Tunaweza Kuendelezaje ‘Upendo Wetu wa Kwanza’?
1. Wakati wa hizi siku za mwisho, je! watu wa Mungu kwa ujumla wameuacha ‘upendo wao wa kwanza’?
“WATU wako wanajitoa kwa hiari, siku ya uwezo wako.” (Zaburi 110:3) Kama unabii huo ulivyotangulia kutabiri, watumishi wa Mungu leo wamekuwa wakijikaza sana katika kufanya mapenzi yake, wakiushika sana upendo wao wa kwanza waliomwonyesha Yehova. Wakiwa tengenezo, Mashahidi wa Yehova wamedumisha shauku na juhudi yao kwa ajili ya utumishi wake muda wote wenye magumu wa huu “umalizio wa mfumo wa mambo.”—Mathayo 24:3, 14, NW.
2, 3. (a) Kwa sababu gani huenda mtu mmoja mmoja akauacha ‘upendo wake wa kwanza’? (b) Tukikuta maoni ya kutaka kuuacha yakisitawi ndani yetu, inatupasa tufanye nini?
2 Hata hivyo, inawezekana Mkristo mmoja mmoja kuacha upendo aliokuwa nao kwanza. Matatizo ya kila siku huenda yakamfanya asahau mambo makuu ambayo Yehova amemfanyia. Huenda akachoka kungojea makusudi ya Yehova yatimizwe kisha aanze kuvutiwa na faida za kimwili zinazotolewa na ulimwengu, au labda huenda akajisikia ana uhitaji wa kutumia wakati mwingi zaidi katika tafrija kuliko alivyokuwa akifanya hapo kwanza. Huenda akaanza kuyaona madaraka ya Kikristo, kama kuhudhuria mikutano au makusanyiko, kutayarisha hotuba na kushiriki katika utumishi wa shambani kuwa mzigo kwake
3 Tukiona kwamba maoni hayo yanaendelea kusitawi ndani yetu, inatupasa tufuate shauri ambalo Yesu alilitolea kundi la Efeso, ili tusitawishe tena ‘upendo wetu wa kwanza,’ tujitahidi ‘kufanya matendo ya kwanza.’ (Ufunuo 2:4, 5) Inatupasa tutambue kwamba tunahitaji kujipatia tena upendo wenye joto jingi tuliokuwa tukimwonyesha Yehova na juhudi na shauku yetu kwa ajili ya utumishi wake. Tunaweza kufanya hivyo namna gani?
Sitawisha Hali ya Kumpenda Yehova
4. Tunaweza kufuataje mfano wa maoni mema ya mtunga zaburi? (Zaburi 119:97)
4 Mtunga zaburi mwenye kuongozwa na Mungu alisema: “Sheria yako naipenda mno ajabu, ndiyo kutafakari kwangu mchana kutwa.” (Zaburi 119:97) Hayo ni maoni mazuri sana juu ya sheria ya Mungu! Inathawabisha zaidi sana kumtumikia Yehova tukiwa na maoni kama hayo kuliko kuendelea kujilazimisha bila kutaka tufanye tunalolijua kuwa haki. Tunahitaji kukuza tamaa ya kufanya lililo haki, kulifanya kwa sababu tunataka.—Zaburi 25:4, 5.
5. (a) Paulo alipendekeza nini ili kulinda hali ya kiroho yetu? (b) Tunaweza kuhifadhi ubora wa hali ya kiroho yetu kwa njia gani?
5 Shetani angependa kutukaza mpaka tuuache ‘upendo wetu wa kwanza,’ kwa maana yeye ndiye adui mkubwa zaidi wa hali ya kiroho yetu. Ili wampinge, mtume Paulo aliwahimiza Waefeso wavae “suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu.” (Waefeso 6:13, NW) Kati ya silaha hizo yako mambo manne ya Kikristo yaliyo ya maana kabisa: kweli, uadilifu, imani na tumaini la wokovu. (Waefeso 6:14-17; 1 Wathesalonike 5:8) Bila shaka, tunajifunza habari za mambo hayo tunapoingia katika kundi mara ya kwanza. Lakini silaha za chuma zinaweza kupata kutu ikiwa hazitunzwi. Vivyo hivyo, sisi tusipoyatunza mambo hayo yaliyo ya maana kabisa, silaha zetu za kiroho zitaharibika kisha zishindwe kutukinga vya kutosha. Vyo vyote iwavyo, ni lazima sisi tuzuie jambo hilo lisitukie,
Jifunze na Utafakari
6. Misionari mmoja alitatuaje tatizo la kudumisha hali yake ya kiroho akiwa gerezani?
6 Mwaka wa 1958 misionari Stanley Jones alianza kutumikia miaka saba katika kifungo cha kuwekwa kizuizini akiwa peke yake katika gereza la China. Yeye aliendelezaje upendo wake kwa Yehova ukiwa wenye nguvu alipokuwa ametengwa na ndugu zake Wakristo akiwa peke yake, hata bila kuwa na Biblia? Yeye anaeleza kwamba aliyaandika maandiko yote ambayo angeweza kukumbuka na pia mitajo yo yote ya maneno ya Biblia ambayo aliweza kuona katika safu “za kidini” za magazeti ya utangazaji wa habari aliyokuwa akipelekewa nyakati nyingine. Kwa njia hiyo alijiwekea akiba ya maandiko ya Biblia ambayo yakawa msingi wa orodha ya funzo la kibinafsi na ya kutafakari. Kwa kuwa alizungukwa na watu wenye kupinga imani zake, alijua kwamba kama angekosa kuendelea kujaza moyo na akili zake mawazo ya Mungu, imani yake ingefifia upesi.
7. Sisi tunaelekeana na mikazo gani, na ni lazima tujikinge namna gani na mikazo hiyo?
7 Ni kweli kwamba walio wengi kati yetu hawako gerezani. Hata hivyo, muda mwingi tunakuwa wazi katika hali ya kuweza kuingiwa na mawazo ya ulimwengu huu. Ingawa vitumbuizo ambavyo ulimwengu unatolea watu havipingani nyakati zote na kanuni za Kikristo kwa njia ya moja kwa moja, hakika vitumbuizo hivyo haviendelezi mambo kama kweli, uadilifu, imani na tumaini la wokovu. Kwa hiyo, tusipotumia wakati tuwe tukiimarisha mioyo na akili zetu, inaelekea kwamba tutadhoofika kiroho kisha upendo wetu utakuwa baridi.
8. Ni baraka gani inayomjia mtu anayejifunza Neno la Mungu na kulitafakari?
8 Ikiwa sisi tunatumia wakati kujiimarisha wenyewe kupitia funzo la kibinafsi na kutafakari, tutakuwa kama mtu yule ambaye “sheria ya [Yehova] ndiyo impendezayo” na ambaye anasoma katika sheria hiyo kwa sauti ya chini mchana na usiku. Mtunga zaburi anasema hivi juu ya mtu huyo: “Atakuwa kama mti uliopandwa kandokando ya vijito vya maji, uzaao matunda yake kwa majira yake, wala jani lake halinyauki; na kila alitendalo litafanikiwa.”—Zaburi 1:2, 3.
9. Tunaweza kukuzaje upendo wa kutaka kujifunza Biblia na kuitafakari? (Zaburi 77:11,12)
9 Tukisema namna mambo yalivyo, wengi wetu kwa asili hawana mwelekeo wa kutaka kujifunza. Hata hivyo, ikiwa tunataka kufanya hivyo, tunaweza kujizoeza wenyewe tufurahie kujifunza. Mfikirie mtu anayependa kuzoeza maungo kwa kukimbia ili kujifurahisha tu. Labda hapo kwanza minofu ya mwili itapata maumivu. Lakini, pole kwa pole mwili wake utajirekebisha, na baada ya muda mfupi mkimbiaji huyo atayafurahia mazoezi yake ikiwa ataendelea kuvumilia. Paulo alimwambia Timotheo hivi: “Nawe ujizoeze kupata utauwa.” (1 Timotheo 4:7) Kujifunza Biblia ni sehemu moja ya utawa. (Mithali 2:1-6) Mara ya kwanza huenda mtu akahitaji kujitia nidhamu ndipo aweze kujifunza bila kuelekeza fikira kwenye mambo mengine. Lakini, baada ya muda mfupi tutakuwa na upendezi halisi wa kutaka kujifunza mawazo mapya au kujipatia ufahamu wenye kina kirefu zaidi juu ya mambo tunayoyajua tayari. Hapo ndipo funzo letu litatupatia raha ya kweli.—Zaburi 119:103, 104.
10. Kwa sababu gani habari zile zile zinarudiwa-rudiwa katika vichapo vya kutusaidia kujifunza?
10 Huenda wengine wakawa na maoni ya kwamba kwa kuwa wao wanajua yale mafundisho ya msingi ya Biblia hawahitaji tena kutumia wakati katika funzo la kibinafsi. Huenda hata wakalalamika wakati habari zile zile zinaporudiwa-rudiwa katika vichapo vya mafunzo ya Biblia. Lakini Biblia inasema kuna uhitaji wa vikumbusho. (Zaburi 119:95, 99; 2 Petro 3:1; Yuda 5) Tusipoendelea kujikumbusha juu ya ile kweli, juu ya viwango vya Mungu vya uadilifu, juu ya imani yetu na tumaini letu la wokovu, moyo wetu utavutwa na mambo mengine.
11. Ni nini mengine ya mambo ambayo Paulo alizungumza katika barua aliyoandikia Waefeso?
11 Ifikirie barua ambayo Paulo aliwaandikia Waefeso. Yeye aliwakumbusha vile hali yao ilivyokuwa imekuwa kabla hawajawa Wakristo, na akaeleza habari za tengenezo ambalo sasa walikuwa washiriki walo. (Waefeso 2:12; 4:4-6,17,18) Alitaja kusudi zuri ajabu ambalo Yehova analo kuelekea wanadamu na pia sehemu ambayo wanadamu wanashiriki katika kusudi hilo. (Waefeso 1:8-12; 2:4-6) Kisha aliwakumbusha juu ya kanuni za Kikristo ambazo zingewasaidia wapate mafanikio katika jamaa na katika kundi.—-Waefeso 4:1, 2; 5:21—6:4.
12. Kwa sababu gani Paulo aliwaambia Waefeso mambo waliyokuwa wamekwisha kuyajua?
12 Huenda ikawa mengine ya mambo ambayo Paulo aliandika yakawa yalikuwa mageni kwa Wakristo Waefeso, lakini mengi bila shaka yalihusu habari walizokuwa wamesikia mapema. Hata hivyo, Paulo alitaka kuwakumbusha hayo na labda awape ufahamu mpya kuhusu mambo hayo. Hivyo aliwasaidia Waefeso wasugue silaha zao za kiroho zing’ae zaidi kisha ‘wapate kufahamu pamoja na wataktifu wote jinsi ulivyo upana, na urefu, na kimo, na kina.’—Waefeso 1:15-17; 3:14-19.
13, 14. (a) Kujifunza na kutafakari kutatusaidia namna gani? (b) Ni vitu gani vingine vilivyo katika ‘suti ya silaha kutoka kwa Mungu’?
13 pia funzo la kibinafsi tulilo nalo litatuburudisha na kuongeza sana ufahamu wetu juu ya mawazo mengi ya msingi, na vilevile litatusaidia tuyashike sana mambo yenye kina kirefu zaidi ya Neno la Mungu. (1 Wakorintho 2:10) Kwa njia hiyo, ‘suti yetu ya silaha kutoka kwa Mungu’ itamzuia Shetani asituachishe upendo wetu wenye joto tunaomwonyesha Yehova na Mwanaye.
14 Kati ya mambo mengine, mtume Paulo alitaja sehemu nyingine za silaha za kiroho zetu ambazo hatujazungumza. Alisema kwamba Wakristo wanapaswa kuvisha ‘nyayo zao vile vifaa vya zile habari njema za amani’ na kwamba wanapaswa kuukubali “ule upanga wa ile roho, yaani, neno la Mungu.” (Waefeso 6:11-17, NW) Sehemu hizo zinatusaidiaje kudumisha ‘upendo wetu wa kwanza’?
Endelea Kuwa Mtendaji Katika Kuhubiri Ufalme
15. Ni njia gani mpya ambayo misionari mmoja aliyefungwa gerezani alitafuta ili ‘azidi sana kutenda kazi ya Bwana sikuzote’? (1 Wakorintho 15:58)
15 Mwaka wa 1958, wakati misionari Harold King alipoanza kifungo chake cha miaka minne na nusu katika gereza la China, alielekeana na tatizo lile lile lililomwelekea Stanley Jones: “Ili niendeleze uthamini wangu wa mambo ya kiroho ukiwa hai, nilipanga niwe na mpango wa utendaji wa ‘kuhubiri.’” Yeye alijitayarishia mahubiri fulani ya Biblia kutokana na maandiko aliyokumbuka, kisha akawa akiwahubiria watu wasiokuwapo, wa kuwazia tu. Mwishowe, aliongoza funzo la Biblia la mtu wa kuwazia tu. Matokeo yakawa nini? Alipofunguliwa, alikuwa na utayari na hamu ya kuwahubiria tena watu halisi!
16. Ni nini sababu moja ya maana inayopasa kutufanya tujishughulishe katika utumishi wa Yehova?
16 Yeye alitumia njia ya ajabu ya kutenda kupatana na kweli fulani ya maana, ya kwamba: Ili tubaki tukiwa na afya ya kiroho ni lazima tuendelee kujishughulisha katika utumishi wa Mungu. Mtume Petro alisema hivi: “Kazeni akili zenu kwa ajili ya utendaji.” (1 Petro 1:13, NW) Naye mtume Paulo alitoa kitia-moyo hiki: “Mwimarike, msitikisike, mkazidi sana kutenda kazi ya Bwana sikuzote, kwa kuwa mwajua ya kwamba taabu yenu siyo bure katika Bwana.”—1 Wakorintho 15:58.
17. Ni jambo gani lililostahili kuangaliwa kuhusu Wakristo waaminifu katika kundi la Filadelfia?
17 Inastahili kuangaliwa kwamba ingawa Wakristo katika Efeso walikuwa wameruhusu ‘upendo wao wa kwanza’ upoe, Wakristo wa kundi jingine la ujirani huo walikuwa wameendelea kujishughulisha, na bado upendo wao ulikuwa thabiti. Yesu aliliambia hivi kundi hilo jaminifu la Filadelfia: “Nayajua matendo yako. Tazama, nimekupa mlango uliofunguliwa mbele yako, ambao hapana awezaye kuufunga.”—Ufunuo 3:8.
18. Ni utendaji gani utakaotusaidia tudumishe ‘upendo wetu wa kwanza’ ukiwa hai?
18 Ni matendo gani yatasaidia shahidi wa Yehova wa kisasa adumishe ‘upendo wake wa kwanza’? Kati ya mengine, ni matendo yanayopatana na amri hii ya Yesu: “Kwa hiyo nendeni mkafanye wanafunzi kutoka watu wa mataifa yote.” (Mathayo 28:19, NW) Harold King alitambua umaana wa kufanya hivyo. Ndivyo pia na mtume Paulo. Ndiyo sababu Paulo aliwashauri Waefeso wavishe ‘nyayo zao vile vifaa vya zile habari njema za amani’ na kuwa tayari wakiwa na “ule upanga wa ile roho, yaani, neno la Mungu.”
19. Kazi ya kuhubiri, ambayo ni uthibitisho wa juhudi yetu, inajengaje juhudi yetu?
19 Kuna uhusiano wa karibu kati ya juhudi na kazi ya kuhubiri na kufanya wanafunzi. Ni kweli kwamba juhudi ndiyo inayotufanya tutake kutenda kazi hiyo. Lakini kazi ya kuhubiri nayo inachochea juhudi yetu halafu. Baada ya Yesu kumhubiria mwanamke Msamaria, aliwaambia wafuasi wake hivi: “Chakula changu ndicho hiki, niyatende mapenzi yake aliyenipeleka.” (Yohana 4:34) Kufundisha watu ile kweli kulikuwa kumemlisha yeye, kukamjenga. Vivyo hivyo, wakati sisi tunaposema na wengine juu ya Ufalme wa Mungu, kufanya hivyo kunakaza mambo ya maana kabisa katika akili na moyo wetu na kuongeza ujuzi wetu wa namna mbalimbali katika kuitetea ile kweli. (1 Petro 3:15) Zaidi ya hilo, roho ya Mungu inapoendelea kutuunga mkono katika kazi hiyo, sisi ‘tunapashwa moto kwa roho’ na kuiona ikifanya kazi juu ya wengine.—Warumi 12:11, NW.
20. Kuhubiri na kujifunza kibinafsi ni mambo yanayoshirikiana namna gani kutuendeleza tukiwa wenye nguvu?
20 Je! kazi ya kuhubiri inapasa kuichukua nafasi ya funzo la kibinafsi? Hapana. Usawaziko unahitajiwa kati ya utendaji huo wa namna mbili. Tukila chakula kingi cha kimwili lakini tusifanye mazoezi yo yote, mwishowe mwili wetu unaumia. Kwa upande mwingine, tukifanya mazoezi mengi bila kula chakula cha kutosha, hatimaye tutamaliza nguvu zetu za kimwili. Vivyo hivyo, tukijitia sana katika funzo la kibinafsi bila kuwahubiria wengine, inaelekea kwamba tutakosa usawaziko. Mtume Petro alishirikisha “utendaji” na ‘kukaza akili zetu.’ (1 Petro 1:13, NW) Tukiwahubiria wengine bila ya sisi kufanya funzo la kibinafsi—hasa ikiwa watu tunaohubiria hawaitikii sana—basi huenda tukamalizika. Lakini, tukijitia katika funzo la kibinafsi na kwenda nje tukaeleze wengine mambo ambayo tumejifunza, tutabaki tukiwa na afya ya kiroho.
Komboa Wakati
21, 22. (a) Ni kizuizi gani kikubwa ambacho Shetani ametokeza tusidumishe ‘upendo wetu wa kwanza’? (b) Paulo alipendekeza Waefeso wakishinde kizuizi hicho kwa njia gani, na kwa sababu gani inatupasa sisi tufuate shauri alilotoa?
21 Alipokuwa akieleza moja la matatizo makubwa zaidi yaliyompata gerezani Stanley Jones alisema: “Nilikuwa na wakati mwingi sana.” Tatizo lake lilikuwa kinyume kabisa cha lile linalopata wengi wa Mashahidi wa Yehova. Walio wengi kati yetu wanapungukiwa na wakati sikuzote. Kwa sababu gani iwe hivyo? Mtume Yohana alisema hivi: “Ulimwengu mzima uko katika uwezo wa yule mwovu.” (1 Yohana 5:19, NW) Ulimwengu wa Shetani unashughulisha sana watu daima hivi kwamba hawana nafasi kubwa ya kufikiri, achia mbali kujifunza kwenyewe. Sisi si sehemu ya ulimwengu, lakini kwa uhakika tunajisikia tukisongwa na matokeo ya njia ya maisha ya ulimwengu huu. Kwa kutumia mavutano ulimwengu wenyewe, “yule mwovu” angependa kutushughulisha sana mpaka tukose wakati wa kumtolea Mungu utumishi wetu.
22 Paulo alitambua tatizo hilo kisha akawapa Waefeso shauri hili lenye kuthaminika sana: “Angalieni sana jinsi mnavyoenenda; si kama watu wasio na hekima, bali kama watu wenye hekima; mkiukomboa wakati kwa maana zamani hizi ni za uovu. Kwa sababu hiyo msiwe wajinga, bali mfahamu ni nini yaliyo mapenzi ya [Yehova].” (Waefeso 5:15-17) Tusipokomboa wakati tufanye ‘mapenzi ya Yehova,’ mkazo wa kuishi katika hizi “zamani za uovu” utaelekea kupoza upendo wetu.
23. Ni funzo la kibinafsi la namna gani na utendaji wa kuhubiri wa namna gani utakaotusaidia tuendeleze ‘upendo wetu wa kwanza’ ukiwa hai?
23 Ni kweli kwamba Wakristo wengine wana wajibu mzito wa kutimiza au ni wagonjwa na hivyo wanapungukiwa sana na kipimo cha utumishi wanaomfanyia Mungu. (Luka 21:1-4) Lakini kupatana na shauri ambalo Paulo aliwapa watumwa Wakristo, lo lote tunaloweza kufanya linapasa kufanywa “kwa nafsi yote.” (Waefeso 6:5, 6, NW) Funzo la kibinafsi halitakuwa kamwe lenye kufurahika ikiwa tutaokoa vidakika vichache tu tulifanye kidogo kidogo wakati uo huo tukiendelea kuelekeza fikira kwenye kipindi cha televisheni (au redio). Vivyo hivyo, huduma yetu ya shambani haitakuwa na matokeo makubwa katika kutufanya tuendeleze ‘upendo wetu wa kwanza’ na kufanya juhudi yetu iendelee kuwa hai ikiwa baada ya tafrija moja na kabla ya ile nyingine ndipo tunatumia saa moja au mbili kila mwezi ili tuonyeshe kwamba angalau tumefanya kitu.—Linganisha 1 Timotheo 4:8.
Sali Upate Msaada
24. Ni msaada gani zaidi tunaouhitaji kabisa katika hali yetu ya kiroho ambao Paulo aliwatajia Waefeso?
24 Akimalizia mazungumzo yake juu ya ‘suti kamili ya silaha kutoka kwa Mungu,’ Paulo alihimiza waamini wenzake waukubali ‘ule upanga wa ile roho, yaani, neno la Mungu, huku kwa kila namna ya sala na kusihi wakiendelea kuomba katika kila pindi katika roho.’ (Waefeso 6:17, 18, NW) Tukiendelea kuhusiana na Yehova kwa ukaribu kupitia sala, hatutauacha ‘upendo wetu wa kwanza,’ hata tukilazimika kuvumilia mikazo mingi au hata kama tumetumikia miaka mingi kama Yohana tukiwa katika mfumo huu wa mambo. Paulo alisema hivi katika barua nyingine: “Nayaweza mambo yote katika yeye anitiaye nguvu.”—Wafilipi 4:13.
25. Kwa kurudia, ni misaada gani ambayo Yehova ametoa ili kutusaidia tusiache ‘upendo wetu wa kwanza’?
25 Walio wengi kati yetu wanachoka mara kwa mara. Lakini ujumbe ambao Yesu alipelekea kundi la Waefeso unaonyesha kwamba tunaweza kuepuka na ni lazima tuepuke kuuacha ‘upendo wetu wa kwanza.’ Kama vile Yehova alivyowasaidia Waefeso kupitia Paulo, Timotheo na wengine, yeye anatusaidia sisi leo kupitia tengenezo lake. Nasi pia tukijizoeza wenyewe kufurahia kujifunza na kutafakari na ‘kukaza akili zetu’ kwa ajili ya ule utendaji mwema wa kueleza wengine mambo tunayojifunza, huku tukisali tupate msaada wa Yehova ili tuvumilie katika kufanya mapenzi yake, hapo tutakuwa tunafanya kazi njema? Kupatana na yale ambayo mtume Paulo aliambia Wagalatia, “tusichoke katika kutenda mema; maana tutavuna kwa wakati wake, tusipozimia roho.”—Wagalatia 6:9.—Kutoka w11/1/83.
Wewe Ungejibuje?
□ Tusipopanga orodha ya wakati wa kujifunza na kutafakari juu ya Neno la Mungu, ni jambo gani linaloweza kupata upendo tunaomwonyesha Yehova?
□ Kwa sababu gani ni jambo lenye kuthaminika sana tujifunze si kweli mpya-mpya tu bali pia kweli na kanuni ambazo tumekwisha kuzisikia tayari?
□ Kwa sababu gani kuwahubiria wengine ni jambo linalohitajiwa kabisa ndipo tuweze kudumisha ‘upendo wetu wa kwanza’?
□ Kujifunza na kuhubiri ni mambo yanayoshirikianaje katika kutufanya tuendelee kuwa na afya ya kiroho?
□ Kwa sababu gani haitupasi kamwe kupuza sala tunapojitahidi kudumisha ‘upendo wetu wa kwanza’?
[Picha katika ukurasa wa 17]
Funzo linaweza kufurahika, nalo linauendeleza upendo wetu kwa Mungu ukiwa mpya-mpya
[Picha katika ukurasa wa 20]
Kusema na wengine juu ya ile kweli kunautia nguvu upendo tunaomwonyesha Yehova