: “Kwa maana kama zilivyokuwa siku za Noa, ndivyo kutakavyokuwa [kuwapo] kwa Mwana wa watu. . . . Nao hawakujua hata garika ilipokuja na kuwaondosha wote.”​—Mathayo 24:37, 39, ZSB.

Maoni ya Kikristo juu ya Jeuri

11. (a) Kwa sababu gani Mungu alivikubali vita vya Israeli wa kale? (b) Pasipo shaka Mungu na Kristo wana maoni gani juu ya vita vya kisasa? (Linganisha 2 Wakorintho 10:3, 4.)

11 Ni kweli kwamba vita vilipigwa na watumishi wa Mungu wa nyakati za kale. Lakini ni lazima tukumbuke kwamba hivyo vilikuwa vita vya kitheokrasi, vilivyoamriwa na Mungu. Israeli walifanya mapigano kwa kusudi la kuyaondoa katika “nchi” ya Mungu mataifa yenye tabia za ufisadi na yenye kuabudu mashetani. (Mambo ya Walawi 18:24-27; Kumbukumbu la Torati 7:1-6) Je! vita vya mataifa vinakubaliwa na Mungu, hasa vile vita vilivyopigwa ili kujipatia utawala wa ulimwengu tangu mwaka wa 1914? Wakati Wakatoliki wanapochinja Wakatoliki, Waprotestanti kuchinja Waprotestanti, au Waislamu kuchinja Waislamu wenzao, je! wanatenda kupatana na mapenzi ya Mungu ambaye “alifanya kila taifa la wanadamu kutoka katika mmoja”? Pasipo shaka Kristo, yule Mwana-Mfalme wa Amani, ana maoni ya namna gani juu ya umwagaji wa damu uliotokea katika Jumuiya ya Wakristo wakati ilipoanza Vita ya Ulimwengu ya Kwanza kisha Vita ya Ulimwengu ya Pili? (Matendo 17:24-26; Isaya 9:6) Acha tuangalie kiwango kipya cha hali ya juu zaidi ambacho Mwana-Mfalme wa Amani aliwekea Wakristo muda mfupi tu kabla hajaelekeana na kifo chenye jeuri.

12, 13. (a) Kwa sababu gani Yesu alihakikisha kwamba wanafunzi wake wamechukua panga? (b) Wakati huo Yesu alionyesha jambo gani wazi juu ya vita vya kitheokrasi?

12 Kwa kuifikiria sehemu aliyo nayo katika kutimiza unabii, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake usiku uliotangulia kukamatwa kwake: “Naye asiye na upanga, na auze joho yake akanunue. Kwa kuwa nawaambia, hayo yaliyoandikwa hayana budi kutimizwa kwangu; ya kuwa, Alihesabiwa pamoja na wahalifu.” Walipomjibu, “Bwana, tazama, hapa pana panga mbili,” yeye aliwaambia: “Basi.” (Luka 22:36-38) Basi (au, imetosha) kwa kitu gani? Kwa kusudi la kukazia barabara somo la maana kwa Wakristo.

13 Hakika kusingaliweza kuwa na sababu yenye nguvu ya kutumia upanga wakati huo yenye kupita kuutumia kwa kusudi la kulinda Mwana wa Mungu mwenyewe! Hata hivyo hayakuwa mapenzi ya Mungu Yesu aachiliwe wakati huo. Kwa hiyo wakati mtume Petro alipotumia upanga wake kupiga mtumwa wa kuhani mkuu, Yesu alimwambia: “Rudisha upanga wako mahali pake; maana wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:52, 53; Yohana 18:10, 11) Kwa njia hiyo Yesu alionyesha wazi kwamba kuanzia wakati huo vita vya kitheokrasi havingetia ndani tena matumizi ya silaha za kimwili.

14. Kama ilivyosemwa na Yesu, ni nini kinachohusika katika ‘kutokuwa sehemu ya ulimwengu’?

14 Ni wazi kwamba maneno hayo yalipatana na yale ambayo Yesu alikuwa amewaambia wanafunzi wake jioni iyo hiyo, kwamba wangeteswa kwa sababu ya ‘kutokuwa sehemu ya ulimwengu.’ Yalipatana na sala ambayo Yesu alimpelekea Baba yake jioni iyo hiyo. Katika sala hiyo alikazia kwamba wanafunzi wake wangefanana naye kwa ‘kutokuwa sehemu ya ulimwengu.’ Sala yenyewe ilikubaliana na vile Yesu alivyomwambia Pilato: “Ufalme wangu si sehemu ya ulimwengu huu. Kama ufalme wangu ungalikuwa sehemu ya ulimwengu huu, watumishi wangu wangalinipigania ili kwamba nisitolewe nipewe kwa Wayahudi. Lakini, kama ilivyo, ufalme wangu si wa kutoka chanzo hiki.”​—Yohana 15:19, 20;17:14-16, NW; 18:36.

15. (a) Kujitenga na ulimwengu kumeongoza watu kwenye umoja gani? (b) Ni pande gani mbalimbali za umoja huo zinazoelezwa kwenye Isaya 2:2-4?

15 Je! wewe sasa umejitenga na ulimwengu huu na njia zake zenye jeuri, kama vile Yesu na wanafunzi wake walivyojitenga katika karne ya kwanza? Ikiwa ndivyo, basi umeanza kushiriki umoja mzuri ajabu wa ulimwenguni pote ulio na Mashahidi wa Yehova peke yao. Ni umoja unaoletwa na kutii sheria za Mungu na mapenzi yake anayotaka yafanywe siku hizi. Kwa sasa “mkutano mkubwa” wa Wakristo wapenda amani “wa kila taifa, na kabila, na jamaa, na lugha” unamiminika kwenye hekalu kuu la kiroho la Yehova ili kuabudu huko. (Ufunuo 7:9, 10, 15) Kwenye Isaya 2:2-4 wanasimuliwa hivi: “Na itakuwa katika siku za mwisho, mlima wa nyumba ya [Yehova] utawekwa imara juu ya milima, nao utainuliwa juu ya vilima; na mataifa yote watauendea makundi makundi. Na mataifa mengi watakwenda na kusema, Njoni, twende juu mlimani kwa [Yehova], nyumbani kwa Mungu wa Yakobo, naye atatufundisha njia zake, nasi tutakwenda katika mapito yake; maana katika Sayuni itatoka sheria, na neno la [Yehova] katika Yerusalemu. Naye atafanya hukumu katika mataifa mengi, atawakemea watu wa kabila nyingi; nao watafua panga zao ziwe majembe, na mikuki yao iwe miundu; taifa halitainua upanga juu ya taifa lingine, wala hawatajifunza vita tena kamwe.”

16. (a) Mashahidi wa Yehova wanatofautianaje na ulimwengu? (b) Mika 4:1-5 inatabiri nini, kwa habari ya ufanisi wa watu wa Mungu, sababu ya kupata ufanisi huo na matokeo ya mwisho? (c) Ni kwa sababu ya nini ulizo zaidi linatokea?

16 Hao si watu wenye kupunga-punga bendera za kutukuza mataifa yao mbali mbali, bali ni kundi moja la watu wenye amani walioungana, watu wa kutoka mataifa yote. Wao kwa kweli ni watu wasiokuwamo katika ulimwengu wenye kufanya vita. Baada ya kueleza namna ‘wanavyofua panga zao ziwe miundu,’ Mika 4:1-5 inaeleza habari ya ufanisi wao wa kiroho na taraja lao la kuishi milele duniani kwa umoja. Unabii wenyewe unawatofautisha na mataifa ya ulimwengu huu, ukisema: “Kwa maana mataifa yote watakwenda, kila moja kwa jina la mungu wake, na sisi tutakwenda kwa jina la [Yehova], Mungu wetu, milele na milele.” Lakini tunapoendelea kutembea kwa jina la Mungu, tunaelekeana na mikazo mingi kutoka kwenye ulimwengu wenye jeuri. Inatupasa tushughulikeje na hali zinazoweza kutokea? Makala inayofuata inatoa jibu la Biblia kwa ulizo hilo.

[Maelezo ya Chini]

a Biblia ya New World Translation, English Revised Version, Moffatt, The Living Bible.

b The New English Bible.

Wewe ungetoa majibu gani kwa maulizo yanayofuata:

□ Hali ya ulimwengu inauonyeshaje wakati wetu kuwa ndio siku za mwisho?

□ Kulingana na maandishi yaliyo katika Mwanzo, Mungu ana maoni gani juu ya jeuri?

□ Ni ulinganifu gani mbalimbali unaoonekana kati ya siku za Noa na nyakati za kisasa?

□ Kupatana na mfano aliouweka Yesu na maneno aliyoyasema, inawapasa Wakristo waendelee kujitenga kwa njia gani?

□ Maandiko ya Isaya 2:2-4 na Mika 4:1-5 yanatujulisha kwamba inatupasa kutembea na Mungu kwa njia gani, na ni nini matokeo ya kufanya hivyo?

[Picha katika ukurasa wa 12]

Yesu alisema, “Wote waushikao upanga, wataangamia kwa upanga’’

    Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
    Toka
    Ingia
    • Kiswahili
    • Shiriki
    • Mapendezi
    • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
    • Masharti ya Utumiaji
    • Sera ya Faragha
    • Mpangilio wa Faragha
    • JW.ORG
    • Ingia
    Shiriki