“Upendo Wako wa Kwanza”
“Nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza. Basi, kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu.”—UFUNUO 2:4, 5.
1, 2. (a) Ni mashauri gani ambayo Yesu alielekezea kundi la Efeso? (b) Labda mashauri hayo yalitokeza nini?
JE! WEWE ni shahidi wa Yehova ambaye siku za nyuma ametumia miaka mingi katika utumishi wa uaminifu? Ikiwa ndivyo, wewe ungeonaje kama mtu uliyeheshimu sana angekuambia maneno hayo yaliyoonyeshwa mwanzoni? Je! ungeudhika? Au ungefikiri amekosea na angepaswa kuambia mtu mwingine hivyo, wala si wewe?
2 Karibu miaka 1,900 iliyopita kundi, au eklesia, la huko Efeso katika Asia Ndogo liliambiwa maneno hayo katika ujumbe liliopelekewa na Yesu Kristo aliyefufuliwa. Bila shaka maneno yake yaliwashtua. Wakristo hao wa Efeso walikuwa wamevumilia katika jina la Yehova na kupinga sana mavutano ya waasi-imani kwa miaka zaidi ya 40. (Matendo 18:18, 19; Waefeso 1:1, 2) Yesu alisema, “Nayajua matendo yako, na taabu yako, na subira yako, na ya kuwa huwezi kuchukuliana na watu wabaya, tena umewajaribu wale wajiitao mitume, nao sio, ukawaona kuwa waongo.” (Ufunuo 2:2) Wao walikuwa wangali “katika ile kweli,” kama tusemavyo. Kwa hiyo tatizo lao lilikuwa nini?
3. Tatizo la Wakristo Waefeso lilikuwa nini?
3 Walikuwa wameacha ‘upendo wao wa kwanza.’ Hawakuwa tena wakitumikia kwa joto lile lile la upendo wa Kikristo waliomwonyesha Yehova hapo kwanza. Kwa sababu hiyo, walikuwa wamelegeza mwendo. Basi, Yesu aliwaonya hivi: “Kumbuka ni wapi ulikoanguka; ukatubu, ukayafanye matendo ya kwanza.”—Ufunuo 2:5.
4. Tunaweza kuchukua onyo gani kutokana na yaliyowapata Waefeso?
4 Hapo pana onyo kwa watumishi wa Yehova leo. Ni wazi kwamba kuna uwezekano wa kupoa hata upande wa wale ambao wamekuwa Wakristo watendaji kwa muda mrefu. Huenda kwa nje bado wakaonekana kuwa wenye nguvu, lakini huenda kwa ndani wakawa wamekwisha kuacha upendo wenye kina kirefu waliokuwa wakimwonyesha Yehova hapo kwanza. Katika barua aliyoandikia Wakorintho, Paulo alionya hivi: “Anayejidhania kuwa amesimama na aangalie asianguke.” (1 Wakorintho 10:12) Ili kutusaidia katika jambo hilo, acheni tuone namna Waefeso walivyopata upendo wao na namna walivyosaidiwa kuudumisha.
Ukristo Katika Efeso
5, 6. Ni namna gani na wakati gani habari njema zilikuja kuhubiriwa katika Efeso?
5 Katika karne ya kwanza ya Wakati wa Kawaida wetu, mji wa Efeso ulikuwa mji mkuu wenye utajiri na shughuli nyingi, tena ulikuwa kao kuu la ibada ya kufuata desturi yenye usitawi ya kumwabudu Artemi (au, Diana) mungu-mke wa kipagani. Fundisho juu ya Yesu kuwa ndiye Masihi wa Yehova lilisikiwa huko kufikia mwaka wa 52 W.K., na si baada ya hapo, wakati Paulo alipofika kutoka Korintho pamoja na Akila na Prisila, hao wakiwa ni watu waliooana. Paulo mwenyewe hakuweza kubaki huko, lakini Akila na Prisila walibaki. Wakati Apolo, msemaji mzuri sana, alipoanza kufundisha huko habari za Yesu “kwa usahihi,” Wakristo hao wawili waliooana walisaidia kumwondolea ufahamu usio sawa aliokuwa nao juu ya mambo yaliyohusu ubatizo. Apolo alisonga mbele akawa mfanya kazi mwenye kuwaka bidii katika kundi la karne ya kwanza.—Matendo 18:24-28.
6 Miezi kadha baadaye, Paulo alirudi Efeso akakuta kikundi cha wanafunzi kama 12 hivi waliokuwa wamebatizwa kwa ubatizo wa Yohana. Waliitikia maneno ya Paulo, wakabatizwa upya. Halafu, kwa muda wa miezi mitatu akahubiri katika sinagogi la huko. Lakini wakati hesabu iliyo kubwa ya Wayahudi walipokataa kuitikia, Paulo na wale wanafunzi wapya walihama wakaenda kwenye jumba la shule ya Tirano ambako alianza kutoa hotuba za kila siku.—Matendo 19:8-10.
7, 8. Ni matukio gani makubwa yaliyotukia wakati wa ukuzi wa mwanzo-mwanzo wa kundi la huko Efeso?
7 Sasa kikaanza kipindi cha kufurahisha sana katika Efeso. Yehova alifanya matendo ya ajabu ya kuponya watu kwa kutumia Paulo. Watu waliogusa tu nguo zake walipona, na neno la kuhubiri kwake likaenea katika sehemu za jimbo lote. (Matendo 19:11-17) Katika barua ambayo aliiandika wakati huo, Paulo aliliambia kundi la Korintho lililokuwa ng’ambo ile nyingine ya Bahari ya Aegea maneno haya: “Mimi ninabaki katika Efeso mpaka ile sikukuu ya Pentekoste; kwa maana nimefunguliwa mlango mkubwa unaoongoza kwenye utendaji, lakini kuna wapinzani wengi.”—1 Wakorintho 16:8, 9, NW.
8 Paulo alikaa Efeso zaidi ya miaka miwili. Wengi walipata kujua habari za upendo mwingi ajabu ambao Yehova alikuwa ameonyesha kwa kutuma Mwanaye mzaliwa pekee ili wale wanaojizoeza imani wapate uzima wa milele. Waliikubali kweli, kisha walionyesha Yehova na Mwanaye upendo thabiti. Waliokuwa wazoeaji wa maajabu ya kiuchawi “wakakusanya vitabu vyao, wakavichoma moto mbele ya watu wote; wakafanya hesabu ya thamani yake, wakaona ya kwamba yapata fedha hamsini elfu. Hivyo ndivyo neno la [Yehova] lilivyozidi na kushinda kwa nguvu.” (Matendo 19:19, 20) Ebu wazia huo ulikuwa ushuhuda mkubwa kama nini!
9. Upendo wa lile kundi jipya ulijaribiwaje uonekane ulikuwa au haukuwa mwingi?
9 Baada ya muda mfupi, upendo wa Waefeso ulijaribiwa uonekane ulikuwa mwingi kadiri gani. Katika Efeso wafua-fedha wengi walijipatia mali nyingi kwa kutengeneza vihekalu vya fedha vya Artemi. Demetrio, mmoja wao, aliliona kundi hilo changa la Kikristo kuwa tisho kwa njia yao ya kujipatia riziki, basi akahutubia wafua-fedha wenzake na kuwachochea wafanye ghasia. Maisha ya Wakristo wa huko yalikuwa hatarini mpaka karani wa mji alipotuliza kundi hilo la wafanya ghasia. (Matendo 19:23-41) Huenda kukawa kulikuwa na majaribu yanayofanana na hilo yasiyoandikwa katika Biblia, kwa kuwa Paulo aliitaja juujuu habari ya kwamba ‘alipigana na wanyama wakali huko Efeso.’ (1 Wakorintho 15:32, HNWW) Hata hivyo, upendo wenye joto jingi ambao Waefeso walikuwa nao kwa Yehova uliwasaidia kuvumilia.
10. Halafu Paulo alijaribu namna gani kuwatia moyo wazee Waefeso?
10 Mwishowe, Paulo aliondoka Efeso. Lakini katika mwaka wa 56 W.K., alipokuwa katika safari yake ya kwenda Yerusalemu, alijikuta mwenyewe katika Mileto, kilometa 48 tu kutoka huko. Kwa hiyo akaitisha mkutano wa wazee wa Efeso na kuwatia moyo wafuate mfano wake mwenyewe na kuchunga kundi la Mungu lililokuwa chini ya uangalizu wao. Aliwaonya hasa juu ya “mbwa-mwitu wakali” ambao wangetokea kati yao na kupoteza wanafunzi. Alifunua pia kwamba ilielekea kuwa asingewaona tena uso kwa uso. Basi “wakalia sana wote, wakamwangukia Paulo shingoni, wakambusu-busu.”—Matendo 20:17-38.
11. Paulo alipata habari gani juu ya Waefeso alipokuwa Roma?
11 Paulo alipofika Yerusalemu alikamatwa na mwishowe akapelekwa Roma akiwa mfungwa. Akiwa huko, alielekeza tena mawazo yake kwa ndugu zake wa Efeso, naye akaandika barua inayopatikana katika Biblia ikiwa chini ya kichwa kinachosema “Kwa Waefeso.” Upendo ambao Wakristo wa Efeso walimwonyesha Yehova na Mwanaye ulikuwa ungali thabiti wakati huo, kwa kuwa Paulo aliwaambia hivi: “Mimi nami, tangu nilipopata habari za imani yenu katika Bwana Yesu, na pendo lenu kwa watakatifu wote, siachi kutoa shukrani kwa ajili yenu.”—Waefeso 1:15-17.
12. Akiwa Roma Paulo aliandika shauri gani ambalo lingaliwasaidia Waefeso wadumishe ‘upendo wao wa kwanza’?
12 Katika barua yake, Paulo alitoa mashauri mema yaliyokusudiwa kuwasaidia wafanye upendo wao uendelee kuwa hai. Aliwakumbusha kwamba walikuwa wakiishi katika siku mbovu na, kwa hiyo, walipaswa ‘kuukomboa wakati,’ si kuacha mambo mengine yawakoseshe nafasi ya kufanya mapenzi ya Mungu. (Waefeso 5:15-17) Paulo aliwakumbusha Waefeso pia kwamba adui zao wa kweli hawakuwa wanadamu waliojaribu kuwapinga. Bali, yeye alisema, “Sisi tunako kushindana mweleka . . . juu ya majeshi ya roho waovu katika mahali pa kimbingu.” Kwa hiyo, aliwatia nguvu kwa uthabiti wavae silaha za kiroho na kupashana habari na Mungu kwa ukaribu kupitia sala.—Waefeso 6:11-18, NW.
13. Paulo aliwezaje kusaidia Waefeso?
13 Paulo aliwaandikia Waefeso barua yao karibu na mwaka wa 60 au 61 wa Wakati wa Kawaida wetu. (Waefeso 1:1) Muda mfupi baadaye Timotheo alitembelea Efeso na, akiwa huko, akapokea barua kutoka kwa Paulo tunayoiita Timotheo wa Kwanza. Katika barua hiyo Paulo alimtia moyo kijana huyo wa kiume aendelee kukaa Efeso ili ‘aambie watu fulani waachane na zile hadithi tupu na orodha ndefu za mababu, ambazo huleta tu ubishi.’ (1 Timotheo 1:3, 4, HNWW) Bila shaka kuwapo kwa Timotheo mjini kulisaidia Wakristo walio wengi wa Efeso wadumishe upendo wao wenye juhudi waliomwonyesha Yehova yajapokuwako mavutano mabaya yaliyowazunguka.
14. (a) Yehova alikuwa amewatia nguvu Waefeso namna gani? (b) Ijapokuwa hivyo, ni jambo gani lililowapata?
14 Karibu na mwaka wa 65 W.K., Paulo alimwandikia Timotheo barua yake ya pili. Katika barua hiyo alitaja kwamba alikuwa ametuma mjumbe mwingine, Tikiko, aende Efeso. (2 Timotheo 4:12) Hapo ndipo zinapoishia habari tunazosoma juu ya Efeso mpaka Yesu alipopeleka baadaye ujumbe wake ulioandikwa katika kitabu cha Ufunuo. Wakristo wa huko Efeso walikuwa matunda yaliyotokana na kuhubiri kwa mtume Paulo. Wao walikuwa wamefaidika na ziara za baadaye zilizofanywa na Wakristo wenye kutokeza kama Timotheo, kisha wakapokea mashauri kupitia barua iliyoongozwa na roho takatifu, nao walikuwa sehemu ya ule “mwili mmoja.” (Waefeso 4:4) Hata hivyo waliuacha ‘upendo wao wa kwanza.’
Mashauri Thabiti Yalihitajiwa
15, 16. (a) Kwa sababu gani huenda wengine wakawa na maoni ya kwamba ingetazamiwa kwamba Waefeso wangeacha kiasi fulani cha joto la upendo wao wa kwanza? (b) Je! Yesu alikuwa na maoni hayo?
15 Huenda wengine wakawa na maoni ya kwamba kiasi fulani cha kupoa kwa joto la upendo wa Waefeso ni jambo la kikawaida tu linaloweza kutokea kwa vyo vyote. Ingawaje, kulikuwa kumekuwa na kundi katika Efeso kwa muda wa miaka zaidi ya 40 wakati Yesu alipopeleka ujumbe wake kupitia Yohana. Bila shaka, wengi hawakuukumbuka kibinafsi ule mfano mwema uliowekwa na Akila na Prisila wala kule kuhubiri kwenye uchangamfu mwingi kwa Apolo. Ilikuwa imepita miaka 30 tangu mtume Paulo afe. Yerusalemu ulikuwa umeharibiwa makumi mawili na nusu ya miaka kabla ya wakati huo. Kwa hiyo ingeweza kutazamiwa kwamba Wakristo Waefeso wangejikalia kwa starehe, waache kuuona uhitaji wa kufanya haraka na kuwa na juhudi.
16 Lakini, Yesu hakulikubali elekeo hilo kwa kulitolea kisababu cho chote. Wengine waliokuwa wamekuwa Wakristo kwa muda mrefu kama Waefeso au kwa muda mrefu zaidi ya wao hawakuwa wameacha ‘upendo wao wa kwanza.’ Mtume Yohana, aliyeuandika ujumbe wa Yesu akapelekea Waefeso, alikuwa amekuwa mfuasi wa Kristo kwa miaka zaidi ya 20 kufikia wakati ambao Paulo alileta habari njema Efeso. Zaidi ya hilo, wale wa kundi la Filadelfia walionyesha ushuhuda thabiti kwamba wao hawakuwa wameuacha ‘upendo wao wa kwanza.’—Ufunuo 3:7-11.
17. Ni shauri gani ambalo Yesu aliwapa Wakristo Waefeso?
17 Basi, Yesu hakuwa akipita kiasi alipowaambia kwa imara Waefeso hao kwamba kama hawangetubu na kuamsha tena upendo wao, ilielekea kwamba wangepata hasara ya kushindwa. Alisema: “Nitakiondoa kinara chako katika mahali pake, usipotubu.” (Ufunuo 2:5) Hilo halikuwa tisho hasa, bali kwa kiasi kikubwa lilikuwa onyo la upendo kwa Wakristo hao, likawahimiza watende kwa hekima wasipoteze mapendeleo yao.
Sababu Inayofanya ‘Upendo wa Kwanza’ Upotezwe
18, 19. (a) Waisraeli walikuwa na juhudi gani walipowekwa huru kwa kutolewa Misri? (b) Kwa sababu gani waliiacha juhudi hiyo?
18 Ni kwa sababu gani watu wanapoteza upendo wa kwanza waliokuwa wakimwonyesha Yehova na juhudi ya kufanya mapenzi yake? Biblia haituambii lililowapata Waefeso. Lakini kuna mifano mingine katika Biblia ya jambo la mfano huo lililotukia. Wakumbuke Waisraeli walioongozwa na Musa wakatolewa Misri. Watu wakombolewa wa Mungu walikuwa na shauku nyingi sana baada ya kushuhudia maajabu ya Yehova yaliyofikia upeo kwa kumwangamiza Farao na majeshi yake katika Bahari Nyekundu. Waliimba kwa nguvu nyingi wakisema, “Ee [Yehova], katika miungu ni nani aliye kama wewe?” (Kutoka 15:11; Zaburi 136:1,15) Baadaye, Yehova alipofanya agano nao, wote pamoja walitamka hivi: “Hayo yote aliyoyanena [Yehova] tutayatenda, nasi tutatii.”—Kutoka 24:7.
19 Hata hivyo maoni ya moyo wa Waisraeli yalibadilika upesi. Ukosefu wa maji kwa muda, ulaji wa chakula kile kile kimoja, kuogopa Wakanaani na matatizo mengine yaliwafanya wakasahau matendo hodari ya Yehova na agano alilokuwa amefanya nao. Jamani, wakiwa katika mahali salama pa mbali, nchi yao ya utumwa, Misri, ilianza kuonekana kuwa ya kuvutia! Waliusahau ukatili waliotendwa na Wamisri na mawazo yao yakawa tu juu ya ‘wale samaki, yale matango, yale matikiti, zile mboga, vile vitunguu na vitunguu saumu’ walivyokula walipokuwa huko.—Hesabu 11:5.
20, 21. (a) Wayahudi wa siku za Koreshi walisikia habari gani za kusisimua, nazo zilikuwa na matokeo gani? (b) Ni nini kilichofifisha shauku yao?
20 Wakumbuke, pia, wale Wayahudi waliorudi kutoka utumwa wa Kibabuloni mwaka wa 537 K.W.K. Ebu wazia msisimuko waliokuwa nao walipolisikia tangazo hili la Koreshi: “[Yehova] . . . ameniagiza nimjengee nyumba katika Yerusalemu, ulioko Yuda. Basi kila mtu katika ninyi nyote mlio watu wake, Mungu wake na awe pamoja naye, na akwee mpaka Yerusalemu, ulioko Yuda, akaijenge nyumba ya [Yehova], Mungu wa Israeli.” (Ezra 1:2, 3) Makumi ya maelfu waliitikia, kisha kukawa na mteremo mkubwa wakati msingi wa hekalu jipya ulipomaliza kuwekwa.—Ezra 2:64; 3:10-13.
21 Lakini, shauku hiyo ilififia upesi. Adui waliokuwa jirani zao walipinga na wakafanya werevu kupata amri rasmi la kukomesha kazi ya kujenga hekalu. (Ezra, sura ya 4) Wayahudi walianza kujijengea nyumba nzuri. (Hagai 1:4) Bila shaka, bado walijifikiria kuwa wazoeaji wa dini ya Kiyahudi. Hawakuwa wameiacha imani yao. Lakini walikuwa wameuacha ule upendo wenye joto waliokuwa wameonyesha kuelekea Yehova na faida za ibada ya kweli. Bila shaka, walifikiri walikuwa na usawaziko na kiasi katika mambo waliyokuwa wakifanya. Lakini Yehova hakukubaliana nao. Alituma manabii Hagai na Zekaria kuchochea juhudi yao na kuwatia moyo wamalize kuijenga nyumba ya Yehova.—Ezra 5:1, 2.
22, 23. (a) Ni nini kinachoweza kuwafanya Wakristo leo waache upendo wao wa kwanza? (b) Ni maulizo gani yanayobaki ambayo tutazungumza?
22 Jambo linalofanana na hilo linaweza kupata Wakristo wakati wetu. Matatizo ya kila siku ya kuishi katika ulimwengu usio wa Kikristo yanaweza kufanya furaha yao ififie. Muda fulani ukiisha kupita, huenda wakaiona ile kweli kuwa ya zamani na isiyosisimua. Hata huenda ikatukia kwamba, baada ya muda kupita na kufuta akilini kumbukumbu la namna mambo yalivyokuwa katika ulimwengu hapo zamani, Mkristo anaweza kuutamani ule unaoitwa uhuru, kuwa na hali ya kutotaka madaraka ya kutimiza, kama watu wa ulimwengu walivyo. (Waefeso 2:11, 12) Au huenda Wakristo wakalemewa na maoni ya watu wanaowazunguka. Huenda wakakuza maoni ya kwamba ni jambo la akili zaidi kujistarehesha zaidi katika utumishi wa Mungu, kulegeza mwendo kidogo.—Yeremia 17:9.
23 Bila shaka jambo la namna hiyo liliwapata Wakristo Waefeso, lakini ni wazi kwamba Yesu aliona wangeweza kurudia hali yao ya kwanza. Kwa kweli, kupitia mtume Paulo walikuwa wamekwisha kupokea mashauri mengi ambayo, kama wangeyatumia, yangewasaidia warudishe ‘upendo wao wa kwanza.’ Mashauri hayo yenye kuthaminika yalikuwa nini? Na je! yatatusaidia sisi leo tudumishe ‘upendo wetu wa kwanza’? Tutazungumza jambo hilo katika makala inayofuata.
Wewe Unaweza Kukumbuka—
□ Ni tatizo gani lililokuwa katika kundi la Efeso?
□ Ni msaada gani Yehova alikuwa amewapa?
□ Sababu gani Waisraeli siku za Musa waliacha juhudi yao?
□ Ni nini kilichofanya Waisraeli wa wakati wa Ezra waache shauku yao?
□ Ni nini kinachoweza kutufanya tuache ‘upendo wetu wa kwanza’?
[Picha katika ukurasa wa 12]
Washiriki wa kundi la Efeso waliuacha upendo wao wa kwanza, labda kwa sababu ya utafutaji wa vitu vya kimwili
[Picha katika ukurasa wa 14]
Hagai aliwauliza Wayahudi: ‘Huu ndio wakati wa ninyi kukaa katika nyumba zenu zenye mapambo ya mbao, na hali nyumba ya Mungu inakaa hali ya kuharibika?’